Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Pamoja na Mungu Nyakati Hizi za Misukosuko

Tembea Pamoja na Mungu Nyakati Hizi za Misukosuko

Tembea Pamoja na Mungu Nyakati Hizi za Misukosuko

“Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.”—MWANZO 5:24.

1. Ni baadhi ya mambo gani katika nyakati zetu yanayofanya maisha yawe magumu sana?

NYAKATI za misukosuko! Maneno hayo hufafanua vema miaka yenye misukosuko na jeuri ambayo wanadamu wameona tangu Ufalme wa Kimasihi ulipozaliwa mwaka wa 1914. Kwa muda huo wote, wanadamu wamekuwa wakiishi katika “siku za mwisho.” Misiba kama vile njaa, magonjwa, matetemeko ya nchi, na vita, imewakumba kwa kiwango kikubwa zaidi. (2 Timotheo 3:1; Ufunuo 6:1-8) Waabudu wa Yehova wamepatwa na misiba hiyo pia. Kwa kadiri fulani, leo sote hukabili matatizo na hali zinazosababisha wasiwasi. Matatizo ya kiuchumi, misukosuko ya kisiasa, uhalifu, na magonjwa ni baadhi ya mambo yanayofanya maisha yawe magumu sana.

2. Watumishi wa Yehova wamekabili matatizo gani?

2 Isitoshe, watumishi wengi wa Yehova wamevumilia mateso mengi makali kwa kuwa Shetani anaendelea kupigana vita na wale “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:17) Ijapokuwa sisi sote hatujateswa moja kwa moja, Wakristo wote wa kweli wanahitaji kupambana na Shetani Ibilisi na ile roho anayoeneza miongoni mwa wanadamu. (Waefeso 2:2; 6:12) Tunahitaji kuwa macho kila wakati ili tusiathiriwe na roho hiyo, kwa kuwa tunaikabili kazini, shuleni, na mahali popote ambapo tunakutana na watu wasiopendezwa na ibada safi.

Tembea Pamoja na Mungu, Si na Mataifa

3, 4. Ni kwa njia gani Wakristo ni tofauti na ulimwengu?

3 Katika karne ya kwanza, Wakristo pia walipigana vikali na roho ya ulimwengu huu, na jambo hilo liliwafanya wawe tofauti sana na wale waliokuwa nje ya kutaniko la Kikristo. Paulo alieleza kuhusu tofauti hiyo alipoandika hivi: “Kwa hiyo, nasema hili na kulitolea ushahidi katika Bwana, kwamba msiendelee tena kutembea kama vile mataifa wanavyotembea pia katika ubatili wa akili zao, huku wakiwa katika giza kiakili, na kutenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutojua ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Wakiisha kuishiwa na ufahamu wote wa maadili, walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Waefeso 4:17-19.

4 Maneno hayo yanafafanua waziwazi giza zito la kiroho na la kiadili lililopo katika ulimwengu wa leo, sawa na ilivyokuwa katika siku za Paulo! Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo Wakristo ‘hawaendelei kutembea kama vile mataifa wanavyotembea.’ Badala yake, wanafurahia pendeleo la pekee la kutembea pamoja na Mungu. Naam, huenda watu fulani wakatilia shaka ikiwa ni sawa kusema kwamba wanadamu duni wasio wakamilifu wanaweza kutembea pamoja na Yehova. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kuwa inawezekana. Isitoshe, Yehova anataka wafanye hivyo. Katika karne ya nane kabla ya Wakati Wetu wa Kawaida, nabii Mika aliandika maneno haya kwa mwongozo wa roho ya Mungu: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—Mika 6:8.

Tunawezaje Kutembea na Mungu na kwa Nini Tufanye Hivyo?

5. Mwanadamu asiye mkamilifu anawezaje kutembea pamoja na Mungu?

5 Tunawezaje kutembea pamoja na Mungu mwenye nguvu zote ambaye haonekani? Ni wazi kwamba hatuwezi kutembea pamoja naye kama tunavyotembea na wanadamu wenzetu. Katika Biblia, neno “kutembea” linaweza kumaanisha “kufuata mwendo fulani.” * Basi, yule anayetembea pamoja na Mungu anafuata mwendo wa maisha ulioagizwa na Mungu na unaompendeza. Kufuata mwendo huo hutufanya tuwe tofauti na watu wengi. Lakini, huo tu ndio mwendo unaomfaa Mkristo. Kwa nini? Kuna sababu nyingi.

6, 7. Kwa nini kutembea pamoja na Mungu ndiyo njia bora kabisa ya maisha?

6 Kwanza, Yehova ndiye Muumba wetu, Chanzo cha uhai wetu, na Mwandalizi wa vitu vyote tunavyohitaji ili tuendelee kuwa hai. (Ufunuo 4:11) Hivyo, ni yeye tu aliye na haki ya kutuambia jinsi tunavyopaswa kutembea. Zaidi ya hayo, kutembea pamoja na Mungu ndiyo njia ya maisha yenye faida zaidi. Yehova amefanya maandalizi ili wale wanaotembea pamoja naye wapate msamaha wa dhambi na tumaini hakika la uzima wa milele. Pia, Baba yetu mwenye upendo mwingi sana hutoa mashauri yenye hekima yanayowasaidia wale wanaotembea pamoja naye kufanikiwa maishani sasa, licha ya kwamba wao si wakamilifu na wanaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani. (Yohana 3:16; 2 Timotheo 3:15, 16; 1 Yohana 1:8; 2:25; 5:19) Sababu nyingine inayotufanya tutembee pamoja na Mungu ni kwamba utayari wetu wa kufanya hivyo huchangia amani na umoja katika kutaniko.—Wakolosai 3:15, 16.

7 Mwishowe, sababu ya maana zaidi ni kwamba tunapotembea pamoja na Mungu tunaonyesha msimamo wetu kuhusiana na lile suala kuu lililotokezwa katika bustani ya Edeni, yaani, suala la enzi kuu. (Mwanzo 3:1-6) Kupitia maisha yetu, tunaonyesha kwamba tunamuunga Yehova mkono kabisa, na tunatangaza bila woga kwamba ni yeye tu aliye na haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu. (Zaburi 83:18) Hivyo, tunatenda kupatana na sala yetu kwamba jina la Mungu litakaswe na mapenzi yake yatendeke. (Mathayo 6:9, 10) Wale wanaochagua kutembea pamoja na Mungu wana hekima iliyoje! Wanaweza kuwa na uhakika kwamba wanafuata njia inayofaa kwa sababu Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” Hawezi kamwe kukosea.—Waroma 16:27.

8. Nyakati za Enoko na za Noa zilifananaje na nyakati zetu?

8 Hata hivyo, je, inawezekana kuishi kama Wakristo wakati ambapo kuna misukosuko mingi na watu wengi hawataki kumtumikia Yehova? Tunapata jibu la swali hilo tunapochunguza mifano ya waaminifu wa kale ambao walidumisha utimilifu wao licha ya kuishi nyakati ngumu sana. Wawili kati yao ni Enoko na Noa. Wote waliishi nyakati kama zetu. Uovu ulikuwa umezidi. Katika siku za Noa, dunia ilijaa jeuri na ukosefu wa adili. Hata hivyo, Enoko na Noa walipinga roho ya ulimwengu wa siku zao, nao wakatembea pamoja na Yehova. Waliwezaje kufanya hivyo? Ili tujibu swali hilo, katika makala hii tutachunguza mfano wa Enoko. Katika makala inayofuata tutamkazia fikira Noa.

Enoko Alitembea na Mungu Nyakati za Misukosuko

9. Tuna habari zipi kumhusu Enoko?

9 Enoko ndiye mtu wa kwanza ambaye Maandiko yanamtaja kuwa alitembea pamoja na Mungu. Simulizi la Biblia linasema: “Baada ya kumzaa Methusela, Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 5:22) Simulizi hilo linaendelea kutaja miaka ambayo Enoko aliishi. Ingawa aliishi kwa muda mrefu kwa kulinganisha na muda ambao watu katika siku zetu huishi, bado ulikuwa mfupi katika siku zake. Kisha simulizi hilo linasema: “Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.” (Mwanzo 5:24) Inaonekana kwamba Yehova alimhamisha Enoko kutoka katika nchi ya walio hai hadi katika usingizi wa kifo kabla ya wapinzani kumwangamiza. (Waebrania 11:5, 13) Zaidi ya kutajwa katika mistari hiyo mifupi, Enoko ametajwa katika sehemu nyingine chache za Biblia. Hata hivyo, kutokana na habari tulizo nazo na kwa kutegemea mambo mengine, tunaweza kusema kwamba Enoko aliishi nyakati za misukosuko.

10, 11. (a) Uovu ulieneaje baada ya Adamu na Hawa kuasi? (b) Enoko alihubiri ujumbe gani wa kinabii, na watu waliitikiaje?

10 Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo uovu ulienea haraka katika jamii ya wanadamu baada ya Adamu kutenda dhambi. Biblia inatueleza kwamba mwana mzaliwa wa kwanza wa Adamu, Kaini, ndiye aliyekuwa mwanadamu wa kwanza kuua alipomuua ndugu yake Abeli. (Mwanzo 4:8-10) Baada ya Abeli kuuawa kikatili, Adamu na Hawa walipata mwana mwingine, nao wakamwita Sethi. Tunasoma hivi kumhusu: “Sethi akazaa mwana pia naye akamwita jina lake Enoshi. Wakati huo watu wakaanza kuliitia jina la Yehova.” (Mwanzo 4:25, 26) Inasikitisha kwamba huko “kuliitia jina la Yehova” kulifanywa kwa njia ya kumwasi Yehova. * Miaka mingi baada ya Enoshi kuzaliwa, mzao fulani wa Kaini aliyeitwa Lameki alitunga wimbo kwa ajili ya wake zake wawili na kutangaza kwamba alikuwa amemuua kijana aliyemtia jeraha. Kisha Lameki akaonya hivi: “Ikiwa Kaini atalipizwa kisasi mara 7, basi Lameki ni mara 77.”—Mwanzo 4:10, 19, 23, 24.

11 Maelezo hayo mafupi yanaonyesha kwamba uasi ulioanzishwa na Shetani katika bustani ya Edeni ulisababisha uovu uenee haraka kati ya wazao wa Adamu. Enoko alikuwa nabii wa Yehova katika ulimwengu huo, na maneno yake yenye nguvu yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanahusu nyakati zetu pia. Yuda aliandika unabii huu wa Enoko: “Tazama! Yehova alikuja pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwathibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomwogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema juu yake.” (Yuda 14, 15) Maneno hayo yatatimia kwa ukamili wakati wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Hata hivyo, tuna uhakika kwamba hata katika siku za Enoko, “watenda-dhambi [wengi] wasiomwogopa Mungu” waliudhika waliposikia unabii wa Enoko. Yehova alionyesha upendo ulioje kwa kumhamisha Enoko ili wasimuumize!

Ni Nini Kilichomwimarisha Enoko Kutembea na Mungu?

12. Ni nini kilichofanya Enoko awe tofauti na watu wa nyakati zake?

12 Katika bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walimsikiliza Shetani, naye Adamu akamwasi Yehova. (Mwanzo 3:1-6) Mwana wao Abeli hakutenda kama wao, naye Yehova akamtazama kwa kibali. (Mwanzo 4:3, 4) Kwa kusikitisha, wazao wengi wa Adamu hawakuwa kama Abeli. Hata hivyo, Enoko, aliyezaliwa mamia ya miaka baadaye, alikuwa kama Abeli. Kulikuwa na tofauti gani kati ya Enoko na wazao wengi wa Adamu? Mtume Paulo alijibu swali hilo alipoandika hivi: “Kwa imani Enoko alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemhamisha; kwa maana kabla ya kuhamishwa kwake alikuwa ametolewa ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema.” (Waebrania 11:5) Enoko alikuwa sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ wa kabla ya Ukristo ambao walikuwa mifano bora ya imani. (Waebrania 12:1) Imani ndiyo iliyomwezesha Enoko kuendelea kufanya yaliyo sawa katika maisha yake ya zaidi ya miaka 300. Hiyo ni zaidi ya mara tatu ya muda ambao wanadamu wengi leo huishi!

13. Enoko alikuwa na imani ya aina gani?

13 Paulo alieleza kuhusu imani ya Enoko na ya mashahidi wengine alipoandika hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Naam, imani ni tarajio hakika, linalotegemea uhakikisho wa kwamba mambo tunayoyatumaini yatatimia. Imani inahusisha tarajio lenye nguvu sana ambalo linabadili maoni yetu kuhusu mambo yaliyo muhimu zaidi maishani mwetu. Imani ya aina hiyo ndiyo iliyomwezesha Enoko kutembea pamoja na Mungu hata ingawa watu wa nyakati zake hawakufanya hivyo.

14. Imani ya Enoko ilitegemea ujuzi gani sahihi?

14 Imani ya kweli inategemea ujuzi sahihi. Enoko alijua mambo gani? (Waroma 10:14, 17; 1 Timotheo 2:4) Bila shaka, alijua mambo yaliyotukia Edeni. Huenda pia alikuwa amesikia jinsi maisha yalivyokuwa katika bustani ya Edeni, ambayo huenda bado ilikuwapo wakati huo, ingawa wanadamu walizuiwa wasiingie ndani. (Mwanzo 3:23, 24) Na alijua kusudi la Mungu kwamba wazao wa Adamu wataijaza dunia na kuifanya iwe kama Paradiso hiyo ya kwanza. (Mwanzo 1:28) Isitoshe, Enoko alithamini kabisa ahadi ya Yehova ya kutokeza Uzao ambao ungeponda kichwa cha Shetani na kukomesha matokeo mabaya ya uwongo wa Shetani. (Mwanzo 3:15) Naam, unabii wa Enoko ulioongozwa kwa roho ya Mungu na kuhifadhiwa katika kitabu cha Yuda, unahusu kuharibiwa kwa uzao wa Shetani. Kwa kuwa Enoko alikuwa na imani, tunajua kwamba alimwabudu Yehova huku akiamini kwamba “yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Hivyo, ingawa Enoko hakujua mambo yote tunayoyajua, ujuzi aliokuwa nao ulitosha kuwa msingi wa imani thabiti. Imani hiyo ilimwezesha kudumisha utimilifu wake nyakati za misukosuko.

Iga Mfano wa Enoko

15, 16. Tunawezaje kuiga mfano wa Enoko?

15 Kwa kuwa, kama Enoko, tunataka kumpendeza Yehova katika nyakati hizi za misukosuko, inafaa tumwige. Tunahitaji kupata na kuendelea kuwa na ujuzi sahihi kumhusu Yehova na kusudi lake. Lakini mengi zaidi yanahitajika. Tunahitaji kukubali ujuzi huo sahihi uongoze maisha yetu. (Zaburi 119:101; 2 Petro 1:19) Tunahitaji kuongozwa na maoni ya Mungu, na kujitahidi sikuzote kumpendeza katika mambo yote tunayofikiria na kutenda.

16 Hatujui ni nani wengine waliomtumikia Yehova nyakati za Enoko, lakini huenda alikuwa peke yake au kulikuwa na wengine wachache. Sisi pia ni wachache ulimwenguni, lakini hilo halituvunji moyo. Yehova atatutegemeza hata nani awe dhidi yetu. (Waroma 8:31) Enoko alionya kwa ujasiri kuhusu uharibifu wa watu wasiomwogopa Mungu uliokuwa ukikaribia. Sisi pia huhubiri kwa ujasiri kuhusu “hii habari njema ya ufalme” licha ya dhihaka, upinzani, na mateso. (Mathayo 24:14) Enoko hakuishi kwa muda mrefu kama watu wengi wa siku zake. Lakini hakuweka tumaini lake katika ulimwengu huo. Alikazia fikira jambo kubwa zaidi. (Waebrania 11:10, 35) Sisi pia tunakazia fikira kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Hivyo, hatutumii ulimwengu huu kwa ukamili. (1 Wakorintho 7:31) Badala yake, tunatumia nguvu na mali zetu hasa kumtumikia Yehova.

17. Tunajua mambo gani ambayo Enoko hakujua, nasi tunapaswa kufanya nini?

17 Enoko aliamini kwamba Uzao ulioahidiwa na Mungu ungetokea kwa wakati wa Yehova unaofaa. Sasa karibu miaka 2,000 imepita tangu Uzao huo, Yesu Kristo, kutokea, kuandaa fidia, na kutufungulia njia ili sisi pamoja na mashahidi wengine waaminifu wa zamani kama Enoko tuweze kurithi uzima wa milele. Uzao huo, ambao umetawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ulimporomosha Shetani kutoka mbinguni hadi duniani, nasi tunaona dhiki inayosababishwa na jambo hilo. (Ufunuo 12:12) Ndiyo, tunajua mambo mengi sana kuliko Enoko. Basi, acheni tuwe na imani thabiti kama yeye. Acheni maisha yetu yote yaongozwe na uhakika wa kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Naam, kama Enoko, acheni tutembee pamoja na Mungu japo tunaishi nyakati za misukosuko.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona Buku la 1 la kitabu Insight on the Scriptures, ukurasa wa 220, fungu la 6 (au Étude Perspicace Des Écritures, ukurasa wa 228, fungu la 4 katika Kifaransa), kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 10 Kabla ya siku za Enoshi, Yehova alizungumza na Adamu. Abeli alimtolea Yehova toleo lililokubalika. Pia, kabla Kaini hajachochewa kuua kwa sababu ya hasira yenye wivu, Mungu alizungumza naye. Hivyo, yaonekana watu walianza “kuliitia jina la Yehova” kwa njia mpya, si katika ibada safi.

Ungejibuje?

• Ni nini maana ya kutembea pamoja na Mungu?

• Kwa nini kutembea pamoja na Mungu ndiyo njia bora ya maisha?

• Ni nini kilichomwezesha Enoko atembee pamoja na Mungu japo aliishi nyakati za misukosuko?

• Tunawezaje kumwiga Enoko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kwa imani, ‘Enoko aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli’

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tunasadiki kabisa kwamba ahadi za Yehova zitatimia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Woman, far right: FAO photo/B. Imevbore; collapsing building: San Hong R-C Picture Company