Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wabarikiwa kwa Kufunga Safari Ndefu

Wabarikiwa kwa Kufunga Safari Ndefu

Wabarikiwa kwa Kufunga Safari Ndefu

RIPOTI moja kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inasema kwamba dada wawili wa familia moja waliamua kusafiri mbali katika eneo lenye vita ili wahudhurie Kusanyiko la Wilaya la “Mtukuzeni Mungu” huko Lisala. Zaidi ya kutazamia kufundishwa kiroho na kufurahia ushirika wa Kikristo kwenye kusanyiko hilo, walitazamia pia kukutana na wawakilishi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Kinshasa. Kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi hiyo, hawakuwa wameona ndugu yeyote kutoka ofisi ya tawi kwa miaka mingi, na walitaka kutumia nafasi hiyo kukutana nao.

Dada hao wawili walisafiri kwa mtumbwi kutoka kwenye mji wa kwao wa Basankusu hadi Lisala. Hiyo ilikuwa safari ya kilometa 300 kupitia misitu na mito miwili. Walisafiri kwa majuma matatu. Kwa kuwa wote wawili ni watumishi wa wakati wote, mmoja akiwa ametumika kwa miaka 3 na yule mwingine kwa miaka 19, walitumia nafasi hiyo kutangaza habari njema za Ufalme. Walihubiri kwa saa 110 njiani, na kugawanya trakti 200 na magazeti 30.

Walipokuwa mtoni, iliwabidi wasafiri kati ya viboko na mamba ambao wanapatikana sana katika eneo hilo. Hawangeweza kusafiri mtoni usiku! Pia walipitia vituo vingi vya ukaguzi vya wanajeshi.

Ijapokuwa hiyo ilikuwa safari ndefu sana na yenye kuchosha, dada hao walifurahia jitihada zao. Walikuwa na shangwe nyingi sana walipohudhuria kusanyiko huko Lisala. Waliichangamkia ile kweli kutoka moyoni na kutiwa moyo na ndugu na dada 7,000 waliohudhuria. Baada ya kusanyiko, walipitia magumu yaleyale katika safari ya kurudi nyumbani ambako walipata familia zao zikiwa salama salimini.