Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wangeweza Kuachiliwa Papo Hapo”

“Wangeweza Kuachiliwa Papo Hapo”

“Wangeweza Kuachiliwa Papo Hapo”

GENEVIÈVE DE GAULLE, mpwa wa kike wa Charles de Gaulle, aliyekuwa rais wa Ufaransa, alipata kuwajua kibinafsi Mashahidi wa Yehova katika kambi ya mateso ya Nazi huko Ravensbrück, kaskazini mwa Ujerumani. Aliandika maneno yaliyo juu katika barua moja mnamo Agosti 1945.

Kambi ya mateso ya Auschwitz, Poland, ilikombolewa Januari 27, 1945. Tangu mwaka wa 1996, tarehe hiyo imekuwa siku ya kuwakumbuka watu walioteseka chini ya Utawala wa Hitler huko Ujerumani.

Wakati wa hotuba rasmi ya kumbukumbu Januari 27, 2003, rais wa Bunge la Serikali ya Baden-Württemberg, Peter Straub, alisema hivi: “Wote walioteswa kwa sababu ya imani zao za kidini au za kisiasa na ambao walikuwa tayari kufa badala ya kutii utawala wa Hilter wanastahili heshima kubwa, heshima ambayo ni vigumu kuieleza kwa maneno. Mashahidi wa Yehova ndiyo dini pekee iliyokataa kabisa kukubali madai ya utawala wa Hitler: Hawakuinua mkono wao ili kumpigia Hitler saluti. Walikataa kula kiapo cha uaminifu kwa ‘Mtawala na Serikali,’ kama vile tu walivyokataa kufanya utumishi wa kijeshi. Na watoto wao hawakujiunga na Chama cha Vijana cha Hitler.”

Yesu Kristo alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Hivyo, msimamo wa Mashahidi wa Yehova ulitegemea tu sababu za kidini. Straub aliendelea kusema: “Mashahidi wa Yehova walilazimishwa kuvalia beji ya rangi ya zambarau yenye pembe tatu. Walikuwa ndio wafungwa pekee katika kambi ya mateso ambao wangeweza kukomesha kifungo chao na kuepuka kuuawa. Walihitaji tu kutia sahihi kwenye fomu ili kuikana imani yao.”

Kwa Mashahidi wengi, kuikana imani yao lilikuwa jambo lisilowazika. Hivyo, Mashahidi 1,200 hivi walikufa wakati wa utawala wa Nazi. Na 270 waliuawa kwa kukataa kwenda vitani kwa sababu ya kuheshimu dhamiri yao. Walitii maneno haya: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Kama alivyoeleza Ulrich Schmidt, rais wa Bunge la Serikali ya North Rhine-Westphalia, Mashahidi wa Yehova hawakuwa watu wa pekee. Ikizungumzia hotuba yake, broshua Landtag Intern iliwataja kuwa “watu wa kawaida ambao kwa kufuata dhamiri yao walishikilia kwa uthabiti imani yao ya kidini, wakawa jasiri na kupinga mawazo ya Nazi kwa sababu ya imani yao ya Kikristo.” Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu anapendezwa na wote wanaobaki washikamanifu kwake chini ya hali ngumu. Tunasoma hivi kwenye Methali 27:11: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 30]

Courtesy of United States Holocaust Memorial Museum