Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wenye Furaha Ni Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho”

“Wenye Furaha Ni Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho”

“Wenye Furaha Ni Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho”

WAKATI ndege wanapoamka asubuhi, wao huimba kwa muda mfupi, kisha huruka kwenda kutafuta chakula. Jioni, wao hurudi kwenye viota vyao, kisha huimba kwa muda mfupi na kulala. Katika majira fulani, wao hujamiiana, hutaga mayai, na kulea makinda yao. Wanyama wengine pia hufanya mambo kama hayo.

Sisi wanadamu ni tofauti. Ni kweli kwamba sisi hula, hulala na kuzaa, lakini wengi wetu hatutosheki na mambo hayo. Tunataka kujua kwa nini tupo hapa. Tunataka kujua kusudi la maisha yetu. Pia tunatamani kuwa na tumaini la wakati ujao. Mahitaji hayo muhimu yanaonyesha sifa ambayo wanadamu pekee wanayo, yaani, uhitaji na uwezo wa kufahamu mambo ya kiroho.

Tumeumbwa kwa Mfano wa Mungu

Biblia inaeleza kwa nini kiasili mwanadamu ana uhitaji wa kiroho: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwanzo 1:27) Kuumbwa “kwa mfano wa Mungu” kunamaanisha kwamba ingawa tumetiwa doa na hali ya kutokamilika na dhambi, tuna uwezo wa kuonyesha sifa fulani za Mungu. (Waroma 5:12) Kwa mfano, tunaweza kuwa wabunifu. Isitoshe, tuna hekima ya kadiri fulani, tunaelewa maana ya kutekeleza haki, na tuna uwezo wa kuonyeshana upendo kwa kujitolea. Tunaweza kukumbuka yaliyopita na kufanya mipango kwa ajili ya wakati ujao.—Methali 4:7; Mhubiri 3:1, 11; Mika 6:8; Yohana 13:34; 1 Yohana 4:8.

Uwezo wetu wa kuyafahamu mambo ya kiroho unadhihirishwa waziwazi na tamaa yetu ya asili ya kumwabudu Mungu. Tusipotosheleza uhitaji huo wa kuwa na uhusiano mzuri na Muumba wetu, hatuwezi kupata furaha ya kweli na yenye kudumu. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hata hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili kutosheleza tamaa hiyo kwa kujifunza ile kweli, yaani, mambo ya kweli kumhusu Mungu, viwango vyake, na kusudi lake kwa wanadamu. Tunaweza kuipata wapi kweli hiyo? Katika Biblia.

“Neno Lako Ni Kweli”

Mtume Paulo aliandika: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Maneno hayo ya Paulo yanapatana na ya Yesu ambaye alisema hivi katika sala kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” Leo tunajua kwamba Neno hilo ni Biblia Takatifu, na lingekuwa jambo la busara kuchunguza kama imani na viwango vyetu vinapatana na Biblia.—Yohana 17:17.

Kwa kulinganisha imani yetu na Neno la Mungu, tunawaiga watu wa Beroya ya kale ambao walihakikisha kwamba mafundisho ya Paulo yalipatana na Maandiko. Badala ya kuwakosoa Waberoya, Luka aliwasifu kwa mtazamo wao. Aliandika: “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Kwa kuwa leo kuna mafundisho mengi yenye kupingana kuhusu dini na maadili, ni muhimu kuiga Waberoya ambao walikuwa wasikivu.

Njia nyingine ya kuitambua kweli ni kutazama jinsi inavyobadili maisha ya watu. (Mathayo 7:17) Kwa mfano, kuishi kupatana na kweli ya Biblia kunapaswa kumfanya mtu awe mume bora, baba bora, mke bora, au mama bora. Jambo hilo huifanya familia iwe yenye furaha zaidi na humletea mtu uradhi. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika.”—Luka 11:28.

Maneno ya Yesu yanatukumbusha maneno ya Baba yake wa mbinguni, aliyewaambia hivi Waisraeli wa kale: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Bila shaka, wote wanaopenda wema na uadilifu wanaweza kuchochewa na sihi hiyo ya Yehova yenye uchangamfu!

Wengine Hupendelea “Masikio Yao Yafurahishwe”

Mungu aliwatolea Waisraeli sihi hiyo ya kutoka moyoni kwa sababu walikuwa wakipotoshwa na mafundisho ya uwongo ya dini. (Zaburi 106:35-40) Sisi pia tunapaswa kujilinda na uwongo. Paulo aliandika hivi kuhusu wale wanaodai kuwa Wakristo: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli.”—2 Timotheo 4:3, 4.

Viongozi wa dini hufurahisha masikio ya watu kwa kutoshutumu mazoea yanayotosheleza tamaa mbaya. Mazoea hayo ni kama vile ngono nje ya ndoa, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na ulevi. Biblia inaonyesha waziwazi kwamba wale wanaokubali mambo hayo na wale wanaoyafanya “hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10; Waroma 1:24-32.

Bila shaka, ili tuishi kupatana na viwango vya Biblia tunahitaji ujasiri, hasa ikiwa tunadhihakiwa, lakini inawezekana kuishi kupatana na viwango hivyo. Kuna watu wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wanatumia dawa za kulevya, walikuwa walevi, waasherati, wahuni wa mitaani, wezi, na wadanganyi. Hata hivyo, walitii Neno la Mungu na kwa msaada wa roho takatifu wakabadili maisha yao ili ‘watembee kwa kumstahili Yehova.’ (Wakolosai 1:9, 10; 1 Wakorintho 6:11) Baada ya kufanya amani pamoja na Mungu, walipata amani ya akili na, kama tutakavyoona, walipata pia tumaini la kweli la wakati ujao.

Tumaini la Ufalme

Tumaini la Biblia la kuwepo kwa amani ya kudumu kwa wanadamu watiifu litatimizwa kupitia Ufalme wa Mungu. Yesu alisema hivi katika sala yake ya mfano: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Naam, ni Ufalme wa Mungu tu unaoweza kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatendeka hapa duniani. Kwa nini? Kwa sababu Ufalme huo wa mbinguni, yaani, serikali inayoongozwa na Yesu Kristo, ndiyo njia ya Mungu ya kuonyesha haki Yake ya kuitawala dunia.—Zaburi 2:7-12; Danieli 7:13, 14.

Akiwa Mfalme wa Ufalme huo wa mbinguni, Yesu Kristo atawakomboa wanadamu watiifu kutoka katika aina zote za utumwa, kutia ndani dhambi ya Adamu isiyoepukika na matokeo yake ambayo ni ugonjwa na kifo. Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linasema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye [Yehova Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

Amani ya kudumu itakuwepo katika dunia yote. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hilo? Sababu inaonyeshwa kwenye andiko la Isaya 11:9, linalosema: “[Raia za Ufalme huo] hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Naam, kila mtu duniani atakuwa na ujuzi sahihi kumhusu Mungu na atamtii. Je, tazamio hilo halikuchangamshi moyo? Ikiwa ndivyo, sasa ndio wakati wa kuanza kupata ujuzi muhimu kumhusu Yehova.

Je, Utasikiliza Ujumbe wa Ufalme?

Kupitia Ufalme, Mungu atabatilisha kazi zote za Shetani na kuwaelimisha watu katika njia Zake za uadilifu. Hivyo, haishangazi kwamba Yesu alikazia Ufalme huo katika mafundisho yake. Alisema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kristo aliwaamuru wanafunzi wake wawaeleze wengine ujumbe huohuo. (Mathayo 28:19, 20) Alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Mwisho huo unakaribia sana. Basi, ni muhimu sana kwa watu wanyoofu kusikiliza habari hizo njema zenye kuokoa uhai!

Albert, anayetajwa katika makala inayotangulia, alisikia ujumbe wa Ufalme wakati mke wake na mwana wake walipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni, Albert alikuwa na shaka. Hata alimwomba kasisi wao aje kumtembelea mke wake na mwana wake ili kufunua uwongo wa Mashahidi. Lakini kasisi huyo hakutaka kujihusisha na jambo hilo. Hivyo, Albert akaamua kusikiliza mazungumzo hayo ya Biblia ili kuona kama Mashahidi hufundisha mambo yoyote ya uwongo. Baada ya kusikiliza pindi moja tu, alijiunga na funzo hilo, akiwa na hamu ya kujifunza mambo mengi zaidi. Baadaye alieleza ni kwa nini mtazamo wake ulibadilika. Alisema: “Huu ndio ujumbe ambao nimeutafuta sikuzote.”

Mwishowe, Albert alianza kutosheleza uhitaji wake wa kiroho, naye hakutazama nyuma. Kweli ya Biblia ilimpa kile alichokuwa akitafuta maishani mwake, yaani, suluhisho kwa ukosefu wa haki na ufisadi ambao umeenea sana, na tumaini la wakati ujao. Kweli ya Biblia ilimpa amani ya akili. Je, uhitaji wako wa kiroho unatoshelezwa? Tafadhali soma maswali katika sanduku kwenye ukurasa wa 6. Ikiwa ungependa habari zaidi, Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

JE, UHITAJI WAKO WA KIROHO UNATOSHELEZWA?

Je, unaridhishwa na chakula cha kiroho unachopata? Tunakualika usome maswali yanayofuata na utie alama yale unayoweza kujibu kwa usahihi.

□ Mungu ni nani, na anaitwaje?

□ Yesu Kristo ni nani? Kwa nini ilimpasa kufa? Unaweza kufaidikaje na kifo chake?

□ Je, kweli kuna Ibilisi? Ikiwa ndivyo, alitoka wapi?

□ Inakuwaje tunapokufa?

□ Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu?

□ Ufalme wa Mungu ni nini?

□ Mungu ameweka viwango gani vya maadili?

□ Mungu amewapa waume na wake madaraka gani katika familia? Ni kanuni gani za Biblia zinazochangia furaha ya familia?

Ikiwa huna hakika kuhusu jibu la swali lolote kati ya maswali hayo, unaweza kuomba broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Broshua hiyo imechapishwa na Mashahidi wa Yehova katika lugha 300 hivi, nayo ina masomo 16 ya msingi ya Biblia na inatoa majibu ya Kimaandiko kwa maswali yote yaliyoorodheshwa hapo juu.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Tofauti na wanyama, wanadamu wana uhitaji wa kiroho

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.”—2 Timotheo 4:3

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufalme wa Kimasihi wa Mungu utaleta amani ya kudumu