Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”

“Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”

“Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”

NI WENGI kama nzige wanaoharibu mashamba yenye rutuba. Ni wakati wa utawala wa waamuzi katika taifa la Israeli, nao Waisraeli wamekata tamaa. Kwa kipindi cha miaka saba, wakati tu mbegu zinapoanza kuchipuka, makundi ya wapanda-ngamia kutoka Midiani, Amaleki, na maeneo ya Mashariki wamekuwa wakivamia nchi. Mifugo ya waporaji huvamia nchi hiyo wakitafuta malisho nao hula mimea yote. Lakini Waisraeli hawana punda, wala fahali, wala kondoo. Waisraeli wanateseka sana chini ya utawala wenye kutisha wa Wamidiani hivi kwamba wanalazimika kutumia maghala ya chini ya udongo yaliyokuwa katika milima, mapango, na mahali palipo pagumu kufikiwa.

Kwa nini wanakabili hali hiyo mbaya? Waisraeli waasi-imani wanaabudu miungu ya uwongo. Kwa sababu hiyo, Yehova anawaacha wakandamizwe. Waisraeli wanaposhindwa kuendelea kuvumilia hali hiyo, wanamlilia Yehova ili awasaidie. Je, atawasikiliza? Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo ambayo Waisraeli wanakabili?—Waamuzi 6:1-6.

Mkulima Mwenye Kujihadhari au “Mwanamume Shujaa na Mwenye Nguvu”?

Ili kupura ngano, wakulima Waisraeli walikuwa wakitumia fahali na chombo cha kupuria. Walikuwa wakipura ngano mahali palipo wazi ili makapi yapeperushwe na upepo wakati wa kupepeta. Lakini sasa hawawezi kufanya hivyo kwa sababu wanaogopa kuvamiwa na waporaji. Hivyo, ili asionekane na Wamidiani, Gideoni anapura ngano katika shinikizo la divai. Huenda shinikizo hilo ni mtungi wa divai uliositiriwa ambao umechongwa kwenye mwamba. (Waamuzi 6:11) Akiwa hapo anaweza kutumia fimbo kupigapiga kiasi kidogo-kidogo tu cha masuke. Gideoni anatumia mbinu yoyote ile chini ya hali hizo ngumu.

Wazia jinsi Gideoni anavyoshangaa malaika wa Yehova anapotokea na kumwambia: “Yehova yupo pamoja nawe, Ee mwanamume shujaa na mwenye nguvu.” (Waamuzi 6:12) Kwa kuwa anapura nafaka kwa siri akiwa katika shinikizo la divai, Gideoni hawezi kujiona kuwa shujaa. Hata hivyo, maneno hayo yanaonyesha kwamba Mungu ana hakika kwamba Gideoni anaweza kuwa kiongozi shujaa katika taifa la Israeli. Vyovyote vile, Gideoni mwenyewe anahitaji kuhakikishiwa jambo hilo.

Anapotumwa na Yehova ‘akawaokoe Israeli kutoka katika mkono wa Midiani,’ Gideoni anajibu hivi kwa unyenyekevu: “Nakuomba radhi, Yehova. Nitawaokoa Israeli na nini? Tazama! Elfu yangu ndiyo ndogo zaidi katika Manase, na mimi ndiye mdogo zaidi katika nyumba ya baba yangu.” Kwa kujihadhari, Gideoni anamwomba ishara inayothibitisha kwamba Mungu atakuwa pamoja naye anapowapiga Wamidiani, naye Yehova anakubali ombi hilo linalofaa la kutaka uhakikisho. Hivyo, Gideoni anamtayarishia chakula malaika huyo aliyemtembelea, kisha moto unapanda kutoka katika mwamba na kuteketeza zawadi hiyo. Baada ya kutulizwa na Yehova, Gideoni anajenga madhabahu mahali hapo.—Waamuzi 6:12-24.

“Baali na Ajitetee Mwenyewe Kisheria”

Waisraeli wanakandamizwa na Wamidiani. Hata hivyo, tatizo kuu zaidi wanalokabili ni kuwa watumwa wa ibada ya Baali. Yehova ni “Mungu mwenye wivu,” na hawezi kukubali mtu yeyote amtumikie huku akiabudu miungu mingine. (Kutoka 34:14) Kwa hiyo, Yehova anamwamuru Gideoni abomoe madhabahu ya Baali, ambayo ni ya baba yake, na kuukata ule mti mtakatifu. Kwa kuwa Gideoni anahofia hatua ambayo baba yake angechukua iwapo angebomoa madhabahu hiyo wakati wa mchana, anaamua kuibomoa usiku, akisaidiwa na watumishi kumi.

Gideoni ana sababu mzuri ya kujihadhari, kwani waabudu wa Baali wanaoishi katika eneo hilo wanapotambua kwamba Gideoni “amedharau kitu kitakatifu,” wanataka auawe. Yoashi, baba ya Gideoni, anatumia hoja zisizoweza kupingwa ili kusababu na waabudu hao anaposema kwamba ikiwa Baali ni Mungu, basi anaweza kujitetea. Kisha Yoashi anaanza kumwita mwana wake Yerubaali, jina linalomaanisha, “Baali na Ajitetee Mwenyewe Kisheria.”—Waamuzi 6:25-32.

Nyakati zote, Mungu huwabariki watumishi wake wanaosimama imara kutetea ibada ya kweli. Wamidiani na watu wengine wanaowaunga mkono wanapoivamia tena nchi ya Waisraeli, ‘roho ya Yehova inamfunika Gideoni.’ (Waamuzi 6:34) Gideoni, ambaye sasa anaongozwa na roho ya Mungu, au nguvu yake ya utendaji, anakusanya askari kutoka katika kabila la Manase, Asheri, Zebuloni, na Naftali.—Waamuzi 6:35.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Pigano

Ijapokuwa Gideoni ana jeshi lenye watu 32,000, bado anamwomba Mungu ampe ishara. Umande ukija juu ya manyoya yaliyoachwa katika uwanja wa kupuria huku nchi yote ikibaki kavu, itakuwa wazi kwamba Mungu atawaokoa Israeli kupitia kwake. Yehova anafanya muujiza huo, kisha Gideoni anaomba tena ukavu uje juu ya manyoya peke yake, na umande uje juu ya nchi yote. Yehova anafanya muujiza huo wa pili na hivyo kumpa Gideoni uhakikisho. Je, Gideoni anajihadhari kupita kiasi? La, kwani Yehova anamjibu anapomwomba ampe uhakikisho. (Waamuzi 6:36-40) Hatutazamii miujiza kama hiyo itukie leo. Hata hivyo, tunaweza kupata mwongozo na uhakikisho wa Yehova kupitia Neno lake.

Sasa Mungu anasema kwamba jeshi la Gideoni ni kubwa mno. Waisraeli wakiwashinda maadui wao wakiwa na jeshi kubwa hivyo, huenda wakajisifu kwa kudai kwamba wao ndio waliojiokoa. Lakini ni sharti Yehova atukuzwe kwa sababu ya ushindi huo unaotarajiwa. Tatizo hilo litatatuliwaje? Gideoni anatumia kanuni fulani iliyo katika Sheria ya Musa na kuwaomba wanaoogopa warudi nyumbani. Anapofanya hivyo, watu 22,000 kati ya wale walio pamoja naye wanarudi nyumbani, na anabaki na watu 10,000 tu.—Kumbukumbu la Torati 20:8; Waamuzi 7:2, 3.

Mungu anasema kwamba bado watu hao ni wengi mno. Gideoni anaambiwa awapeleke kwenye maji. Mwanahistoria Myahudi anayeitwa Yosefo anasema kwamba Gideoni alipeleka jeshi lake kwenye mto wakati wa joto kali la mchana. Vyovyote vile, Gideoni anatazama jinsi wanavyokunywa maji. Watu 300 tu kati yao ndio wanaoteka maji kwa mikono yao na kuyaramba huku wakiwa macho kukabili shambulizi. Watu hao 300 tu walio macho ndio watakaoandamana na Gideoni. (Waamuzi 7:4-8) Jiweke katika hali yao. Kwa kuwa mnakabili maadui 135,000, bila shaka ungekata kauli kwamba mnaweza kushinda kwa nguvu za Yehova tu wala si kwa nguvu zenu!

Mungu anamwambia Gideoni aende na mtumishi fulani wakapeleleze kambi ya Wamidiani. Wakiwa katika kambi hiyo, Gideoni anamsikia mtu fulani akimsimulia mwenzake kuhusu ndoto yake. Mwenzake anafasiri ndoto hiyo bila kukawia na kusema inamaanisha kwamba Mungu ameazimia kuwatia Wamidiani mkononi mwa Gideoni. Hilo hasa ndilo jambo ambalo Gideoni anatamani sana kusikia. Ana hakika kwamba Yehova atamwezesha yeye pamoja wale watu 300 walio pamoja naye kuwashinda Wamidiani.—Waamuzi 7:9-15.

Mbinu za Pigano

Wale watu 300 wanagawanywa katika vikosi vitatu. Kila kikosi kina watu 100. Kila mmoja anapewa baragumu na mtungi mkubwa mtupu. Ndani ya kila mtungi kuna mwenge. Hili ndilo agizo la kwanza ambalo Gideoni anatoa: ‘Nitazameni, na iwe kwamba vile nitakavyofanya, fanyeni vivyo hivyo. Nitakapokuwa nimekwisha kupiga baragumu, ninyi pia zipigeni baragumu, nanyi mpaaze sauti, “Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”’—Waamuzi 7:16-18, 20.

Askari hao 300 Waisraeli wanasonga polepole hadi kwenye ukingo wa kambi ya maadui. Ni saa nne hivi za usiku, baada tu ya walinzi kubadilishana zamu. Huu waonekana kuwa wakati bora wa kushambulia, kwani itachukua muda fulani kwa walinzi ambao wametoka tu kuanza zamu yao kuona vizuri gizani.

Wazia hofu inayowakumba Wamidiani! Kwa ghafula, kimya cha usiku kinakatizwa na kishindo cha kuvunjwa kwa ile mitungi 300, kupigwa kwa zile baragumu 300, na makelele ya wale watu 300. Wamidiani wanashtuliwa hasa wanaposikia maneno haya, “Upanga wa Mungu na wa Gideoni!,” nao wanapaaza kilio. Katika hali hiyo, hawawezi kuwatambua maadui wao. Wale watu 300 wanaendelea kusimama mahali pao Yehova anapowafanya maadui wao wauane. Wamidiani wanashindwa kabisa, hawawezi kutoroka, nao maadui waliosalia wanafuatiliwa na kuuawa. Hivyo, Wamidiani hawawezi kamwe kuwakandamiza Waisraeli tena. Hatimaye, uvamizi wa muda mrefu wa Wamidiani waliomiliki nchi ya Waisraeli unakomeshwa.—Waamuzi 7:19-25; 8:10-12, 28.

Gideoni anaendelea kuwa mnyenyekevu, licha ya ushindi huo. Waefraimu wanaohisi kwamba wamepuuzwa kwa kutohusishwa katika mapigano hayo, wanapotafuta kwa ukali kugombana naye anawajibu kwa upole. Jibu lake la upole linageuza ghadhabu yao na kuwatuliza.—Waamuzi 8:1-3; Methali 15:1.

Sasa kuna amani na Waisraeli wanamsihi Gideoni awe mfalme wao. Hilo ni jaribu kubwa wee! Lakini Gideoni anakataa kuwatawala. Anatambua ni nani aliyewashinda Wamidiani. Gideoni anawaambia: “Mimi mwenyewe sitatawala juu yenu, wala mwanangu hatatawala juu yenu. Yehova ndiye atakayetawala juu yenu.”—Waamuzi 8:23.

Hata hivyo, kwa kuwa Gideoni si mkamilifu, nyakati nyingine anakosa busara. Kwa sababu fulani anatumia baadhi ya vitu walivyoteka nyara vitani ili kutengeneza efodi, kisha anaiweka katika jiji lake ili ionekane. Kulingana na masimulizi, Waisraeli wote wanaanza kufanya “uasherati” nayo. Wanaiabudu, nayo inakuwa mtego kwa Gideoni na kwa nyumba yake. Hata hivyo, Gideoni hawi mwabudu-sanamu, kwani Maandiko yanasema kwamba yeye ni mtu anayemwamini Yehova.—Waamuzi 8:27; Waebrania 11:32-34.

Mambo Tunayojifunza

Masimulizi yanayomhusu Gideoni yanatuonya na kututia moyo. Tunaonywa kwamba ikiwa Yehova ataiondoa roho yake juu yetu na kuacha kutubariki kwa sababu tuna mwenendo mpotovu, hali yetu ya kiroho itakuwa kama ya wakaaji maskini wa nchi iliyoharibiwa na nzige. Tunaishi katika nyakati za hatari, hivyo tusisahau kamwe kwamba baraka ya Yehova “ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.” (Methali 10:22) Tunabarikiwa na Mungu kwa kuwa ‘tunamtumikia kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe.’ Tukikosa kufanya hivyo, atatutupa mbali.—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

Tunatiwa moyo na masimulizi yanayomhusu Gideoni kwa kuwa yanaonyesha kwamba Yehova anaweza kuwaokoa watu wake kutoka katika hali yoyote ile inayoumiza, naye hutumia hata watu wanaoonwa kuwa dhaifu au wasio na uwezo ili kuwaokoa. Ushindi wa Gideoni na watu wake 300 dhidi ya Wamidiani 135,000, unathibitisha kwamba Mungu ana nguvu zisizo na mipaka. Huenda tukapatwa na hali ngumu na kuhisi kwamba hatuna uwezo dhidi ya maadui wengi wanaotukabili. Hata hivyo, masimulizi ya Biblia yanayomhusu Gideoni yanatuchochea kumtegemea Yehova, kwani atawabariki na kuwaokoa watu wote wanaomwamini.