Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inaweza Kukusaidia Upate Shangwe

Biblia Inaweza Kukusaidia Upate Shangwe

Biblia Inaweza Kukusaidia Upate Shangwe

IJAPOKUWA Biblia si kitabu cha kitiba, inazungumzia matokeo ambayo hisia zinazofaa na zisizofaa zinaweza kuwa nayo kwa akili na afya ya mtu. Inasema: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.” Pia tunasoma hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 17:22; 24:10) Kuvunjika moyo kunaweza kutudhoofisha, kutufanya tuhisi kuwa wanyonge na kwamba tuko hatarini na kutotaka kubadilika wala kutafuta msaada.

Kuvunjika moyo kunaweza kumwathiri mtu kiroho pia. Watu wanaohisi kuwa hawafai mara nyingi huhisi kwamba hawawezi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu wala kukubaliwa naye. Simone, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, hakuamini kwamba alikuwa “mtu ambaye angeweza kukubaliwa na Mungu.” Hata hivyo, tunaposoma Neno la Mungu, Biblia, tunaona kwamba Mungu huwakubali wale wanaojitahidi kumpendeza.

Mungu Anajali

Biblia hutuambia kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” Mungu haudharau “moyo uliovunjika na kupondwa,” lakini yeye anaahidi “kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.”—Zaburi 34:18; 51:17; Isaya 57:15.

Pindi moja Yesu, Mwana wa Mungu, alilazimika kuwaeleza wanafunzi wake kwamba Mungu huona wema wa watumishi Wake. Kwa kutumia mfano, aliwaeleza kwamba Mungu hujua shomoro anapoanguka chini—jambo ambalo watu wengi wangeona halina maana. Pia alieleza kwamba Mungu hutambua mambo madogo sana kuhusu wanadamu, hata hesabu ya nywele kwenye vichwa vyao. Yesu alimalizia mfano wake kwa kusema: “Kwa hiyo msiogope: ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.” (Mathayo 10:29-31) * Yesu alionyesha kwamba Mungu anawathamini wanadamu wenye imani hata ingawa wanaweza kuhisi hawafai. Hata mtume Petro anatukumbusha kwamba “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Dumisha Maoni Yaliyosawazika

Neno la Mungu linatusihi tudumishe maoni yaliyosawazika kuhusu jinsi tunavyojiona. Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika: “Kupitia fadhili zisizostahiliwa nilizopewa namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali kufikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama Mungu alivyomgawia kipimo cha imani.”—Waroma 12:3.

Bila shaka hatungependa kujifikiria sana hivi kwamba tuwe na kiburi; wala hatungependa kuhisi kuwa hatufai na kutojifikiria hata kidogo. Badala yake, lengo letu linapaswa kuwa kudumisha maoni yanayofaa kujielekea, tukikumbuka kupungukiwa kwetu na uwezo wetu. Mwanamke mmoja Mkristo alisema hivi: “Mimi si mbaya; wala mimi si bora kuliko wengine. Nina sifa nzuri na sifa mbaya, na hivyo ndivyo kila mtu alivyo.”

Bila shaka, kuwa na maoni kama hayo yenye usawaziko si rahisi. Huenda ikachukua jitihada nyingi sana kuepuka maoni yasiyofaa ambayo labda tumekuwa nayo kwa miaka mingi. Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu, tunaweza kubadili utu wetu na maoni yetu kuhusu maisha. Kwa kweli, hivyo ndivyo Neno la Mungu linavyotuhimiza tufanye. Tunasoma hivi: ‘Ondoleeni mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza na ambao unaharibiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’—Waefeso 4:22-24.

Kwa kujitahidi kubadili ‘nguvu zinazoendesha akili zetu,’ yaani, mwelekeo mkuu wa akili zetu, tunaweza kubadili utu wetu na badala ya kuwa na maoni yasiyofaa tunaweza kuwa na maoni yanayofaa. Lena, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alitambua kwamba ilibidi aondolee mbali maoni ya kwamba hakuna mtu anayeweza kumpenda au kumsaidia, ili abadili jinsi anavyojiona. Ni kanuni gani ya Biblia iliyomsaidia Lena, Simone, na wengine kufanya mabadiliko kama hayo?

Kanuni za Biblia Zinazotusaidia Kuwa na Shangwe

“Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Kwanza kabisa, sala inaweza kutusaidia kupata shangwe ya kweli. Simone anasema: “Ninapovunjika moyo, mimi humwomba Yehova msaada. Yeye amenitia nguvu na kuniongoza katika hali zote.” Mtunga-zaburi anapotusihi tumtupie Yehova mzigo wetu, kwa hakika anatukumbusha kwamba Yehova anatujali na pia anatuona kuwa watu wanaostahili kusaidiwa na kutegemezwa naye. Katika usiku wa Pasaka ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu walihuzunika kwa sababu Yesu aliwaambia kwamba alikuwa karibu kuondoka. Yesu aliwatia moyo wasali kwa Baba, kisha akaongeza: “Ombeni nanyi mtapokea, ili shangwe yenu ipate kujazwa.”—Yohana 16:23, 24.

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Kama Yesu alivyofundisha, ni muhimu kutoa ili kupata furaha ya kweli maishani. Tukifuata ukweli huo wa Biblia, tutaweza kufikiria mahitaji ya wengine badala ya kufikiria jinsi ambavyo tumepungukiwa. Tunapata uradhi tunapowasaidia wengine na kuona jinsi wanavyothamini. Lena anaamini kwamba kuwaambia jirani zake habari njema kutoka katika Biblia kwa ukawaida kunamsaidia katika njia mbili. Anasema: “Kwanza, jambo hilo huniletea furaha na uradhi ambao Yesu alitaja. Pili, wengine hunitia moyo sana, na jambo hilo hunisaidia kupata shangwe.” Tukijitolea kuwasaidia wengine, tutaona ukweli wa maneno haya ya Methali 11:25: “Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”

“Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” (Methali 15:15) Kila mmoja wetu ana uhuru wa kuchagua kuwa na maoni yasiyofaa au yanayofaa kujihusu na kuhusu hali zake. Tunaweza kuwa na maoni yasiyofaa kuhusu kila kitu na kuhisi tunateseka au tunaweza kuchagua kuwa na maoni yanayofaa, kuwa ‘wachangamfu moyoni,’ na kuwa wenye shangwe kana kwamba tuko kwenye karamu. Simone anasema: “Ninajitahidi iwezekanavyo kuwa na maoni yanayofaa. Mimi hujifunza na kuhubiri kwa bidii, na kudumu katika sala. Pia mimi hujitahidi kushirikiana na watu walio na maoni mazuri, nami hujitahidi kuwasaidia wengine.” Mtazamo huo wa moyoni hutokeza shangwe ya kweli kama vile Biblia inavyotuhimiza: “Shangilieni katika Yehova na kuwa na shangwe, enyi waadilifu; na mpige vigelegele vya shangwe, ninyi nyote mlio wanyoofu katika moyo.”—Zaburi 32:11.

“Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Kuzungumza na mtu tunayempenda au mshauri tunayemtumaini kunaweza kutusaidia kukabiliana na maoni yasiyofaa na kuyashinda kabla hayajatulemea. Tunapozungumza na wengine wao hutusaidia kuona mambo kwa njia inayofaa na yenye usawaziko. “Kueleza hisia zangu hunisaidia sana,” asema Simone. “Unahitaji kumweleza mtu mwingine jinsi unavyohisi. Mara nyingi unahitaji tu kueleza yaliyo moyoni mwako.” Kwa kufanya hivyo, utaona ukweli wa methali hii ambayo inasema: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie.”—Methali 12:25.

Unachoweza Kufanya

Tumezungumzia tu baadhi ya kanuni nzuri za Biblia zinazoweza kutusaidia kushinda hisia zisizofaa na kupata shangwe ya kweli. Ikiwa unapambana na hisia zisizofaa, tunakutia moyo uchunguze Neno la Mungu, Biblia, kwa makini zaidi. Jifunze kuwa na maoni yenye usawaziko kujihusu na kuhusu uhusiano wako pamoja na Mungu. Tunatumaini kwamba kwa kuongozwa na Neno la Mungu, utaweza kupata shangwe ya kweli katika yote unayofanya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Sehemu hiyo ya Andiko imezungumziwa kwa undani kwenye ukurasa wa 22 na 23.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kufuata kanuni za Biblia huongeza shangwe