Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, kucheza michezo ya kompyuta yenye jeuri kwaweza kuathiri uhusiano wa mtu na Yehova?

Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliandika hivi: “Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.” (Zaburi 11:5) Katika lugha ya awali, neno “kuchukia” linaweza kuwa na maana ya “adui.” Kwa hiyo, mtu yeyote anayependa jeuri anajifanya kuwa adui ya Mungu. Basi, swali ambalo tunahitaji kufikiria ni hili: Je, kucheza michezo fulani ya kompyuta kunaweza kumfanya mtu apende jeuri?

Michezo ya kompyuta yenye jeuri hutukuza matumizi ya silaha. Inamfundisha mchezaji kupigana. Gazeti The Economist linasema hivi: “Jeshi la Marekani linatumia michezo ya kompyuta katika mazoezi. Michezo fulani ambayo inatumiwa jeshini, inapatikana madukani.”

Ni kweli kwamba wote wanaocheza michezo ya kompyuta yenye jeuri hawawadhuru watu halisi. Lakini huenda kupendezwa na vitumbuizo kama hivyo kukaonyesha nini kuhusu hali ya mioyo yao? (Mathayo 5:21, 22; Luka 6:45) Ungekata kauli gani kuhusu mtu anayefurahia kuwadunga wengine kisu, kuwapiga risasi, kuwalemaza, na kuwaua watu wa kuwaziwa? Vipi mtu huyo akitumia saa nyingi kila juma kutosheleza tamaa hiyo ya kupenda jeuri, na hata kuwa mtumwa wa michezo hiyo? Angalau utakata kauli kwamba ameanza kupenda jeuri kama vile mtu anayetazama picha chafu anavyositawisha tamaa mbaya.—Mathayo 5:27-29.

Ni kwa kiwango gani Yehova humchukia mtu anayependa jeuri? Daudi alisema kwamba Yehova ‘hakika anamchukia.’ Katika siku za Noa, Yehova alionyesha kwamba anawachukia kabisa wale wanaopenda jeuri. Yehova alimwambia Noa hivi: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu, kwa maana dunia imejaa jeuri kwa sababu yao; na tazama mimi ninawaharibu pamoja na dunia.” (Mwanzo 6:13) Mungu wa kweli aliuharibu ulimwengu wote wa wanadamu kwa sababu ya njia zao zenye jeuri. Alimhifadhi tu Noa na familia yake, yaani, watu wanane ambao hawakupenda jeuri.—2 Petro 2:5.

Watu wanaotaka kuwa marafiki wa Yehova ‘wanafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao kuwa miundu.’ Badala ya kujifunza kupenda jeuri, wao ‘hawajifunzi vita tena.’ (Isaya 2:4) Ili kuendelea kuwa marafiki wa Mungu badala ya kuwa adui zake, tunapaswa ‘kugeuka kutoka katika yaliyo mabaya na kufanya yaliyo mema.’ Tunahitaji ‘kutafuta amani na kuifuatilia.’—1 Petro 3:11.

Namna gani ikiwa tayari tumecheza michezo ya video yenye jeuri? Tunapaswa kuazimia kabisa kumpendeza Yehova kwa kuacha kutenda mambo anayochukia. Bila shaka, tunapaswa kuomba msaada wa roho takatifu ya Mungu ili tuache mazoea hayo yenye kudhuru kiroho. Tunaweza kuyaacha tukiruhusu sifa kama vile amani, wema, na kujizuia zifanye maisha yetu yapatane na njia za Mungu.—Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23.