Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika Israeli la kale, ni nini kilichomaanishwa na nuru ya kimuujiza, ambayo wakati mwingine huitwa Shekina, iliyotokea katika Patakatifu Zaidi pa maskani na hekalu?

Yehova, ambaye ni Baba mwenye upendo na Mlinzi wa watu wake, alidhihirisha waziwazi kwamba alikuwepo katikati ya Waisraeli. Njia moja ambayo alifanya hivyo ilikuwa kupitia wingu tukufu ambalo lilihusiana sana na mahali pake pa ibada.

Nuru hiyo iliyoonekana waziwazi ilionyesha kwamba Yehova alikuwepo, ingawa hakuwa anaonekana. Ilionekana katika Patakatifu Zaidi pa maskani na pa hekalu ambayo Sulemani alijenga. Nuru hiyo ya kimuujiza haikumaanisha kwamba Yehova alikuwepo kihalisi. Mungu hawezi kutoshea katika jengo lolote ambalo limefanywa na wanadamu. (2 Mambo ya Nyakati 6:18; Matendo 17:24) Nuru hiyo iliyotokezwa na Mungu katika patakatifu pake ilimpa kuhani mkuu uhakika wa kwamba kuwapo kwa Yehova kuliwapa ulinzi na kuliwatimizia mahitaji yao, naye kuhani mkuu angewahakikishia pia Waisraeli wote jambo hilo.

Katika lugha ya Kiaramu iliyotumiwa baada ya Biblia kuandikwa, nuru hiyo iliitwa Shekina (shekhi·nahʹ), neno linalomaanisha “kile kinachokaa” au “makao.” Neno hilo halionekani katika Biblia, lakini linapatikana katika tafsiri za Kiaramu za Maandiko ya Kiebrania zinazoitwa Targumi.

Alipokuwa akitoa maagizo ya kujenga maskani, Yehova alimwambia Musa hivi: “Utakiweka kifuniko hicho juu ya Sanduku, na ndani ya Sanduku utaweka ushuhuda nitakaokupa. Nami nitakutokea hapo na kusema nawe toka juu ya kifuniko hicho, toka katikati ya wale makerubi wawili walio juu ya sanduku.” (Kutoka 25:21, 22) Sanduku linalotajwa hapo ni lile lililokuwa na kifuniko cha dhahabu ndani ya Patakatifu Zaidi. Palikuwa na makerubi wawili wa dhahabu juu ya kifuniko cha Sanduku hilo.

Yehova angezungumza kutoka wapi? Alijibu swali hilo alipomwambia Musa hivi: “Nitaonekana katika wingu juu ya kifuniko hicho.” (Mambo ya Walawi 16:2) Wingu hilo lilielea juu ya Sanduku takatifu katikati ya makerubi wawili wa dhahabu. Biblia haisemi wingu hilo lilikuwa na urefu wa kadiri gani au umbali wake juu ya makerubi ulifikia wapi.

Wingu hilo jangavu liliangazia Patakatifu Zaidi. Kwa kweli, ni lenyewe tu ndilo lililoangazia chumba hicho. Nuru hiyo ilimwezesha kuhani mkuu kuona alipoingia katika chumba cha ndani zaidi Siku ya Upatanisho. Alikuwa akisimama mbele za Yehova.

Je, nuru hiyo ya kimuujiza inamaanisha chochote kwa Wakristo? Mtume Yohana aliona katika maono jiji ambalo ndani yake “usiku hautakuwa humo.” Jiji hilo ni Yerusalemu Jipya, ambalo linafanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta waliofufuliwa ili kutawala pamoja na Yesu. Nuru ya jiji hilo la mfano haitokani na jua wala mwezi. Utukufu wa Yehova Mungu ndio unaoangazia moja kwa moja tengenezo hilo, kama vile tu wingu la Shekina lilivyoangazia Patakatifu Zaidi. Pia, Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, ndiye “taa” ya jiji hilo. Kwa upande mwingine, “jiji” hilo linaangaza nuru yake ya kiroho na wema juu ya watu waliokombolewa kutoka katika mataifa yote ili kuwaongoza.—Ufunuo 21:22-25.

Kwa sababu wanapokea baraka nyingi hizo kutoka kwa Mungu, waabudu wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika kwamba yeye ni Mchungaji wao anayewalinda na Baba anayewapenda.