Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafsiri ya Royal Bible—Hatua Kubwa Katika Usomi

Tafsiri ya Royal Bible—Hatua Kubwa Katika Usomi

Tafsiri ya Royal Bible—Hatua Kubwa Katika Usomi

MELI moja iliondoka Hispania ikielekea peninsula ya Italia mapema katika karne ya 16. Katika sehemu ya chini ya meli hiyo kulikuwa na mizigo yenye thamani sana, yaani, karibu nakala zote zilizochapishwa kati ya mwaka wa 1514 na 1517 za tafsiri ya Complutensian Polyglot. Kwa ghafula, kukawa na dhoruba kali. Wafanyakazi wa meli hiyo walijitahidi kuiokoa, lakini jitihada zao hazikufanikiwa. Meli hiyo ikazama pamoja na mizigo yake yenye thamani.

Kwa sababu ya msiba huo, chapa mpya ya Biblia ya Polyglot ilihitajiwa. Mwishowe, Christophe Plantin, mchapishaji mwenye ustadi, alikubali kufanya kazi hiyo ngumu. Alihitaji mtu tajiri wa kugharimia kazi hiyo kubwa. Hivyo, akamwomba mfalme wa Hispania, Philip wa 2, aitegemeze kirasmi kazi hiyo. Kabla ya kukubali, mfalme aliuliza maoni ya wasomi mbalimbali wa Hispania, kati yao akiwemo msomi mashuhuri wa Biblia Benito Arias Montano. Msomi huyo alimwambia Mfalme Philip hivi: “Zaidi ya kumtolea Mungu utumishi na kufaidi Kanisa Katoliki, kazi hiyo itamletea pia Mtukufu Mfalme sifa nyingi na heshima.”

Kutokeza chapa iliyorekebishwa ya tafsiri ya Complutensian Polyglot kungekuwa hatua muhimu katika jamii. Hivyo, Philip akaamua kuutegemeza kabisa mradi wa Plantin. Alimkabidhi Arias Montano kazi kubwa ya kuchapisha tafsiri ambayo baadaye iliitwa Royal Bible, au tafsiri ya Antwerp Polyglot. *

Philip alipendezwa sana na maendeleo ya kazi ya kutafsiri Biblia ya Polyglot hivi kwamba akaomba awe akipokea kila ukurasa ili asahihishe. Bila shaka, Plantin hakutaka kazi yake icheleweshwe kwa kuituma Hispania ili Mfalme Philip aisahihishe kisha asubiri isafirishwe tena hadi Antwerp. Mwishowe, Philip alipokea tu karatasi ya kwanza iliyochapwa na labda baadhi ya kurasa za kwanza-kwanza. Wakati huohuo, Montano aliendelea na kazi ya kusahihisha huku akisaidiwa na maprofesa watatu mashuhuri wa Louvain na binti ya Plantin.

Alipenda Neno la Mungu

Arias Montano alishirikiana vizuri na wasomi wa Antwerp. Plantin alimpenda kwa sababu hakuwa na ubaguzi, nao urafiki na ushirikiano wao ukadumu maisha yao yote. Montano hakuwa tu msomi bora lakini pia alilipenda sana Neno la Mungu. * Akiwa bado kijana, alitaka sana kumaliza masomo yake ili ajitoe kabisa kujifunza Maandiko.

Arias Montano aliamini kwamba tafsiri ya Biblia inapaswa kuwa ya neno kwa neno kwa kadiri iwezekanavyo. Alijitahidi kutafsiri kwa usahihi yale yaliyoandikwa katika maandishi ya awali ili kumpa msomaji nafasi ya kusoma Neno la Mungu lenyewe. Montano alifuata mwito wa Erasmus, aliyewahimiza wasomi “wahubiri kuhusu Kristo kutoka katika maandishi kama yalivyoandikwa katika lugha za awali.” Kwa karne nyingi watu hawakujua maana ya lugha za awali za Biblia kwa sababu hawakuelewa tafsiri za Kilatini.

Kupanga Maandishi ya Tafsiri ya Polyglot

Arias Montano alipata maandishi yote ambayo Alfonso de Zamora alitayarisha na kurekebisha ili kuchapisha tafsiri ya Complutensian Polyglot, kisha akayatumia kwa ajili ya tafsiri ya Royal Bible. *

Mwanzoni tafsiri ya Royal Bible ilikusudiwa kuwa chapa ya pili ya tafsiri ya Complutensian Polyglot, lakini tafsiri hiyo haikufanyiwa marekebisho tu. Maandishi ya Kiebrania na ya Kigiriki ya Septuajinti yaliyokuwa katika tafsiri ya Complutensian Bible ndiyo yaliyotumiwa; kisha maandishi mapya yakaongezwa na pia nyongeza yenye habari nyingi. Hatimaye, tafsiri mpya ya Polyglot ilikuwa na mabuku manane. Kuchapishwa kwa tafsiri hiyo kulichukua miaka mitano, tangu mwaka wa 1568 hadi 1572. Huo ni muda mfupi sana ukilinganishwa na kazi ngumu iliyofanywa. Mwishowe, nakala 1,213 zilichapishwa.

Ingawa tafsiri ya Complutensian Polyglot ya mwaka wa 1517 ilionekana kuwa “kazi bora ya uchapishaji,” tafsiri mpya ya Antwerp Polyglot iliipita ile ya kwanza kwa upande wa usomi na thamani ya habari zilizokuwemo. Ilikuwa hatua nyingine muhimu katika historia ya uchapishaji na, la muhimu zaidi, katika kutayarisha maandishi bora ya Biblia.

Mashambulizi ya Maadui wa Neno la Mungu

Haishangazi kwamba muda mfupi baadaye maadui wa tafsiri sahihi ya Biblia walijitokeza. Ingawa tafsiri ya Antwerp Polyglot ilikubaliwa na papa, na Arias Montano alisifika kuwa msomi anayeheshimiwa, Montano alishtakiwa mbele ya Baraza la Kuhukumu Wazushi. Wapinzani walidai eti tafsiri yake ilionyesha kwamba maandishi ya Kilatini ya Santes Pagninus yaliyorekebishwa upya yalikuwa tafsiri sahihi zaidi ya Kiebrania na Kigiriki cha awali kuliko tafsiri ya Vulgate, iliyotafsiriwa karne nyingi mapema. Pia walimshtaki Montano kuwa alichunguza lugha za awali katika jitihada zake za kutokeza tafsiri sahihi ya Biblia, huku wakiliona jambo hilo kuwa uzushi.

Baraza hilo hata lilisema kwamba “Mfalme hakupata heshima zaidi kwa kugharimia kazi hiyo.” Washiriki wa Baraza hilo walilalamika kwamba Montano hakuiheshimu vya kutosha tafsiri ya Vulgate ambayo ilikubaliwa rasmi. Licha ya mashtaka hayo, hawakupata ushahidi wa kutosha ili kumhukumu Montano au Biblia yake ya Polyglot. Mwishowe, tafsiri ya Royal Bible ilipendwa sana, nayo ikawa tafsiri ya msingi iliyotumiwa katika vyuo mbalimbali.

Kifaa Muhimu Katika Kutafsiri Biblia

Ingawa tafsiri ya Antwerp Polyglot haikukusudiwa kwa ajili ya watu kwa ujumla, baadaye ilikuwa muhimu kwa watafsiri wa Biblia. Kama vile tafsiri iliyoitangulia ya Complutensian Polyglot, tafsiri ya Antwerp Polyglot ilichangia kuboresha maandishi ya Biblia yaliyokuwapo. Pia iliwasaidia watafsiri kuboresha uelewaji wao wa lugha za awali. Tafsiri hiyo ilitumiwa sana kutafsiri Biblia za lugha nyingine kuu za Ulaya. Kwa mfano, kichapo The Cambridge History of the Bible kinaripoti kwamba watafsiri wa tafsiri mashuhuri ya King James Version, au Authorized Version, ya mwaka wa 1611 walitumia sana tafsiri ya Antwerp Polyglot kutafsiri lugha za awali. Tafsiri ya Royal Bible pia ilikuwa na uvutano wenye nguvu juu ya tafsiri mbili muhimu za Polyglot Bible zilizochapishwa katika karne ya 17.—Ona sanduku “Biblia za Polyglot.”

Mojawapo ya faida za tafsiri ya Antwerp Polyglot ni kwamba iliwasaidia wasomi wa Ulaya kupata kwa mara ya kwanza tafsiri ya lugha ya Syriac ya Maandiko ya Kigiriki. Maandishi hayo ya lugha ya Syriac yaliambatanishwa na tafsiri ya neno kwa neno ya Kilatini. Maandishi hayo yaliyoongezwa yalikuwa muhimu sana, kwa kuwa tafsiri ya lugha ya Syriac ilikuwa mojawapo ya tafsiri za kale zaidi za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Tafsiri ya lugha ya Syriac ya karne ya tano W.K., ilitegemea maandishi yaliyoandikwa katika karne ya pili W.K. Kulingana na kichapo The International Standard Bible Encyclopedia, “umuhimu wa tafsiri ya Peshitta [ya lugha ya Syriac] katika uchambuzi wa maandishi ya awali unakubaliwa na wengi. Tafsiri hiyo ni mojawapo ya vyanzo vya habari vya kale zaidi na muhimu sana kuhusu mapokeo ya zamani.”

Wala dhoruba ya bahari wala mashambulizi ya Baraza la Kuhukumu Wazushi la Hispania hayakuzuia tafsiri ya Complutensian Polyglot iliyoboreshwa na iliyoongezwa kutokea tena katika mwaka wa 1572 ikiwa sasa tafsiri ya Royal Bible. Historia ya Biblia ya Polyglot ya Antwerp ni mfano mwingine wa jitihada ambazo watu wanyoofu wamefanya ili kutetea Neno la Mungu.

Iwe walijua hilo au la, kazi isiyo na ubinafsi ya watu hao waliojitolea inaonyesha ukweli wa maneno ya unabii ya Isaya. Yapata miaka elfu tatu iliyopita, aliandika: “Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.”—Isaya 40:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Iliitwa Royal Bible kwa sababu iligharimiwa na Mfalme Philip, na iliitwa Antwerp Polyglot kwa sababu ilichapishwa katika jiji la Antwerp ambalo wakati huo lilikuwa sehemu ya Milki ya Hispania.

^ fu. 7 Alijua vizuri lugha ya Kiarabu, Kigiriki, Kiebrania, Kilatini, na lugha ya Syriac, lugha tano kubwa ambazo zilitumiwa katika tafsiri ya Biblia hiyo ya Polyglot. Alikuwa stadi katika uchunguzi wa vitu vya kale, tiba, sayansi ya mambo ya asili, na theolojia, naye alitumia ustadi huo vizuri katika kutayarisha nyongeza ya Biblia hiyo.

^ fu. 10 Kwa maelezo zaidi kuhusu umuhimu wa tafsiri ya Complutensian Polyglot, ona Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 2004.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

BIBLIA ZA POLYGLOT

“Biblia ya Polyglot ni Biblia ambayo ina maandishi katika lugha mbalimbali,” anaeleza msomi Mhispania Federico Pérez Castro. “Hata hivyo, kwa kawaida, maneno hayo yanarejelea Biblia ambazo maandishi yake yako katika lugha za awali. Kulingana na maelezo hayo, idadi ya Biblia za Polyglot ni ndogo sana.”

1. Tafsiri The Complutensian Polyglot (1514-1517), iliyogharimiwa na Kadinali Cisneros, ilichapishwa huko Alcalá de Henares, Hispania. Mabuku yake sita yalikuwa na maandishi ya Biblia katika lugha nne: Kiebrania, Kigiriki, Kiaramu, na Kilatini. Watafsiri wa karne ya 16 walitumia tafsiri hiyo ya Maandiko ya Kiebrania na Kiaramu kutafsiri lugha nyinginezo.

2. Tafsiri The Antwerp Polyglot (1568-1572), iliyorekebishwa na Benito Arias Montano, iliongeza kwenye maandishi ya Complutensian tafsiri ya Peshitta ya lugha ya Syriac ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na Targumi ya Kiaramu ya Jonathan. Maandishi ya Kiebrania yaliyokuwa na alama za irabu na za matamshi, yalifanyiwa marekebisho kulingana na maandishi ya Kiebrania ya Jacob ben Hayyim. Hivyo, yakawa maandishi ya msingi ya Maandiko ya Kiebrania yaliyotumiwa na watafsiri wa Biblia.

3. Tafsiri The Paris Polyglot (1629-1645) iligharimiwa na mwanasheria Mfaransa Guy Michel le Jay. Ilitegemea tafsiri ya Antwerp Polyglot, ingawa ilikuwa pia na maandishi fulani ya Kisamaria na Kiarabu.

4. Tafsiri The London Polyglot (1655-1657), iliyorekebishwa na Brian Walton, ilitegemea pia tafsiri ya Antwerp Polyglot. Tafsiri hiyo ya Polyglot ilitia ndani tafsiri za kale za Biblia katika Kiethiopia na Kiajemi, ingawa tafsiri hizo hazikusaidia sana kufanya maandishi ya Biblia yaeleweke vizuri.

[Hisani]

Banner and Antwerp Polyglots (two underneath): Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid; Antwerp Polyglot (on top): By courtesy of Museum Plantin-Moretus/Stedelijk Prentenkabinet Antwerpen; London Polyglot: From the book The Walton Polyglot Bible, Vol. III, 1655-1657

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mfalme wa Hispania, Philip wa 2

[Hisani]

Philip II: Biblioteca Nacional, Madrid

[Picha katika ukurasa wa 10]

Arias Montano

[Hisani]

Montano: Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mashini za kuchapishia za awali huko Antwerp, Ubelgiji

[Hisani]

Press: By courtesy of Museum Plantin-Moretus/Stedelijk Prentenkabinet Antwerpen

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kushoto: Christophe Plantin na ukurasa unaoonyesha jina la tafsiri ya “Antwerp Polyglot”

[Hisani]

Title page and Plantin: By courtesy of Museum Plantin-Moretus/Stedelijk Prentenkabinet Antwerpen

[Picha katika ukurasa wa 11]

Juu: Sura ya 15 ya kitabu cha Kutoka katika safu nne za maandishi

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Title page and Plantin: By courtesy of Museum Plantin-Moretus/Stedelijk Prentenkabinet Antwerpen

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid