Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Wafalme

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Wafalme

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Wafalme

KITABU cha Pili cha Wafalme kinaendeleza masimulizi ya Kitabu cha Kwanza cha Wafalme. Kinazungumzia wafalme 29, yaani, wafalme 12 wa ufalme wa kaskazini wa Israeli na wafalme 17 wa ufalme wa kusini wa Yuda. Kitabu cha Pili cha Wafalme kinasimulia pia utendaji wa nabii Eliya, Elisha, na Isaya. Ingawa masimulizi hayafuatani kulingana na jinsi yalivyotukia, kitabu hicho kinahusisha mambo yaliyotukia wakati wa uharibifu wa Samaria na Yerusalemu. Kwa ujumla, Kitabu cha Pili cha Wafalme kinazungumzia kipindi cha miaka 340, kuanzia mwaka wa 920 K.W.K. hadi 580 K.W.K. wakati nabii Yeremia alipomaliza kukiandika.

Tunaweza kufaidikaje kutokana na Kitabu cha Pili cha Wafalme? Kinatufundisha nini kumhusu Yehova na jinsi alivyoshughulika na watu wake? Tunaweza kujifunza nini kutokana na matendo ya wafalme, manabii, na watu wengine wanaotajwa katika kitabu hicho? Hebu tuone mambo tunayoweza kujifunza katika Kitabu cha Pili cha Wafalme.

ELISHA ACHUKUA MAHALI PA ELIYA

(2 Wafalme 1:1–8:29)

Mfalme Ahazia wa Israeli anaanguka nyumbani mwake na kuwa mgonjwa. Nabii Eliya anamwambia kwamba atakufa. Ahazia anakufa, na Yehoramu ndugu yake, anaanza kutawala. Wakati huohuo, Yehoshafati anatawala Yuda. Eliya anachukuliwa juu katika dhoruba ya upepo, na msaidizi wake, Elisha, anakuwa nabii baada yake. Elisha anafanya miujiza mingi katika miaka 60 hivi inayofuata ya huduma yake.—Ona sanduku “Miujiza ya Elisha.”

Mfalme fulani Mmoabu anapoasi Israeli, Yehoramu, Yehoshafati, na mfalme wa Edomu wanaenda kumkabili vitani. Wanapewa ushindi kwa sababu ya uaminifu wa Yehoshafati. Baadaye, mfalme wa Siria anapanga kushambulia Israeli kwa ghafula. Hata hivyo, Elisha anaharibu mpango huo. Mfalme wa Siria anakasirika sana na anapeleka “farasi na magari ya vita na jeshi kubwa” ili kumkamata Elisha. (2 Wafalme 6:14) Elisha anafanya miujiza miwili na kuwafanya Wasiria warudi kwa amani. Baada ya muda, Ben-hadadi, mfalme wa Siria, anazingira Samaria. Jambo hilo linasababisha njaa kali, lakini Elisha anatabiri kwamba itakwisha.

Muda fulani baadaye, Elisha anaenda Damasko. Mfalme Ben-hadadi, ambaye sasa ni mgonjwa, anamtuma Hazaeli kuuliza ikiwa atapona. Elisha anatabiri kwamba mfalme huyo atakufa na kwamba Hazaeli atatawala badala yake. Kesho yake, Hazaeli anamuua mfalme huyo kwa kumfunika usoni kwa “tandiko lenye mapambo” lenye umajimaji kisha anaanza kutawala. (2 Wafalme 8:15) Huko Yuda, Yehoramu mwana wa Yehoshafati anakuwa mfalme, halafu mwana wake, Ahazia, anatawala baada yake.—Ona sanduku “Wafalme wa Yuda na wa Israeli.”

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:9—Kwa nini Elisha aliomba ‘sehemu mbili za roho ya Eliya’? Ili atimize jukumu lake akiwa nabii wa Israeli, Elisha alihitaji kuwa na roho ileile kama ya Eliya, yaani, roho ya ujasiri na ya kutoogopa chochote. Kwa kutambua jambo hilo, Elisha aliomba sehemu mbili za roho ya Eliya. Elisha alikuwa amewekwa rasmi na Eliya ili awe nabii baada yake na alikuwa mtumishi wake kwa miaka sita, kwa hiyo alimwona Eliya kuwa baba yake wa kiroho. Elisha alikuwa kama mwana mzaliwa wa kwanza wa kiroho wa Eliya. (1 Wafalme 19:19-21; 2 Wafalme 2:12) Hivyo, kama vile mzaliwa wa kwanza alivyopata sehemu mbili za urithi wa baba yake, Elisha aliomba na kupata sehemu mbili za urithi wa kiroho kutoka kwa Eliya.

2:11—‘Eliya alipopanda katika ile dhoruba ya upepo’ alielekea ‘mbingu’ zipi? Mbingu hizo si sehemu za mbali za ulimwengu unaoonekana wala si makao ya kiroho ya Mungu pamoja na wana wake ambao ni malaika. (Kumbukumbu la Torati 4:19; Zaburi 11:4; Mathayo 6:9; 18:10) ‘Mbingu’ ambazo Eliya alipanda kuzielekea ni angahewa. (Zaburi 78:26; Mathayo 6:26) Inaonekana kwamba gari la vita lenye moto lilisonga kasi katika angahewa la dunia na kumhamisha Eliya kwenye sehemu nyingine ya dunia, ambako aliendelea kuishi kwa kipindi fulani. Kwa hakika, baada ya miaka kupita, Eliya alimwandikia barua Yehoramu mfalme wa Yuda.—2 Mambo ya Nyakati 21:1, 12-15.

5:15, 16—Kwa nini Elisha hakukubali zawadi ya Naamani? Elisha alikataa zawadi hiyo kwa sababu alitambua kwamba muujiza wa kumponya Naamani ulifanywa kwa nguvu za Yehova, bali si kwa nguvu zake. Hangefikiria kamwe kupata faida kutokana na kazi aliyopewa na Mungu. Leo, waabudu wa kweli hawataki kujifaidi kupitia utumishi wao kwa Yehova. Wao hutii shauri hili la Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8.

5:18, 19—Je, Naamani alikuwa akiomba msamaha kwa sababu alilazimika kushiriki tendo la kidini? Inaonekana mfalme wa Siria alikuwa mzee na dhaifu na ilimbidi ajitegemeze kwa kumwegemea Naamani. Mfalme huyo alipoinama ili kumwabudu Rimoni, Naamani aliinama pia. Hata hivyo, Naamani aliinama ili kumtegemeza mfalme bali si kumwabudu. Naamani alikuwa akimwomba Yehova amsamehe kwa kufanya kazi hiyo ya kiserikali. Elisha aliamini maneno ya Naamani na kumwambia: “Nenda kwa amani.”

Mambo Tunayojifunza:

1:13, 14. Kujifunza kwa kutazama na kuwa wanyenyekevu kunaweza kuokoa uhai.

2:2, 4, 6Hata ingawa huenda Elisha alikuwa mtumishi wa Eliya kwa miaka sita, Elisha alisisitiza kwamba hatamwacha Eliya. Huo ni mfano bora wa ushikamanifu na urafiki!—Methali 18:24.

2:23, 24. Inaonekana Elisha alidhihakiwa hasa kwa sababu mtu mwenye kipara alikuwa amevaa vazi rasmi la Eliya. Watoto hao walimtambua Elisha kuwa mwakilishi wa Yehova na hawakumtaka hapo. Walimwambia ‘aende juu,’ yaani, aendelee kwenda juu hadi Betheli au apandishwe juu kama Eliya. Inaonekana kwamba watoto hao walionyesha mtazamo wa upinzani wa wazazi wao. Bila shaka, ni muhimu wazazi wawafundishe watoto wao kuwaheshimu wawakilishi wa Mungu!

3:14, 18, 24. Sikuzote neno la Yehova hutimia.

3:22. Mwangaza wa asubuhi ulifanya maji yaonekane kama damu, labda kwa sababu mitaro iliyotoka tu kuchimbwa ilikuwa na udongo mwekundu wa mfinyanzi. Yehova anaweza kuamua kutumia nguvu za asili kutimiza makusudi yake.

4:8-11. Mwanamke mmoja huko Shunemu alimwonyesha Elisha ukarimu kwa sababu alitambua kwamba alikuwa “mtu mtakatifu wa Mungu.” Je, hatupaswi kuwatendea vivyo hivyo waabudu waaminifu wa Yehova?

5:3. Msichana mdogo Mwisraeli alikuwa na imani katika uwezo wa Mungu wa kufanya miujiza. Pia alikuwa na ujasiri wa kuzungumza kuhusu imani yake. Je, ninyi vijana mnajitahidi kuimarisha imani yenu katika ahadi za Mungu na kuwa na ujasiri wa kuwaeleza walimu wenu na wanafunzi wenzenu kuhusu ile kweli?

5:9-19. Mfano wa Naamani unaonyesha kwamba mtu mwenye kiburi anaweza kujifunza kuwa mnyenyekevu.—1 Petro 5:5.

5:20-27. Udanganyifu ulileta matokeo mabaya sana! Kufikiria maumivu ya kihisia na msiba unaotokana na kufanya mabaya huku tukijifanya kuwa tunamtumikia Mungu kutatusaidia kuepuka kufuata njia hiyo.

ISRAELI NA YUDA WAPELEKWA UHAMISHONI

(2 Wafalme 9:1–25:30)

Yehu atiwa mafuta kuwa mfalme wa Israeli. Anachukua hatua mara moja na kuipiga nyumba ya Ahabu. Kwa ustadi, Yehu ‘anaangamiza ibada ya Baali kutoka katika Israeli.’ (2 Wafalme 10:28) Athalia, mama ya Ahazia, anaposikia kwamba mwana wake ameuawa na Yehu, ‘anasimama na kuuangamiza uzao wote wa ufalme wa Yuda’ kisha ananyakua ufalme. (2 Wafalme 11:1) Yehoashi, mtoto mchanga wa Ahazia, ndiye tu anayeokolewa, na baada ya kufichwa kwa miaka sita anawekwa rasmi kuwa mfalme wa Yuda. Kuhani Yehoyada anamfundisha Yehoashi, naye Yehoashi anaendelea kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova.

Wafalme wote wanaotawala Israeli baada ya Yehu wanafanya mabaya machoni pa Yehova. Elisha anakufa kifo cha kawaida wakati wa utawala wa mjukuu wa Yehu. Mfalme wa nne wa Yuda baada ya Yehoashi ni Ahazi, naye ‘hafanyi yaliyo sawa machoni pa Yehova.’ (2 Wafalme 16:1, 2) Lakini mwana wake, Hezekia, anakuwa mfalme ‘anayeendelea kushikamana na Yehova.’ (2 Wafalme 17:20; 18:6) Katika mwaka wa 740 K.W.K., wakati Hezekia anapotawala Yuda na Hoshea anatawala Israeli, Mfalme Shalmanesa wa Ashuru ‘analiteka Samaria kisha anapeleka Israeli uhamishoni katika Ashuru.’ (2 Wafalme 17:6) Baadaye, wageni wanapelekwa katika eneo la Israeli, na dini ya Wasamaria inaanzishwa.

Kati ya wafalme saba wanaotawala Yuda baada ya Hezekia, ni Yosia tu anayechukua hatua ya kuondoa ibada ya uwongo kutoka katika nchi hiyo. Hatimaye, katika mwaka wa 607 K.W.K., Wababiloni wanateka Yerusalemu, na ‘Yuda wanaenda uhamishoni kutoka katika nchi yao.’—2 Wafalme 25:21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

13:20, 21—Je, muujiza huu unaunga mkono kuabudu mabaki ya vitu vya kale vya kidini? La. Biblia haionyeshi kwamba mifupa ya Elisha iliabudiwa. Nguvu za Mungu ndizo zilizotokeza muujiza huo, sawa na ilivyokuwa katika miujiza yote ambayo Elisha alifanya alipokuwa hai.

15:1-6—Kwa nini Yehova alimpiga Azaria (Uzia) kwa ukoma? “Mara tu [Uzia] alipopata nguvu, moyo wake ukawa na majivuno . . . , hivi kwamba akatenda kwa ukosefu wa uaminifu kwa Yehova Mungu wake, akaingia katika hekalu la Yehova ili kufukiza uvumba juu ya madhabahu ya uvumba.” Makuhani ‘waliposimama kumpinga Uzia’ na kumwambia ‘aondoke ndani ya patakatifu,’ Uzia akawa na ghadhabu juu ya makuhani, akapigwa kwa ukoma.—2 Mambo ya Nyakati 26:16-20.

18:19-21, 25—Je, Hezekia alikuwa amefanya mapatano na Misri? La. Rabshake alitoa shtaka la uwongo, na pia alidanganya alipodai kwamba amekuja kwa “kupewa mamlaka kutoka kwa Yehova.” Mfalme Hezekia mwaminifu alimtegemea Yehova peke yake.

Mambo Tunayojifunza:

9:7, 26. Hukumu kali juu ya nyumba ya Ahabu inaonyesha kwamba Yehova huchukia ibada ya uwongo na kumwaga damu isiyo na hatia.

9:20. Sifa ya Yehu ya kuendesha gari kwa kasi sana ilionyesha bidii yake ya kutimiza utume wake. Je, unajulikana kuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii?—2 Timotheo 4:2.

9:36, 37; 10:17; 13:18, 19, 25; 14:25; 19:20, 32-36; 20:16, 17; 24:13. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba ‘neno linalotoka katika kinywa cha Yehova hakika hufanikiwa sikuzote.’—Isaya 55:10, 11.

10:15. Kama vile Yehonadabu alivyokubali kwa moyo wote mwaliko wa Yehu wa kupanda gari pamoja naye, “umati mkubwa” humuunga mkono kwa utayari Yesu Kristo, Yehu wa leo, pamoja na wafuasi wake watiwa-mafuta.—Ufunuo 7:9.

10:30, 31. Ingawa Yehu alifanya makosa, Yehova alithamini mambo yote aliyofanya. Naam, ‘Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yetu.’—Waebrania 6:10.

13:14-19. Kwa kuwa Yehoashi, mjukuu wa Yehu, hakuwa na bidii bali alipiga chini kwa mishale mara tatu tu, alifanikiwa kidogo tu kuwashinda Wasiria. Yehova anatarajia tufanye kazi aliyotupa kwa moyo wote na kwa bidii.

20:2-6. Yehova ndiye “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.

24:3, 4Kwa sababu ya hatia ya damu ya Manase, Yehova “hakukubali kutoa msamaha” kwa Yuda. Mungu huheshimu damu ya watu wasio na hatia. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atalipiza kisasi damu ya watu wasio na hatia kwa kuwaharibu wale wanaoimwaga.—Zaburi 37:9-11; 145:20.

Kinatufaidi

Kitabu cha Pili cha Wafalme kinaonyesha kwamba Yehova ni Mtimizaji wa ahadi. Kupelekwa uhamishoni kwa falme mbili, kwanza ufalme wa Israeli kisha wa Yuda, kunatuonyesha waziwazi utimizo wa hukumu ya kinabii kwenye Kumbukumbu la Torati 28:15–29:28. Kitabu cha Pili cha Wafalme kinaonyesha kwamba Elisha alikuwa nabii mwenye bidii nyingi kwa ajili ya jina la Yehova na ibada ya kweli. Hezekia na Yosia wanasimuliwa kuwa wafalme wanyenyekevu wanaoheshimu Sheria ya Mungu.

Tunapotafakari kuhusu mtazamo na matendo ya wafalme, manabii, na watu wengine wanaotajwa katika Kitabu cha Pili cha Wafalme, je, hatujifunzi mambo muhimu tunayoweza kufanya na vilevile kuepuka? (Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:11) Naam, “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

MIUJIZA YA ELISHA

1. Maji ya Yordani yanagawanywa.—2 Wafalme 2:14

2. Maji mabaya ya Yeriko yanafanywa kuwa yenye afya.—2 Wafalme 2:19-22

3. Watoto wakorofi wanashambuliwa na dubu. —2 Wafalme 2:23, 24

4. Majeshi yanaandaliwa maji.—2 Wafalme 3:16-26

5. Mjane anapewa mafuta ya kutumiwa kwa chakula. —2 Wafalme 4:1-7

6. Mwanamke Mshunamu aliyekuwa tasa anapata mtoto.—2 Wafalme 4:8-17

7. Mtoto anafufuliwa. —2 Wafalme 4:18-37

8. Mchuzi wenye sumu unafanywa uweze kulika. —2 Wafalme 4:38-41

9. Watu 100 wanalishwa mikate 20.—2 Wafalme 4:42-44

10. Naamani anaponywa ukoma wake.—2 Wafalme 5:1-14

11. Gehazi apata ukoma wa Naamani.—2 Wafalme 5:24-27

12. Kichwa cha shoka kinafanywa kielee.—2 Wafalme 6:5-7

13. Mtumishi aona magari ya vita ya malaika. —2 Wafalme 6:15-17

14. Jeshi la Siria lapofushwa.—2 Wafalme 6:18

15. Jeshi la Siria larudishiwa uwezo wa kuona. —2 Wafalme 6:19-23

16. Mfu anafufuka. —2 Wafalme 13:20, 21

[Chati/Picha katika ukurasa wa 12]

WAFALME WA YUDA NA WA ISRAELI

Sauli/Daudi/Sulemani: 1117/1077/1037 K.W.K. *

UFALME WA YUDA TAREHE (K.W.K.) UFALME WA ISRAELI

Rehoboamu ․․․․․․ 997 ․․․․․․ Yeroboamu

Abiya/Asa ․․․․ 980/978 ․․․․

․․ 976/975/952 ․․ Nadabu/Baasha/Ela

․․ 951/951/951 ․․ Zimri/Omri/Tibni

․․․․․․ 940 ․․․․․․ Ahabu

Yehoshafati ․․․․․․ 937 ․․․․․․

․․․․ 920/917 ․․․․ Ahazia/Yehoramu

Yehoramu ․․․․․․ 913 ․․․․․․

Ahazia ․․․․․․ 906 ․․․․․․

(Athalia) ․․․․․․ 905 ․․․․․․ Yehu

Yehoashi ․․․․․․ 898 ․․․․․․

․․․․ 876/859 ․․․․ Yehoahazi/Yehoashi

Amazia ․․․․․․ 858 ․․․․․․

․․․․․․ 844 ․․․․․․ Yeroboam wa Pili

Azaria (Uzia) ․․․․․․ 829 ․․․․․․

․․ 803/791/791 ․․ Zekaria/Shalumu/Menahemu

․․․․ 780/778 ․․․․ Pekaya/Peka

Yothamu/Ahazi ․․․․ 777/762 ․․․․

․․․․․․ 758 ․․․․․․ Hoshea

Hezekia ․․․․․․ 746 ․․․․․․

․․․․․․ 740 ․․․․․․ Samaria linatekwa

Manase/Amoni/Yosia ․․ 716/661/659 ․․

Yehoahazi/Yehoyakimu ․․․․ 628/628 ․․․․

Yehoyakini/Sedekia ․․․․ 618/617 ․․․․

Yerusalemu linaharibiwa ․․․․․․ 607 ․․․․․․

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 66 Tarehe fulani ni makadirio ya mwaka wa kwanza wa utawala.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Naamani alijinyenyekeza na kuponywa kwa nguvu za Yehova

[Picha katika ukurasa wa 9]

Eliya alipatwa na nini ‘alipopanda katika ile dhoruba ya upepo’?