Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utatoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu?

Je, Utatoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu?

Je, Utatoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu?

‘Tunatoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.’—2 WAKORINTHO 3:18.

1. Musa aliona nini, na ni nini kilichotukia baadaye?

NI MOJAWAPO ya maono yenye kuogopesha sana ambayo mwanadamu amewahi kuona. Akiwa peke yake juu ya Mlima Sinai, Musa alitoa ombi lisilo la kawaida ambalo lilikubaliwa. Aliruhusiwa kuona jambo ambalo hakuna mwanadamu mwingine yeyote aliwahi kuona, yaani, utukufu wa Yehova. Ni kweli kwamba Musa hakumwona Yehova moja kwa moja. Sura ya Mungu ni yenye utukufu mwingi sana hivi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumwona na kuendelea kuishi. Lakini Yehova aliweka “mkono” wake juu ya Musa kama kisitiri cha kumlinda mpaka Alipopita, huku akitumia malaika. Kisha Yehova akamruhusu Musa kuona mwangaza uliobaki baada ya wonyesho huo wa utukufu Wake. Pia, Yehova alizungumza na Musa kupitia malaika. Biblia inaeleza kilichotukia baadaye inaposema: “Sasa ikawa kwamba Musa alipoteremka kutoka katika Mlima Sinai, . . . ngozi ya uso wake ilikuwa ikitoa miale kwa sababu alikuwa amesema [na Yehova].”—Kutoka 33:18–34:7, 29.

2. Mtume Paulo aliandika nini kuhusu utukufu ambao Wakristo hutoa mrudisho wake?

2 Hebu wazia ukiwa juu ya mlima huo pamoja na Musa. Inaweza kusisimua kama nini kuona utukufu wenye kustaajabisha wa Mweza-Yote na kusikiliza maneno yake! Linaweza kuwa pendeleo kubwa kama nini kuteremka Mlima Sinai pamoja na Musa, mpatanishi wa agano la Sheria! Lakini, je, ulijua kwamba kwa njia fulani Wakristo wa kweli hutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko Musa? Wazo hilo lenye kuamsha fikira linazungumziwa katika barua fulani iliyoandikwa na mtume Paulo. Aliandika kwamba Wakristo watiwa-mafuta ‘hutoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.’ (2 Wakorintho 3:7, 8, 18) Kwa njia fulani, Wakristo walio na tumaini la kuishi duniani hutoa pia mrudisho wa utukufu wa Mungu.

Jinsi Wakristo Wanavyotoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu

3. Ni kwa njia gani tumejua mambo fulani kumhusu Yehova ambayo Musa hakuyajua?

3 Tunawezaje kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu? Hatujamwona wala kumsikia Yehova kwa njia ambayo Musa alimwona na kumsikia. Hata hivyo, tumejua mambo fulani kumhusu Yehova ambayo Musa hakuyajua. Yesu alikuja akiwa Masihi miaka 1,500 hivi baada ya Musa kufa. Hivyo, Musa hangeweza kujua jinsi ambavyo Sheria ingetimia kuhusiana na Yesu, ambaye alikufa ili kuwakomboa wanadamu kutokana na utawala mkatili wa dhambi na kifo. (Waroma 5:20, 21; Wagalatia 3:19) Isitoshe, Musa alijua kwa kiasi fulani tu kusudi tukufu la Yehova, ambalo linahusiana sana na Ufalme wa Kimasihi, na Paradiso ya kidunia itakayoletwa na Ufalme huo. Hivyo, tunaona utukufu wa Yehova, si kwa macho yetu halisi, bali kwa macho ya imani inayotegemea mafundisho ya Biblia. Zaidi ya hayo, tumeisikia sauti ya Yehova, si kupitia malaika, bali kupitia Biblia, na hasa kupitia vitabu vya Injili ambavyo vinaeleza kwa njia bora sana mafundisho na huduma ya Yesu.

4. (a) Wakristo watiwa-mafuta hutoaje mrudisho wa utukufu wa Mungu? (b) Ni kwa njia zipi wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?

4 Ingawa Wakristo hawatoi mrudisho wa utukufu wa Mungu kupitia miale inayong’aa usoni, nyuso zao hung’aa kwa kiasi fulani wanapowaeleza wengine kuhusu utu mtukufu wa Yehova na makusudi yake matukufu. Kuhusu siku zetu, nabii Isaya alitabiri kwamba watu wa Mungu “hakika watatangaza juu ya utukufu [wa Yehova] kati ya mataifa.” (Isaya 66:19) Isitoshe, kwenye 2 Wakorintho 4:1, 2, tunasoma hivi: “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii . . . tumeyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu, si kutembea kwa ujanja, wala kulichanganya na kitu neno la Mungu, bali kwa kufanya kweli iwe wazi tukijipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.” Paulo alikuwa akizungumza hasa kuhusu Wakristo watiwa-mafuta, ambao ni “wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:6) Lakini huduma yao imewachochea watu wengi sana ambao wamepata tumaini la kuishi milele duniani. Huduma ya vikundi hivyo viwili inatia ndani kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia mafundisho yao na pia kupitia matendo yao. Tuna daraka na pendeleo la kutoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Mungu Aliye Juu Zaidi!

5. Ufanisi wetu wa kiroho unathibitisha nini?

5 Leo, kama vile Yesu alivyotabiri, habari njema tukufu za Ufalme wa Mungu zinahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wa mataifa yote, makabila, vikundi vya watu, na lugha wamekubali kwa uchangamfu habari njema hizo na wamebadili maisha yao ili wafanye mapenzi ya Mungu. (Waroma 12:2; Ufunuo 7:9) Kama vile Wakristo wa karne ya kwanza, hawawezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo wameyaona na kuyasikia. (Matendo 4:20) Leo, watu zaidi ya milioni sita wanatoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, na hiyo ni idadi kubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Je, wewe ni mmoja wao? Ufanisi wa kiroho wa watu wa Mungu unatoa uthibitisho wenye nguvu kwamba Yehova anawabariki na kuwalinda. Tunatambua waziwazi kwamba tuna roho ya Yehova tunapoona majeshi yenye nguvu yaliyosimama dhidi yetu. Acheni sasa tuone sababu zinazounga mkono jambo hilo.

Watu wa Mungu Hawatanyamazishwa

6. Kwa nini unahitaji imani na ujasiri ili kumuunga mkono Yehova?

6 Tuseme umeombwa ufike mahakamani ili utoe ushahidi dhidi ya mhalifu sugu. Unajua kwamba mhalifu huyo ana genge lenye nguvu na kwamba atajitahidi juu chini ili akuzuie usifichue habari zake. Ili utoe ushahidi dhidi ya mhalifu huyo, itakubidi uwe jasiri na uwe na uhakika wa kwamba wenye mamlaka watakulinda. Sisi pia tunakabili hali kama hiyo. Tunapotoa ushahidi kumhusu Yehova na makusudi yake, tunatoa ushahidi dhidi ya Shetani Ibilisi na kumfichua kuwa muuaji na mwongo anayeipotosha dunia yote inayokaliwa. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Unahitaji imani na ujasiri ili kumuunga mkono Yehova na kumpinga Ibilisi.

7. Shetani ana uwezo mwingi kadiri gani, naye hujaribu kufanya nini?

7 Bila shaka, Aliye Mkuu Zaidi ni Yehova. Ana nguvu nyingi sana kuliko Shetani. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza na pia yuko tayari kutulinda tunapomtumikia kwa ushikamanifu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Hata hivyo, Shetani ndiye mtawala wa roho waovu na wa ulimwengu wa wanadamu waliojitenga na Mungu. (Mathayo 12:24, 26; Yohana 14:30) Kwa kuwa ametupwa duniani akiwa na “hasira kali,” Shetani huwapinga vikali watumishi wa Yehova, naye hutumia ulimwengu ulio chini ya uongozi wake kujaribu kuwanyamazisha wale wote wanaohubiri habari njema. (Ufunuo 12:7-9, 12, 17) Anafanyaje hivyo? Anatumia angalau njia tatu.

8, 9. Shetani hutumiaje upendo wa vitu vya kimwili, na kwa nini tunapaswa kuchagua kwa uangalifu watu wa kushirikiana nao?

8 Njia moja ambayo Shetani hutumia ili kutukengeusha ni mahangaiko ya maisha. Watu katika hizi siku za mwisho wanapenda pesa, wanajipenda wenyewe, na wanapenda raha. Hawampendi Mungu. (2 Timotheo 3:1-4) Kwa kuwa wanahangaikia tu shughuli zao za maisha, watu wengi ‘hawajali’ juu ya habari njema tunazowapelekea. Hawataki kujifunza kweli za Biblia. (Mathayo 24:37-39) Mtazamo kama huo unaweza kutuathiri na kutulegeza kiroho. Tukisitawisha upendo kwa ajili ya mali na raha za maisha, upendo wetu kwa Mungu utapoa.—Mathayo 24:12.

9 Hiyo ndiyo sababu Wakristo huchagua kwa uangalifu watu wa kushirikiana nao. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Acheni ‘tutembee’ na wale wanaotoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Inafurahisha sana kufanya hivyo! Tunapokusanyika pamoja na ndugu na dada zetu wa kiroho kwenye mikutano yetu na pindi nyinginezo, tunatiwa moyo na upendo wao, imani yao, shangwe yao, na hekima yao. Ushirika huo unaofaa huimarisha azimio letu la kuendelea kutimiza huduma yetu.

10. Shetani ametumiaje dhihaka juu ya wale wanaotoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?

10 Njia ya pili ambayo Shetani hutumia kujaribu kuwazuia Wakristo wote wasitoe mrudisho wa utukufu wa Mungu ni dhihaka. Mbinu hiyo haitushangazi. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu Kristo alidhihakiwa—alichekwa kwa dharau, alitendewa kwa dharau, na hata akatemewa mate. (Marko 5:40; Luka 16:14; 18:32) Wakristo wa mapema walidhihakiwa pia. (Matendo 2:13; 17:32) Watumishi wa Yehova wa leo hukabili hali kama hiyo. Kulingana na mtume Petro, wangeitwa “manabii wa uwongo.” Petro alitabiri hivi: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki na dhihaka zao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, . . . mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Petro 3:3, 4) Watu wa Mungu hudhihakiwa kwamba wamezubaa. Viwango vya maadili vya Biblia huonwa kuwa vimepitwa na wakati. Wengi huona ujumbe tunaohubiri kuwa upumbavu. (1 Wakorintho 1:18, 19) Kwa kuwa sisi ni Wakristo, huenda tukadhihakiwa shuleni, kazini, na nyakati nyingine hata katika familia. Lakini sisi hatuvunjiki moyo, bali tunaendelea kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa kuhubiri, na kama Yesu tunajua kwamba Neno la Mungu ndiyo kweli.—Yohana 17:17.

11. Shetani ametumiaje mateso ili kujaribu kuwanyamazisha Wakristo?

11 Njia ya tatu ambayo Ibilisi hutumia ili kujaribu kutunyamazisha ni upinzani au mateso. Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mathayo 24:9) Naam, sisi Mashahidi wa Yehova tumekabili mateso makali katika maeneo mengi ya dunia. Tunajua kwamba zamani za kale Yehova alitabiri kutakuwa na chuki, au uadui, kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wanaomtumikia Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:15) Pia tunajua kwamba tukidumisha utimilifu tunapokabili majaribu, tunaunga mkono enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Kujua hilo kunaweza kutuimarisha hata katika hali ngumu sana. Tukiendelea kuazimia kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, hakuna mateso yoyote yatakayotunyamazisha kabisa.

12. Kwa nini tunapaswa kushangilia tunapodumu waaminifu licha ya upinzani wa Shetani?

12 Je, wewe hupinga vishawishi vya ulimwengu na kuwa mwaminifu licha ya dhihaka na upinzani? Ikiwa ndivyo, basi una sababu ya kushangilia. Yesu aliwahakikishia hivi wale ambao wangemfuata: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:11, 12) Uvumilivu wako unaonyesha kwamba una roho takatifu ya Yehova yenye nguvu, na inakuimarisha kutoa mrudisho wa utukufu wake.—2 Wakorintho 12:9.

Yehova Anatusaidia Kuvumilia

13. Ni sababu gani kuu tuliyo nayo ya kuvumilia katika huduma ya Kikristo?

13 Sababu kuu inayotufanya tuvumilie katika huduma ni kwamba tunampenda Yehova na tunafurahia kutoa mrudisho wa utukufu wake. Wanadamu huiga watu ambao wanapenda na kuheshimu, na Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi kuigwa. Kwa sababu ya upendo wake mwingi, alimtuma Mwana wake duniani ili kutoa ushahidi kuhusu kweli na kuwakomboa wanadamu watiifu. (Yohana 3:16; 18:37) Kama Mungu, tunatamani watu wa namna zote wafikie toba na wokovu; na ndiyo sababu tunawahubiria. (2 Petro 3:9) Tamaa hiyo, pamoja na azimio letu la kumwiga Mungu, hutuchochea kuendelea kutoa mrudisho wa utukufu wake kupitia huduma yetu.

14. Yehova hutuimarishaje kuvumilia katika huduma yetu?

14 Hata hivyo, nguvu zetu za kuvumilia katika huduma ya Kikristo hutoka kwa Yehova. Yeye hutusaidia na kutuimarisha kupitia roho yake, tengenezo lake, na Neno lake, Biblia. Yehova ‘huwatolea uvumilivu’ wale wanaotaka kutoa mrudisho wa utukufu wake. Yeye hujibu sala zetu na kutupa hekima ili tukabiliane na majaribu. (Waroma 15:5; Yakobo 1:5) Isitoshe, Yehova haruhusu tupatwe na jaribu lolote ambalo hatuwezi kulihimili. Tukimtegemea Yehova, atafanyiza njia ili tuendelee kutoa mrudisho wa utukufu wake.—1 Wakorintho 10:13.

15. Ni nini kinachotusaidia kuvumilia?

15 Uvumilivu katika huduma yetu huonyesha kwamba tuna roho ya Mungu. Kwa mfano: Tuseme mtu fulani anakuomba uende nyumba kwa nyumba ukiwagawia watu mkate bila malipo. Anakuomba ufanye kazi hiyo kwa wakati wako na ulipie gharama zako. Isitoshe, muda si muda unagundua kwamba ni watu wachache sana wanaotaka mkate wako; wengine hata wanapinga jitihada zako za kuugawa. Je, unaweza kuendelea kufanya kazi hiyo mwezi baada ya mwezi, miaka nenda miaka rudi? Huenda usifanye hivyo. Hata hivyo, huenda umetumia pesa zako na wakati wako ili kuhubiri habari njema kwa bidii kwa miaka mingi, au hata kwa makumi ya miaka. Kwa nini? Hapana shaka ni kwa sababu unampenda Yehova na kupitia roho yake amebariki jitihada zako kwa kukusaidia kuvumilia!

Kazi Itakayokumbukwa

16. Uvumilivu katika huduma utakuwa na matokeo gani kwetu na kwa wale wanaotusikiliza?

16 Huduma ya agano jipya ni zawadi isiyo na kifani. (2 Wakorintho 4:7) Vivyo hivyo, huduma ya Kikristo inayofanywa na kondoo wengine duniani kote ni hazina. Kama vile Paulo alivyomwandikia Timotheo, unapoendelea kuvumilia katika huduma yako, unaweza ‘kujiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.’ (1 Timotheo 4:16) Hebu fikiria maana ya maneno hayo. Habari njema unayohubiri huwapa wengine nafasi ya kuishi milele. Unaweza kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wale unaowasaidia kiroho. Hebu wazia jinsi utakavyofurahia kuishi milele katika Paradiso pamoja na wale uliowasaidia kujifunza juu ya Mungu! Bila shaka, hawatasahau jitihada ulizofanya kuwasaidia. Naam, utapata uradhi mwingi sana!

17. Kwa nini kipindi chetu ni cha pekee sana katika historia ya wanadamu?

17 Unaishi katika kipindi cha pekee sana katika historia ya wanadamu. Habari njema haitahubiriwa tena kamwe katika ulimwengu wa wanadamu waliojitenga na Mungu. Noa aliishi katika ulimwengu kama huo, naye aliuona ukipitilia mbali. Hapana shaka alishangilia kujua kwamba amefanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu kwa kujenga safina iliyomwezesha yeye na familia yake kuokolewa! (Waebrania 11:7) Wewe pia unaweza kushangilia kama yeye. Hebu wazia jinsi utakavyohisi katika ulimwengu mpya utakapokumbuka utendaji wako katika hizi siku za mwisho, huku ukijua kwamba ulifanya yote unayoweza kuendeleza mambo ya Ufalme.

18. Yehova anawatiaje moyo watumishi wake, naye anawahakikishia nini?

18 Basi, acheni tuendelee kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Tukifanya hivyo, tutakumbuka jambo hilo milele. Yehova pia hukumbuka kazi zetu. Biblia inatutia moyo hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu. Lakini tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho, ili msiwe goigoi, bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Waebrania 6:10-12.

Je, Unaweza Kueleza?

• Wakristo hutoaje mrudisho wa utukufu wa Mungu?

• Ni baadhi ya mbinu zipi ambazo Shetani hutumia kujaribu kuwanyamazisha watu wa Mungu?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba tuna roho ya Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Uso wa Musa ulitoa mrudisho wa utukufu

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Tunatoa mrudisho wa utukufu wa Mungu katika huduma yetu