Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Amehesabu “Nywele Zenyewe za Kichwa Chenu”

Yehova Amehesabu “Nywele Zenyewe za Kichwa Chenu”

Yehova Amehesabu “Nywele Zenyewe za Kichwa Chenu”

“Hakuna hata [shomoro] mmoja . . . atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote.”—MATHAYO 10:29, 30.

1, 2. (a) Kwa nini Ayubu alifikiri kwamba Mungu amemwacha? (b) Je, Ayubu alisema hivyo kwa sababu alikuwa amemwasi Yehova? Eleza.

“NAKULILIA, lakini hunijibu, nasimama kuomba lakini hunisikilizi. Umegeuka kuwa mkatili kwangu, wanitesa kwa mkono wako wenye nguvu.” Ni wazi kwamba mtu aliyesema maneno hayo alikuwa akiteseka sana! Alipoteza mali yake yote, watoto wake walikufa katika msiba mbaya sana, na sasa alikuwa na ugonjwa wenye kudhoofisha. Mtu huyo ni Ayubu, na kisa chake chenye kuhuzunisha kimeandikwa katika Biblia kwa faida yetu.—Ayubu 30:20, 21, Biblia Habari Njema.

2 Huenda ikaonekana kwamba Ayubu alikuwa amemwasi Mungu, lakini si kweli. Ayubu alikuwa akieleza tu mfadhaiko aliokuwa nao moyoni. (Ayubu 6:2, 3) Hakujua kwamba Shetani ndiye aliyekuwa akimtesa, kwa hiyo alifikiri kimakosa kwamba Mungu amemwacha. Pindi moja, Ayubu hata alimwambia Yehova hivi: “Kwa nini unaficha uso wako na kuniona mimi kama adui yako?” *Ayubu 13:24.

3. Huenda tukafikiri nini tunapokabili matatizo?

3 Leo, watumishi wengi wa Yehova huteseka sana kwa sababu ya vita, migogoro ya kisiasa na ya kijamii, misiba ya kiasili, uzee, magonjwa, umaskini, na marufuku ya serikali. Yaelekea hata wewe unakabili matatizo fulani. Nyakati nyingine huenda ukafikiri kwamba Yehova anauficha uso wake mbali nawe. Unajua vizuri jinsi andiko la Yohana 3:16 linavyosema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee.” Hata hivyo, unapoteseka bila kutarajia kupata kitulizo, huenda ukajiuliza: ‘Je, kweli Mungu ananipenda mimi? Je, anaona jinsi ninavyoteseka? Je, ananijali mimi binafsi?’

4. Paulo alihitaji kuvumilia hali gani yenye kuendelea, na hali kama hiyo inaweza kutuathiri kwa njia zipi?

4 Fikiria kisa cha mtume Paulo. Aliandika hivi: “Nilipewa mwiba katika mwili, malaika wa Shetani, aendelee kunipiga kofi.” Kisha akaongeza hivi: “Mara tatu nilimsihi Bwana kwamba huo uniondoke.” Yehova alisikia maombi yake. Hata hivyo, alimwonyesha Paulo kwamba hangetatua tatizo lake kimuujiza. Badala yake, Paulo angehitaji kutegemea nguvu za Mungu ili zimsaidie kuvumilia “mwiba katika mwili” wake. * (2 Wakorintho 12:7-9) Kama Paulo, huenda unakabili jaribu fulani lenye kuendelea. Huenda ukawaza hivi, ‘Kwa kuwa inaonekana kwamba Yehova hajaondoa jaribu langu, je, inawezekana kwamba yeye hajui hali yangu au hanijali?’ Jibu ni hapana! Maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume wake muda mfupi baada ya kuwachagua yanathibitisha kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wa watumishi wake waaminifu. Hebu tuone jinsi maneno hayo yanavyoweza kututia moyo leo.

“Msiogope”—Kwa Nini?

5, 6. (a) Yesu aliwasaidiaje mitume kutoogopa mambo ambayo wangekabili? (b) Paulo alionyeshaje uhakika kwamba Yehova anamjali?

5 Yesu aliwapa mitume nguvu zisizo za kawaida, kutia ndani “mamlaka juu ya roho wachafu, ili wawafukuze na kuponya kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu.” Lakini hilo halikumaanisha kwamba hawangekabili matatizo na majaribu yoyote. Kinyume chake, Yesu alieleza waziwazi baadhi ya mambo ambayo wangekabili. Hata hivyo, aliwahimiza hivi: “Msiwaogope wale ambao wanaua mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mwogopeni yeye anayeweza kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.”—Mathayo 10:1, 16-22, 28.

6 Yesu alitoa mifano miwili ili kuwasaidia mitume wake kuelewa kwa nini hawapaswi kuogopa. Aliwaambia hivi: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.” (Mathayo 10:29-31) Ona kwamba Yesu alihusianisha kutoogopa majaribu na kuwa na uhakika kwamba Yehova anatujali sisi binafsi. Mtume Paulo alikuwa pia na uhakika huo. Aliandika: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu? Yeye ambaye hakujizuia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini yeye pia pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?” (Waroma 8:31, 32) Hata ukikabili matatizo ya aina gani, wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anakujali kibinafsi maadamu unaendelea kuwa mshikamanifu kwake. Tutaelewa hilo vizuri zaidi tunapochunguza kwa undani himizo ambalo Yesu aliwapa mitume wake.

Thamani ya Shomoro

7, 8. (a) Shomoro walionwaje siku za Yesu? (b) Huenda ni kwa nini Mathayo 10:29 inatumia neno la Kigiriki linalorejelea “shomoro” wadogo?

7 Mifano ya Yesu inaonyesha vizuri sana jinsi Yehova anavyomjali kila mmoja wa watumishi Wake. Kwanza fikiria mfano wa shomoro, au shore. Katika siku za Yesu, shomoro walikuwa chakula, lakini kwa kawaida walionwa kuwa ndege waharibifu kwa sababu waliharibu mimea. Shomoro walikuwa wengi sana na waliuzwa kwa bei ya chini sana hivi kwamba shomoro wawili walinunuliwa kwa senti zisizozidi tano za Marekani, kulingana na thamani ya leo. Mtu aliyenunua shomoro wanne aliongezewa shomoro mmoja kana kwamba shomoro huyo hakuwa na thamani yoyote!—Luka 12:6.

8 Fikiria pia ukubwa wa ndege huyo. Hata shomoro aliyekomaa ni mdogo sana akilinganishwa na ndege wengine wengi. Hata hivyo, neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “shomoro” katika Mathayo 10:29 linarejelea shomoro wadogo. Ni wazi kwamba Yesu alitaka mitume wake wafikirie ndege mdogo zaidi na mwenye thamani ndogo zaidi. Kama kichapo kimoja kinavyosema, “Yesu anamtaja ndege mdogo sana na hata anakazia udogo wa ndege huyo!”

9. Mfano wa Yesu wa shomoro unakazia jambo gani muhimu sana?

9 Mfano wa Yesu wa shomoro unakazia jambo muhimu sana: Vitu ambavyo havina thamani machoni pa wanadamu ni muhimu kwa Yehova Mungu. Yesu alikazia zaidi ukweli huo kwa kuongezea kwamba shomoro mdogo hawezi ‘kuanguka chini’ bila Yehova kujua. * Funzo ni wazi. Ikiwa Yehova Mungu anamjali ndege mdogo sana na mwenye thamani ndogo zaidi, basi anahangaikia hata zaidi hali ya mwanadamu ambaye ameamua kumtumikia!

10. Ni nini maana ya maneno haya: “Nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote”?

10 Baada ya kutoa mfano huo wa shomoro, Yesu alisema: “Nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote.” (Mathayo 10:30) Maneno hayo rahisi lakini yenye maana sana hukazia zaidi mfano wa Yesu kuhusu shomoro. Fikiria hili: Kichwa cha mwanadamu cha wastani kina nywele 100,000 hivi. Kwa kawaida, ni kana kwamba nywele zote zinafanana na mara nyingi hatukazii uangalifu unywele mmoja. Hata hivyo, Yehova Mungu anajua na anahesabu kila unywele. Kama Yehova anafanya hivyo, je, kuna jambo lolote kutuhusu ambalo hawezi kujua? Bila shaka, Yehova anaelewa utu wa pekee wa kila mtumishi wake. Kwa kweli, yeye “huona jinsi moyo ulivyo.”—1 Samweli 16:7.

11. Daudi alionyeshaje uhakika wa kwamba Yehova anamjua binafsi?

11 Daudi ambaye alikabili matatizo mengi, alikuwa na hakika kwamba Yehova alimjua. Aliandika hivi: “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua. Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali.” (Zaburi 139:1, 2) Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anakujua wewe binafsi. (Yeremia 17:10) Usikate kauli haraka kwamba wewe ni mdogo sana hivi kwamba macho ya Yehova yanayoweza kuona kila kitu hayawezi kukuona!

“Uyaweke Machozi Yangu Katika Kiriba Chako”

12. Tunajuaje kwamba Yehova anajua vizuri matatizo yanayowakabili watu wake?

12 Mbali na kumjua kila mmoja wa watumishi wake, Yehova pia anajua vizuri matatizo ambayo kila mmoja wao anakabili. Kwa mfano, Waisraeli walipokuwa wakidhulumiwa wakiwa watumwa, Yehova alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” (Kutoka 3:7) Inafariji kama nini kujua kwamba tunapovumilia jaribu, Yehova anaona hali yetu na kusikia vilio vyetu! Bila shaka hapuuzi mateso yetu.

13. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anawahurumia kikweli watumishi wake?

13 Hisia za Yehova kuelekea Waisraeli zinaonyesha pia kwamba anawahurumia wale walio na uhusiano pamoja naye. Hata ingawa mara nyingi waliteseka kwa sababu ya ukaidi wao wenyewe, Isaya aliandika hivi kumhusu Yehova: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.” (Isaya 63:9) Basi, ukiwa mtumishi mwaminifu wa Yehova, unaweza kuwa na hakika kwamba unapohisi uchungu, Yehova pia anahisi uchungu. Je, hilo halikuchochei ukabiliane na matatizo bila woga na kuendelea kujitahidi kabisa kumtumikia?—1 Petro 5:6, 7.

14. Zaburi ya 56 ilitungwa chini ya hali gani?

14 Zaburi ya 56 ambayo ilitungwa na Daudi alipokuwa akimtoroka Mfalme Sauli aliyetaka kumuua inaonyesha kwamba Mfalme Daudi alikuwa na hakika kuwa Yehova alimjali na kumhurumia. Daudi alitorokea Gathi, lakini aliogopa kwamba angekamatwa alipotambuliwa na Wafilisti. Aliandika hivi: “Adui zangu wameendelea kutanua kinywa mchana kutwa, kwa maana kuna wengi wanaofanya vita juu yangu kwa kujitakia makuu.” Kwa sababu ya hali hiyo hatari, Daudi alimgeukia Yehova. Alisema: “Mchana kutwa wanaendelea kuharibu mambo yangu ya kibinafsi; mawazo yao yote yako juu yangu kwa ajili ya ubaya.”—Zaburi 56:2, 5.

15. (a) Daudi alimaanisha nini alipomwomba Yehova ayaweke machozi yake katika kiriba au katika kitabu? (b) Tunapovumilia hali yenye kujaribu imani yetu tunaweza kuwa na uhakika gani?

15 Kisha Daudi anasema maneno haya yenye kuvutia katika Zaburi 56:8: “Wewe mwenyewe umetoa habari juu ya kuwa kwangu mkimbizi. Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako. Je, hayamo katika kitabu chako?” Maneno hayo kuhusu utunzaji wa Yehova wenye upendo yanagusa moyo sana! Tunapofadhaika, tunaweza kumlilia Yehova tukitokwa na machozi. Hata Yesu aliyekuwa mtu mkamilifu alifanya hivyo. (Waebrania 5:7) Daudi alisadiki kwamba Yehova alimwangalia na angekumbuka uchungu wake, kana kwamba anahifadhi machozi yake katika kiriba au kuyaandika katika kitabu. * Huenda unahisi kwamba machozi yako yanaweza kujaza kiriba hicho au kurasa nyingi za kitabu hicho. Ikiwa ndivyo ilivyo, jipe moyo. Biblia inatuhakikishia hivi: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

Kuwa Rafiki wa Karibu wa Mungu

16, 17. (a) Tunajuaje kwamba Yehova hapuuzi matatizo ambayo watu wake hukabili? (b) Yehova amefanya nini ili watu wawe na urafiki wa karibu pamoja naye?

16 Kujua kwamba Yehova amehesabu ‘nywele zenyewe za kichwa chetu’ kunatusaidia kuelewa jinsi Mungu tuliye na pendeleo la kumwabudu alivyo mwenye kujali na mwenye upendo. Ingawa ni lazima tungoje ulimwengu mpya alioahidi ili kuteseka na maumivu yote yaishe, Yehova anawafanyia watu wake jambo zuri sana leo. Daudi aliandika: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa, pia agano lake, ili kuwafanya walijue.”—Zaburi 25:14.

17 “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova.” Hilo ni wazo lisiloeleweka kwa wanadamu wasio wakamilifu! Hata hivyo, Yehova anawaalika wale wanaomwogopa wawe wageni katika hema lake. (Zaburi 15:1-5) Na Yehova anawafanyia nini wageni wake? Daudi anasema kwamba anawafanya wajue agano lake. Yehova huwaeleza mambo yake, kwa kuwafunulia manabii “jambo lake la siri” ili wajue makusudi yake na mambo wanayopaswa kufanya ili waishi kupatana nayo.—Amosi 3:7.

18. Tunajuaje kwamba Yehova anataka tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye?

18 Kwa kweli, inachangamsha moyo kujua kwamba sisi wanadamu wasio wakamilifu tunaweza kuwa marafiki wa karibu wa Aliye Juu Zaidi, Yehova Mungu. Hata anatuhimiza tufanye hivyo. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Yehova anataka tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Tayari amechukua hatua za kutusaidia kuwa na uhusiano huo. Dhabihu ya fidia ya Yesu imetufungulia njia ya kuwa na urafiki pamoja na Mungu Mweza-Yote. Biblia inasema: “Kwa habari yetu, sisi tunaonyesha upendo, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.

19. Uvumilivu unawezaje kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova?

19 Uhusiano huo wa karibu unaimarika zaidi tunapovumilia matatizo makubwa. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yakobo 1:4) Ni “kazi” gani inayotimizwa kwa kuvumilia matatizo? Kumbuka ule “mwiba katika mwili” wa Paulo. Uvumilivu ulimsaidiaje Paulo? Paulo alisema hivi kuhusu majaribu yake: “Kwa furaha zaidi, basi, ni afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu, ili nguvu za Kristo zibaki juu yangu kama hema. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na matusi, na hali za uhitaji, na mateso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:9, 10) Paulo alimwomba Yehova ampe nguvu alizohitaji—“nguvu zinazopita zile za kawaida” ikiwa ni lazima—ili aweze kuvumilia. Kwa njia hiyo alimkaribia zaidi Kristo na Yehova Mungu.—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:11-13.

20. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza na kutufariji tunapokabili matatizo?

20 Huenda Yehova ameruhusu majaribu yako yaendelee. Ikiwa ndivyo ilivyo, kumbuka ahadi yake kwa wale wanaomwogopa: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Atakufariji na kukutegemeza kama anavyoahidi. Yehova amehesabu ‘nywele zenyewe za kichwa chako.’ Anaona uvumilivu wako. Anahisi uchungu wako. Anakujali kabisa. Naye ‘hatasahau kamwe kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Waebrania 6:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Daudi aliyekuwa mwadilifu na pia wana waaminifu wa Kora walisema maneno kama hayo.—Zaburi 10:1; 44:24.

^ fu. 4 Biblia haitaji ‘mwiba ambao Paulo alikuwa nao katika mwili.’ Huenda alikuwa na tatizo fulani la afya, labda macho yake hayakuona vizuri. Au huenda maneno “mwiba katika mwili” yakamaanisha mitume wa uwongo na wengine ambao walipinga huduma na utume wa Paulo.—2 Wakorintho 11:6, 13-15; Wagalatia 4:15; 6:11.

^ fu. 9 Wasomi fulani wanasema kwamba kuanguka kwa shomoro chini huenda hakumaanishi kufa tu. Wanasema kwamba neno la lugha ya awali huenda linamaanisha ndege kutua chini ili kutafuta chakula. Ikiwa ni hivyo, basi ingemaanisha kwamba Mungu humkazia uangalifu na kumjali ndege huyo katika maisha ya kila siku, si wakati tu anapokufa.—Mathayo 6:26.

^ fu. 15 Zamani viriba vilitengenezwa kutokana na ngozi ya kondoo, mbuzi, na ng’ombe. Maziwa, siagi, jibini, au maji yalitiwa katika viriba hivyo. Viriba vilivyotengenezwa kwa ngozi iliyotayarishwa kwa njia ya pekee vilitumiwa kubebea mafuta au divai.

Je, Unakumbuka?

• Ni mambo gani yanayoweza kumfanya mtu ahisi kwamba Mungu amemwacha?

• Tunajifunza nini kutokana na mifano ya Yesu kuhusu shomoro na kuhesabiwa kwa nywele za kichwa chetu?

• Ni nini maana ya machozi ya mtu kuwekwa katika “kiriba” au “kitabu” cha Yehova?

• Tunawezaje kuwa na “urafiki wa karibu pamoja na Yehova”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kwa nini Yehova hakuondoa “mwiba katika mwili” wa Paulo?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yesu wa shomoro?

[Hisani]

© J. Heidecker/VIREO

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tukisoma Biblia kwa ukawaida, tutaona kwa hakika kwamba Mungu anatujali sisi binafsi