Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Alikuwa Mungu au Mwanadamu?

Je, Yesu Alikuwa Mungu au Mwanadamu?

Je, Yesu Alikuwa Mungu au Mwanadamu?

“MIMI ndiye nuru ya ulimwengu. Yule anayenifuata hatatembea kamwe katika giza, bali atakuwa na nuru ya uzima.” (Yohana 8:12) Maneno hayo yalisemwa na Yesu Kristo. Msomi mmoja wa karne ya kwanza aliandika hivi kumhusu: “Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.” (Wakolosai 2:3) Isitoshe, Biblia inasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ili tupate uradhi wa kiroho, tunapaswa kuwa na ujuzi sahihi kumhusu Yesu.

Watu wengi duniani wamesikia kumhusu Yesu Kristo. Amekuwa na uvutano mkubwa katika historia ya wanadamu. Hata kalenda zinazotumiwa katika sehemu nyingi za ulimwengu zinategemea mwaka ambao inadhaniwa alizaliwa. “Watu wengi hutaja tarehe zinazotangulia mwaka huo kuwa K.K., au kabla ya Kristo,” kinasema kitabu The World Book Encyclopedia. “Wanatumia A.D., au anno Domini (katika mwaka wa Bwana wetu), wanapotaja tarehe za baada ya mwaka huo.”

Hata hivyo, watu wana maoni mbalimbali kumhusu Yesu. Kwa wengine, alikuwa mtu wa pekee anayejulikana katika historia. Lakini wengine wanamwabudu kama Mungu Mweza-Yote. Wasomi fulani Wahindu wamemlinganisha Yesu Kristo na Krishna, mungu wa Wahindu ambaye watu wengi wanasema ni mungu katika mwili. Je, Yesu alikuwa mwanadamu tu, au alikuwa mtu anayepaswa kuabudiwa? Kwa kweli, Yesu alikuwa nani? Alitoka wapi? Alikuwa na utu wa aina gani? Na yuko wapi leo? Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, kitabu kinachozungumzia habari nyingi kumhusu Yesu kinatoa majibu ya kweli kwa maswali hayo.