Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha “Neno” la Yehova Likulinde

Acha “Neno” la Yehova Likulinde

Acha “Neno” la Yehova Likulinde

MNAMO mwaka wa 490 K.W.K., Waathene elfu 10 hadi elfu 20 hivi walikabili jeshi lenye nguvu sana la Waajemi katika pigano maarufu la Marathon. Mbinu muhimu ya jeshi la Wagiriki ilikuwa kupigana wakiwa kikosi cha askari waliosongamana. Ngao zao zilikuwa kama ukuta usioweza kupenywa ilio na mikuki iliyotokeza. Vikosi hivyo vilivyosongamana viliwawezesha Waathene kulishinda jeshi hilo kubwa sana la Waajemi.

Wakristo wa kweli wanapiga vita vya kiroho. Wanapambana na maadui wenye nguvu nyingi sana, yaani, watawala wasioonekana wa ulimwengu huu wenye uovu, wanaofafanuliwa katika Biblia kuwa “watawala wa ulimwengu wa giza hili, . . . majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12; 1 Yohana 5:19) Watu wa Mungu wanaendelea kushinda. Hata hivyo, hawashindi kwa nguvu zao. Yehova anasifiwa kwa ushindi huo, kwa kuwa ndiye anayewalinda na kuwafundisha, kama Zaburi 18:30 inavyosema: “Neno la Yehova limetakaswa. Yeye ni ngao kwa wale wote wanaomkimbilia.”

Naam, Yehova hutumia “neno” lake lililotakaswa, ambalo linapatikana katika Maandiko Matakatifu, kuwalinda watumishi wake wasipate madhara ya kiroho. (Zaburi 19:7-11; 119:93) Sulemani aliandika hivi kuhusu hekima ya Neno la Mungu: “Usiiache, nayo itakutunza. Ipende, nayo itakulinda.” (Methali 4:6; Mhubiri 7:12) Hekima ya Mungu hutulindaje tusipate madhara? Fikiria kisa cha Waisraeli wa kale.

Watu Waliolindwa na Hekima ya Mungu

Sheria ya Yehova iliwalinda na kuwaongoza Waisraeli katika maisha yao yote. Kwa mfano, sheria zilizohusu chakula, usafi, na kumtenga mtu aliyekuwa najisi, ziliwalinda wasipate magonjwa mengi ya kuambukiza ambayo yalikumba mataifa mengine. Baada ya bakteria kugunduliwa katika karne ya 19, ndipo viwango vya sayansi vilipoanza kukaribia viwango vya Sheria ya Mungu. Sheria zilizohusu kumiliki mashamba, kukomboa, kusamehe madeni, na kutoza riba ziliwanufaisha Waisraeli, kwani ziliwawezesha kuwa na jamii imara iliyofuatia haki katika biashara. (Kumbukumbu la Torati 7:12, 15; 15:4, 5) Isitoshe, kufuata Sheria ya Yehova kulihifadhi rutuba ya mashamba ya Waisraeli! (Kutoka 23:10, 11) Amri zilizokataza ibada ya uwongo ziliwalinda kiroho, ziliwazuia wasikandamizwe na mashetani, wasiwatoe watoto wao kuwa dhabihu, na pia wasiathiriwe na matendo mengine mengi maovu kama vile zoea la kuinamia sanamu zisizo na uhai, ambalo huwavunjia watu heshima.—Kutoka 20:3-5; Zaburi 115:4-8.

Kwa wazi, “neno” la Yehova halikuwa “neno lisilo na thamani” kwa Waisraeli, badala yake lilimaanisha uhai na maisha marefu kwa wale wote waliolisikiliza. (Kumbukumbu la Torati 32:47) Ijapokuwa leo Wakristo hawako chini ya agano la Sheria, wale wote ambao husikiliza “neno” la Yehova hupata manufaa pia. (Wagalatia 3:24, 25; Waebrania 8:8) Kwa hakika, badala ya kuwa na sheria nyingi, Wakristo huongozwa na kulindwa na kanuni za Biblia zinazohusu mambo mengi.

Watu Wanaolindwa na Kanuni

Sheria zinaweza kuhusu mambo machache na huenda zikawa za muda tu. Hata hivyo, kanuni za Biblia, ambazo ni kweli za msingi, huhusu mambo mengi sana na hutumika daima. Kwa mfano, fikiria ile kanuni ya Yakobo 3:17, ambayo inasema hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani.” Kweli hiyo ya msingi inaweza kuwalindaje watu wa Mungu leo?

Andiko hilo huzungumzia usafi wa kiadili. Hivyo, wale wanaothamini usafi wa kiadili hawaepuki tu ukosefu wa maadili, bali pia huepuka mambo yanayoongoza kwenye ukosefu wa maadili, kutia ndani kuwazawaza kuhusu ngono na ponografia. (Mathayo 5:28) Hali kadhalika, watu wanaochumbiana ambao huzingatia kanuni ya Yakobo 3:17, huepuka matendo yanayoweza kuwafanya washindwe kujizuia. Kwa kuwa wanaongozwa na kanuni, hawajihusishi katika ukosefu wa maadili, labda wakiwazia kwamba kwa kuwa hawavunji sheria hususa, mwenendo wao unakubaliwa na Yehova. Wanajua kwamba Yehova “huona jinsi moyo ulivyo” naye huchukua hatua inayofaa. (1 Samweli 16:7; 2 Mambo ya Nyakati 16:9) Watu hao wenye hekima hulinda miili yao kutokana na magonjwa ya zinaa yanayoenea sana leo, nao hudumisha hali yao nzuri ya kiakili na kihisia.

Pia, kulingana na Yakobo 3:17, hekima ya Mungu ni “yenye kufanya amani.” Tunajua kwamba Shetani hujaribu kutufanya tumkasirishe Yehova kwa kuingiza roho ya jeuri katika mioyo yetu. Yeye hutumia vitu kama vile vitabu, sinema, na muziki usiofaa. Yeye hutumia pia michezo ya kompyuta ambayo baadhi yake huhusisha ukatili mkubwa sana na mauaji! (Zaburi 11:5) Ongezeko la mauaji ya kijeuri linathibitisha kwamba Shetani anafanikiwa. Miaka michache iliyopita, gazeti The Sydney Morning Herald la Australia likizungumzia mauaji ya aina hiyo lilimnukuu Robert Ressler, ambaye alisema kwamba wauaji aliowahoji katika miaka ya 1970 walichochewa na picha chafu, lakini ambazo “hazikuwa chafu sana kama picha zinazoonyeshwa leo.” Hivyo, Ressler alihisi kwamba “wakati ujao ungekuwa mbaya, yaani, karne ambayo ingefuata ingekuwa na ongezeko la wauaji wanaowaua watu wengi, mmoja baada ya mwingine.”

Miezi kadhaa baada ya habari hiyo kutolewa, mfyatuaji risasi aliwaua watoto 16 na mwalimu wao katika shule ya watoto wachanga huko Dunblane, Scotland, kisha akajiua. Mwezi uliofuata, mfyatuaji risasi mwingine mwenye kichaa aliwaua watu 32 huko Port Arthur, mji wenye utulivu wa Tasmania, Australia. Katika miaka ya karibuni, nchi ya Marekani imekumbwa na visa vya mauaji shuleni, visa ambavyo vimewafanya Wamarekani wajiulize, Kwa nini mambo haya yanatukia? Mnamo Juni 2001, nchi ya Japani ilitajwa sana katika habari za ulimwengu kwa sababu mtu mwenye kichaa aliingia katika shule fulani na kuwadunga kisu na kuwaua watoto 8 wa darasa la pili na kuwakata-kata watu wengine 15. Bila shaka, kuna visababishi vingi sana vya matendo hayo ya uovu. Hata hivyo, matendo ya jeuri kwenye vyombo vya habari huonwa kuwa mojawapo ya mambo yanayochangia hali hiyo. Mwaustralia Phillip Adams, ambaye ni mwandishi wa magazeti, aliandika hivi: “Ikiwa tangazo la biashara la sekunde 60 linaweza kuongeza mauzo ya bidhaa kwa kiasi kikubwa sana, bila shaka sinema ya urefu wa saa mbili, inayogharimu mamilioni ya pesa itabadili mitazamo ya watu.” Haishangazi kwamba polisi walipata video 2,000 za jeuri na picha chafu katika nyumba ya yule mfyatuaji risasi wa Port Arthur.

Wale wote wanaoshikamana na kanuni za Biblia hulinda akili na mioyo yao isiathiriwe na namna zote za burudani ambazo humchochea mtu kutamani jeuri. Hivyo, “roho ya ulimwengu” hairuhusiwi kuingia katika akili na mioyo yao. Badala yake, ‘wanafundishwa kwa roho ya Mungu,’ nao hujitahidi kuyapenda matunda yake kama vile amani. (1 Wakorintho 2:12, 13; Wagalatia 5:22, 23) Wanafanya hivyo kwa kujifunza Biblia, kwa kusali, na kwa kutafakari mambo yanayofaa kwa ukawaida. Pia, wao huepuka kushirikiana na watu wanaopenda jeuri, lakini hushirikiana na wale ambao kama wao, wanatamani sana ulimwengu mpya wa Yehova. (Zaburi 1:1-3; Methali 16:29) Naam hekima kutoka kwa Mungu ni ulinzi.

Acha “Neno” la Yehova Liulinde Moyo Wako

Alipojaribiwa jangwani, Yesu alimpinga Shetani kwa kunukuu kwa usahihi Neno la Mungu. (Luka 4:1-13) Lakini Yesu hakujadiliana na Ibilisi ili ionekane ni nani kati yao aliyekuwa na ujuzi mwingi kuliko mwingine. Kwa kutumia Maandiko kumjibu, Yesu alisema yaliyokuwa moyoni mwake, na hiyo ndiyo sababu iliyofanya mbinu ya Ibilisi iliyofanikiwa katika shamba la Edeni, isifanikiwe katika kisa cha Yesu. Tukijaza mioyo yetu maneno ya Yehova, sisi pia tutashinda mbinu za Shetani. Hakuna jambo lililo muhimu zaidi ya hilo, kwa maana “[moyoni] ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.”—Methali 4:23.

Isitoshe, tunapaswa kuendelea kuulinda moyo wetu daima. Shetani aliposhindwa kumshawishi Yesu jangwani, hakukoma kumjaribu. (Luka 4:13) Vivyo hivyo, ataendelea kutujaribu, akitumia mbinu mbalimbali ili avunje utimilifu wetu. (Ufunuo 12:17) Hivyo, tumwige Yesu kwa kulipenda sana Neno la Mungu na kuendelea kumwomba atupe roho takatifu na hekima. (1 Wathesalonike 5:17; Waebrania 5:7) Naye Yehova anaahidi kwamba wote wanaomkimbilia hawatapata madhara yoyote ya kiroho.—Zaburi 91:1-10; Methali 1:33.

Neno la Mungu Hulilinda Kutaniko

Shetani hawezi kamwe kuuzuia “umati mkubwa” usiokoke ile dhiki kuu. (Ufunuo 7:9, 14) Hata hivyo, kwa hasira yeye hujaribu kuwapotosha Wakristo ili angalau baadhi yao wapoteze kibali cha Yehova. Mbinu hiyo ilifanikiwa katika taifa la kale la Israeli na kusababisha watu 24,000 wafe wakiwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hesabu 25:1-9) Bila shaka, Wakristo wanaotubu kikweli baada ya kufanya dhambi hupewa msaada ili warudie hali nzuri. Lakini watenda-dhambi wasiotubu, kama Zimri anayetajwa katika Biblia, huhatarisha hali ya kiroho na ya kiadili ya wengine. (Hesabu 25:14) Kama askari katika kikosi kilichosongamana ambao wametupa ngao zao, watenda-dhambi hao hujihatarisha na pia kuwahatarisha wengine.

Kwa sababu hiyo, Biblia huamuru hivi: “Mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo. . . . Ondoeni yule mtu mwovu kati yenu.” (1 Wakorintho 5:11, 13) Bila shaka unasadiki kwamba “neno” hilo la hekima hutusaidia kudumisha usafi wa kiadili na wa kiroho wa kutaniko la Kikristo.

Tofauti na kutaniko la Kikristo, dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo na vilevile waasi-imani huona kuwa sehemu za Biblia zinazopinga maoni ambayo watu wengi wanayo kuhusu maadili zimepitwa na wakati. Hivyo, wao huachilia dhambi nzito za kila namna, hata zile zinazofanywa na makasisi. (2 Timotheo 4:3, 4) Hata hivyo, ona kwamba andiko la Methali 30:5, ambalo pia linarejelea “neno” la Yehova lililo kama ngao, linafuatwa na amri hii katika mstari wa 6: “Usiongeze chochote katika maneno [ya Mungu] asije akakukaripia, wala usionekane kuwa mwongo.” Naam, wale ambao hubadilisha Biblia ni waongo wa kiroho, waongo wenye kuchukiza zaidi! (Mathayo 15:6-9) Na tuthamini sana pendeleo la kuwa sehemu ya tengenezo linaloheshimu sana Neno la Mungu.

Tunalindwa na “Harufu Tamu”

Kwa kuwa watu wa Mungu hushikamana na Biblia na kuwahubiria wengine ujumbe wake unaofariji, wao hutoa “harufu tamu” ya uzima, iliyo kama manukato, ambayo humfurahisha Yehova. Lakini kwa watu wasio waadilifu, wahubiri wa ujumbe huo hutoa harufu ambayo tafsiri ya Habari Njema kwa Watu Wote inasema hivi kuihusu: “Harufu hiyo ni kifo.” Naam, ulimwengu wa Shetani umewapotosha sana waovu hivi kwamba hawafurahi nao hata huchukizwa wakati “harufu tamu ya Kristo” inapotolewa. Kwa upande mwingine, wale ambao huhubiri habari njema kwa bidii huwa “harufu tamu ya Kristo katikati ya wale wanaookolewa.” (2 Wakorintho 2:14-16) Watu hao wenye mioyo minyoofu huchukizwa na unafiki na uwongo wa kidini ambao huenezwa na dini za uwongo. Hivyo, tunapofungua Neno la Mungu na kuwapa watu ujumbe wa Ufalme, wao huvutiwa na Kristo na hutaka kujifunza zaidi.—Yohana 6:44.

Hivyo, usivunjike moyo wengine wanapokosa kukubali ujumbe wa Ufalme. Badala yake, ione “harufu tamu ya Kristo” kuwa ulinzi wa kiroho, ambayo humfukuzia mbali kutoka kwenye milki ya kiroho ya watu wa Mungu mtu yeyote anayeweza kuleta madhara, huku ikiwavutia wale walio na mioyo minyoofu.—Isaya 35:8, 9.

Ijapokuwa askari Wagiriki katika pigano la Marathon walikabili jeshi kubwa mno, walipata ushindi kwa sababu walikuwa wamesongamana na walishikilia ngao zao kwa nguvu zao zote. Hali kadhalika, Mashahidi waaminifu wa Yehova wana hakika kwamba watapata ushindi kamili katika pigano lao la kiroho, kwa kuwa hilo ndilo ‘fungu lao la urithi.’ (Isaya 54:17) Hivyo, kila mmoja wetu na amkimbilie Yehova kwa kuendelea “kulishika sana neno la uzima.”—Wafilipi 2:16.

[Picha katika ukurasa wa 31]

‘Hekima inayotoka juu ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani’