Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu

Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu

Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu

“Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.”—MIKA 4:5.

1. Hali ya maadili ilikuwaje katika siku za Noa, na Noa alikuwa tofauti kwa njia gani?

ENOKO ndiye mtu wa kwanza anayetajwa katika Biblia kuwa alitembea pamoja na Mungu. Wa pili alikuwa Noa. Simulizi linasema: “Noa alikuwa mtu mwadilifu. Alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:9) Kufikia wakati wa Noa, wanadamu kwa ujumla walikuwa wameiacha ibada safi. Hali hiyo mbaya ilizidishwa na malaika wasio waaminifu waliokuwa na mahusiano yasiyo ya asili pamoja na wanawake, nao wakazaa watoto walioitwa Wanefili, yaani, “watu wenye nguvu” au “wanaume wenye sifa” wa siku hizo. Haishangazi kwamba dunia ilijaa jeuri! (Mwanzo 6:2, 4, 11) Hata hivyo, Noa hakuonekana na kosa, naye alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Mungu alipomwamuru ajenge safina ili kuokoa uhai, Noa alitii naye “akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.” (Mwanzo 6:22) Ndiyo, Noa alitembea pamoja na Mungu.

2, 3. Noa alituwekea mfano gani bora?

2 Paulo alimtia Noa katika orodha yake ya mashahidi waaminifu alipoandika hivi: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu kuwa wenye hatia, naye akawa mrithi wa uadilifu unaolingana na imani.” (Waebrania 11:7) Huo ni mfano bora kama nini! Akiwa na uhakika wa kwamba maneno ya Yehova yatatimia, Noa alitumia wakati, nguvu, na mali ili kutimiza amri za Mungu. Vivyo hivyo, wengi leo hukataa kutumia nafasi wanazopata katika ulimwengu huu na badala yake wanatumia wakati wao, nguvu zao, na mali zao ili kutii amri za Yehova. Imani yao inaonekana wazi, nayo itawawezesha wao na wengine pia wapate wokovu.—Luka 16:9; 1 Timotheo 4:16.

3 Inaonekana ilikuwa vigumu kwa Noa na familia yake kuwa na imani, sawa na ilivyokuwa kwa Enoko, babu ya baba ya Noa, ambaye alizungumziwa katika makala iliyotangulia. Kama vile ilivyokuwa katika siku za Enoko, katika siku za Noa pia waabudu wa kweli walikuwa wachache. Ni watu wanane tu waliokuwa waaminifu na waliookoka Gharika. Noa alihubiri uadilifu katika ulimwengu wenye jeuri na ukosefu wa adili. Isitoshe, yeye na familia yake walikuwa wakijenga safina kubwa ya mbao ili kujitayarisha kwa ajili ya gharika ya ulimwenguni pote, ingawa hakuna mtu aliyewahi kuona gharika kama hiyo. Haikosi kwamba watu waliowatazama walishangaa sana.

4. Yesu alikazia kosa gani la watu walioishi siku za Noa?

4 Inafaa kutambua kwamba Yesu alipozungumzia siku za Noa, yeye hakuongea kuhusu jeuri, dini ya uwongo au ukosefu wa adili, ingawa hayo ni mambo mabaya sana. Kosa ambalo Yesu alikazia ni kwamba watu walikataa kutii onyo lililotolewa. Alisema kwamba watu walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina.” Je, kulikuwa na ubaya wowote kula, kunywa, kuoa, au kuolewa? Watu hao walikuwa wakiishi maisha ya “kawaida” tu! Lakini gharika ilikuwa karibu kutokea, na Noa alihubiri uadilifu. Maneno yake na mwenendo wake ulipaswa kuwa onyo kwao. Lakini “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.

5. Noa na familia yake walihitaji sifa zipi?

5 Tunapofikiria nyakati hizo, tunatambua kwamba Noa alifuata njia ya hekima. Hata hivyo, kabla ya Gharika, ujasiri ulihitajiwa ili kuwa tofauti na wengine. Noa na familia yake walihitaji kuwa na usadikisho wenye nguvu ili wajenge safina kubwa na kuijaza wanyama wa kila aina. Je, kuna wakati ambapo watu hao wachache waaminifu walihisi kwamba ni afadhali waishi maisha ya “kawaida” tu na kuepuka kuvuta fikira za watu? Hata ikiwa walifikiri hivyo nyakati nyingine, waliendelea kuwa watimilifu. Baada ya miaka mingi sana—muda mrefu kuliko muda ambao sisi tutavumilia katika mfumo huu wa mambo—imani ya Noa ilimwezesha kuokoka Gharika. Hata hivyo, Yehova aliwahukumu wote walioishi maisha ya “kawaida” na ambao hawakutilia maanani umuhimu wa nyakati walizoishi.

Wanadamu Wakabili Jeuri Tena

6. Hali ilikuwaje baada ya Gharika?

6 Maji ya Gharika yalipopungua, wanadamu walianza maisha mapya. Lakini bado hawakuwa wakamilifu na “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu” uliendelea kuwa “mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Isitoshe, ingawa roho waovu hawangejibadilisha na kuvaa tena miili ya wanadamu, bado walikuwa watendaji sana. Baada ya muda mfupi tu, ulimwengu wa wanadamu wasiomwogopa Mungu ulionyesha kwamba ulikuwa “unakaa katika nguvu za yule mwovu,” na kama ilivyo leo, waabudu wa kweli walihitaji kupambana na “hila za Ibilisi.”—1 Yohana 5:19; Waefeso 6:11, 12.

7. Jeuri iliongezekaje duniani baada ya Gharika?

7 Baada ya Gharika, angalau kuanzia wakati wa Nimrodi, wanadamu walianza tena kutenda kwa jeuri. Kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu na maendeleo ya teknolojia, jeuri imeongezeka kadiri ambavyo miaka imepita. Zamani, kulikuwa na upanga, mkuki, upinde, mshale, na magari ya vita yaliyokokotwa na farasi. Baadaye, kukawa na bunduki, mizinga, na silaha nyingine za hali ya juu zilizotengenezwa mwanzoni mwa karne ya 20. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu silaha mpya zenye kuogopesha zilitumiwa, kama vile ndege, vifaru, nyambizi, na gesi za sumu. Katika vita hivyo, silaha hizo ziliua mamilioni ya watu. Je, hilo lilitarajiwa? Ndiyo.

8. Andiko la Ufunuo 6:1-4 limetimizwaje?

8 Katika mwaka wa 1914, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu huko mbinguni, na “siku ya Bwana” ikaanza. (Ufunuo 1:10) Katika maono yaliyoandikwa katika kitabu cha Ufunuo, Yesu anaonekana akiwa Mfalme anayeendesha farasi mweupe kwa ushindi. Wapanda-farasi wengine wanamfuata, na kila mmoja wao anawakilisha pigo fulani linalowakumba wanadamu. Mmoja wao anamwendesha farasi mwenye rangi ya moto, naye amepewa ruhusa ya ‘kuondoa amani duniani ili wauane; naye amepewa upanga mkubwa.’ (Ufunuo 6:1-4) Farasi huyo na mpandaji wake wanafananisha vita, na ule upanga mkubwa unafananisha uharibifu mkubwa sana unaosababishwa na vita vya sasa na silaha kali zinazotumiwa. Leo, silaha hizo zinatia ndani silaha za nyuklia, kila moja ikiwa na uwezo wa kuua makumi ya maelfu ya watu; roketi zinazoweza kusafirisha silaha hizo hadi maeneo ya mbali sana; na pia silaha kali za maangamizi makubwa za kemikali na kibiolojia.

Tunatii Maonyo ya Yehova

9. Ulimwengu wa leo unafananaje na ule wa kabla ya Gharika?

9 Katika siku za Noa, Yehova aliwaangamiza wanadamu kwa sababu ya jeuri nyingi sana ya watu waovu iliyochochewa na Wanefili. Namna gani leo? Je, sasa jeuri imepungua duniani kuliko ilivyokuwa wakati huo? Sivyo hata kidogo! Isitoshe, kama ilivyokuwa katika siku za Noa, leo watu wanaendelea kufanya shughuli zao huku wakijaribu kuishi maisha ya “kawaida,” na kukataa kutii maonyo yanayotolewa. (Luka 17:26, 27) Basi, je, kuna sababu yoyote ya kutilia shaka kwamba Yehova atawaangamiza tena wanadamu? Hakuna.

10. (a) Ni onyo gani ambalo linatolewa mara nyingi katika unabii wa Biblia? (b) Ni ipi iliyo njia bora tu tunayoweza kuifuata leo?

10 Mamia ya miaka kabla ya Gharika, Enoko alitabiri kuhusu uharibifu ambao ungetokea katika siku zetu. (Yuda 14, 15) Yesu pia alizungumza kuhusu “dhiki kuu” inayokaribia. (Mathayo 24:21) Manabii wengine walionya kuhusu wakati huo. (Ezekieli 38:18-23; Danieli 12:1; Yoeli 2:31, 32) Na katika kitabu cha Ufunuo, tunasoma maelezo yaliyo wazi kuhusu uharibifu huo wa mwisho. (Ufunuo 19:11-21) Tukiwa mtu mmoja-mmoja tunamwiga Noa na kuwa wahubiri wa uadilifu wenye bidii. Sisi hutii maonyo ya Yehova na kuwasaidia wanadamu wenzetu kwa upendo wafanye hivyo. Hivyo, kama Noa, tunatembea pamoja na Mungu. Naam, ni muhimu wote wale wanaopenda uhai waendelee kutembea pamoja na Mungu. Tunawezaje kufanya hivyo licha ya matatizo tunayokabili kila siku? Tunahitaji kusitawisha imani yenye nguvu kwamba kusudi la Mungu litatimia.—Waebrania 11:6.

Endelea Kutembea Pamoja na Mungu Nyakati za Misukosuko

11. Sisi huwaigaje Wakristo wa karne ya kwanza?

11 Katika karne ya kwanza, Wakristo watiwa-mafuta waliitwa watu wa “Ile Njia.” (Matendo 9:2) Maisha yao yote yalitegemea imani katika Yehova na Yesu Kristo. Walitembea katika njia ambayo Bwana wao alitembea. Leo, Wakristo waaminifu hufanya vivyo hivyo.

12. Ni nini kilichotukia baada ya Yesu kufanya muujiza wa kuulisha umati?

12 Umuhimu wa imani unaonekana katika jambo lililotukia wakati wa huduma ya Yesu. Pindi moja, Yesu alifanya muujiza wa kuulisha umati wa wanaume 5,000 hivi. Watu walishangaa na kufurahi. Lakini ona jambo lililofuata. Tunasoma hivi: “Watu hao walipoona ishara alizofanya, wakaanza kusema: ‘Kwa hakika huyu ndiye nabii aliyepaswa kuja ulimwenguni.’ Kwa hiyo Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” (Yohana 6:10-15) Usiku huo alisafiri akaenda mahali pengine. Inaonekana watu wengi walikata tamaa Yesu alipokataa kuwa mfalme. Alikuwa ameonyesha kwamba ana hekima ya kutosha kuwa mfalme na kwamba ana uwezo wa kutosheleza mahitaji ya kimwili ya watu. Lakini wakati wa Yehova wa kumweka awe Mfalme haukuwa umefika. Zaidi ya hayo, Ufalme wa Yesu ungekuwa mbinguni, si duniani.

13, 14. Watu wengi walikuwa na mtazamo gani, na imani yao ilijaribiwaje?

13 Hata hivyo, kama Yohana anavyosema, watu hao walijitahidi juu chini kumfuata Yesu wakampata “ng’ambo ya bahari.” Kwa nini walimfuata baada ya yeye kukataa jitihada zao za kumfanya awe mfalme? Wengi walikuwa na mtazamo wa kimwili, huku wakitaja waziwazi kuhusu chakula ambacho Yehova aliandaa nyikani katika siku za Musa. Ni kana kwamba walimtaka Yesu aendelee kuwapa chakula. Akitambua nia yao mbaya, Yesu alianza kuwafundisha kweli za kiroho ambazo zingeweza kubadili mawazo yao. (Yohana 6:17, 24, 25, 30, 31, 35-40) Kwa sababu hiyo, wengine walianza kumnung’unikia, hasa alipotoa mfano huu: “Kwa kweli kabisa ninawaambia, Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe. Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.”—Yohana 6:53, 54.

14 Mara nyingi mifano ya Yesu iliwachochea watu kuonyesha ikiwa kweli walitamani kutembea pamoja na Mungu. Mfano huu ulitimiza kusudi hilohilo. Ulichochea hisia kali. Tunasoma hivi: “Wengi kati ya wanafunzi wake, waliposikia hilo, wakasema: ‘Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?’” Kisha Yesu akawaeleza kwamba wanapaswa kuelewa maneno yake kwa njia ya kiroho. Alisema: “Roho ndiyo inayotokeza uzima; mwili hauna faida hata kidogo. Maneno ambayo nimewaambia ni roho na ni uzima.” Lakini wengi hawakutaka kusikiliza. Simulizi hilo linasema: “Kwa sababu ya hili wengi kati ya wanafunzi wake wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye.”—Yohana 6:60, 63, 66.

15. Baadhi ya wafuasi wa Yesu walikuwa na mtazamo gani unaofaa?

15 Hata hivyo, baadhi ya wanafunzi wa Yesu walitenda kwa njia tofauti. Ni kweli kwamba wanafunzi hao washikamanifu hawakuelewa kwa ukamili yale ambayo Yesu alisema. Hata hivyo, waliendelea kumwamini kwa uthabiti. Petro, mmoja wa wanafunzi hao washikamanifu, alionyesha maoni ya wanafunzi wote waliobaki, aliposema: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:68) Huo ni mtazamo mzuri sana, mfano bora kwelikweli!

16. Tunaweza kujaribiwaje, na tunapaswa kusitawisha mtazamo gani unaofaa?

16 Leo, sisi pia tunaweza kujaribiwa kama wanafunzi hao wa mapema. Huenda tukakata tamaa kwa sababu ahadi za Yehova hazitimizwi haraka kama tulivyotarajia. Huenda tukaona kwamba ufafanuzi wa Maandiko katika vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia ni mgumu kueleweka. Huenda tukavunjwa moyo na mwenendo wa Mkristo mwenzetu. Je, itakuwa sawa kuacha kutembea pamoja na Mungu kwa sababu hizo au nyingine kama hizo? Sivyo! Wanafunzi waliomwacha Yesu walikuwa na maoni ya kimwili. Tunapaswa kuepuka kutenda kama wao.

“Sisi Si Namna ya Watu Wanaorudi Nyuma”

17. Tunaweza kusaidiwaje kuendelea kutembea pamoja na Mungu?

17 Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Kupitia Biblia, Yehova anatuambia hivi waziwazi: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isaya 30:21) Kutii Neno la Mungu hutusaidia ‘kuendelea kuangalia sana jinsi tunavyotembea.’ (Waefeso 5:15) Kujifunza Biblia na kutafakari yale tunayojifunza hutuwezesha ‘kuendelea kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3) Naam, kama Yesu alivyosema, “roho ndiyo inayotokeza uzima; mwili hauna faida hata kidogo.” Mwongozo pekee unaotegemeka tunaoweza kufuata ili kuelekeza hatua zetu ni mwongozo wa kiroho, ambao hupatikana kupitia Neno la Yehova, roho yake, na tengenezo lake.

18. (a) Wengine hufanya nini kwa kukosa hekima? (b) Sisi husitawisha imani ya aina gani?

18 Leo, wale wanaoudhika kwa sababu ya maoni ya kimwili au matarajio yasiyotimizwa mara nyingi huanza kujishughulisha sana na mambo ya ulimwengu huu. Kwa kutotambua umuhimu wa nyakati tunazoishi, hawaoni uhitaji wa ‘kuendelea kukesha,’ nao huchagua kufuatia mambo ya ubinafsi badala ya kutanguliza faida za Ufalme. (Mathayo 24:42) Kutembea katika njia hiyo ni kukosa hekima. Ona maneno haya ya mtume Paulo: “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Kama Enoko na Noa, sisi pia tunaishi nyakati za misukosuko, lakini kama wao, tuna pendeleo la kutembea pamoja na Mungu. Tukifanya hivyo, tuna tarajio lililohakikishwa kwamba tutaona ahadi za Yehova zikitimizwa, uovu ukikomeshwa, na ulimwengu mpya wenye uadilifu ukija. Hilo ni tarajio zuri kama nini!

19. Mika anaelezaje njia ya waabudu wa kweli?

19 Kwa mwongozo wa roho ya Mungu, nabii Mika alisema kwamba mataifa ya ulimwengu ‘yatatembea kila moja katika jina la mungu wake.’ Kisha akasema hivi kujihusu yeye mwenyewe na waabudu wengine waaminifu: “Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Ikiwa azimio lako ni kama la Mika, dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova hata nyakati za misukosuko ziwe mbaya namna gani. (Yakobo 4:8) Acheni kila mmoja wetu atamani kutoka moyoni mwake kutembea pamoja na Yehova Mungu wetu sasa na mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele!

Ungejibuje?

• Siku za Noa zinafananaje na nyakati za leo?

• Noa na familia yake walifuata njia gani, nasi tunawezaje kuiga imani yao?

• Baadhi ya wafuasi wa Yesu walikuwa na mtazamo gani usiofaa?

• Wakristo wa kweli wameazimia kufanya nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kama ilivyokuwa katika siku za Noa, leo watu wanahangaikia tu shughuli zao za kila siku

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tukiwa wahubiri wa Ufalme “sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma”