Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafuasi wa Menno Watafuta Kweli ya Biblia

Wafuasi wa Menno Watafuta Kweli ya Biblia

Wafuasi wa Menno Watafuta Kweli ya Biblia

ASUBUHI moja mnamo Novemba 2000, wamishonari fulani wa Mashahidi wa Yehova nchini Bolivia, walichungulia kwenye dirisha la nyumba yao ndogo na kuona kikundi cha wanaume na wanawake langoni. Watu hao waliokuwa wamevaa mavazi yasiyo na madoido walikuwa na wasiwasi. Wamishonari walipowafungulia, maneno yao ya kwanza yalikuwa, “Tunataka kujua kweli ya Biblia.” Wageni hao walikuwa Wafuasi wa Menno. Wanaume walikuwa wamevalia nguo za kazi na wanawake walikuwa na aproni nyeusi, na walisemezana katika lahaja ya Kijerumani. Walikuwa na woga na walitazama-tazama nyuma ili waone ikiwa walikuwa wakifuatwa. Hata hivyo, mwanamume mmoja kijana alisema hivi alipokuwa akipanda ngazi ya nyumba: “Ninataka kuwajua watu wanaotumia jina la Mungu.”

Wageni hao walistarehe walipokaribishwa na kuandaliwa viburudisho. Walikuwa wamesafiri kutoka kijiji cha mbali cha wakulima, ambako kwa miaka sita walikuwa wakipokea gazeti la Mnara wa Mlinzi kwa njia ya posta. “Tumesoma kwamba kutakuwa na paradiso duniani. Je, hilo ni kweli?” wakauliza. Mashahidi waliwaonyesha jibu la Biblia. (Isaya 11:9; Luka 23:43; 2 Petro 3:7, 13; Ufunuo 21:3, 4) Kisha, mkulima mmoja akawaambia wenzake, “Mwaona, ni kweli kwamba kutakuwa na paradiso duniani!” Wengine wakarudia-rudia kusema hivi: “Tumepata kweli.”

Wafuasi wa Menno ni akina nani? Wanaamini nini? Ili kujibu maswali hayo, tunahitaji kuchunguza mambo yaliyotukia katika karne ya 16.

Wafuasi wa Menno Ni Akina Nani?

Katika miaka ya 1500, wakati kutafsiri na kuchapisha Biblia katika lugha za kawaida kulipopamba moto huko Ulaya, watu wengi walitaka kujifunza Biblia barani humo. Martin Luther na viongozi wengine wa Marekebisho Makubwa ya Kidini waliyakataa mafundisho mengi ya Kanisa Katoliki. Hata hivyo, yale makanisa mapya ya Protestanti yaliendeleza desturi nyingi zisizotokana na Biblia. Kwa mfano, makanisa mengi yalidai watoto wote waliotoka tu kuzaliwa wabatizwe ili wawe wafuasi wa makanisa hayo. Hata hivyo, watu fulani waliotafuta kweli walitambua kwamba kabla mtu hajabatizwa, alihitaji kujifunza na kisha kuamua mwenyewe kuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo. (Mathayo 28:19, 20) Wahubiri wenye bidii waliokuwa na imani hiyo walianza kusafiri katika miji na vijiji wakifundisha Biblia na kuwabatiza watu wazima. Hivyo, wakaitwa Wanabaptisti, neno linalomaanisha “kubatizwa mara ya pili.”

Menno Simons alikuwa mmoja wa watu waliochunguza dini ya Wanabaptisti ili apate kweli. Yeye alikuwa kasisi wa Kanisa Katoliki katika kijiji cha Witmarsum, kaskazini mwa Uholanzi. Kufikia mwaka wa 1536, alikuwa amejitenga kabisa na Kanisa Katoliki, na tangu hapo akawa akisakwa na viongozi wa kanisa hilo. Mnamo 1542, Maliki Mtakatifu wa Roma, Charles wa Tano, aliahidi mwenyewe kwamba yeyote ambaye angemkamata Menno angepokea zawadi ya gilda 100 (pesa za zamani za Uholanzi). Hata hivyo, Menno aliwakusanya baadhi ya Wanabaptisti katika makundi. Punde yeye na wafuasi wake wakaanza kuitwa Wafuasi wa Menno.

Wafuasi wa Menno Leo

Muda si muda, kwa sababu ya mateso maelfu ya Wafuasi wa Menno walilazimika watoke Ulaya Magharibi na kukimbilia Amerika Kaskazini. Huko, walipata nafasi ya kuendelea kutafuta kweli na kueneza sana ujumbe wao. Lakini hawakujifunza Biblia na kuhubiri kwa bidii kama babu zao. Wengi wao walishikilia sana mafundisho fulani yasiyopatana na Biblia kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu, na moto wa mateso. (Mhubiri 9:5; Ezekieli 18:4; Marko 12:29) Leo, wamishonari wao hujitahidi sana kutoa huduma za kitiba na za kijamii kuliko wanavyojitahidi kueneza Injili.

Inakadiriwa kwamba kuna Wafuasi 1,300,000 wa Menno katika nchi 65. Lakini wengi wao husema kwamba hawana umoja, kama Menno Simons alivyosema karne nyingi zilizopita. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, waligawanyika sana kwa sababu ya kuwa na maoni yaliyotofautiana kuhusu mizozo ya ulimwengu. Wengi wao huko Amerika Kaskazini walikataa kujiunga na jeshi kwa sababu Biblia inakataza kufanya hivyo. Lakini kitabu An Introduction to Mennonite History kinasema hivi: “Kufikia mwaka wa 1914, makanisa ya Wafuasi wa Menno huko Ulaya Magharibi yalikuwa yameacha kupinga utumishi wa kijeshi.” Leo, Wafuasi fulani wa Menno hufuata mitindo ya kisasa. Baadhi yao bado hutumia vishikio vya zamani vya kufunga nguo badala ya vifungo, na wanaamini kwamba wanaume hawapaswi kunyoa ndevu.

Wafuasi fulani wa Menno, ambao wameazimia kujitenga na ulimwengu wa leo, wamehamia maeneo ambayo wameruhusiwa na wenye mamlaka waishi bila usumbufu. Kwa mfano, nchini Bolivia, inakadiriwa kwamba kuna Wafuasi 38,000 wa Menno wanaoishi katika vijiji vingi vya mbali, na kila kijiji kina kanuni zake za mwenendo. Motokaa haziruhusiwi katika vijiji fulani, lakini vigari vinavyokokotwa na farasi ndivyo tu vinavyoruhusiwa. Redio, televisheni, na muziki umepigwa marufuku katika vijiji vingine. Na katika vijiji fulani watu hukatazwa hata wasijifunze lugha ya nchi wanamoishi. Mkaaji wa kijiji fulani alisema hivi: “Wahubiri hawataki tujifunze Kihispania ili waendelee kutudhibiti.” Wengi huhisi kwamba wanakandamizwa nao huogopa kutengwa na jamii, jambo linalomwogopesha yeyote ambaye hajawahi kuishi nje ya jamii hiyo.

Jinsi Mbegu ya Kweli Ilivyopandwa

Akiwa chini ya hali zilizotajwa katika fungu lililotangulia, Johann, mkulima aliye Mfuasi wa Menno alipata gazeti la Mnara wa Mlinzi nyumbani kwa jirani yake. Johann na familia yake walikuwa wamehamia Mexico kutoka Kanada, na baadaye wakahamia Bolivia. Johann alitamani kupata msaada ili ajue kweli ya Biblia. Aliazima gazeti hilo.

Baadaye, alipokuwa akiuza mazao yake mjini, Johann alimwendea Shahidi aliyekuwa akiwatolea watu magazeti ya Mnara wa Mlinzi sokoni. Shahidi huyo alimwelekeza kwa mmishonari anayeongea Kijerumani, na muda si muda Johann akaanza kupokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi ya Kijerumani kwa njia ya posta. Walisoma kila gazeti kwa makini na kulipitisha kutoka familia moja hadi nyingine katika kijiji hicho mpaka likachakaa kabisa. Nyakati nyingine familia kadhaa zilikusanyika na kujifunza toleo fulani la Mnara wa Mlinzi hadi usiku wa manane na kusoma maandiko yote ya Biblia yaliyokuwamo katika gazeti. Johann alisadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ndio watu wanaofanya mapenzi ya Mungu duniani. Kabla hajafa, Johann alimwambia mkewe na watoto wake hivi: “Msiache kusoma Mnara wa Mlinzi. Litawasaidia kuelewa Biblia.”

Baadhi ya watu wa familia ya Johann walianza kuwaeleza majirani wao yale waliyokuwa wakijifunza katika Biblia. Waliwaambia hivi: “Dunia haitaharibiwa, bali Mungu ataifanya iwe paradiso. Na Mungu hawatesi watu katika moto wa mateso.” Muda si mrefu, wahubiri wa kanisa walijulishwa jambo hilo nao wakatisha kutenga familia ya Johann ikiwa hawangeacha kuhubiri. Baadaye, walipokuwa wakizungumzia upinzani wa wazee wao, mwanamume mmoja kijana alisema hivi: “Hatuna sababu ya kuwalalamikia wazee wa kanisa. Sote tunaijua dini ya kweli, lakini hatujachukua hatua yoyote.” Maneno hayo yalimgusa moyo baba ya kijana huyo. Punde si punde, watu kumi katika familia hiyo wakafunga safari ya siri ili kuwatafuta Mashahidi wa Yehova nao wakafika kwenye nyumba ya wamishonari, kama ilivyotajwa mwanzoni.

Siku iliyofuata, wamishonari walifunga safari ya kuwatembelea marafiki wao wapya huko kijijini. Motokaa ya wamishonari hao ndiyo iliyokuwa gari pekee barabarani. Walishangaa kuona vigari vilivyokokotwa na farasi, huku wenyeji wakishangaa kuwaona wageni hao. Hatimaye wakaketi mezani pamoja na watu kumi kutoka katika familia mbili za Wafuasi wa Menno.

Siku hiyo, walijifunza sura ya kwanza ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, * kwa muda wa saa nne. Wakulima hao walikuwa wametafuta maandiko ya ziada ya Biblia kwa kila fungu, nao walitaka kujua kama wameyaelewa vizuri. Baada ya swali kuulizwa, wakulima hao walisemezana katika lahaja yao ya Kijerumani kwa dakika kadhaa, kisha mmoja wao akajibu katika Kihispania kwa niaba ya wenzake. Ilikuwa siku yenye furaha sana, lakini sawa tu na Menno Simons alivyokabili majaribu alipoanza kutafuta kweli ya Biblia yapata miaka 500 iliyopita, wao pia wangekabili majaribu.

Kukabili Majaribu kwa Sababu ya Kweli

Siku chache baadaye, wazee wa kanisa walienda nyumbani kwa familia ya Johann na kuwatisha wote waliokuwa wakizungumza na Mashahidi na kuwalazimisha wafanye uamuzi. Waliwaambia hivi: “Tumesikia Mashahidi wa Yehova waliwatembelea. Ni lazima mwakataze wasirudi, na msipotupa vitabu vyao ili tuviteketeze, mtatengwa na jamii.” Hilo lilikuwa jaribu kubwa mno kwa sababu walikuwa wamejifunza Biblia pamoja na Mashahidi mara moja tu.

Mume mmoja alisema hivi: “Hatuwezi kufanya hivyo. Watu hao walikuja kutufundisha Biblia.” Wazee wa kanisa walitendaje? Waliwatenga kwa sababu ya kujifunza Biblia! Hilo lilikuwa pigo baya sana. Familia moja ilipoteza mapato kwa sababu maziwa yao hayakuchukuliwa wakati gari la kukokotwa la kiwanda cha jibini lilipopitia kwao. Mume fulani alifutwa kazi. Mwingine alizuiwa kununua bidhaa kwenye duka kijijini humo, na binti yake mwenye umri wa miaka kumi alifukuzwa shule. Majirani walizingira nyumba moja ili kumnyang’anya mume fulani mkewe, wakisema kwamba hangeweza kuishi na mume aliyetengwa na jamii. Licha ya hayo yote, familia hizo zilizokuwa zikijifunza Biblia hazikuacha kutafuta kweli.

Wamishonari walikuwa wakisafiri kwa muda mrefu kila juma ili kuongoza mafunzo hayo ya Biblia. Jambo hilo liliimarisha sana familia hizo! Familia fulani zilisafiri kwa saa mbili kwa vigari vilivyokokotwa na farasi ili ziwepo kwa ajili ya funzo. Familia hizo ziliguswa moyo wakati mmishonari mmoja alipoombwa kutoa sala kwa mara ya kwanza. Wafuasi wa Menno katika vijiji hivyo hawasali kamwe kwa sauti, hivyo, ilikuwa mara yao ya kwanza kusikia mtu akisali kwa ajili yao. Wanaume waliokuwapo walitokwa na machozi. Na wazia jinsi walivyoshangaa wakati wamishonari walipokuja na tepu-rekoda. Muziki haukuruhusiwa kamwe katika kijiji chao. Walifurahia sana muziki mtamu wa Kingdom Melodies hivi kwamba wakaamua kuimba nyimbo za Ufalme baada ya kila funzo! Lakini bado walikuwa na tatizo lingine. Wangewezaje kujiruzuku katika hali hizo ngumu?

Wanapata Ndugu Wenye Upendo

Kwa sababu walitengwa na jamii, wao wenyewe walianza kutengeneza jibini. Wamishonari waliwatafutia wateja. Shahidi mmoja wa siku nyingi huko Amerika Kaskazini, ambaye alikuwa amelelewa katika jamii ya Wafuasi wa Menno huko Amerika Kusini, alisikia kuhusu tatizo la familia hizo. Alitaka sana kuwasaidia, na siku chache baada ya kupata habari zao, alisafiri hadi Bolivia ili kuwatembelea. Mbali na kuwatia moyo kiroho, alisaidia familia hizo kununua gari lao wenyewe ili waweze kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na vilevile kupeleka mazao yao sokoni.

Mmoja wao anasema hivi: “Tulitaabika baada ya kutengwa na jamii. Tulienda kwenye Jumba la Ufalme tukiwa wenye huzuni, lakini tukarudi tukiwa na shangwe.” Bila shaka, Mashahidi wa eneo hilo walitambua matatizo yao na kuwasaidia. Baadhi yao walijifunza Kijerumani, na Mashahidi kadhaa huko Ulaya waliojua Kijerumani walihamia Bolivia ili wasaidie kuongoza mikutano ya Kikristo katika Kijerumani. Muda si muda, watu 14 kutoka katika jamii hiyo wakaanza kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme.

Katika Oktoba 12, 2001, yapata mwaka mmoja baada ya ile ziara ya kwanza ya kuwatembelea wamishonari, 11 kati ya watu hao ambao awali walikuwa Wanabaptisti, walibatizwa tena. Wakati huo, walibatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova. Tangu wakati huo, wengine pia wamebatizwa. Baadaye mmoja wao alisema hivi: “Tangu tulipojifunza kweli ya Biblia, tunahisi kama watumwa waliowekwa huru.” Mwingine alisema: “Wafuasi wengi wa Menno husema kwamba hawana upendo miongoni mwao. Lakini Mashahidi wa Yehova huwajali wenzao. Nahisi salama nikiwa kati yao.” Ikiwa unatafuta kweli ya Biblia, unaweza kukabili magumu. Lakini ukimwomba Yehova msaada na ukionyesha imani na ujasiri kama familia hizo, utafanikiwa na kupata furaha kama wao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Watu wanakubali kwa furaha vitabu vya Biblia katika Kijerumani

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ijapokuwa muziki haukuruhusiwa kamwe, sasa wao huimba baada ya kila funzo la Biblia