Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kumwogopa Yehova—Hiyo Ndiyo Hekima”

“Kumwogopa Yehova—Hiyo Ndiyo Hekima”

“Kumwogopa Yehova—Hiyo Ndiyo Hekima”

“HUU ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:13) Hiyo ni kauli yenye nguvu sana ambayo Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alitoa kwa mwongozo wa roho ya Mungu! Pia mzee wa ukoo Ayubu alielewa thamani ya kumwogopa Mungu, aliposema hivi: “Tazama! Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima, na kuacha ubaya ni uelewaji.”—Ayubu 28:28.

Biblia inakazia sana umuhimu wa kumwogopa Yehova. Kwa nini ni hekima kumwogopa na kumheshimu Mungu? Ni katika njia gani kumwogopa Mungu hutufaidi tukiwa mtu mmoja-mmoja au tukiwa kikundi cha waabudu wa kweli? Maswali hayo yanajibiwa katika Methali sura ya 14 mstari wa 26 hadi 35. *

Chanzo cha “Uhakika Wenye Nguvu”

Sulemani anasema hivi: “Katika kumwogopa Yehova kuna uhakika wenye nguvu, na wanawe watakuwa na kimbilio.” (Methali 14:26) Yehova, Mungu Mweza-Yote aliye mshikamanifu, ndiye chanzo cha tumaini la mtu anayemwogopa Mungu. Haishangazi kwamba mtu huyo hukabili wakati ujao akiwa na uhakika wenye nguvu! Anaishi kwa muda mrefu na kupata baraka.

Hata hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu wakati ujao wa wale wanaoweka matumaini yao katika ulimwengu—miradi yake, mashirika yake, dhana zake, na mali zake? Hata wawe na matumaini gani, wakati wao ujao ni mfupi, kwa kuwa Biblia inasema: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Hivyo, je, tuna sababu yoyote ya ‘kuupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu’?—1 Yohana 2:15.

Ni hatua gani ambazo wazazi wanaomwogopa Mungu wanaweza kuchukua ili kuhakikisha kwamba ‘kutakuwa na kimbilio’ kwa watoto wao? Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Njooni, enyi wana, nisikilizeni; nitawafundisha kumwogopa Yehova.” (Zaburi 34:11) Watoto wanapofundishwa kumwogopa Mungu kupitia kielelezo na maagizo ya wazazi, yaelekea watakomaa na kuwa wanaume na wanawake wanaomtumaini Yehova kabisa.—Methali 22:6.

Sulemani anaendelea kusema: “Kumwogopa Yehova ni kisima cha uzima, ili kuepuka mitego ya kifo.” (Methali 14:27) Kumwogopa Yehova ni “kisima cha uzima” kwa sababu Mungu wa kweli ni “chemchemi ya maji yaliyo hai.” (Yeremia 2:13) Kumjua Yehova na Yesu Kristo kunaweza kumaanisha kwetu uzima wa milele. (Yohana 17:3) Pia kumwogopa Mungu kunatuepusha na mitego ya kifo. Jinsi gani? Andiko la Methali 13:14 linasema hivi: “Sheria ya mwenye hekima ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya kifo.” Tunapomwogopa Yehova, kutii sheria zake, na kuruhusu Neno lake liongoze hatua zetu, tunalindwa kutokana na mazoea na hisia zenye kudhuru ambazo zinaweza kutokeza kifo cha mapema.

“Pambo la Mfalme”

Karibu muda wote wa utawala wake, Sulemani alikuwa mfalme aliyemwogopa na kumtii Yehova. Hilo lilimsaidia kufanikiwa katika utawala wake. Ni nini huamua ikiwa mfalme fulani anatawala vizuri? Andiko la Methali 14:28 linajibu hivi: “Wingi wa watu ni pambo la mfalme, lakini kukosekana kwa watu ni uharibifu wa ofisa mkuu.” Kufanikiwa kwa mfalme huonyeshwa na hali njema ya raia wake. Watu wengi wakitamani kuendelea kutawaliwa naye, hilo huonyesha kwamba yeye ni mtawala mzuri. Sulemani alikuwa “na raia kutoka bahari [Nyekundu] mpaka bahari [ya Mediterania] na kutoka ule Mto [Efrati] mpaka miisho ya dunia.” (Zaburi 72:6-8) Utawala wake ulikuwa na amani na ufanisi usio na kifani. (1 Wafalme 4:24, 25) Utawala wa Sulemani ulifanikiwa. Kwa upande mwingine, kukataliwa na raia ni aibu kwa mtawala.

Hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu utukufu wa Sulemani Mkuu, Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo? Fikiria raia alio nao hata leo. Toka upande mmoja wa dunia hadi ule mwingine, wanaume na wanawake zaidi ya milioni sita wanaomwogopa Mungu tayari wamechagua kuishi chini ya utawala wa Kristo. Wanamwamini Yesu na wameunganishwa katika ibada ya kweli ya Mungu aliye hai. (Yohana 14:1) Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu, wote walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa. Kisha dunia paradiso itajaa watu wenye furaha, waadilifu ambao wamemthamini Mfalme wao. Hilo litaonyesha wazi kabisa mafanikio ya utawala wa Kristo. Acheni tushikamane sana na tumaini letu zuri la Ufalme.

Faida za Kimwili na za Kiroho

Kumwogopa na kumheshimu Mungu kunaweza kutufanya tuwe na utulivu moyoni na amani ya akili. Hilo ni kweli kwa sababu sehemu mbalimbali za hekima zinatia ndani uamuzi mzuri na utambuzi. Andiko la Methali 14:29 linasema: “Yule ambaye si mwepesi wa hasira ana utambuzi mwingi, lakini anayekosa subira anainua upumbavu.” Utambuzi hutusaidia kuelewa kwamba hasira isiyozuiliwa ina matokeo mabaya kwa hali yetu ya kiroho. ‘Uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, na magomvi’ yanaorodheshwa kati ya matendo ambayo yanaweza kutuzuia ‘tusirithi ufalme wa Mungu.’ (Wagalatia 5:19-21) Tunashauriwa tusiendelee kukasirika hata tukiwa na sababu halali ya kufanya hivyo. (Waefeso 4:26, 27) Kukosa subira kunaweza kutufanya tuseme na kutenda kwa upumbavu na kujuta baadaye.

Akionyesha madhara makubwa ya kimwili yanayosababishwa na hasira, mfalme wa Israeli anasema: “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama, lakini wivu hufanya mifupa iwe na ubovu.” (Methali 14:30) Magonjwa yanayosababishwa na hasira na ghadhabu yanatia ndani matatizo ya kupumua, kupanda kwa shinikizo la damu, magonjwa ya ini, na magonjwa yanayoathiri kongosho. Madaktari pia wamesema kwamba hasira na ghadhabu ni hisia zinazozidisha au kusababisha magonjwa kama vile vidonda vya tumbo, mabaka yanayotokea kwenye ngozi, pumu, magonjwa ya ngozi, na matatizo ya kumeng’enya chakula. Kwa upande mwingine, “amani rohoni humpa mtu afya.” (Methali 14:30, Biblia Habari Njema) Hivyo, tunakuwa wenye hekima ‘tunapofuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.’—Waroma 14:19.

Kumwogopa Mungu Hutusaidia Tusiwe na Ubaguzi

Sulemani anasema hivi: “Yeye anayempunja mtu wa hali ya chini amemletea shutuma Mtengenezaji wake, lakini anayemwonyesha maskini kibali anamtukuza Yeye.” (Methali 14:31) Mtu anayemwogopa Mungu anatambua kwamba wanadamu wote wamefanyizwa na Mtengenezaji mmoja, Yehova Mungu. Hivyo, mtu wa hali ya chini ni mwanadamu mwenzako, na jinsi unavyomtendea kutamfurahisha au kumhuzunisha Muumba wa mwanadamu. Ili kumtukuza Mungu, tunapaswa kuwatendea wengine kwa haki na bila ubaguzi. Mkristo aliye maskini anapaswa kusaidiwa kiroho bila ubaguzi. Tunapaswa kuwahubiria maskini na matajiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.

Akizungumzia faida nyingine ya kumwogopa Mungu, mfalme mwenye hekima anasema hivi: “Kwa sababu ya ubaya wake mwovu atasukumwa chini, lakini mwadilifu atakuwa akipata kimbilio katika utimilifu wake.” (Methali 14:32) Mwovu anasukumwaje chini? Wasomi fulani wa Biblia wamesema kwamba hilo linamaanisha hakuna uwezekano wa mtu huyo kurudia hali yake ya kawaida baada ya kupatwa na msiba. Kwa upande mwingine, msiba unapotokea, mtu anayemwogopa Mungu anapata kimbilio katika utimilifu wake kwa Mungu. Kwa kumtumaini Yehova kabisa hadi kifo, anaonyesha azimio lilelile aliloonyesha Ayubu, aliyesema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

Ili tudumishe utimilifu tunahitaji kumwogopa Mungu na kusitawisha hekima. Basi hekima inaweza kupatikana wapi? Andiko la Methali 14:33 linajibu hivi: “Hekima hukaa moyoni mwa mtu mwenye uelewaji, nayo hujulikana kati ya wajinga.” Ndiyo, hekima inaweza kupatikana moyoni mwa mtu mwenye uelewaji. Hata hivyo, hekima inawezaje kujulikana kati ya wajinga? Kulingana na kitabu kimoja, “mpumbavu ambaye anatamani kuonekana kuwa mwenye hekima, huropoka maneno anayofikiri kuwa ya hekima, lakini anapofanya hivyo anaonekana kuwa mpumbavu.”

“Huinua Taifa”

Baada ya kutuonyesha jinsi mtu anayemwogopa Mungu anavyotenda, mfalme wa Israeli anatuonyesha pia matokeo ya kumwogopa Mungu kwa taifa zima anaposema hivi: “Uadilifu huinua taifa, lakini dhambi ni aibu kwa vikundi vya mataifa.” (Methali 14:34) Kanuni hiyo ilionekana wazi kuhusu taifa la Israeli. Kushikamana na viwango vya juu vya Mungu kulifanya Waisraeli wainuliwe juu ya mataifa jirani. Hata hivyo, kurudia-rudia matendo ya kutotii kulifanya Waisraeli waaibishwe na hatimaye kukataliwa na Yehova. Kanuni hiyo inawahusu watu wa Mungu leo. Kutaniko la Kikristo ni tofauti na ulimwengu kwa sababu linashikamana na kanuni za uadilifu za Mungu. Hata hivyo, ili kudumisha hali hiyo ya juu, kila mmoja wetu anapaswa kuishi maisha safi kiadili. Kutenda dhambi kunatuaibisha na pia kunaleta suto juu ya kutaniko na juu ya Mungu.

Akizungumza kuhusu jambo linalomfurahisha mfalme, Sulemani anasema: “Furaha ya mfalme imo katika mtumishi anayetenda kwa ufahamu, lakini ghadhabu yake humjia mtu anayetenda kwa aibu.” (Methali 14:35) Nalo andiko la Methali 16:13 linasema hivi: “Midomo ya uadilifu ni furaha ya mfalme mkuu; naye humpenda mtu anayesema mambo ya unyoofu.” Ndiyo, Kiongozi na Mfalme wetu, Yesu Kristo, anafurahi sana tunapotenda kwa uadilifu na ufahamu na kutumia midomo yetu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Basi, acheni tuwe wenye shughuli nyingi katika kazi hiyo, huku tukifurahia baraka zinazotokana na kumwogopa Mungu wa kweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa maelezo kuhusu Methali 14:1-25, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 2004, ukurasa wa 26-29, na Julai 15, 2005, ukurasa wa 17-20.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Watu wanaweza kufunzwa kumwogopa Mungu