Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo”

“Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo”

“Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo”

“Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.”—2 WAKORINTHO 13:5.

1, 2. (a) Tunaweza kuathiriwaje tunapokuwa na shaka kuhusu mambo tunayoamini? (b) Ni hali gani iliyotukia katika karne ya kwanza huko Korintho ambayo huenda iliwafanya watu fulani wawe na shaka kuhusu njia ambayo wanapaswa kufuata?

MTU fulani anayetembea katika eneo la mashambani anafika kwenye njia panda. Kwa kuwa hana uhakika kuhusu njia inayoelekea mahali anapoenda, anawaomba watu wanaopita wamwonyeshe njia, lakini habari wanazotoa zinapingana. Akiwa amevurugika anashindwa kuendelea na safari yake. Tunaweza kuathiriwa kwa njia hiyohiyo tunapokuwa na shaka kuhusu mambo tunayoamini. Uwezo wetu wa kufanya maamuzi unaweza kuathiriwa na kutufanya tukose uhakika kuhusu njia ambayo tunapaswa kufuata.

2 Yaelekea baadhi ya watu waliathiriwa kwa njia hiyohiyo wakati hali fulani ilipotokea katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Korintho, Ugiriki. ‘Mitume walio bora sana’ walikuwa wakitilia shaka mamlaka ya mtume Paulo, wakisema: “Barua zake ni nzito na zenye nguvu nyingi, lakini kuwapo kwake mwenyewe kimwili ni dhaifu na maneno yake ni yenye kudharaulika.” (2 Wakorintho 10:7-12; 11:5, 6) Huenda maoni hayo yaliwafanya wengine katika kutaniko la Korintho wawe na shaka kuhusu njia wanayopaswa kufuata.

3, 4. Kwa nini tupendezwe na shauri la Paulo kwa Wakorintho?

3 Paulo alianzisha kutaniko la Korintho wakati wa ziara yake huko katika mwaka wa 50 W.K. Alikaa Korintho “kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha kati yao neno la Mungu.” Kwa kweli, ‘wengi kati ya Wakorintho waliosikia walianza kuamini na kubatizwa.’ (Matendo 18:5-11) Paulo alihangaikia sana hali ya kiroho ya waamini wenzake huko Korintho. Isitoshe, Wakorintho walikuwa wamemwandikia barua ili kumwomba awashauri kuhusu mambo fulani. (1 Wakorintho 7:1) Hivyo akawapa shauri bora sana.

4 Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Kutumia shauri hilo kungewasaidia akina ndugu huko Korintho wasiwe na shaka kuhusu njia ambayo wanapaswa kufuata. Shauri hilo linaweza kutufaidi katika njia hiyohiyo. Hivyo, tunawezaje kutumia shauri la Paulo? Tunaweza kufanya nini ili kujijaribu kama tuko katika imani? Na ni mambo gani yanayohusika katika kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo?

“Endeleeni Kujijaribu Kama Ninyi Mko Katika Imani”

5, 6. Ni kipimo gani kinachotusaidia kujijaribu kama tuko katika imani, na kwa nini hicho ndicho kipimo kinachofaa kabisa?

5 Katika jaribio lolote lile, kwa kawaida kitu au mtu hujaribiwa kwa kutumia kipimo au kiwango fulani. Katika habari hii, kile kinachojaribiwa si imani, yaani, mambo yote ambayo tumeamini. Badala yake, sisi wenyewe ndio tunaojaribiwa. Na kuna kipimo kikamilifu kinachotumiwa katika jaribio hilo. Wimbo mmoja uliotungwa na mtunga-zaburi Daudi unasema hivi: “Sheria ya Yehova ni kamilifu, huirudisha nafsi. Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima. Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.” (Zaburi 19:7, 8) Biblia ina sheria kamilifu za Yehova, maagizo yake manyoofu, vikumbusho vyake vyenye kutegemeka, na amri zake safi. Ujumbe uliomo katika Biblia ndicho kipimo kinachofaa kabisa kutumiwa katika jaribio hilo.

6 Mtume Paulo anasema hivi kuhusu ujumbe huo uliotoka kwa Mungu: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Naam, neno la Mungu linaweza kupima mioyo yetu, yaani, jinsi tulivyo kwa ndani. Tunawezaje kutumia ujumbe huo wenye makali na wenye nguvu maishani mwetu? Mtunga-zaburi anataja waziwazi kile kinachohusika. Aliimba hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye . . . mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) “Sheria ya Yehova” inapatikana katika Neno lake lililoandikwa, Biblia. Tunapaswa kufurahia kulisoma Neno la Yehova. Bila shaka, tunapaswa kutenga wakati kulisoma kwa sauti ya chini, au kutafakari juu ya Neno hilo. Tunapofanya hivyo, tunahitaji kuacha mambo yaliyoandikwa humo yatupime.

7. Ni ipi njia kuu ya kujijaribu kama tuko katika imani?

7 Kwa hiyo, njia kuu ya kujijaribu kama tuko katika imani ni kusoma Neno la Mungu na kutafakari, huku tukichunguza ikiwa mwenendo wetu unapatana na yale tunayojifunza. Tunafurahi kwamba tunasaidiwa kwa njia nyingi kuelewa Neno la Mungu.

8. Vichapo vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutusaidiaje kujijaribu kama tuko katika imani?

8 Yehova ameandaa mafundisho na maagizo kupitia vichapo vinavyofafanua Maandiko ambavyo vinatolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Kwa mfano, fikiria sanduku lenye kichwa “Maswali ya Kutafakari” linalopatikana mwishoni mwa sura nyingi za kitabu Mkaribie Yehova. * Sehemu hiyo ya kitabu hicho hutusaidia sana kutafakari. Habari nyingi zinazozungumziwa katika magazeti yetu ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! hutusaidia pia kujijaribu kama tuko katika imani. Mwanamke mmoja Mkristo alisema hivi kuhusu makala zinazozungumzia kitabu cha Methali ambazo zimekuwa zikichapishwa hivi majuzi katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi: “Makala hizo hunisaidia sana. Zinanisaidia kuchunguza ikiwa usemi, mwenendo, na mtazamo wangu unapatana na viwango vya uadilifu vya Yehova.”

9, 10. Ni maandalizi gani kutoka kwa Yehova yanayotusaidia kujijaribu kama tuko katika imani?

9 Pia, sisi hupokea miongozo mingi na kutiwa moyo sana kwenye mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Hayo ni baadhi ya maandalizi ya kiroho ambayo Mungu amewatayarishia wale ambao Isaya alitabiri hivi juu yao: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote yatamiminika huko. Na vikundi vingi vya watu hakika vitaenda na kusema: ‘Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova, . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.’” (Isaya 2:2, 3) Bila shaka, ni baraka kupokea mafundisho hayo kuhusu njia za Yehova.

10 Isitoshe, tunajijaribu kama tuko katika imani kwa kufuata mashauri ya wale walio na sifa za kustahili kiroho, kutia ndani wazee Wakristo. Biblia inasema hivi kuwahusu: “Akina ndugu, hata mtu akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mmoja wenu akiendelea kujiangalia, ili wewe pia usije ukajaribiwa.” (Wagalatia 6:1) Tunafurahia kama nini njia hiyo ya kuturekebisha!

11. Kujijaribu kama tuko katika imani kunahusisha nini?

11 Wanaume waliowekwa rasmi, vichapo vyetu, na mikutano ya Kikristo, ni maandalizi bora kutoka kwa Yehova. Hata hivyo, kujijaribu kama tuko katika imani kunahusisha kujichunguza. Kwa hiyo, tunaposoma vichapo vyetu au kusikiliza mashauri ya Kimaandiko, tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Je, maneno haya yanafafanua jinsi nilivyo? Je, mimi hufanya jambo linalotajwa hapa? Je, ninafuata mafundisho yote ya Kikristo?’ Hali yetu ya kiroho inategemea mtazamo wetu kuelekea habari tunazopokea kupitia maandalizi hayo. Biblia inasema hivi: “Mtu wa kimwili hayapokei mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake .  . . . Hata hivyo, mtu wa kiroho huchunguza mambo yote.” (1 Wakorintho 2:14, 15) Je, hatupaswi kujitahidi kudumisha mtazamo mzuri wa kiroho kuelekea mambo tunayosoma katika vitabu vyetu, magazeti, na vichapo vingine, na vilevile kuelekea mambo tunayosikia kwenye mikutano yetu na kutoka kwa wazee?

“Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo”

12. Kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo kunatia ndani nini?

12 Kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo kunatia ndani kujichunguza. Naam, tunaweza kuwa katika kweli, lakini hali yetu ya kiroho ikoje? Kuthibitisha jinsi tulivyo kunatia ndani kuonyesha kwamba tumekomaa na tunathamini kikweli maandalizi ya kiroho.

13. Kulingana na Waebrania 5:14, ni nini kinachothibitisha kwamba tumekomaa?

13 Tunaweza kuchunguza nini ndani yetu ili kuthibitisha kwamba sisi ni Wakristo wakomavu? Mtume Paulo aliandika hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Tunathibitisha kwamba tumekomaa kwa kuzoeza nguvu zetu za ufahamu. Kama vile misuli fulani ya mwili wa mwanariadha inavyohitaji kuzoezwa tena na tena ili afaulu katika michezo, nguvu zetu za ufahamu zinahitaji kuzoezwa kwa kutumia kanuni za Biblia.

14, 15. Kwa nini tunapaswa kujifunza kwa bidii mambo mazito ya Neno la Mungu?

14 Lakini kabla ya kuzoeza nguvu zetu za ufahamu, tunahitaji kwanza kupata ujuzi. Ili tuzipate, ni lazima tujifunze kibinafsi kwa bidii. Tunapojifunza kibinafsi kwa ukawaida, hasa kuhusu mambo mazito ya Neno la Mungu, nguvu zetu za ufahamu huongezeka. Kwa miaka mingi, habari nyingi nzito zimezungumziwa katika Mnara wa Mlinzi. Sisi hutendaje tunapopokea makala zinazozungumzia mafundisho mazito ya ile kweli? Je, sisi huepuka kuzisoma kwa sababu tu zina ‘mambo fulani yaliyo magumu kueleweka’? (2 Petro 3:16) Badala ya kufanya hivyo sisi hujitahidi hata zaidi kuelewa mambo yanayozungumziwa.—Waefeso 3:18.

15 Vipi tukiona kwamba ni vigumu kuwa na funzo la kibinafsi? Ni muhimu tujitahidi kusitawisha au kuwa na tamaa ya kujifunza. * (1 Petro 2:2) Ili tukue kufikia ukomavu tunahitaji kujifunza kula chakula kigumu, yaani, mafundisho mazito ya Neno la Mungu. Tusipokula chakula hicho, nguvu zetu za ufahamu hazitaongezeka. Hata hivyo, kuthibitisha kwamba tumekomaa kunatia ndani mengi zaidi ya kupata nguvu za ufahamu. Kila siku tunapaswa kutumia ujuzi ambao tunapata tunapojifunza kibinafsi kwa bidii.

16, 17. Mwanafunzi Yakobo anatoa shauri gani kuhusu kuwa “watendaji wa neno”?

16 Isitoshe, tunathibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo kwa kuonyesha uthamini kwa ile kweli kupitia matendo yetu ya imani. Mwanafunzi Yakobo anatumia mfano mzuri sana kueleza jinsi ya kujichunguza kuhusiana na jambo hilo, anaposema hivi: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu, mkijidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli. Kwa maana ikiwa yeyote ni msikiaji wa neno, na si mtendaji, huyo ni kama mtu anayeutazama uso wake wa asili katika kioo. Kwa maana yeye hujitazama, naye huenda zake na kusahau mara moja yeye ni mtu wa namna gani. Lakini yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:22-25.

17 Yakobo anamaanisha hivi: ‘Tazama kioo cha neno la Mungu na ujichunguze. Endelea kufanya hivyo, na ujichanganue kwa kutumia mambo unayojifunza katika neno la Mungu. Kisha, usisahau haraka mambo uliyoona. Fanya marekebisho yanayohitajiwa.’ Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kufuata shauri hilo nyakati nyingine.

18. Kwa nini si rahisi kufuata shauri la Yakobo?

18 Kwa mfano, fikiria takwa la kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Paulo aliandika hivi: “Kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Waroma 10:10) Ili tutumie kinywa chetu kufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu, tunahitaji kufanya marekebisho kadhaa. Si rahisi kwa wengi wetu kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Tunahitaji kufanya mabadiliko mengi na kujinyima mambo mengi ili tushiriki kwa bidii katika kazi hiyo na kuifanya iwe muhimu zaidi maishani mwetu. (Mathayo 6:33) Lakini tunapofanya kazi hiyo tuliyopewa na Mungu, sisi hufurahi kwa sababu inamletea Yehova sifa. Basi, je, sisi ni watangazaji wa Ufalme wenye bidii?

19. Matendo yetu ya imani yanapaswa kutia ndani nini?

19 Matendo yetu ya imani yanapaswa kuwa mengi kadiri gani? Paulo anasema hivi: “Mambo mliyojifunza na vilevile mkayapokea na kuyasikia na kuyaona kuhusiana nami, mzoee kuyafanya hayo; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.” (Wafilipi 4:9) Tunathibitisha jinsi tulivyo kwa kuzoea kufanya mambo ambayo tumejifunza, tumepokea, tumesikia, na kuona, yaani, mambo yote yanayohusika katika kuwa wanafunzi wa Yesu na katika wakfu wetu wa Kikristo. Yehova anatuagiza hivi kupitia nabii Isaya: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—Isaya 30:21.

20. Ni nani ambao ni baraka kubwa katika kutaniko?

20 Wanaume na wanawake wanaojifunza Neno la Mungu kwa bidii, wanaohubiri habari njema kwa juhudi nyingi, wanaodumisha utimilifu wao, na kutetea Ufalme kwa ushikamanifu ni baraka kubwa katika kutaniko. Wao hufanya kutaniko wanaloshirikiana nalo liwe thabiti. Wao hutoa msaada mkubwa sana, hasa kwa sababu kuna wapya wengi sana ambao wanahitaji kusaidiwa. Tunapotii shauri la Paulo la ‘kuendelea kujijaribu kama tuko katika imani na kuendelea kuthibitisha sisi wenyewe jinsi tulivyo,’ tunawatia wengine moyo.

Furahia Kufanya Mapenzi ya Mungu

21, 22. Tunawezaje kufurahia kufanya mapenzi ya Mungu?

21 Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliimba hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zaburi 40:8) Daudi alifurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu sheria ya Yehova ilikuwa ndani ya moyo wake. Daudi hakuwa na shaka kuhusu njia aliyopaswa kuifuata.

22 Sheria ya Mungu inapokuwa ndani yetu, hatuwi na shaka yoyote kuhusu njia tunayopaswa kuifuata. Tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Basi, acheni ‘tujitahidi sana’ kuendelea kumtumikia Yehova kutoka moyoni.—Luka 13:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 15 Ili upate madokezo mazuri kuhusu kujifunza, soma ukurasa wa 27-32 katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Tunawezaje kujijaribu kama tuko katika imani?

• Kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo kunatia ndani nini?

• Tunathibitishaje kwamba sisi ni Wakristo wakomavu?

• Matendo yetu ya imani hutusaidiaje kujichunguza?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unajua njia kuu ya kujijaribu kama uko katika imani?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tunathibitisha kwamba sisi ni Wakristo wakomavu kwa kuzoeza nguvu zetu za ufahamu

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tunathibitisha jinsi tulivyo kwa kuwa ‘watendaji wa neno, bali si wasikiaji wasahaulifu’