Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunapaswa Kujali Jinsi Wengine Wanavyotuona?

Je, Tunapaswa Kujali Jinsi Wengine Wanavyotuona?

Je, Tunapaswa Kujali Jinsi Wengine Wanavyotuona?

KARIBU kila mtu hupenda kusifiwa. Kupongezwa kunaweza kutufanya tufurahi na kuhisi kwamba tumetimiza jambo fulani. Kukubaliwa hutufanya tutake kufanya mambo vizuri hata zaidi. Sisi huhisi tofauti tunapofikiria kwamba watu wengine hawapendi mambo tunayofanya. Ubaridi au uchambuzi unaweza kutuvunja moyo. Jinsi watu wanavyotuona kunaweza kuchochea sana maoni tuliyo nayo kujihusu.

Lingekuwa kosa kupuuza jinsi wengine wanavyotuona. Kwa kweli, tunaweza kufaidika wengine wanapochunguza mwenendo wetu. Yanapotegemea kanuni za juu za maadili, maoni ya wengine yanaweza kutufaidi na kutuchochea kuwa wanyoofu. (1 Wakorintho 10:31-33) Hata hivyo, mara nyingi maoni ya watu si ya haki. Fikiria maoni yenye kupotoka ambayo wakuu wa makuhani na wengine walikuwa nayo juu ya Yesu Kristo ‘walipoanza kupiga kelele, wakisema: “Mtundike mtini! Mtundike mtini!”’ (Luka 23:13, 21-25) Huenda ikafaa kupuuza maoni yanayotegemea habari za uwongo au yanayochochewa na wivu au ubaguzi. Hivyo, tunahitaji kutenda ifaavyo na kuitikia maoni ya wengine kwa hekima.

Ni Maoni ya Nani Yaliyo Muhimu?

Tunataka kukubaliwa na wale tunaoshirikiana nao kwa ukaribu katika ibada ya kweli. Hao wanatia ndani watu wa familia ambao ni waamini na pia ndugu na dada zetu Wakristo. (Waroma 15:2; Wakolosai 3:18-21) Kuwapenda na kuwaheshimu waamini wenzetu na pia “ubadilishanaji wa kitia-moyo” miongoni mwao ni muhimu kwetu. (Waroma 1:11, 12) Kwa ‘unyenyekevu wa akili, tunawaona wengine kuwa bora kuliko sisi.’ (Wafilipi 2:2-4) Isitoshe, tunataka na tunathamini kukubaliwa na “wale wanaoongoza” katikati yetu, yaani, wazee katika kutaniko.—Waebrania 13:17.

Pia “ushuhuda mzuri kutoka kwa watu walio nje” ni jambo linalopendeza. (1 Timotheo 3:7) Inatia moyo kama nini kuona watu wa ukoo wasio waamini, wafanyakazi wenzetu, na majirani wetu wakituheshimu! Na je, hatujaribu kuwavutia watu tunaowahubiria ili wapendezwe na ujumbe wa Ufalme? Tunaposifika katika jamii kuwa watu safi kiadili na wanyoofu hilo humletea Mungu utukufu. (1 Petro 2:12) Hata hivyo, hatuwezi kuvunja kanuni za Biblia ili kuwapendeza wengine, wala hatuwezi kutenda kwa unafiki ili kuwavutia. Tunapaswa kutambua kwamba haiwezekani kumpendeza kila mtu. Yesu alisema hivi: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.” (Yohana 15:19) Je, tunaweza kufanya jambo lolote ili kuheshimiwa na wale wanaotupinga?

Kuheshimiwa na Wapinzani

Yesu alitoa onyo hili: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 10:22) Nyakati nyingine hisia hizo zenye chuki hutokeza shutuma kali. Huenda maofisa wa serikali wenye upendeleo wakasema kwamba sisi ni “wachochezi” au “wanamapinduzi.” Wapinzani wenye kusema mambo waziwazi wanaweza kutushutumu kuwa madhehebu hatari yanayopaswa kunyamazishwa. (Matendo 28:22) Nyakati nyingine, shutuma hizo za uwongo zinaweza kupingwa. Jinsi gani? Kwa kufuata shauri hili la mtume Petro: “[Iweni] tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Petro 3:15) Isitoshe, tunapaswa “kuwa na maneno yenye afya yasiyoweza kulaumiwa; ili mtu anayepinga aone aibu, akiwa hana jambo lolote baya la kusema juu yetu.”—Tito 2:8.

Ingawa tunajaribu kuliondolea jina letu suto, hatupaswi kuvunjika moyo tunaposhutumiwa isivyofaa. Yesu, Mwana mkamilifu wa Mungu, alishutumiwa kuwa mwenye kukufuru, mchochezi, na hata kuwa ana roho waovu. (Mathayo 9:3; Marko 3:22; Yohana 19:12) Mtume Paulo aliharibiwa sifa. (1 Wakorintho 4:13) Yesu na Paulo walipuuza shutuma hizo nao wakaendelea kuwa wenye shughuli nyingi katika utendaji wao. (Mathayo 15:14) Walijua kwamba hawangeweza kukubaliwa na adui zao, kwani “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Leo, tunakabili tatizo kama hilo. Hatupaswi kutishwa wapinzani wenye chuki wanaposambaza uwongo mwingi kutuhusu.—Mathayo 5:11.

Maoni Yaliyo Muhimu Zaidi

Yale watu wanayofikiri kutuhusu yanatofautiana, ikitegemea nia yao na yale ambayo wamesikia kutuhusu. Wengine wanatusifu na kutuheshimu, na wengine wanatutukana na kutuchukia. Hata hivyo, kwa kuwa tunaongozwa na kanuni za Biblia, tuna kila sababu ya kuwa wenye furaha na amani.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Tunakubaliwa na Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, tunapokubali kwa shukrani Neno la Mungu lituongoze katika kila jambo. Hata hivyo, maoni yaliyo muhimu zaidi ni yale ya Yehova na ya Mwana wake. Yale wanayofikiri kutuhusu ndiyo muhimu sana. Kwa vyovyote vile, maisha yetu yanategemea kibali chao.—Yohana 5:27; Yakobo 1:12.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

“Kusifiwa huniaibisha, kwa kuwa moyoni mimi hutamani kusifiwa.”—RABINDRANATH TAGORE, MTUNGA-MASHAIRI MHINDI

[Picha katika ukurasa wa 31]

Maoni ya waamini wenzetu ni muhimu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 30]

Culver Pictures