Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kutembea Kama Vile Yesu Kristo Alivyotembea

Endelea Kutembea Kama Vile Yesu Kristo Alivyotembea

Endelea Kutembea Kama Vile Yesu Kristo Alivyotembea

“Yeye anayesema kwamba anakaa katika muungano na [Mungu] yuko chini ya wajibu yeye mwenyewe pia kuendelea kutembea kama vile huyo [Yesu] alivyotembea.”—1 YOHANA 2:6.

1, 2. Ni nini kinachohusika katika kumtazama Yesu kwa makini?

MTUME Paulo aliandika hivi: “Acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu, huku tukimtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.” (Waebrania 12:1, 2) Ili tuendelee kuwa waaminifu tunahitaji kumtazama kwa makini Yesu Kristo.

2 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno la lugha ya awali linalotafsiriwa ‘tazama kwa makini’ linamaanisha “kukazia uangalifu bila kukengeushwa,” “kuacha kutazama kitu fulani ili kuona kingine,” na “kuendelea kutazama.” Kitabu kimoja kinasema hivi: “Mkimbiaji Mgiriki aliye katika uwanja wa michezo anapoacha kukazia fikira shindano la mbio na mradi ambao anajitahidi sana kuufikia, na badala yake kuwakazia fikira watazamaji, mwendo wake hupungua. Jambo kama hilo humpata Mkristo pia.” Tunaweza kukosa kufanya maendeleo ya kiroho tukikengeushwa na mambo fulani. Tunapaswa kumtazama kwa makini Yesu Kristo. Kwa nini tumtazame huyo Wakili Mkuu? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “wakili mkuu” linamaanisha “kiongozi mkuu, ambaye huongoza jambo lolote lile na kuweka kielelezo.” Ili tumtazame Yesu kwa makini tunahitaji kuiga kielelezo chake.

3, 4. (a) Tunahitaji kufanya nini ili tutembee kama vile Yesu Kristo alivyotembea? (b) Inafaa tufikirie maswali gani?

3 Biblia inasema hivi: “Yeye anayesema kwamba anakaa katika muungano na [Mungu] yuko chini ya wajibu yeye mwenyewe pia kuendelea kutembea kama vile huyo [Yesu] alivyotembea.” (1 Yohana 2:6) Ni lazima tukae katika muungano na Mungu kwa kushika amri za Yesu kama vile yeye alivyoshika amri za Baba yake.—Yohana 15:10.

4 Kwa hiyo, ili tutembee kama vile Yesu alivyotembea tunahitaji kumtazama kwa makini akiwa Kiongozi Mkuu na kufuata hatua zake kwa ukaribu. Inafaa tufikirie maswali haya muhimu yanayohusiana na jambo hilo: Kristo hutuongozaje leo? Kuiga jinsi alivyotembea kunapaswa kutuchocheaje? Tunapata faida gani tunaposhikamana na kielelezo ambacho Yesu Kristo aliweka?

Jinsi Kristo Anavyowaongoza Wafuasi Wake

5. Yesu aliwapa wafuasi wake ahadi gani kabla ya kwenda mbinguni?

5 Kabla ya kwenda mbinguni, Yesu Kristo aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake na kuwapa kazi muhimu. Alisema hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Katika pindi hiyo, Kiongozi huyo Mkuu aliwaahidi pia kwamba atakuwa pamoja nao wanapofanya kazi hiyo, aliposema hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20) Ni katika njia gani Yesu Kristo yuko pamoja na wafuasi wake wakati huu wa umalizio wa mfumo wa mambo?

6, 7. Yesu anatuongozaje kupitia roho takatifu?

6 Yesu alisema: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yohana 14:26) Roho takatifu, inayotumwa katika jina la Yesu, hutuongoza na kutuimarisha leo. Inatuelimisha kiroho na kutusaidia kuelewa “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Isitoshe, sifa za kimungu kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia” ni “matunda ya roho.” (Wagalatia 5:22, 23) Tunaweza kusitawisha sifa hizo kwa msaada wa roho takatifu.

7 Tunapojifunza Maandiko na kujitahidi kutumia mambo tunayojifunza, roho ya Yehova hutusaidia kuongeza hekima, utambuzi, uelewaji, ujuzi, hukumu, na uwezo wa kufikiri. (Methali 2:1-11) Pia, roho takatifu hutusaidia kuvumilia vishawishi na majaribu. (1 Wakorintho 10:13; 2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13) Wakristo wanahimizwa ‘wajisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, na kuukamilisha utakatifu.’ (2 Wakorintho 7:1) Je, tunaweza kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya utakatifu, au vya usafi, bila msaada wa roho takatifu? Njia moja ambayo Yesu anatumia leo kutuongoza ni roho takatifu, na Yehova Mungu amempa Mwana wake mamlaka aitumie roho hiyo.—Mathayo 28:18.

8, 9. Kristo hutumiaje “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kuliongoza kutaniko?

8 Ona njia nyingine ambayo Kristo anatumia kuliongoza kutaniko leo. Alipokuwa akizungumzia kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu alisema hivi: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa? Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.”—Mathayo 24:3, 45-47.

9 “Bwana” ni Yesu Kristo. “Mtumwa” ni kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta walio duniani. Jamii hiyo ya mtumwa imepewa kazi ya kutunza masilahi ya Yesu hapa duniani na kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Baraza Linaloongoza ni kikundi kidogo cha waangalizi wanaostahili ambao ni sehemu ya jamii ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Baraza hilo huwakilisha jamii ya mtumwa. Waangalizi hao huongoza kazi ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote na kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Hivyo, Kristo huliongoza kutaniko kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliyetiwa mafuta kwa roho na Baraza lake Linaloongoza.

10. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu wazee, na kwa nini?

10 Uongozi wa Kristo pia unaonekana kupitia “zawadi katika wanadamu,” yaani, wazee Wakristo, au waangalizi. Zawadi hizo zimetolewa “kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:8, 11, 12) Andiko la Waebrania 13:7 linasema hivi kuwahusu: “Wakumbukeni wale ambao wanaongoza katikati yenu, ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mnapotafakari jinsi mwisho wa mwenendo wao unavyokuwa, igeni imani yao.” Wazee huliongoza kutaniko. Kwa kuwa wanamwiga Kristo Yesu, imani yao inastahili kuigwa. (1 Wakorintho 11:1) Tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa mpango huo wa kuwa na wazee kwa kutii na kunyenyekea “zawadi [hizo] katika wanadamu.”—Waebrania 13:17.

11. Kristo huwaongozaje wafuasi wake leo, na ni nini kinachohusika katika kutembea kama vile alivyotembea?

11 Naam, Yesu Kristo anawaongoza wafuasi wake leo kupitia roho takatifu, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na wazee wa kutaniko. Kutembea kama vile Kristo alivyotembea kunahusisha kuelewa njia yake ya kuongoza na kujinyenyekeza chini ya uongozi huo. Kunahusisha pia kuiga njia yake ya kutembea. Mtume Petro aliandika hivi: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Kufuata kielelezo kikamilifu cha Yesu kunapaswa kutuchocheaje?

Uwe Mwenye Usawaziko Unapotumia Mamlaka

12. Ni jambo gani kuhusu kielelezo cha Kristo linalowahusu hasa wazee katika kutaniko?

12 Ingawa Yesu alipokea mamlaka nyingi sana kutoka kwa Baba yake, aliyatumia kwa usawaziko. Wote katika kutaniko, na hasa waangalizi, wanapaswa kuacha ‘usawaziko wao ujulikane kwa watu wote.’ (Wafilipi 4:5; 1 Timotheo 3:2, 3) Kwa kuwa wazee wana mamlaka fulani katika kutaniko, ni muhimu wafuate hatua za Kristo wanapoyatumia.

13, 14. Wazee wanawezaje kumwiga Kristo wanapowatia wengine moyo kumtumikia Mungu?

13 Yesu alitambua kwamba uwezo wa wanafunzi wake una mipaka. Hakuwalazimisha wafanye mambo yaliyopita uwezo wao. (Yohana 16:12) Bila kuwashurutisha, Yesu aliwatia moyo wafuasi wake ‘wajitahidi sana’ kufanya mapenzi ya Mungu. (Luka 13:24) Alifanya hivyo kwa kuwawekea kielelezo na kuwachochea. Vivyo hivyo, wazee Wakristo leo hawawatishi wengine wamtumikie Mungu kwa kuwaaibisha au kuwafanya wahisi wana hatia. Badala yake, wao huwatia moyo wamtumikie Yehova kwa sababu wanampenda yeye, Yesu, na wanadamu wenzao.—Mathayo 22:37-39.

14 Yesu hakutumia vibaya mamlaka aliyopewa kwa kutawala maisha ya watu. Hakuweka viwango visivyoweza kufikiwa au sheria nyingi mno. Aliwachochea watu kwa kufikia mioyo yao huku akitumia kanuni ambazo zilitegemeza sheria zilizotolewa kupitia Musa. (Mathayo 5:27, 28) Kwa kumwiga Yesu Kristo, wazee huepuka kuweka sheria zinazotegemea mapendezi yao au kusisitiza maoni yao. Katika mambo yanayohusiana na mavazi na mapambo au tafrija na burudani, wazee hujitahidi kufikia mioyo wakitumia kanuni za Mungu, kama zile zinazoonyeshwa kwenye Mika 6:8; 1 Wakorintho 10:31-33; na 1 Timotheo 2:9, 10.

Uwe Mwenye Huruma na Mwenye Kusamehe

15. Yesu alishughulikiaje kasoro za wanafunzi wake?

15 Kristo alituachia kielelezo cha kufuata kuhusiana na jinsi alivyoshughulikia kasoro na makosa ya wanafunzi wake. Fikiria mambo mawili yaliyotukia usiku wake wa mwisho akiwa mwanadamu duniani. Baada ya kufika Gethsemane, Yesu ‘alimchukua Petro na Yakobo na Yohana pamoja naye’ na kuwaambia ‘waendelee kukesha.’ Kisha baada ya ‘kusonga mbele kidogo, akaanguka chini na kuanza kusali.’ Aliporudi, “akawakuta wamelala usingizi.” Yesu alitendaje? Alisema: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Marko 14:32-38) Badala ya kuwakemea vikali Petro, Yakobo, na Yohana, aliwahurumia! Usiku huohuo, Petro alimkana Yesu mara tatu. (Marko 14:66-72) Yesu alimtendeaje Petro baadaye? “Bwana alifufuliwa naye alimtokea Simoni [Petro].” (Luka 24:34) Biblia inasema: “Alimtokea Kefa, kisha wale kumi na wawili.” (1 Wakorintho 15:5) Badala ya kuudhika, Yesu alimsamehe na kumwimarisha mtume huyo aliyetubu. Baadaye, Yesu alimpa Petro madaraka makubwa.—Matendo 2:14; 8:14-17; 10:44, 45.

16. Tunawezaje kutembea kama vile Yesu alivyotembea wakati waamini wenzetu wanapotuvunja moyo au kutukosea kwa njia fulani?

16 Waamini wenzetu wanapotuvunja moyo au kutukosea kwa njia fulani kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, je, hatupaswi pia kuwahurumia na kuwasamehe kama vile Yesu alivyofanya? Petro aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili, msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano, bali, kinyume chake, mkitoa baraka.” (1 Petro 3:8, 9) Vipi mtu asipotutendea kama vile Yesu alivyofanya, na kukosa kutuhurumia au kutusamehe? Hata katika hali hiyo, tuko chini ya wajibu wa kujitahidi kumwiga Yesu na kutenda kama vile ambavyo angetenda.—1 Yohana 3:16.

Tanguliza Mambo ya Ufalme

17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alitanguliza kufanya mapenzi ya Mungu maishani mwake?

17 Tunahitaji kutembea kama vile Yesu Kristo alivyotembea kwa njia nyingine pia. Jambo kuu zaidi katika maisha ya Yesu lilikuwa kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu. Baada ya kumhubiria mwanamke Msamaria karibu na jiji la Sikari huko Samaria, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Kufanya mapenzi ya Baba yake kulimtegemeza Yesu; kulimjenga, kulimridhisha, na kulimburudisha kama chakula. Bila shaka, tukimwiga Yesu kwa kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu tutapata uradhi na kuishi maisha yenye kusudi.

18. Ni baraka gani zinazotokana na kuwatia moyo watoto kufanya utumishi wa wakati wote?

18 Wazazi wanapowatia moyo watoto wao kuanza utumishi wa wakati wote, wao pamoja na watoto wao hupata baraka nyingi. Baba mmoja mwenye wavulana ambao ni mapacha aliwatia moyo tangu walipokuwa wachanga wajiwekee mradi wa kuwa mapainia. Walipomaliza shule, mapacha hao wakawa mapainia. Akikumbuka shangwe ambayo amepata kutokana na jambo hilo, baba huyo anasema hivi: “Wavulana wetu hawajatuvunja moyo. Tunaweza kusema hivi kwa furaha, ‘Wana ni urithi kutoka kwa Yehova.’” (Zaburi 127:3) Watoto hupata faida gani wanapofanya utumishi wa wakati wote? Mama mmoja mwenye watoto watano anasema: “Upainia umewasaidia watoto wangu wote kusitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, kuboresha mazoea yao ya kujifunza, kujifunza jinsi ya kutumia wakati wao kwa hekima, na kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwao. Ingawa wote walihitaji kufanya marekebisho mengi, hakuna yeyote kati yao anayejuta kwa sababu ya uchaguzi aliofanya.”

19. Vijana wanapaswa kufikiria mambo gani kuhusu wakati ujao?

19 Enyi vijana, mnataka kufanya nini wakati ujao? Je, mnajitahidi kuwa mabingwa wa kazi fulani ya kilimwengu? Au je, mnajitahidi kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi yenu kuu maishani? Paulo alitoa shauri hili: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” Kisha akaongeza hivi: “Kwa hiyo mwache kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.”—Waefeso 5:15-17.

Uwe Mshikamanifu

20, 21. Ni katika njia gani Yesu alikuwa mshikamanifu, nasi tunawezaje kuiga ushikamanifu wake?

20 Ili tutembee kama vile Yesu alivyotembea tunahitaji kuiga ushikamanifu wake. Biblia inasema hivi kuhusu ushikamanifu wa Yesu: “Ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu. Zaidi ya hayo, alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” Yesu alitetea kwa ushikamanifu enzi kuu ya Yehova kwa kujinyenyekeza kufanya mapenzi ya Mungu. Alikuwa mtiifu mpaka alipokufa juu ya mti wa mateso. Ni lazima ‘tuwe na mtazamo huo wa akili’ na kujinyenyekeza kwa ushikamanifu kufanya mapenzi ya Mungu.—Wafilipi 2:5-8.

21 Pia, Yesu alikuwa mshikamanifu kwa mitume wake waaminifu. Licha ya udhaifu na kutokamilika kwao, Yesu aliwapenda “mpaka mwisho.” (Yohana 13:1) Vivyo hivyo, hatupaswi kuruhusu kutokamilika kwa ndugu zetu kutufanye tuwe wachambuzi.

Shikamana na Kielelezo Kilichowekwa na Yesu

22, 23. Kuna faida gani za kufuata kielelezo kilichowekwa na Yesu?

22 Bila shaka, tukiwa wanadamu wasio wakamilifu hatuwezi kufuata kwa ukamili hatua za yule aliye Kielelezo chetu kikamilifu. Hata hivyo, tunaweza kujitahidi kufuata hatua zake kwa ukaribu. Ili tufanye hivyo tunahitaji kuelewa na kujinyenyekeza kwa njia ambayo Kristo anatumia kuongoza na kushikamana na kielelezo alichoweka.

23 Tunapata baraka nyingi tunapomwiga Kristo. Tunapata kusudi na uradhi maishani kwa sababu tunakazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu badala ya mapenzi yetu wenyewe. (Yohana 5:30; 6:38) Tunakuwa na dhamiri njema. Tunawawekea wengine kielelezo pia kwa njia tunayotembea. Yesu aliwaalika wote wanaotaabika na kulemewa na mizigo waje kwake na kupata burudisho kwa ajili ya nafsi zao. (Mathayo 11:28-30) Tunapofuata kielelezo cha Yesu, sisi pia tunaweza kuwaburudisha wengine tunaposhirikiana nao. Basi, acheni tuendelee kutembea kama vile Yesu alivyotembea.

Je, Unakumbuka?

• Kristo anawaongozaje wafuasi wake leo?

• Wazee wanawezaje kuiga uongozi wa Kristo wanapotumia mamlaka yao waliyopewa na Mungu?

• Tunawezaje kuiga kielelezo cha Yesu tunaposhughulikia kasoro za wengine?

• Vijana wanawezaje kutanguliza mambo ya Ufalme?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazee Wakristo hutusaidia kufuata uongozi wa Kristo

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Enyi vijana, mnafanya mipango gani ili muwe na maisha ya Kikristo yenye kuridhisha?