Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni “Mthawabishaji wa Wale Wanaomtafuta Kwa Bidii”

Yehova Ni “Mthawabishaji wa Wale Wanaomtafuta Kwa Bidii”

Yehova Ni “Mthawabishaji wa Wale Wanaomtafuta Kwa Bidii”

“Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—WAEBRANIA 11:6.

1, 2. Kwa nini baadhi ya watumishi wa Yehova wanahisi kwamba hawastahili?

“NIMEKUWA Shahidi wa Yehova kwa miaka 30 hivi, lakini sikuzote mimi huhisi kwamba sistahili kuitwa Shahidi,” asema Barbara. * “Hata ingawa nimekuwa painia na nimekuwa na mapendeleo mengine mengi, hakuna pendeleo hata moja linalonifanya nihisi kwamba ninastahili kuitwa Shahidi.” Keith anahisi vivyo hivyo. Anasema: “Nyakati nyingine nilihisi sistahili kwa sababu watumishi wa Yehova wana sababu nyingi zinazowaletea furaha, lakini mimi sikuwa na furaha. Nilianza kujilaumu na hali yangu ikazidi tu kuwa mbaya.”

2 Watumishi wengi waaminifu wa Yehova, zamani na leo, wamehisi hivyo. Je, nyakati nyingine unahisi hivyo? Huenda ukapata matatizo mengi sana, huku waamini wenzako wakionekana kuwa na furaha na maisha mazuri yasiyo na matatizo yoyote. Basi unaweza kuhisi kwamba huna kibali cha Yehova wala hustahili machoni pake. Usikate kauli haraka-haraka kwamba ndivyo ilivyo. Biblia inatuhakikishia hivi: “[Yehova] hakudharau wala kuchoshwa na mateso ya mwenye kuteseka; naye hakumficha uso wake, naye alipomlilia amsaidie alisikia.” (Zaburi 22:24) Unabii huo kumhusu Masihi unaonyesha kwamba Yehova huwasikiliza waaminifu wake, na vilevile huwapa thawabu.

3. Kwa nini hatuwezi kuepuka matatizo ya mfumo huu wa mambo?

3 Hakuna mtu asiyeweza kupatwa na matatizo ya mfumo huu wa mambo—hata watu wa Yehova. Tunaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani Ibilisi, adui mkubwa wa Yehova. (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Watumishi wa Yehova hawalindwi kimuujiza, badala yake wao ni shabaha kuu ya Shetani. (Ayubu 1:7-12; Ufunuo 2:10) Kwa hiyo, tunahitaji ‘kudumu katika sala’ na ‘kuvumilia chini ya dhiki’ mpaka wakati uliowekwa na Mungu utakapofika, tukiwa na hakika kwamba Yehova anatujali. (Waroma 12:12) Hatupaswi kuruhusu matatizo ya ulimwengu huu yatufanye tufikiri kwamba Yehova, Mungu wetu, hatupendi!

Watu wa Kale Waliovumilia

4. Taja mifano kadhaa ya watumishi waaminifu wa Yehova ambao walivumilia hali zenye kufadhaisha.

4 Watumishi wengi wa kale wa Yehova walivumilia hali zenye kufadhaisha. Kwa mfano, Hana alikuwa na “uchungu katika nafsi” kwa sababu hakuwa na mtoto na hivyo alifikiri kwamba Mungu alikuwa amemsahau. (1 Samweli 1:9-11) Eliya alipokuwa akitafutwa na Malkia Yezebeli muuaji, aliogopa na kusali hivi kwa Yehova: “Inatosha! Sasa, Ee Yehova, iondoe nafsi yangu, kwa maana mimi si bora kuliko mababu zangu.” (1 Wafalme 19:4) Ni wazi kwamba mtume Paulo alifadhaishwa sana na hali yake ya kutokamilika alipokiri hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” Kisha akaongeza hivi: “Maskini mimi!”—Waroma 7:21-24.

5. (a) Hana, Eliya, na Paulo walipewa thawabu gani? (b) Ni kitulizo gani tunachoweza kupata katika Neno la Mungu tunapovunjika moyo?

5 Bila shaka, tunajua kwamba Hana, Eliya, na Paulo walivumilia katika utumishi wa Yehova, Naye aliwapa thawabu kubwa sana. (1 Samweli 1:20; 2:21; 1 Wafalme 19:5-18; 2 Timotheo 4:8) Hata hivyo, walikuwa na hisia mbalimbali za kibinadamu, kama vile huzuni, kuvunjika moyo, na woga. Basi, hatupaswi kushangaa tukihisi nyakati nyingine tumevunjika moyo. Lakini unaweza kufanya nini mahangaiko ya maisha yakikufanya uhisi kwamba Yehova hakupendi kamwe? Unaweza kupata kitulizo katika Neno la Mungu. Kwa mfano, katika makala iliyotangulia, tulizungumzia maneno ya Yesu ya kwamba Yehova amehesabu ‘nywele zenyewe za kichwa chetu.’ (Mathayo 10:30) Maneno hayo yenye kutia moyo yanaonyesha kwamba Yehova anapendezwa kikweli na kila mmoja wa watumishi wake. Kumbuka pia mfano wa Yesu kuhusu shomoro. Ikiwa hakuna hata ndege mmoja kati ya ndege hao wadogo anayeweza kuanguka chini bila Yehova kujua, basi kwa nini apuuze matatizo yanayokupata?

6. Biblia inawezaje kuwafariji wale wanaofadhaika?

6 Je, sisi wanadamu wasio wakamilifu tunaweza kweli kuwa wenye thamani machoni pa Muumba mwenye nguvu zote, Yehova Mungu? Ndiyo! Kuna maandiko mengi ya Biblia yanayotuhakikishia hivyo. Tukitafakari maandiko hayo, tutakubaliana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Fikira zangu zinazofadhaisha zilipokuwa nyingi ndani yangu, faraja zako mwenyewe zilianza kuikumbatia nafsi yangu.” (Zaburi 94:19) Na tuchunguze baadhi ya maneno yenye kufariji katika Neno la Mungu ambayo yatatusaidia kuelewa vizuri kwamba tunathaminiwa na Mungu na kwamba atatupa thawabu tukiendelea kufanya mapenzi yake.

“Mali ya Pekee” ya Yehova

7. Ni unabii gani wenye kutia moyo ambao Yehova alitoa kupitia Malaki kwa taifa hilo lenye ufisadi?

7 Hali ya Wayahudi ilikuwa mbaya sana katika karne ya tano K.W.K. Makuhani walikubali wanyama wasiofaa na kuwatoa dhabihu kwenye madhabahu ya Yehova. Waamuzi walikuwa na ubaguzi. Mazoea kama ulozi, uwongo, upunjaji, na uzinzi yalienea sana. (Malaki 1:8; 2:9; 3:5) Malaki alitoa unabii wenye kustaajabisha kwa taifa hilo lililojaa ufisadi. Baada ya muda, Yehova angewarudisha watu wake katika hali yenye kukubalika. Andiko linasema: “‘Watakuwa wangu,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘siku ile nitakapotokeza mali ya pekee. Nami nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.’”—Malaki 3:17.

8. Kwa nini andiko la Malaki 3:17 linaweza kutumiwa kuhusiana na wale wa umati mkubwa?

8 Unabii wa Malaki unatimizwa siku zetu kuhusiana na Wakristo watiwa-mafuta, taifa la kiroho la wale 144,000. Taifa hilo kwa kweli ni “mali ya pekee” au “watu wa kuwa mali ya pekee” kwa Yehova. (1 Petro 2:9) Unabii wa Malaki unaweza pia kuwatia moyo wale wa “umati mkubwa,” ambao ‘wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wakiwa wamevikwa kanzu nyeupe.’ (Ufunuo 7:4, 9) Wanakuwa kundi moja pamoja na watiwa-mafuta, wakiwa chini ya Mchungaji mmoja, Yesu Kristo.—Yohana 10:16.

9. Kwa nini Yehova anawaona watu wake kuwa “mali ya pekee”?

9 Yehova anawaonaje wale wanaochagua kumtumikia? Kama andiko la Malaki 3:17 linavyosema, anawaona kama baba mwenye upendo anavyomwona mwanaye. Hebu ona jinsi anavyowasifu sana watu wake. Anawaita “mali ya pekee.” Tafsiri nyingine zinasema “watu wangu mwenyewe,” “mali yangu yenye thamani zaidi,” na “vito vyangu.” Kwa nini Yehova anawaona wale wanaomtumikia kuwa watu wa pekee sana hivyo? Kwanza, yeye ni Mungu anayewathamini watumishi wake. (Waebrania 6:10) Anawakaribia wale wanaomtumikia kutoka moyoni naye huwaona kuwa watu wa pekee.

10. Yehova huwalindaje watu wake?

10 Hebu wazia mali yenye thamani ambayo ni ya pekee kwako. Unajitahidi sana kuilinda, sivyo? Yehova hujitahidi vivyo hivyo kuilinda ‘mali yake ya pekee.’ Ni kweli kwamba hawalindi watu wake kutokana na majaribu na misiba yote. (Mhubiri 9:11) Lakini Yehova anaweza na atawalinda kiroho watumishi wake waaminifu. Yeye huwapa nguvu wanazohitaji ili kuvumilia jaribu lolote. (1 Wakorintho 10:13) Ndiyo sababu Musa aliwaambia hivi watu wa kale wa Mungu, Waisraeli: “Iweni hodari na wenye nguvu. . . . Yehova Mungu wako ndiye anayepiga mwendo pamoja nawe. Hatakutupa wala kukuacha kabisa.” (Kumbukumbu la Torati 31:6) Yehova huwapa thawabu watu wake. Wao ni “mali ya pekee” kwake.

Yehova Ni “Mthawabishaji”

11, 12. Kumthamini Yehova akiwa Mthawabishaji wetu kunawezaje kutusaidia kuondoa shaka?

11 Jambo lingine linalothibitisha kwamba Yehova anawathamini watumishi wake ni kwamba anawapa thawabu. Aliwaambia Waisraeli hivi: “‘Tafadhali, mnijaribu kwa njia hii,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’” (Malaki 3:10) Bila shaka, hatimaye Yehova atawapa watumishi wake thawabu ya uzima wa milele. (Yohana 5:24; Ufunuo 21:4) Thawabu hiyo ya pekee sana inaonyesha kina cha upendo na ukarimu wa Yehova. Inaonyesha pia kwamba anawathamini kikweli wale wanaochagua kumtumikia. Kujifunza kumwona Yehova kuwa Mthawabishaji mkarimu kunaweza kutusaidia kuondoa shaka yoyote tuliyo nayo kuhusu msimamo wetu mbele za Mungu. Naam, Yehova anatuhimiza tumwone kuwa Mthawabishaji! Paulo aliandika hivi: “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

12 Ni wazi kwamba tunamtumikia Yehova kwa sababu tunampenda, si kwa sababu tu anaahidi kutupa thawabu. Hata hivyo, kutazamia kwa hamu tumaini la kupata thawabu si jambo lisilofaa wala la ubinafsi. (Wakolosai 3:23, 24) Yehova huchukua hatua ya kuwapa thawabu wale wanaomtafuta kwa bidii kwa sababu anawapenda na anawathamini sana.

13. Kwa nini mpango wa fidia unathibitisha kwa njia kubwa zaidi kwamba Yehova anatupenda?

13 Mpango wa fidia huthibitisha kwa njia kubwa zaidi kwamba Yehova anawathamini sana wanadamu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mpango wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ni kinyume cha maoni ya kwamba Yehova hatuthamini wala hatupendi. Kwa wazi, ikiwa Yehova alilipa bei kubwa sana hivyo kwa ajili yetu, kwa kumtoa Mwanaye mzaliwa-pekee, bila shaka lazima awe anatupenda sana.

14. Paulo aliionaje fidia?

14 Kwa hiyo, ukihisi kwamba hustahili, tafakari juu ya fidia. Naam, ione fidia kuwa zawadi ambayo Yehova alitoa kwa ajili yako. Mtume Paulo aliiona hivyo. Kumbuka alisema: “Maskini mimi!” Lakini aliongeza hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu,” ambaye ‘alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Waroma 7:24, 25; Wagalatia 2:20) Paulo hakuwa akijigamba aliposema hivyo. Alikuwa tu na hakika kwamba Yehova alimthamini yeye binafsi. Kama Paulo, wewe pia unapaswa kuiona fidia kuwa zawadi ambayo Mungu amekupa. Yehova si Mwokozi tu mwenye nguvu, bali pia ni Mthawabishaji mwenye upendo.

Jihadhari na “Hila” za Shetani

15-17. (a) Ibilisi hutumiaje hisia zisizofaa? (b) Kisa cha Ayubu kinaweza kututiaje moyo?

15 Huenda bado ukaona ni vigumu kuamini kwamba maneno yenye kufariji yaliyoongozwa kwa roho ambayo yako katika Neno la Mungu yanakuhusu wewe. Huenda ukahisi kwamba wengine wanaweza kupata thawabu ya kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu, lakini wewe hustahili kuipata. Ufanye nini ikiwa unahisi hivyo?

16 Hapana shaka kwamba unajua himizo la Paulo kwa Waefeso: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:11) Tunapofikiria hila za Shetani, huenda tukakumbuka mara moja mambo kama vile kupenda mali na ukosefu wa adili. Ni wazi kwamba anatumia mambo hayo. Watu wengi wa Mungu wa nyakati za kale na hata wa leo wamenaswa na mitego hiyo. Hata hivyo, hatupaswi kusahau hila nyingine ya Shetani, yaani, jitihada zake za kuwasadikisha watu kwamba Yehova Mungu hawapendi.

17 Ibilisi hutumia kwa ustadi sana hisia hizo ili kujaribu kuwafanya watu wamwache Mungu. Kumbuka maneno ambayo Bildadi alimwambia Ayubu: “Mwanadamu anayeweza kufa anawezaje kuwa upande wa haki mbele za Mungu, au, mtu aliyezaliwa na mwanamke anawezaje kuwa safi? Tazama! Kuna hata mwezi, nao si mwangavu; nazo nyota zenyewe si safi machoni pake. Sembuse mwanadamu anayeweza kufa, ambaye ni funza, na mwana wa binadamu, ambaye ni mnyoo!” (Ayubu 25:4-6; Yohana 8:44) Hapana shaka kwamba maneno hayo yalimvunja moyo sana Ayubu, sivyo? Basi usikubali Shetani akuvunje moyo. Kwa upande mwingine, jihadhari na hila za Shetani ili uwe na ujasiri na nguvu za kujitahidi hata zaidi kufanya yaliyo sawa. (2 Wakorintho 2:11) Yehova alimsahihisha Ayubu, hata hivyo alimpa thawabu pia kwa sababu ya uvumilivu wake kwa kumpa mara mbili ya vitu vyote alivyokuwa amepoteza.—Ayubu 42:10.

Yehova “Ni Mkuu Kuliko Mioyo Yetu”

18, 19. Mungu ni “mkuu kuliko mioyo yetu” jinsi gani, naye “anajua mambo yote” kwa njia gani?

18 Ni kweli kwamba si rahisi kushinda hisia za kuvunjika moyo ikiwa zimetia mizizi. Hata hivyo, roho ya Yehova inaweza kukusaidia hatua kwa hatua kupindua ‘ngome zenye nguvu ambazo zimeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.’ (2 Wakorintho 10:4, 5) Unapolemewa na hisia zisizofaa, tafakari maneno haya ya mtume Yohana: “Kwa jambo hili tutajua kwamba sisi tunatokana na kweli, nasi tutaihakikishia mioyo yetu mbele zake kwa habari ya lolote ambalo huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.”—1 Yohana 3:19, 20.

19 Maneno “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu” yanamaanisha nini? Nyakati nyingine, moyo wetu unaweza kutuhukumu, hasa tunapozingatia sana udhaifu na kutokamilika kwetu na kuhisi kwamba hatustahili. Au huenda ikawa kwamba kwa sababu ya malezi yetu tunakuwa na mwelekeo wenye kupita kiasi wa kujiona hatufai, na kwamba hatuwezi kamwe kumpendeza Yehova. Maneno ya mtume Yohana yanatuhakikishia kwamba Yehova anaelewa hisia hizo kuliko tunavyozielewa! Hakazii uangalifu makosa yetu. Anaona sifa zetu nzuri. Anajua pia nia na makusudi yetu. Daudi aliandika hivi: “Yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Ndiyo, Yehova anatujua vizuri zaidi kuliko tunavyojijua wenyewe!

“Taji la Urembo” na “Kilemba cha Kifalme”

20. Kulingana na unabii wa Isaya wa kurudishwa, Yehova anawaonaje watumishi wake?

20 Kupitia nabii Isaya, Yehova aliwapa watu wake wa kale tumaini la kurudishwa. Wakiwa wamevunjika moyo kwa sababu ya kupelekwa utekwani huko Babiloni, walihitaji sana faraja na uhakikisho huo! Akitabiri kuhusu wakati ambapo wangerudishwa katika nchi yao, Yehova alisema: “Utakuwa taji la urembo mkononi mwa Yehova, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.” (Isaya 62:3) Kwa maneno hayo, Yehova aliwatukuza watu wake na kuwapa heshima. Amelifanyia vivyo hivyo taifa la Israeli wa kiroho leo. Ni kana kwamba aliwakweza ili watu wote wawaone.

21. Unawezaje kuwa na hakika kwamba Yehova atakupa thawabu kwa sababu ya kuvumilia kwa uaminifu?

21 Ingawa unabii huo unatimizwa hasa kuhusiana na watiwa-mafuta, unaonyesha heshima ambayo Yehova anawapa wote wanaomtumikia. Basi unapohisi hustahili, kumbuka kwamba unaweza kuwa mwenye thamani kwa Yehova kama “taji la urembo” na “kilemba cha kifalme” licha ya kwamba wewe si mkamilifu. Kwa hiyo, endelea kuufanya moyo wake ushangilie kwa kujitahidi kabisa kufanya mapenzi yake. (Methali 27:11) Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakupa thawabu kwa sababu ya kuvumilia kwa uaminifu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

Je, Unakumbuka?

• Sisi ni “mali ya pekee” ya Yehova jinsi gani?

• Kwa nini ni muhimu kumwona Yehova kuwa Mthawabishaji?

• Tunapaswa kujilinda kutokana na “hila” gani za Shetani?

• Mungu ni “mkuu kuliko mioyo yetu” jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Paulo

[Picha katika ukurasa wa 26]

Eliya

[Picha katika ukurasa wa 26]

Hana

[Picha katika ukurasa wa 28]

Neno la Mungu lina mambo mengi yanayofariji