Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo Hutoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova

Wakristo Hutoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova

Wakristo Hutoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova

“Yenye furaha ni macho yenu kwa sababu hayo yanaona, na masikio yenu kwa sababu hayo yanasikia.”—MATHAYO 13:16.

1. Ni swali gani ambalo linazuka kuhusiana na jinsi Waisraeli walivyotenda walipomwona Musa kwenye Mlima Sinai?

WAISRAELI waliokuwa wamekusanyika kwenye Mlima Sinai walikuwa na sababu nzuri za kumkaribia Yehova. Alikuwa amewakomboa kutoka Misri kwa mkono wenye nguvu. Alihangaikia mahitaji yao kwa kuwaandalia chakula na maji nyikani. Kisha akawapa ushindi juu ya jeshi la Waamaleki lililowashambulia. (Kutoka 14:26-31; 16:2–17:13) Wakiwa wamepiga kambi nyikani mbele ya Mlima Sinai, watu hao waliogopeshwa sana na mingurumo na radi hivi kwamba wakatetemeka. Baadaye, walimwona Musa akishuka kutoka kwenye Mlima Sinai, huku uso wake ukitoa mrudisho wa utukufu wa Yehova. Lakini, badala ya kustaajabu na kuonyesha uthamini, walirudi nyuma. ‘Waliogopa kumkaribia Musa.’ (Kutoka 19:10-19; 34:30) Kwa nini waliogopa kuona mrudisho wa utukufu wa Yehova, yule aliyekuwa amewafanyia mambo mengi sana?

2. Kwa nini huenda Waisraeli waliogopa kuona utukufu wa Mungu ambao Musa alitoa mrudisho wake?

2 Labda woga wa Waisraeli wakati huo ulihusiana sana na mambo yaliyokuwa yametukia awali. Yehova alikuwa amewaadhibu walipomwasi kimakusudi kwa kutengeneza ndama ya dhahabu. (Kutoka 32:4, 35) Je, walijifunza kutokana na nidhamu ya Yehova na kuithamini? La, wengi wao hawakufanya hivyo. Alipokaribia kufa, Musa alizungumzia tena kisa cha ndama ya dhahabu na pindi nyingine ambazo Waisraeli hawakutii. Aliwaambia watu hivi: ‘Mliasi agizo la Yehova Mungu wenu, nanyi hamkumwamini wala hamkuisikiliza sauti yake. Mmejionyesha kuwa wenye tabia ya kumwasi Yehova tangu siku niliyowajua ninyi.’—Kumbukumbu la Torati 9:15-24.

3. Musa alitumiaje utaji?

3 Fikiria jinsi Musa alivyotenda alipoona woga wa Waisraeli. Simulizi hilo linasema: “Musa alipomaliza kusema nao, alikuwa akiweka utaji juu ya uso wake. Lakini Musa alipokuwa akiingia ndani [ya ile maskani] mbele za Yehova kusema naye, alikuwa akiutoa utaji mpaka wakati wa kutoka kwake nje. Naye akatoka nje na kusema na wana wa Israeli mambo aliyokuwa akiamriwa. Nao wana wa Israeli wakauona uso wa Musa, kwamba ngozi ya uso wa Musa ilitoa miale; naye Musa akaurudisha utaji juu ya uso wake mpaka alipoingia ndani kusema [na Yehova].” (Kutoka 34:33-35) Kwa nini nyakati nyingine Musa aliufunika uso wake kwa utaji? Tunajifunza nini kutokana na hilo? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutusaidia kuchunguza uhusiano wetu pamoja na Yehova.

Walikosa Kutumia Nafasi Walizopata

4. Mtume Paulo alifunua nini kuhusu sababu ya Musa ya kujifunika utaji?

4 Mtume Paulo alieleza kwamba sababu ya Musa ya kujifunika utaji ilihusiana na hali ya Waisraeli ya akilini na ya moyoni. Paulo aliandika hivi: “Wana wa Israeli hawakuweza kuutazama uso wa Musa kwa sababu ya utukufu wa uso wake . . . Nguvu zao za akili zilitiwa uzito.” (2 Wakorintho 3:7, 14) Inasikitisha sana! Waisraeli walikuwa watu wa Yehova waliochaguliwa, naye aliwataka wamkaribie. (Kutoka 19:4-6) Hata hivyo, hawakutaka kuutazama sana mrudisho wa utukufu wa Mungu. Badala ya kuelekeza mioyo yao na akili zao kwa Yehova kwa kujitoa kwa upendo, ni kana kwamba walikuwa wamempa kisogo.

5, 6. (a) Kulikuwa na ulinganifu gani kati ya Waisraeli wa karne ya kwanza na wale wa wakati wa Musa? (b) Kulikuwa na tofauti gani kati ya wale waliomsikiliza Yesu na wale ambao hawakumsikiliza?

5 Hali kama hiyo ilitokea katika karne ya kwanza W.K. Kufikia wakati ambapo Paulo aligeuka na kuwa Mkristo, agano jipya lilikuwa limechukua mahali pa agano la Sheria. Yesu Kristo, Musa Mkuu Zaidi, ndiye mpatanishi wa agano jipya. Kwa maneno na kwa matendo, Yesu alitoa kwa ukamili mrudisho wa utukufu wa Yehova. Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu aliyefufuliwa: “Yeye ndiye mng’ao wa utukufu [wa Mungu] na mwakilisho sawasawa wa utu wake wenyewe.” (Waebrania 1:3) Wayahudi walikuwa na nafasi bora sana! Wangeweza kusikiliza maneno ya uzima wa milele kutoka kwa Mwana wa Mungu mwenyewe! Inasikitisha kwamba watu wengi ambao Yesu aliwahubiria hawakumsikiliza. Yesu alizungumza juu yao aliponukuu unabii huu wa Yehova kupitia Isaya: “Moyo wa watu hawa umekuwa mgumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao; ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa maana kwa mioyo yao na kugeuka, nami niwaponye.”—Mathayo 13:15; Isaya 6:9, 10.

6 Kulikuwa na tofauti kubwa kati ya Wayahudi na wanafunzi wa Yesu, ambao Yesu alisema hivi juu yao: “Yenye furaha ni macho yenu kwa sababu hayo yanaona, na masikio yenu kwa sababu hayo yanasikia.” (Mathayo 13:16) Wakristo wa kweli wanatamani kumjua na kumtumikia Yehova. Wanafurahia kufanya mapenzi yake ambayo yanafunuliwa katika Biblia. Kwa hiyo, Wakristo watiwa-mafuta hutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova katika huduma yao ya agano jipya, na wale wa kondoo wengine wanafanya hivyo pia.—2 Wakorintho 3:6, 18.

Kwa Nini Habari Njema Imefunikwa Utaji?

7. Kwa nini haishangazi kwamba watu wengi hukataa habari njema?

7 Kama tulivyoona, katika siku za Yesu na katika siku za Musa, Waisraeli wengi walikataa kutumia nafasi bora waliyokuwa nayo. Hali iko hivyo leo. Watu wengi wanakataa habari njema tunayohubiri. Hilo halitushangazi. Paulo aliandika hivi: “Basi, ikiwa kwa kweli habari njema tunayotangaza imefunikwa utaji, imefunikwa utaji katikati ya wale wanaoangamia, ambao katikati yao mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Zaidi ya jitihada za Shetani za kujaribu kuficha habari njema, watu wengi pia hufunika nyuso zao kwa utaji kwa sababu hawataki kuona.

8. Ni kwa njia gani watu wengi wanapofushwa kwa sababu ya kutojua, nasi tunawezaje kuepuka kuathiriwa kwa njia hiyohiyo?

8 Macho ya mfano ya watu wengi yamepofushwa kwa sababu ya kutojua. Biblia inasema kwamba mataifa yako ‘katika giza kiakili, na yametenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutojua ambako kumo ndani yao.’ (Waefeso 4:18) Kabla ya kuwa Mkristo, Paulo, ambaye aliifahamu sana Sheria, alikuwa amepofushwa sana kwa sababu ya kutojua hivi kwamba alilitesa kutaniko la Mungu. (1 Wakorintho 15:9) Hata hivyo, Yehova alimfunulia ile kweli. Paulo anaeleza hivi: “Sababu iliyofanya nionyeshwe rehema ilikuwa kwamba kupitia mimi nikiwa ndiye wa kwanza kabisa Kristo Yesu aonyeshe ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaokuwa na imani yao kwake kwa ajili ya uzima wa milele.” (1 Timotheo 1:16) Kama vile Paulo, watu wengi ambao zamani waliipinga kweli ya Mungu sasa wanamtumikia Yehova. Hiyo ni sababu nzuri ya kuendelea kuwahubiria hata wale wanaotupinga. Wakati huohuo, tukijifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kulielewa, tutalindwa tusitende kwa kutojua na hivyo kumkasirisha Yehova.

9, 10. (a) Wayahudi wa karne ya kwanza walionyeshaje kwamba walishikilia sana maoni yao na kwamba hawakutaka kufundishwa? (b) Je, hali kama hiyo iko katika dini zinazodai kuwa za Kikristo leo? Eleza.

9 Watu wengi hawaelewi mambo ya kiroho kwa sababu hawataki kufundishwa na wanashikilia sana maoni yao. Wayahudi wengi walimkataa Yesu na mafundisho yake kwa sababu walishikilia kwa ushupavu Sheria ya Musa. Ni kweli kwamba kuna wale waliomkubali. Kwa mfano, baada ya Yesu kufufuliwa, ‘umati mkubwa wa makuhani ulianza kuitii imani.’ (Matendo 6:7) Hata hivyo, Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi wengi: “Mpaka leo wakati wowote maandishi ya Musa yanaposomwa, utaji hukaa juu ya mioyo yao.” (2 Wakorintho 3:15) Yaonekana Paulo alijua kile ambacho Yesu alikuwa amewaambia viongozi wa dini Wayahudi: “Ninyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mnafikiri kwamba kwa njia yake mtakuwa na uzima wa milele; na hayo yenyewe ndiyo yanayotoa ushahidi juu yangu.” (Yohana 5:39) Maandiko ambayo walikuwa wakiyachunguza kwa makini yalipaswa kuwasaidia kuelewa kwamba Yesu ndiye Masihi. Hata hivyo, Wayahudi walikuwa na maoni yao wenyewe, na hata hawakutaka kusadikishwa na Mwana wa Mungu aliyefanya miujiza.

10 Leo, wengi walio katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wako katika hali hiyohiyo. Sawa na Wayahudi wa karne ya kwanza, “wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Ingawa wengine wao hujifunza Biblia, hawataki kuamini yale inayosema. Hawataki kukubali kwamba Yehova huwafundisha watu wake kupitia jamii yake ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ya Wakristo watiwa-mafuta. (Mathayo 24:45) Hata hivyo, sisi tunaelewa kwamba Yehova anawafundisha watu wake na kwamba sikuzote amefunua kweli yake hatua kwa hatua. (Methali 4:18) Tunapokubali kufundishwa na Yehova tunabarikiwa kujua mapenzi yake na kusudi lake.

11. Ukweli umefichwaje kwa sababu ya watu kuamini tu mambo ambayo wanapenda?

11 Wengine wamepofushwa kwa sababu wanataka tu kuamini mambo wanayopenda. Ilitabiriwa kwamba watu fulani watawadhihaki watu wa Mungu na kuudhihaki ujumbe ambao wanatangaza kuhusu kuwapo kwa Yesu. Mtume Petro aliandika hivi: “Kulingana na kupenda kwao, wao hawalioni jambo hili,” kwamba Mungu alileta gharika juu ya ulimwengu wa siku za Noa. (2 Petro 3:3-6) Vivyo hivyo, watu wengi wanaodai kuwa Wakristo hukubali kwa utayari kwamba Yehova huonyesha rehema, fadhili, na msamaha; lakini wanapuuza au kukataa kwamba yeye huwaadhibu wakosaji. (Kutoka 34:6, 7) Wakristo wa kweli hujitahidi kuelewa yale ambayo Biblia hufundisha hasa.

12. Watu wamepofushwaje na mapokeo?

12 Watu wengi wanaoenda kanisani hupofushwa na mapokeo. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa dini wa siku zake: “Mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.” (Mathayo 15:6) Baada ya kurudi kutoka utekwani huko Babiloni, Wayahudi walirudisha ibada safi kwa bidii, lakini makuhani wakawa na kiburi na kujiona kuwa waadilifu. Sherehe za kidini zikawa za kidesturi tu, na hazikufanywa kwa njia iliyoonyesha heshima ya kweli kwa Mungu. (Malaki 1:6-8) Kufikia wakati wa Yesu, waandishi na Mafarisayo walikuwa wameongeza mapokeo mengi sana katika Sheria ya Musa. Yesu alisema wazi kwamba watu hao ni wanafiki kwa sababu hawakufuata tena kanuni adilifu zilizoitegemeza Sheria. (Mathayo 23:23, 24) Ni lazima Wakristo wa kweli wawe waangalifu wasije wakakubali mapokeo ya kidini yaliyotungwa na wanadamu yawakengeushe kutoka katika ibada safi.

‘Kumwona Yeye Asiyeonekana’

13. Musa aliona utukufu wa Mungu kwa kadiri fulani kupitia njia gani mbili?

13 Akiwa mlimani, Musa aliomba aone utukufu wa Mungu, naye akaonyeshwa mwangaza uliobaki wa utukufu wa Yehova. Alipoingia katika ile maskani, hakujifunika utaji. Musa alikuwa na imani yenye nguvu na alitamani kufanya mapenzi ya Mungu. Ingawa alibarikiwa kuona utukufu wa Yehova kwa kadiri fulani katika maono, ni kana kwamba tayari alikuwa amemwona Mungu kwa macho ya imani. Biblia inasema kwamba Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27; Kutoka 34:5-7) Musa alitoa mrudisho wa utukufu wa Mungu si tu kupitia miale iliyotoka usoni pake kwa muda fulani, bali pia kupitia jitihada zake za kuwasaidia Waisraeli kumjua na kumtumikia Yehova.

14. Yesu aliuonaje utukufu wa Mungu, naye alifurahia nini?

14 Akiwa huko mbinguni, Yesu aliuona utukufu wa Mungu moja kwa moja kwa miaka mingi sana, hata kabla ya ulimwengu kuumbwa. (Methali 8:22, 30) Katika kipindi hicho chote, uhusiano wenye upendo mwingi sana ulisitawi. Yehova Mungu alionyesha upendo mwororo zaidi kwa mwana huyo mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote. Yesu pia alionyesha upendo mwingi sana kwa Mungu, ambaye alimpa uhai. (Yohana 14:31; 17:24) Baba na Mwana walionyeshana upendo mkamilifu. Kama vile Musa, Yesu alifurahia kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia mambo aliyofundisha.

15. Ni katika njia gani Wakristo huukazia uangalifu utukufu wa Mungu?

15 Kama vile Musa na Yesu, Mashahidi wa Mungu waliopo duniani leo wanatamani sana kuukazia uangalifu utukufu wa Yehova. Wao hawajakataa habari njema zilizo tukufu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kunapokuwa na tendo la kugeuka kumwelekea Yehova [ili kufanya mapenzi yake], utaji huondolewa mbali.” (2 Wakorintho 3:16) Tunajifunza Maandiko kwa sababu tunataka kufanya mapenzi ya Mungu. Tunavutiwa na utukufu unaoangazwa na uso wa Mwana wa Yehova, Yesu Kristo, ambaye ni Mfalme mtiwa-mafuta, nasi tunaiga mfano wake. Kama vile Musa na Yesu, tumekabidhiwa huduma ya kuwafundisha wengine kuhusu Mungu mtukufu tunayemwabudu.

16. Kwa nini ni pendeleo kubwa kuijua kweli?

16 Yesu alisali hivi: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, . . . kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Yehova huwapa wanyoofu na watu walio wanyenyekevu moyoni uelewaji wa makusudi yake na utu wake. (1 Wakorintho 1:26-28) Anatulinda na kutufundisha jinsi tunavyoweza kufaidika kikamili maishani. Acheni tutumie vizuri kila nafasi tunayopata ya kumkaribia Yehova kwa kuthamini maandalizi yake mengi yanayotusaidia kumjua vizuri zaidi.

17. Tunapataje kujua sifa za Yehova kwa kadiri kubwa zaidi?

17 Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Sisi . . . tunapotoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova tukiwa na nyuso zisizo na utaji, tunageuzwa na kuwa katika mfano uleule kutoka utukufu mpaka utukufu.” (2 Wakorintho 3:18) Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, kadiri tunavyomjua Yehova, yaani, kujua sifa zake na utu wake uliofunuliwa katika Biblia, ndivyo tunavyozidi kuwa kama yeye. Tukitafakari na kuthamini maisha, huduma, na mafundisho ya Yesu Kristo, tutaiga sifa za Yehova kwa kadiri kubwa zaidi. Tunashangilia kama nini kujua kwamba tunamletea sifa Mungu wetu, ambaye tunajitahidi kutoa mrudisho wa utukufu wake! 

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Waisraeli waliogopa kuona utukufu wa Mungu ambao Musa alitoa mrudisho wake?

• Ni kwa njia gani habari njema ‘ilifunikwa utaji’ katika karne ya kwanza? na ‘imefunikwaje utaji’ katika siku zetu?

• Tunatoaje mrudisho wa utukufu wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Waisraeli hawangeweza kuutazama uso wa Musa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kama vile Paulo, watu wengi ambao zamani waliipinga kweli ya Mungu sasa wanamtumikia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 23]

Watumishi wa Yehova hufurahia kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu