Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini tunaweza kusema kwamba maneno kama vile “yeye peke yake asiyeweza kufa” na yule “ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu amemwona au anaweza kumwona” yanamhusu Yesu badala ya Yehova Mungu?

Mtume Paulo aliandika hivi: “Ufunuo huo yule Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee na mwenye furaha atauonyesha katika nyakati zake wenyewe zilizowekwa, yeye Mfalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana, yeye peke yake asiyeweza kufa, anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa, ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu amemwona au anaweza kumwona.”—1 Timotheo 6:15, 16.

Kwa kawaida wafafanuzi wa Biblia wanajiuliza hivi: ‘Maneno kama vile “yeye peke yake asiyeweza kufa,” “Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee,” na yule “ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu amemwona au anaweza kumwona” yangewezaje kumhusu mtu mwingine isipokuwa Mweza-Yote?’ Ni kweli kwamba, maneno kama hayo yangeweza kutumiwa kumfafanua Yehova. Hata hivyo, muktadha unaonyesha kwamba kwenye andiko la 1 Timotheo 6:15, 16, Paulo alikuwa akizungumza hasa kumhusu Yesu.

Mwishoni mwa mstari wa 14, Paulo anazungumza kuhusu “ufunuo wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (1 Timotheo 6:14) Hivyo, Paulo anapoandika kwenye mstari wa 15 kwamba “ufunuo huo yule Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee na mwenye furaha atauonyesha katika nyakati zake wenyewe zilizowekwa,” anazungumza kuhusu ufunuo wa Yesu, wala si wa Yehova Mungu. Basi, ni nani huyo “Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee”? Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Mwenye Uwezo Mkubwa ambaye Paulo anazungumzia ni Yesu. Kwa nini? Muktadha unaonyesha wazi kwamba Paulo anamlinganisha Yesu na watawala wa kibinadamu. Kwa kweli, kama alivyoandika Paulo, Yesu ni “Mfalme wa wale [wanadamu] wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale [wanadamu] wanaotawala wakiwa mabwana.” * Naam, anapolinganishwa na watawala hao, Yesu ni “Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee.” Yesu amepewa “utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” (Danieli 7:14) Hakuna mtawala wa kibinadamu anayeweza kutoa dai hilo!

Namna gani kuhusu maneno “yeye peke yake asiyeweza kufa”? Mara nyingine tena, ulinganifu unafanywa kati ya Yesu na wafalme wa kibinadamu. Watawala wa dunia hawawezi kudai kwamba wamepewa zawadi ya kutoweza kufa, lakini Yesu anaweza kudai hivyo. Paulo aliandika hivi: “Tunajua kwamba Kristo hafi tena, kwa kuwa sasa amekwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu; kifo si bwana juu yake tena.” (Waroma 6:9) Hivyo, Yesu ndiye mtu wa kwanza kutajwa katika Biblia kuwa alipokea zawadi ya kutoweza kufa. Kwa kweli, wakati Paulo alipokuwa akiandika, Yesu peke yake ndiye aliyekuwa amepewa uzima usioweza kuharibika.

Pia tunapaswa kukumbuka kwamba lingekuwa kosa kwa Paulo kusema kwamba Yehova Mungu peke yake ndiye ana hali ya kutoweza kufa, kwa kuwa Paulo alipoandika maneno hayo, Yesu pia alikuwa na hali ya kutoweza kufa. Lakini Paulo angeweza kusema kwamba Yesu peke yake ndiye ana hali ya kutoweza kufa kwa kumlinganisha na watawala wa dunia.

Isitoshe, ni kweli kwamba baada ya Yesu kufufuliwa na kupaa mbinguni, yeye anaweza kuitwa yule “ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu amemwona au anaweza kumwona.” Bila shaka, wanafunzi wake watiwa-mafuta wangemwona Yesu baada ya kifo chao na kufufuliwa mbinguni wakiwa viumbe wa roho. (Yohana 17:24) Lakini hakuna mtu duniani angemwona Yesu akiwa katika utukufu wake. Hivyo, inaweza kusemwa kwa hakika kwamba tangu kufufuliwa kwa Yesu na kupaa kwake mbinguni, “hakuna hata mmoja kati ya wanadamu” ambaye kwa kweli amemwona.

Kwa kweli, ufafanuzi unaopatikana katika andiko la 1 Timotheo 6:15, 16 unaposomwa kijuujuu tu unaweza kueleweka kwamba unamhusu Mungu. Lakini muktadha wa maneno ya Paulo, pamoja na uthibitisho wa maandiko mengine, huonyesha kwamba Paulo alikuwa akizungumza kumhusu Yesu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Maneno yanayofanana na hayo yanatumiwa kumhusu Yesu kwenye 1 Wakorintho 8:5, 6; Ufunuo 17:12, 14; 19:16.