Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Wakati Gani Unapokuwa na Haki ya Kuudhika?

Ni Wakati Gani Unapokuwa na Haki ya Kuudhika?

Ni Wakati Gani Unapokuwa na Haki ya Kuudhika?

BIBLIA inasema hivi kwenye Mhubiri 7:9: “Kuudhika hukaa katika kifua cha wajinga.” Mstari huo unaonyesha kwamba tunapoudhiwa hatupaswi kuchukua mambo kwa uzito sana; badala yake tunapaswa kuwa tayari kusamehe.

Hata hivyo, je, andiko la Mhubiri 7:9 linamaanisha kuwa hatupaswi kamwe kuudhiwa na chochote au yeyote, kwamba tunapaswa kusamehe wote wanaotukosea licha ya uzito wa kosa au kurudiwa-rudiwa kwa kosa na kwamba hatupaswi kuchukua hatua yoyote? Je, tunapaswa kuwaudhi wengine kwa maneno au kwa matendo eti kwa sababu tunajua kwamba wanaokosewa wanapaswa kuwa tayari kusamehe? Hapana.

Yehova Mungu ndiye mfano bora wa upendo, rehema, kusamehe, na uvumilivu. Hata hivyo, mara nyingi Biblia inazungumzia pindi ambazo watu fulani walimkosea. Kosa lilipokuwa zito, alichukua hatua dhidi ya wakosaji. Ona mifano kadhaa.

Kumkosea Yehova

Simulizi la 1 Wafalme 15:30 linazungumzia dhambi za Yeroboamu “ambazo kupitia hizo alisababisha Israeli kutenda dhambi na kwa kutia uchungu kwake alikomtia uchungu Yehova.” Kwenye 2 Mambo ya Nyakati 28:25, Biblia inasema hivi kuhusu Mfalme Ahazi wa Yuda: “Akajenga mahali pa juu kwa ajili ya kuifukizia miungu mingine moshi wa uvumba, hivi kwamba akamtia uchungu Yehova Mungu wa mababu zake.” Mfano mwingine kwenye Waamuzi 2:11-14 unasema: “Israeli wakaanza kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova, wakatumikia Mabaali . . . , hata wakamtia uchungu Yehova. . . . Ndipo hasira ya Yehova ikawaka juu ya Israeli, akawatia mikononi mwa waporaji.”

Kuna mambo mengine yaliyomtia Yehova uchungu na yakahitaji achukue hatua kali. Kwa mfano, kwenye Kutoka 22:18-20, tunasoma: “Usimhifadhi hai mwanamke mlozi. Mtu yeyote anayelala na mnyama lazima atauawa. Mtu anayetoa dhabihu kwa miungu yoyote isipokuwa kwa Yehova peke yake ataangamizwa.”

Yehova hakuendelea kuwasamehe Waisraeli wa kale walipotenda dhambi nzito na kumtia uchungu bila kutubu kikweli. Mungu aliagiza wakosaji wauawe ikiwa walikataa kutubu au kuchukua hatua yoyote kuonyesha kwamba wamegeuka na kumtii Yehova. Ilikuwa hivyo kwa taifa zima mwaka wa 607 K.W.K., mikononi mwa Wababiloni, na tena mwaka wa 70 W.K., mikononi mwa Waroma.

Naam, Yehova huudhika watu wanaposema na kutenda mambo mabaya, na hata huwaangamiza wakosaji wanaofanya dhambi nzito bila kutubu. Je, hiyo inamaanisha kwamba kulingana na Mhubiri 7:9 hapaswi kuudhika? Hata kidogo. Ana haki ya kuudhika watu wanapofanya dhambi nzito na sikuzote yeye huhukumu kwa haki. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Makosa Mazito Dhidi ya Watu Wengine

Katika Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale, watu waliofanya makosa mazito walichukuliwa hatua kali. Kwa mfano, ikiwa mwizi angevunja nyumba usiku, kisha mwenye nyumba amuue, mwenye nyumba hangekuwa na hatia ya damu. Alitendewa kosa kubwa, naye hakuwa na hatia. Tunasoma: “Mwizi akipatikana akifanya tendo la kuvunja ili kuingia naye apigwe na kuuawa, hakuna hatia ya damu kwa ajili [ya mwenye nyumba].”—Kutoka 22:2.

Mwanamke ambaye amelalwa kinguvu ana haki ya kuudhika sana, kwa kuwa hiyo ni dhambi nzito mbele za Mungu. Chini ya Sheria ya Musa, mwanamume aliyemlala mwanamke kinguvu alipaswa kuuawa “kama vile mtu humwinukia mwenzake na kumuua.” (Kumbukumbu la Torati 22:25, 26) Ingawa hatuko chini ya Sheria hiyo, inatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyohisi kuhusu kosa zito la kumlala mwanamke kinguvu.

Katika siku zetu pia, kumlala mwanamke kinguvu ni kosa zito linalostahili adhabu kali. Anayelalwa kinguvu ana haki ya kuripoti jambo hilo kwa polisi. Kwa kufanya hivyo, mamlaka inayohusika inaweza kumwadhibu mkosaji. Na ikiwa mkosaji ana umri mdogo, wazazi wanaweza kuchukua hatua hizo.

Makosa Madogo

Hata hivyo, mamlaka haihitaji kuchukua hatua kwa kila kosa. Hivyo, hatupaswi kuudhika sana kwa makosa madogo ambayo wengine wanafanya, badala yake tunapaswa kuwa tayari kusamehe. Tunapaswa kusamehe mara nyingi kadiri gani? Mtume Petro alimuuliza Yesu: “Bwana, ndugu yangu atanitendea dhambi mara ngapi nami nimsamehe? Mpaka mara 7?” Yesu akamwambia: “Ninakuambia, si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77.”—Mathayo 18:21, 22.

Kwa upande mwingine, tunapaswa kuendelea kujitahidi kuboresha utu wetu wa Kikristo ili kuepuka kuwaudhi wengine. Kwa mfano, unapokuwa na wengine, je, wakati mwingine unakuwa mkali, unakosa busara, au unatumia matusi? Hayo ni mambo yanayoweza kuwaudhi wengine. Badala ya kumlaumu mtu kwa sababu ameudhika au badala ya kuhisi kwamba yule aliyeudhika anapaswa kuwa tayari kusamehe, mkosaji anapaswa kutambua kwamba yeye ndiye aliyesababisha hali hiyo. Mkosaji anapaswa kujizuia kutenda au kusema kwa njia ambayo inaweza kuwaudhi wengine. Tukifanya hivyo, hatutaumiza hisia za wengine mara nyingi. Biblia inatukumbusha: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Tunapowaudhi wengine, hata bila kukusudia, kuomba msamaha kutasaidia sana kusuluhisha hali hiyo.

Neno la Mungu linatuhimiza “tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Waroma 14:19) Tunapokuwa wenye busara na fadhili, tunatenda kulingana na methali hii: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.” (Methali 25:11) Bila shaka, kufanya hivyo kunaleta hali bora na yenye kupendeza! Upole na usemi wa busara unaweza kubadili mtazamo mgumu wa watu wengine: “Ulimi wa upole unaweza kuvunja mfupa.”—Methali 25:15.

Hivyo, Neno la Mungu linatushauri: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) “Kukolezwa chumvi” kunamaanisha kwamba tufanye maneno yetu yawapendeze wengine, na hivyo kuepuka kuwaudhi. Kwa maneno na matendo, Wakristo wanajitahidi kufuata shauri hili la Biblia: ‘Tafuta amani na kuifuatilia.’—1 Petro 3:11.

Hivyo, ni wazi kwamba andiko la Mhubiri 7:9 linamaanisha hatupaswi kuudhiwa na mambo madogo-madogo yanayofanywa na wengine. Huenda wakafanya mambo hayo kwa sababu ya kutokamilika au hata kimakusudi, lakini si makosa makubwa. Hata hivyo, ikiwa kosa ni zito, inaeleweka kwamba aliyekosewa huenda akaudhika na labda akaamua kuchukua hatua inayofaa.—Mathayo 18:15-17.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Yehova aliwaacha Waisraeli wasiotubu washambuliwe na Waroma mwaka wa 70 W.K.

[Picha katika ukurasa wa 15]

“Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu”