Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Madhara Mabaya ya Kifo

Madhara Mabaya ya Kifo

Madhara Mabaya ya Kifo

“MSICHANA MWENYE UMRI WA MIAKA SITA AJIUA.” Kichwa hicho chenye kushtua katika gazeti fulani kilimhusu msichana mdogo anayeitwa Jackie. Mama yake alikuwa amekufa kutokana na ugonjwa usiotibika. Kabla hajajirusha mbele ya gari-moshi, aliwaambia ndugu zake kwamba anataka ‘kuwa malaika na kuwa pamoja na mama yake.’

Ian alikuwa na umri wa miaka 18 alipomsihi kasisi mmoja amweleze ni kwa nini baba yake alikufa kutokana na kansa. Kasisi alimwambia kwamba kwa sababu baba yake alikuwa mtu mwema, Mungu alimtaka mbinguni. Baada ya kusikia hayo, Ian aliamua hataki kumjua Mungu huyo mkatili. Kwa sababu aliona kwamba maisha hayana kusudi, Ian aliamua kuponda raha. Alianza kunywa pombe na kutumia dawa za kulevya kupindukia. Maisha yake yalikuwa yakienda mrama.

“Walio Hai Wanajua Kwamba Watakufa”

Visa hivyo viwili vyenye kuhuzunisha vinaonyesha jinsi kifo kinavyoweza kuathiri sana maisha ya watu, hasa mpendwa anapokufa ghafula. Sisi sote tunajua kwamba maneno haya ya Biblia ni ya kweli: “Walio hai wanajua kwamba watakufa.” (Mhubiri 9:5) Hata hivyo, watu wengi hawataki kufikiria jambo hilo lenye kuhuzunisha. Vipi wewe? Ijapokuwa sisi sote tunajua kwamba tutakufa, huenda tukawa na shughuli nyingi sana na kukosa kuona umuhimu wa kufikiria kifo ambacho hatutarajii kitatupata karibuni.

Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema hivi: “Watu wengi huogopa kifo nao hujaribu kuepuka kukifikiria.” Hata hivyo, huenda msiba mbaya au ugonjwa hatari ukamlazimisha mtu atambue kwamba anaweza kufa wakati wowote. Au huenda mazishi ya rafiki au mtu wa ukoo yakatukumbusha kwamba sisi sote tutakufa siku moja.

Hata hivyo, katika nchi fulani, waombolezaji kwenye mazishi husema, “Maisha hayana budi kuendelea.” Miaka inapita haraka sana na matatizo yanayosababishwa na uzee hutupata ghafula. Tunapopatwa na matatizo hayo tunajua kwamba kifo kinakaribia. Tunahudhuria mazishi mara nyingi, nasi huhuzunishwa sana wakati marafiki ambao tumewajua tangu tukiwa vijana wanapokufa. Wazee wengi hujiuliza, “Je, kesho itakuwa zamu yangu?”

Swali Muhimu

Hakuna yeyote anayekana kwamba atakufa, lakini huenda asielewe hata kidogo kinachotukia baada ya kifo. Maoni mbalimbali yanayopingana kuhusu kifo yanaweza kumfanya mtu aliye na mashaka akate kauli kwamba hayo yote ni majadiliano ya bure kuhusu jambo lisilojulikana. Mwingine anaweza kuona ni heri aponde raha kwa kuwa hakuna maisha mengine.

Watu wengine hawawezi kuamini kwamba kifo ni mwisho wa kila kitu. Hata hivyo, hawajui ni nini kinachotukia baada ya kifo. Watu fulani wanadhani kwamba wataishi mahali pema milele, hali wengine wanaamini kwamba wataishi tena wakati ujao wakiwa na miili mingine.

Watu waliofiwa hujiuliza, “Wafu wako wapi?” Miaka michache iliyopita, wanachama wa klabu fulani ya kandanda walikuwa wakisafiri kwenda kwenye mashindano wakati lori lilipogongana na basi lao dogo. Basi lao lilibingirika na kuishia kando ya barabara. Wachezaji watano wakafa. Mama ya mchezaji mmoja aliyekufa katika msiba huo ameshindwa kuishi maisha ya kawaida tangu wakati huo. Yeye hutaka kujua mahali alipo mwana wake, naye huenda kwenye kaburi lake kwa ukawaida na kuongea naye kwa saa kadhaa. Anasema hivi kwa huzuni: “Siwezi kuamini kwamba hakuna uhai baada ya kifo, lakini sina uhakika.”

Ni wazi kwamba maoni yetu kuhusu kifo yanaweza kuathiri maisha yetu. Tunapofikiria jinsi watu wanavyotenda na kuhisi wanapofiwa, maswali kadhaa yanazuka. Ungejibuje maswali yafuatayo? Je, ni heri tusifikirie kifo hata kidogo na kuzingatia maisha tu? Je, turuhusu woga wa kifo utudhoofishe? Je, mtu aliyefiwa anaweza kujua mahali ambapo mpendwa wake yupo? Je, tunaweza kujua ukweli kuhusu kifo?