Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, neno “huenda” kwenye Sefania 2:3 linamaanisha kwamba watumishi wa Mungu hawawezi kuwa na uhakika kwamba watapata uzima wa milele?

Andiko hilo linasema hivi: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia, ambao mmetenda uamuzi Wake wa hukumu. Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.” Kwa nini mstari huo unasema “huenda”?

Ili kuelewa jinsi Yehova atakavyoshughulika na waaminifu wake wakati wa Har–Magedoni, inafaa kukumbuka yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu jinsi Mungu atakavyowafanyia wale wanaokufa kabla ya wakati huo wa hukumu. Wengine watafufuliwa na kupata uhai usioweza kufa wakiwa viumbe wa roho mbinguni, na wengine watafufuliwa duniani wakitazamia kuishi milele katika Paradiso. (Yohana 5:28, 29; 1 Wakorintho 15:53, 54) Ikiwa Yehova anawakumbuka na kuwapa thawabu waaminifu wake wanaokufa kabla ya Har–Magedoni, bila shaka atawafanyia vivyo hivyo watumishi wake watakaokuwa hai katika siku ya hasira yake.

Maneno ya mtume Petro yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatia moyo pia. Aliandika hivi: “[Mungu] alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu; na kwa kuyageuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu aliyahukumia adhabu, . . . naye alimkomboa Loti mwadilifu . . . Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.” (2 Petro 2:5-9) Ingawa Yehova aliwaharibu waovu nyakati za zamani, aliwakomboa Noa na Loti waliomtumikia kwa uaminifu. Yehova pia atawakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu atakapoharibu waovu wakati wa Har–Magedoni. “Umati mkubwa” wa watu waadilifu utaokoka.—Ufunuo 7:9, 14.

Basi, inaonekana kwamba kwenye Sefania 2:3, neno “huenda” halitumiwi kwa sababu ya kukosa uhakika kuhusu uwezo wa Mungu wa kuwakomboa watu wanaopata kibali chake. Badala yake, mtu anapoanza kutafuta uadilifu na upole, huwa kuna uwezekano tu wa kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova. Mtu huyo atakombolewa ikiwa ataendelea kutafuta upole na uadilifu.—Sefania 2:3.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu”