Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwapa Thawabu Kubwa Wale Wanaoishika Njia Yake

Yehova Huwapa Thawabu Kubwa Wale Wanaoishika Njia Yake

Simulizi la Maisha

Yehova Huwapa Thawabu Kubwa Wale Wanaoishika Njia Yake

LIMESIMULIWA NA ROMUALD STAWSKI

Vita vya pili vya ulimwengu vilipoanza katika Septemba 1939, kulikuwa na mapigano makali kaskazini mwa Poland. Nikiwa mvulana mdadisi mwenye umri wa miaka tisa, nilienda kwenye uwanja wa vita uliokuwa karibu ili nione mapigano. Yale niliyoona huko yalikuwa yenye kuogopesha sana. Maiti nyingi zilitapakaa kwenye uwanja wa mapigano, na moshi mwingi ulijaa hewani. Ingawa nilikuwa hasa nikifikiria jinsi ningefika salama nyumbani, nilijiuliza akilini maswali kadhaa: “Kwa nini Mungu anaruhusu mambo haya mabaya yatukie? Anaunga mkono upande gani?”

VITA vilipokaribia kwisha, wavulana walilazimishwa kutumikia serikali ya Ujerumani. Yeyote aliyethubutu kukataa alitundikwa mtini au darajani akiwa na ishara kifuani inayosema “msaliti” au “mhujumu.” Mji wetu, Gdynia, ulikuwa katikati ya vikosi vya Ujerumani na vya Sovieti. Tulipoenda nje ya mji kuchota maji, risasi na mabomu yalipita juu ya vichwa vyetu, na ndugu yangu mdogo Henryk akauawa. Kwa sababu ya hali mbaya, mama alituficha sisi watoto wanne katika chumba cha chini ya ardhi kwa ajili ya usalama wetu. Tukiwa humo ndugu yangu Eugeniusz, mwenye umri wa miaka miwili, alikufa kutokana na ugonjwa wa koo.

Kwa mara nyingine tena nilijiuliza: “Mungu yuko wapi? Kwa nini anaruhusu mateso haya yote?” Ingawa nilikuwa Mkatoliki mwenye bidii na nilienda kanisani kwa ukawaida, sikupata majibu kwa maswali hayo.

Niliikubali Kweli ya Biblia

Nilipata majibu kwa maswali yangu kwa njia ambayo sikuwa nimetarajia. Vita viliisha mwaka wa 1945, na mapema mwaka wa 1947, Shahidi mmoja wa Yehova akatutembelea nyumbani kwetu huko Gdynia. Mama yangu alizungumza na Shahidi huyo nami nikasikia baadhi ya mambo yaliyosemwa. Mambo ambayo Shahidi huyo alisema yalionekana kuwa yenye kupatana na akili, hivyo tukakubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa Kikristo. Baada ya mwezi mmoja tu, ingawa nilikuwa bado sijaelewa kikamili kweli iliyomo katika Biblia, nilijiunga na kikundi cha Mashahidi wenyeji nami nikawahubiria wengine kuhusu ulimwengu bora, usio na vita na ukatili. Hilo lilinipa shangwe kubwa.

Katika Septemba 1947, nilibatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko huko Sopot. Mnamo Mei iliyofuata, nilianza utumishi wa painia wa kawaida, huku nikitumia wakati mwingi kuwahubiria wengine ujumbe wa Biblia. Makasisi walipinga vikali kazi yetu nao wakachochea jeuri juu yetu. Wakati mmoja, tulishambuliwa na umati wenye hasira, tukarushiwa mawe, na kupigwa vikali. Katika pindi nyingine, watawa wa kike na viongozi wa dini walichochea kikundi cha watu ili kitushambulie. Tulikimbilia kituo cha polisi, lakini umati huo ulilizunguka jengo hilo na kutisha kutupiga. Mwishowe, maofisa wengine wa polisi wakaja, nasi tukaondolewa hapo tukiwa chini ya ulinzi mkali.

Wakati huo, hakukuwa na kutaniko katika eneo letu. Wakati mwingine tulikaa porini usiku kucha. Tulifurahi kwamba tuliweza kuhubiri licha ya hali hizo. Leo, kuna makutaniko imara katika eneo hilo.

Utumishi wa Betheli na Kifungo

Mwaka wa 1949, nilialikwa Betheli huko Łódź. Lilikuwa pendeleo kubwa kama nini kutumikia mahali kama hapo! Inasikitisha kwamba nilikaa hapo kwa muda mfupi sana. Mnamo Juni 1950, mwezi mmoja kabla ya kazi yetu kupigwa marufuku rasmi, nilikamatwa pamoja na ndugu wengine wa Betheli. Nilipelekwa gerezani na kuhojiwa kikatili.

Kwa kuwa baba yangu alifanya kazi kwenye meli iliyosafiri mara kwa mara kwenda New York, maofisa ambao waliendesha uchunguzi walijaribu kunifanya nikubali kwamba Baba alikuwa akifanyia Marekani upelelezi. Nilihojiwa bila huruma. Isitoshe, wakati huohuo maofisa wanne walijaribu kunishawishi nitoe ushuhuda wa uwongo juu ya Ndugu Wilhelm Scheider, ambaye wakati huo alisimamia kazi yetu nchini Poland. Walinipiga kwenye visigino kwa fimbo. Nilipokuwa nimelala sakafuni huku nikivuja damu, nilihisi kwamba singeweza kuvumilia tena mapigo hayo. Ndipo nikapaaza sauti, “Yehova, nisaidie!” Wale waliokuwa wakinitesa walishangaa sana nao wakaacha kunipiga. Na baada ya dakika chache tu, walishikwa na usingizi. Nilihisi kitulizo nami nikapata nguvu tena. Hilo lilinisadikisha kwamba kwa upendo Yehova huwajibu watumishi wake waliojiweka wakfu wanapomlilia. Jambo hilo liliimarisha imani yangu nalo likanifundisha kumtumaini kabisa Mungu.

Ripoti ya mwisho ya uchunguzi ilitia ndani ushahidi wa uwongo ambao ulidhaniwa ni mimi niliutoa. Nilipokataa, ofisa mmoja akaniambia, “Utaeleza hilo mahakamani!” Mfungwa mwenzangu alinishauri kwamba nisijisumbue sana, kwa kuwa ripoti ya mwisho ilipaswa kuchunguzwa na mwendesha-mashtaka wa jeshi. Hivyo ningeweza kupinga ushahidi huo wa uwongo. Na ndivyo mambo yalivyokuwa.

Kuwa Mwangalizi wa Mzunguko na Kufungwa Tena

Niliachiliwa mnamo Januari 1951. Mwezi mmoja baadaye, nilianza kutumika nikiwa mwangalizi anayesafiri. Licha ya marufuku, nilitumika pamoja na ndugu wengine ili kuimarisha makutaniko na kuwasaidia Mashahidi wenzetu ambao walikuwa wametawanyika kwa sababu ya kusakwa na polisi wa usalama. Tuliwatia moyo akina ndugu waendelee na huduma. Katika miaka ya baadaye, ndugu hao waliwategemeza kwa ujasiri waangalizi wanaosafiri na walifanya kazi ya kuchapisha na kugawa vichapo vya Biblia kisiri.

Siku moja mnamo Aprili 1951, baada ya kuhudhuria mkutano wa Kikristo, nilikamatwa barabarani na maofisa wa usalama ambao walikuwa wakinichunguza kwa makini. Kwa kuwa nilikataa kujibu maswali yao, walinipeleka katika gereza la Bydgoszcz nao wakaanza kunihoji usiku huohuo. Niliamuriwa kusimama kwa kuegemea ukuta kwa muda wa siku sita usiku na mchana bila kula wala kunywa huku kukiwa na moshi mwingi wa sigara za maofisa. Nilipigwa kwa rungu na kuchomwa kwa sigara. Nilipozimia, walinimwagilia maji nao wakaanza tena kunihoji. Nilimsihi Yehova aniimarishe ili nivumilie, naye akanitegemeza.

Kuwa katika gereza la Bydgoszcz kulikuwa na faida fulani. Nikiwa huko niliweza kuwafundisha kweli za Biblia watu ambao haingewezekana kuwafikia. Na kwa kweli nilikuwa na nafasi nyingi za kuhubiri. Mara nyingi kwa sababu ya hali yao yenye kusikitisha na kukatisha tamaa, wafungwa walikuwa tayari kusikiliza habari njema.

Mabadiliko Mawili Muhimu

Punde tu baada ya kuachiliwa mwaka wa 1952, nilikutana na Nela, dada mmoja painia ambaye alikuwa mwenye bidii. Alikuwa akifanya upainia kusini mwa Poland. Baadaye, alifanya kazi mahali fulani pa siri ambapo tulipaita “kiwanda cha kuokea mikate,” mahali ambapo vichapo vyetu vilichapwa. Hiyo ilikuwa kazi ngumu ambayo ilihitaji tahadhari na kujitoa. Tulifunga ndoa mwaka wa 1954, nasi tukaendelea na utumishi wa wakati wote hadi binti yetu, Lidia, alipozaliwa. Ndipo tukaamua kwamba ili niendelee na kazi ya kusafiri, Nela angesimamisha utumishi wake wa wakati wote na kurudi nyumbani ili kumtunza binti yetu.

Katika mwaka huohuo, tulikabili uamuzi mwingine muhimu. Niliombwa kutumika nikiwa mwangalizi wa wilaya katika eneo ambalo ukubwa wake ulikuwa sehemu moja ya tatu ya nchi ya Poland. Tulisali kuhusu jambo hilo. Nilitambua umuhimu wa kuwaimarisha ndugu zetu waliokuwa chini ya marufuku. Ndugu wengi walikamatwa wakati huo, hivyo kulikuwa na uhitaji mkubwa wa kuwatia moyo kiroho. Kwa kuwa Nela alinitegemeza, nilikubali mgawo huo. Yehova alinisaidia kutumika nikiwa mwangalizi wa wilaya kwa miaka 38.

Kusimamia “Viwanda vya Kuokea Mikate”

Siku hizo, mwangalizi wa wilaya alisimamia “viwanda vya kuokea mikate,” vilivyokuwa mahali pa siri. Polisi walitufuata daima, huku wakijaribu kupata na kukomesha kazi yetu ya kuchapisha. Nyakati nyingine walifaulu, lakini hatukuwahi kukosa chakula cha kiroho kifaacho. Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akitulinda.

Ili kualikwa kufanya kazi ngumu na hatari ya kuchapisha, ilihitaji mtu awe mshikamanifu, mwenye tahadhari, mwenye kujitoa, na mtiifu. Hizo ndizo sifa ambazo ziliwezesha “kiwanda cha kuokea mikate” kuendelea kufanya kazi kwa usalama. Ilikuwa vigumu kupata mahali pazuri pa kuchapisha kisiri. Sehemu fulani zilionekana kuwa zilizofaa, lakini akina ndugu waliokuwa katika sehemu hizo hawakuwa waangalifu sana. Katika sehemu nyingine, ingawa ndugu walikuwa waangalifu hali hazikufaa. Ndugu walikuwa tayari kujitoa. Niliwathamini sana ndugu na dada wote ambao nilikuwa na pendeleo la kufanya kazi nao.

Kutetea Habari Njema

Wakati wa miaka hiyo ya matatizo, tulishtakiwa daima kuhusika katika utendaji usio halali na wenye uchochezi na hivyo tukapelekwa mahakamani. Hilo lilikuwa tatizo kwa sababu hatukuwa na mwanasheria wa kututetea. Wanasheria wengine walikuwa wenye huruma, lakini wengi wao waliogopa kujulikana nao hawakutaka kuwachukiza wenye mamlaka. Hata hivyo, Yehova alijua mahitaji yetu, na kwa wakati ufaao aliongoza mambo kwa faida yetu.

Alojzy Prostak, mwangalizi anayesafiri kutoka Kraków, alitendewa kwa ukatili wakati wa kuhojiwa hivi kwamba ilibidi apelekwe kwenye hospitali ya gereza. Kusimama kwake imara licha ya mateso ya kiakili na ya kimwili kulimfanya aheshimiwe na kuwavutia wafungwa wengine katika hospitali hiyo. Mmoja wao alikuwa mwanasheria anayeitwa Witold Lis-Olszewski ambaye alishangazwa na ujasiri wa Ndugu Prostak. Mwanasheria huyo alizungumza mara nyingi na Ndugu Prostak naye akamwahidi hivi: “Punde tu nitakapofunguliwa na kuruhusiwa kuanza tena kazi yangu, nitakuwa tayari kuwatetea Mashahidi wa Yehova.” Alitimiza ahadi yake.

Bw. Olszewski alikuwa na kikundi chake cha wanasheria ambao waliazimia kushikamana na ahadi yao ya kutusaidia. Wakati upinzani ulipokuwa mkali sana, waliwatetea akina ndugu katika kesi 30 hivi kila mwezi, yaani, kesi moja kila siku! Kwa kuwa Bw. Olszewski alihitaji kujua vizuri habari za kesi zote, nilichaguliwa ili kuwasiliana naye. Nilifanya kazi naye kwa miaka saba katika miaka ya 1960 na 1970.

Siku hizo, nilijifunza mambo mengi kuhusu kazi ya sheria. Mara nyingi nilichunguza kesi, maelezo ya wanasheria—yafaayo na yasiyofaa—mbinu za kutetea kisheria, na ushahidi wa waamini wenzangu walioshtakiwa. Yote hayo yalikuwa yenye faida sana na yaliwasaidia akina ndugu, hasa wale walioitwa kutoa ushahidi, kujua mambo ambayo walipaswa kusema na wakati gani ilifaa kunyamaza mbele ya mahakama.

Mara nyingi kesi ilipokuwa ikiendelea, Bw. Olszewski alilala katika nyumba za Mashahidi wa Yehova. Haikuwa kwa sababu hangeweza kulipa chumba cha hoteli, lakini kama alivyosema wakati mmoja, “Kabla ya kesi, ninataka kuwa na mtazamo kama wenu.” Kwa sababu ya msaada wake, tulishinda kesi nyingi. Alinitetea mara nyingi lakini alikataa nisimlipe. Pindi moja, alikataa malipo ya kesi 30. Kwa nini? Alisema hivi: “Ninataka kutoa mchango wangu kwa kazi yenu hata ikiwa ni mdogo.” Na mchango huo haukuwa mdogo. Wenye mamlaka walijua vema kazi ya kikundi cha Bw. Olszewski, lakini hilo halikumzuia kutusaidia.

Ni vigumu kueleza ushahidi mzuri ambao ndugu zetu walitoa wakati wa kesi hizo. Wengi walikuja mahakamani ili kusikiliza kesi hizo na kuwaimarisha ndugu walioshtakiwa. Kesi zilipofikia kilele, nilihesabu idadi ya wale waliokuja kuunga mkono kesi hizo kuwa 30,000 kwa mwaka mmoja. Hakika huo ulikuwa umati mkubwa wa Mashahidi!

Mgawo Mpya

Kufikia mwaka wa 1989 marufuku juu ya kazi yetu yalikuwa yameondolewa. Miaka mitatu baadaye ofisi mpya ya tawi ilijengwa na kuwekwa wakfu. Nilialikwa huko kufanya kazi kwenye idara ya Huduma za Habari za Kihospitali, na nilikubali mgawo huo kwa furaha. Tulifanya kazi tukiwa kikundi cha watu watatu, nasi tuliwategemeza ndugu zetu kukabili tatizo la damu na kuwasaidia kutetea msimamo wao unaotegemea dhamiri yao ya Kikristo.—Matendo 15:29.

Mimi na mke wangu tunashukuru sana kwa pendeleo la kumtumikia Yehova katika huduma ya hadharani. Sikuzote Nela ameniunga mkono na kunitia moyo. Ninashukuru sana kwamba wakati wowote nilipokuwa ninashughulikia migawo ya kiroho au nilipotiwa gerezani, Nela hakuwahi kulalamika kuhusu kutokuwapo kwangu nyumbani. Nyakati za matatizo, aliwafariji wengine badala ya yeye kuathiriwa sana na hisia.

Kwa mfano, mwaka wa 1974, nilikamatwa pamoja na waangalizi wengine wanaosafiri. Baadhi ya ndugu ambao walijua habari hiyo walitaka kumjulisha mke wangu kwa njia ya fadhili. Walipomwona, walimwuliza, “Dada Nela, je, uko tayari kwa habari mbaya zaidi?” Mwanzoni, alipigwa na bumbuazi kwa woga kwa kuwa alifikiri kwamba nimekufa. Alipojua waziwazi kile kilichotokea, alisema hivi kwa furaha: “Yuko hai! Hii si mara yake ya kwanza kufungwa.” Baadaye, ndugu hao waliniambia kwamba walipendezwa sana na mtazamo wake mzuri.

Hata ingawa tulipatwa na mambo mengi yenye kufadhaisha wakati uliopita, sikuzote Yehova ametupa thawabu kubwa kwa kuwa tumeishika njia yake. Tunafurahi sana kuona kwamba binti yetu, Lidia, na mume wake, Alfred DeRusha, wamekuwa wenzi wa ndoa Wakristo walio mifano bora. Wamewalea wana wao, Christopher na Jonathan, kuwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, jambo ambalo linaongeza furaha yetu. Pia ndugu yangu, Ryszard, na dada yangu, Urszula, wamekuwa Wakristo waaminifu kwa miaka mingi.

Yehova hajawahi kutuacha, na tunataka kuendelea kumtumikia kwa moyo wote. Tumejionea wenyewe ukweli wa maneno haya ya Zaburi 37:34: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia.” Tunatazamia wakati huo kwa moyo wetu wote.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kwenye kusanyiko lililofanywa katika bustani ya ndugu mmoja huko Kraków, mwaka wa 1964

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na mke wangu Nela na binti yetu Lidia, mwaka wa 1968

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na mvulana ambaye ni Shahidi, kabla hajapasuliwa moyo bila kutiwa damu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na Dakt. Wites, ambaye ni daktari mkuu anayepasua moyo wa watoto bila kutumia damu, kwenye hospitali moja huko Katowice

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na Nela, mwaka wa 2002