Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina la Mungu Katika Biblia ya Kale ya Kijerumani

Jina la Mungu Katika Biblia ya Kale ya Kijerumani

Jina la Mungu Katika Biblia ya Kale ya Kijerumani

JINA la kibinafsi la Mungu, yaani, Yehova, linapatikana zaidi ya mara 7,000 katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, iliyochapishwa katika Kijerumani mnamo mwaka wa 1971. * Hata hivyo, hiyo si Biblia pekee ya Kijerumani iliyo na jina la Mungu. Yaelekea Biblia ya kwanza ya Kijerumani iliyo na jina la Yehova ilichapishwa miaka 500 hivi iliyopita na Johann Eck, mwanatheolojia Mkatoliki aliyekuwa mashuhuri.

Johann Eck alizaliwa kusini mwa Ujerumani mwaka wa 1486. Alikuwa profesa wa theolojia kwenye chuo kikuu cha Ingolstadt alipokuwa na umri wa miaka 24, na alishikilia wadhifa huo hadi kifo chake katika mwaka wa 1543. Eck aliishi wakati mmoja na Martin Luther, na kwa muda fulani walikuwa marafiki. Hata hivyo, baadaye Luther akawa kiongozi maarufu wa yale Marekebisho Makubwa ya Kidini, huku Eck akiwa mtetezi wa Kanisa Katoliki.

Mtawala wa Bavaria alimwagiza Eck atafsiri Biblia katika Kijerumani, na tafsiri yake ilichapishwa mnamo mwaka wa 1537. Kitabu Kirchliches Handlexikon kinasema kwamba tafsiri hiyo alifuata kwa uangalifu maandishi ya awali na “inastahili kuheshimiwa zaidi kuliko inavyoheshimiwa leo.” Eck alitafsiri hivi andiko la Kutoka 6:3: “Mimi ni Bwana, aliyemtokea Abrahamu, Isaka, na Yakobo nikiwa Mwenyezi Mungu: na jina langu Adonai, sijawafunulia.” Eck aliongeza maelezo haya ya pambizoni kuuhusu mstari huo: “Jina Adonai Jehoua.” Wasomi wengi wa Biblia hufikiri kwamba hiyo ndiyo mara ya kwanza kutumia jina la Mungu katika Biblia ya Kijerumani.

Hata hivyo, jina la Mungu limejulikana na kutumiwa kwa maelfu ya miaka. Jina “Yehova” lilitajwa kwanza katika lugha ya Kiebrania, na katika lugha hiyo jina hilo humtambulisha Mungu wa pekee wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 6:4) Yapata miaka 2,000 iliyopita, maneno ya Yesu, aliposema kwamba alikuwa amelifunua jina la Mungu, yaliandikwa katika Kigiriki. (Yohana 17:6) Tangu wakati huo jina hilo limetangazwa katika lugha nyingi, na baada ya muda usio mrefu, andiko la Zaburi 83:18 litatimizwa, wakati watu wote watakapojua kwamba yule ambaye jina lake ni Yehova, ndiye Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ilichapishwa na Mashahidi wa Yehova katika Kiingereza mwaka wa 1961. Sasa Biblia nzima au sehemu ya Biblia hiyo inapatikana katika lugha zaidi ya 50.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Chapa ya 1558 ya Biblia ya Eck inayotaja jina la Yehova katika maelezo ya pambizoni yanayohusu Kutoka 6:3