Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sheria ya Upendo Katika Mioyo

Sheria ya Upendo Katika Mioyo

Sheria ya Upendo Katika Mioyo

“Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao.”—YEREMIA 31:33.

1, 2. (a) Tutazungumzia nini sasa? (b) Yehova alijionyeshaje kwenye Mlima Sinai?

KATIKA makala mbili zilizotangulia, tulijifunza kwamba wakati Musa aliposhuka Mlima Sinai, uso wake ulitoa miale ya mrudisho wa utukufu wa Yehova. Pia tulizungumzia utaji ambao Musa alijifunika. Sasa, hebu tuzungumzie jambo lingine linalohusiana na mambo hayo, ambalo ni muhimu kwa Wakristo leo.

2 Musa alipokuwa mlimani, alipokea maagizo kutoka kwa Yehova. Wakiwa wamekusanyika mbele ya Mlima Sinai, Waisraeli walishuhudia wonyesho wa kustaajabisha wa Mungu mwenyewe. “Mingurumo na umeme zikaanza kutokea, na wingu zito juu ya mlima na sauti kubwa sana ya pembe, hivi kwamba watu wote waliokuwa kambini wakaanza kutetemeka. . . . Nao Mlima Sinai ukatoa moshi kila mahali, kwa kuwa Yehova alikuwa ameshuka juu yake katika moto; na moshi wake ukawa ukipaa kama moshi wa tanuru, na mlima wote ulikuwa ukitetemeka sana.”—Kutoka 19:16-18.

3. Yehova aliwapa Waisraeli zile Amri Kumi kwa njia gani, na taifa hilo lilipata kuelewa nini?

3 Yehova aliongea na watu kupitia malaika na kutoa zile sheria zinazojulikana kuwa Amri Kumi. (Kutoka 20:1-17) Hivyo, hapakuwa na shaka yoyote kwamba sheria hizo zilitoka kwa Mweza-Yote. Yehova aliandika amri hizo juu ya mabamba ya mawe. Musa aliyavunja-vunja mabamba hayo alipowaona Waisraeli wakiabudu ndama ya dhahabu. Yehova aliandika tena amri hizo juu ya mawe. Wakati huu, Musa alipokuwa akishuka mlima akiwa amebeba mabamba hayo, uso wake ulitoa miale. Kufikia wakati huo, watu wote wangeweza kuelewa kwamba sheria hizo zilikuwa muhimu sana.—Kutoka 32:15-19; 34:1, 4, 29, 30.

4. Kwa nini zile Amri Kumi zilikuwa muhimu sana?

4 Yale mabamba mawili ambapo zile Amri Kumi ziliandikwa yaliwekwa ndani ya sanduku la agano katika Patakatifu Zaidi pa ile maskani na baadaye yaliwekwa katika Patakatifu Zaidi pa hekalu. Sheria zilizoandikwa kwenye mabamba hayo zilikuwa na kanuni kuu za agano la Sheria ya Musa na zilikuwa msingi wa jinsi ambavyo Mungu angelitawala taifa la Israeli. Zilionyesha kwamba Yehova anashughulika na watu fulani hususa, watu waliochaguliwa.

5. Sheria za Mungu kwa Waisraeli zilionyeshaje upendo wake?

5 Sheria hizo zilifunua mengi kumhusu Yehova, hasa jinsi anavyowapenda watu wake. Wale waliozitii waliziona kuwa zawadi yenye thamani kubwa sana! Msomi mmoja aliandika hivi: “Hakuna mfumo wowote wa maadili uliotungwa na wanadamu kabla ya wakati huo au tangu wakati huo . . . unaoweza kukaribia, kuwa sawa, au kuwa bora kuliko maneno hayo kumi ya Mungu.” Yehova alisema hivi kuhusu Sheria ya Musa kwa ujumla: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.”—Kutoka 19:5, 6.

Sheria Iliyoandikwa Moyoni

6. Ni sheria gani ambayo imekuwa na thamani kubwa zaidi kuliko sheria zilizoandikwa juu ya mawe?

6 Naam, sheria hizo kutoka kwa Mungu zilikuwa zenye thamani sana. Lakini, je, ulijua kwamba Wakristo watiwa-mafuta wana kitu chenye thamani zaidi kuliko sheria zilizoandikwa juu ya mawe? Yehova alitabiri kuhusu kufanyizwa kwa agano jipya ambalo lilikuwa tofauti na agano la Sheria lililofanywa pamoja na taifa la Israeli. “Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao.” (Yeremia 31:31-34) Yesu, Mpatanishi wa agano jipya, hakuwapa wafuasi wake moja kwa moja sheria zilizoandikwa. Alikazia sheria ya Yehova katika akili na mioyo ya wanafunzi wake kupitia mambo aliyosema na kufanya.

7. Ni nani waliokuwa wa kwanza kupewa “sheria ya Kristo,” na ni nani walioanza kuifuata baadaye?

7 Sheria hiyo inaitwa “sheria ya Kristo.” Watu wa kwanza kupewa sheria hiyo si Waisraeli wa asili, ambao walikuwa wazao wa Yakobo, bali ni taifa la kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:2, 16; Waroma 2:28, 29) Israeli wa Mungu limefanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Baadaye, “umati mkubwa” kutoka katika mataifa yote, ambao pia unajitahidi kumwabudu Yehova, ulijiunga nao. (Ufunuo 7:9, 10; Zekaria 8:23) Wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” vikundi vyote viwili vinafuata “sheria ya Kristo” na kuiruhusu iongoze mambo yote wanayofanya.—Yohana 10:16.

8. Kuna tofauti gani kati ya Sheria ya Musa na sheria ya Kristo?

8 Tofauti na Waisraeli wa asili, ambao walipaswa kuifuata Sheria ya Musa kwa sababu walizaliwa katika taifa la Israeli, Wakristo wanaendelea kuifuata sheria ya Kristo kwa hiari yao, na mambo kama vile jamii au mahali pa kuzaliwa hayatiliwi maanani. Wanajifunza kumhusu Yehova na njia zake na wanatamani kufanya mapenzi yake. Kwa kuwa sheria ya Mungu imo “ndani yao,” kana kwamba imeandikwa “katika moyo wao,” Wakristo watiwa-mafuta hawamtii Mungu kwa sababu tu anaweza kuwaadhibu wale wasiotii wala hawamtii ili kutimiza tu wajibu. Utii wao unategemea msingi thabiti na wenye nguvu sana, na wale wa kondoo wengine wanatii kwa sababu hiyohiyo, yaani, sheria ya Mungu imo katika mioyo yao.

Sheria Zinazotegemea Upendo

9. Yesu alionyeshaje kwamba sheria za Yehova zilitegemea upendo?

9 Sheria zote za Yehova na masharti yake yanategemea jambo moja: upendo. Sikuzote jambo hilo limekuwa na litakuwa sehemu muhimu ya ibada safi. Yesu alipoulizwa ni ipi iliyo amri kuu zaidi ya Sheria, yeye alisema hivi: “Umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” Amri ya pili ni hii: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Kisha akasema: “Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.” (Mathayo 22:35-40) Hivyo, Yesu alionyesha kwamba si Sheria na zile Amri Kumi tu zilizotegemea upendo, bali ni Maandiko yote ya Kiebrania.

10. Tunajuaje kwamba upendo ndio msingi wa sheria ya Kristo?

10 Je, kumpenda Mungu na jirani ndio msingi wa sheria iliyo katika mioyo ya Wakristo? Bila shaka! Sheria ya Kristo inahusisha kumpenda Mungu kutoka moyoni na inatia ndani amri mpya, yaani, Wakristo wanapaswa kuonyeshana upendo wa kujidhabihu. Wanapaswa kupendana kama vile Yesu alivyofanya, hata akatoa uhai wake kwa hiari kwa ajili ya rafiki zake. Aliwafundisha wanafunzi wake kumpenda Mungu na kupendana kama vile alivyowapenda. Upendo mwingi ambao wanaonyeshana ndio sifa kuu zaidi inayowatambulisha Wakristo wa kweli. (Yohana 13:34, 35; 15:12, 13) Yesu hata aliwafundisha wapende adui zao.—Mathayo 5:44.

11. Yesu alionyeshaje upendo kwa Mungu na kwa wanadamu?

11 Yesu aliweka mfano mkamilifu wa kuonyesha upendo. Akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu mbinguni, alikubali kwa hiari kuja duniani kuendeleza kazi za Baba yake. Zaidi ya kutoa uhai wake akiwa mwanadamu ili watu wengine waishi milele, aliwaonyesha watu jinsi wanavyopaswa kuishi. Alikuwa mnyenyekevu, mwenye fadhili, na mwenye kujali na aliwasaidia wale waliolemewa na kuonewa. Pia alisema “maneno ya uzima wa milele” na kwa bidii aliwasaidia wengine wamjue Yehova.—Yohana 6:68.

12. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba upendo kwa Mungu na kwa jirani unahusiana sana?

12 Upendo kwa Mungu na kwa jirani unahusiana sana. Mtume Yohana alisema hivi: “Upendo unatoka kwa Mungu . . . Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yohana 4:7, 20) Yehova ndiye chanzo cha upendo na ndiye mfano bora wa sifa hiyo. Kila kitu anachofanya huchochewa na upendo. Sisi huwaonyesha wengine upendo kwa sababu tuliumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:27) Tunapoonyesha upendo kwa jirani zetu, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu.

Kupenda Kunamaanisha Kutii

13. Ili tumpende Mungu, tunapaswa kufanya nini kwanza?

13 Tunawezaje kumpenda Mungu, ambaye hatuwezi kumwona? Hatua ya kwanza muhimu ni kumjua. Hatuwezi kumpenda wala kumwamini mtu tusiyemjua. Hivyo, Neno la Mungu linatutia moyo tumjue Mungu kwa kusoma Biblia, kusali, na kushirikiana na wale ambao tayari wanamjua na kumpenda. (Zaburi 1:1, 2; Wafilipi 4:6; Waebrania 10:25) Vile vitabu vinne vya Injili ni muhimu sana, kwa kuwa vinafunua utu wa Yehova kupitia maisha na huduma ya Yesu Kristo. Tamaa yetu ya kumtii Mungu na kuiga utu wake huimarika zaidi tunapomjua na kuthamini upendo aliotuonyesha. Naam, kumpenda Mungu kunahusisha kutii.

14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba sheria za Mungu si mzigo mzito?

14 Tunapowapenda wengine, tunajua mambo wanayopenda na wasiyopenda, nasi tunatenda kupatana na ujuzi huo. Hatutaki kuwachukiza wale tunaowapenda. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Amri hizo si mzigo mzito wala si nyingi mno. Upendo hutuongoza maishani. Hatuhitaji kutia akilini sheria nyingi ili zituongoze katika kila jambo. Badala yake, tunaongozwa na upendo wetu kwa Mungu. Tunapompenda Mungu, tunafurahia kufanya mapenzi yake. Hivyo, tunapata kibali cha Mungu na tunajifaidi wenyewe kwa sababu mwongozo wake ni wenye faida sikuzote.—Isaya 48:17.

15. Ni nini kitakachotuchochea kumwiga Yehova? Eleza.

15 Kumpenda Mungu hutuchochea kuiga sifa zake. Tunapompenda mtu, tunavutiwa na sifa zake na kujitahidi kuwa kama yeye. Fikiria uhusiano kati ya Yehova na Yesu. Walikuwa pamoja mbinguni, labda kwa mabilioni ya miaka. Walipendana sana bila ubinafsi. Yesu alimwiga Baba yake wa mbinguni kwa ukamili sana hivi kwamba aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Tunapozidi kumjua na kumthamini Yehova na Mwana wake, tunachochewa kuwa kama wao. Upendo wetu kwa Yehova, pamoja na msaada wake wa roho takatifu, utatusaidia ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na kujivika utu mpya.’—Wakolosai 3:9, 10; Wagalatia 5:22, 23.

Kuonyesha Upendo kwa Matendo

16. Upendo wetu kwa Mungu na kwa jirani unaonyeshwaje na kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha?

16 Tukiwa Wakristo, sisi huruhusu upendo wetu kwa Mungu na kwa jirani utuchochee kuhubiri juu ya Ufalme na kufanya wanafunzi. Tunapofanya hivyo, tunampendeza Yehova Mungu, “ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Hivyo, tunaweza kupata shangwe tunapowasaidia wengine ili sheria ya Kristo iandikwe katika mioyo yao. Na tunafurahia kuona wakibadili nyutu zao na kuonyesha sifa za Yehova. (2 Wakorintho 3:18) Kwa kweli, zawadi yenye thamani zaidi ambayo tunaweza kuwapa wengine ni kuwasaidia kumjua Mungu. Wale wanaokubali urafiki pamoja na Yehova wanaweza kuufurahia milele.

17. Kwa nini ni jambo la hekima kusitawisha upendo kwa Mungu na kwa jirani badala ya kupenda vitu vya kimwili?

17 Tunaishi katika ulimwengu ambamo vitu vya kimwili huthaminiwa sana, na hata kupendwa. Hata hivyo, vitu hivyo haviwezi kudumu milele. Vinaweza kuibwa au kuharibika. (Mathayo 6:19) Biblia inatuonya hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:16, 17) Naam, Yehova atadumu milele, na wale wanaompenda na kumtumikia watadumu milele pia. Hivyo basi, je, si jambo la hekima kusitawisha upendo kwa Mungu na kwa watu badala ya kufuatia vitu vya ulimwengu ambavyo havidumu?

18. Mmishonari mmoja alionyeshaje upendo wa kujidhabihu?

18 Wale wanaofuatia upendo humletea Yehova sifa. Fikiria mfano wa Sonia, ambaye ni mmishonari huko Senegal. Alijifunza Biblia pamoja na mwanamke anayeitwa Heidi, ambaye alikuwa ameambukizwa virusi vya UKIMWI na mume wake asiyeamini. Baada ya mume wake kufa, Heidi alibatizwa, lakini muda si muda afya yake ikadhoofika naye akalazwa hospitalini akiugua UKIMWI. Sonia anasema: “Wafanyakazi hospitalini walijitahidi juu chini, lakini walikuwa wachache. Washiriki wa kutaniko waliombwa wajitolee kumshughulikia Heidi hospitalini. Usiku wa pili, nilikalia mkeka kando ya kitanda cha Heidi na kumshughulikia mpaka alipokufa. Daktari aliyesimamia matibabu alisema hivi: ‘Tatizo letu kubwa ni kwamba mara nyingi hata watu wa ukoo huwaacha watu wao wakati wanapojua kwamba wana UKIMWI. Kwa nini wewe unakubali kujihatarisha kwa niaba yake na huna uhusiano wowote naye wala hutoki katika nchi moja wala jamii moja naye?’ Nilimweleza daktari huyo kwamba kwa maoni yangu Heidi ni dada yangu na ni kana kwamba tuna mama na baba mmoja. Kwa sababu nilimwona kuwa dada yangu, nilifurahia kumtunza.” Sonia hakupata madhara yoyote kwa kumtunza Heidi kwa upendo.

19. Tukiwa na sheria ya Mungu katika mioyo yetu, tunapaswa kufanya nini?

19 Watumishi wengi wa Yehova wameonyesha upendo wa kujidhabihu. Leo, watu wa Mungu hawatambuliwi kwa sheria zilizoandikwa. Badala yake, tunaona utimizo wa maneno ya Waebrania 8:10: “‘Hili ndilo agano nitakalofanya pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo,’ asema Yehova. ‘Nitazitia sheria zangu katika akili yao, nami nitaziandika katika mioyo yao. Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.’” Acheni sikuzote tuthamini sheria ya upendo ambayo Yehova ameandika katika mioyo yetu, na kutumia kila nafasi tunayopata kuonyesha upendo.

20. Kwa nini sheria ya Kristo ni kitu chenye thamani kubwa sana?

20 Ni pendeleo kubwa sana kumtumikia Mungu pamoja na akina ndugu na dada zetu ulimwenguni pote ambao wanaonyesha upendo huo! Wale walio na sheria ya Kristo katika moyo wao wana kitu chenye thamani kubwa sana katika ulimwengu huu usio na upendo. Hawafurahii tu kupendwa na Yehova, bali wanafurahia pia upendo wenye nguvu ulio kati yao. “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” Ingawa Mashahidi wa Yehova wanapatikana katika nchi nyingi, wanazungumza lugha nyingi, na wana utamaduni tofauti-tofauti, wanafurahia umoja wa kidini usio na kifani. Umoja huo huleta kibali cha Yehova. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Huko [kati ya watu waliounganishwa na upendo] Yehova aliamuru baraka iwepo, naam, uzima mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 133:1-3.

Je, Unaweza Kujibu?

• Zile Amri Kumi zilikuwa muhimu kadiri gani?

• Ni nini ile sheria iliyoandikwa katika mioyo?

• Upendo una sehemu gani katika “sheria ya Kristo”?

• Tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Waisraeli walikuwa na sheria zilizoandikwa juu ya mabamba ya mawe

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wakristo wana sheria ya Mungu katika mioyo yao

[Picha katika ukurasa wa 28]

Sonia pamoja na msichana kutoka Senegal kwenye kusanyiko la wilaya la 2004