Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Kwa Imani, Si Kwa Kuona!

Tembea Kwa Imani, Si Kwa Kuona!

Tembea Kwa Imani, Si Kwa Kuona!

“Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.”—2 WAKORINTHO 5:7.

1. Ni nini kinachoonyesha kwamba mtume Paulo alitembea kwa imani, si kwa kuona?

NI MWAKA wa 55 W.K. Miaka 20 hivi imepita tangu mtesaji wa Wakristo, aliyeitwa Sauli, alipokubali Ukristo. Ijapokuwa muda mrefu umepita, hajaruhusu imani yake katika Mungu idhoofike. Bado ana imani thabiti ingawa hajaona mambo yaliyo mbinguni kwa macho. Kwa sababu hiyo, alipokuwa akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa na tumaini la mbinguni, mtume Paulo alisema hivi: “Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.”—2 Wakorintho 5:7.

2, 3. (a) Tunaonyeshaje kwamba tunatembea kwa imani? (b) Ni nini maana ya kutembea kwa kuona?

2 Ili tutembee kwa imani tunahitaji kuamini kabisa uwezo wa Mungu wa kuongoza maisha yetu. Tunapaswa kuamini kabisa kwamba anajua kwelikweli mambo yanayoweza kutufaidi. (Zaburi 119:66) Tunapofanya maamuzi maishani na kutenda kupatana nayo, sisi hufikiria “mambo tusiyoyaona.” (Waebrania 11:1, BHN) Mambo hayo yanatia ndani “mbingu mpya na dunia mpya” iliyoahidiwa. (2 Petro 3:13) Kwa upande mwingine, kutembea kwa kuona kunamaanisha kufuata njia ya maisha inayotegemea tu mambo tunayoyaona kwa macho. Jambo hilo ni hatari kwa sababu linaweza kutufanya tupuuze kabisa mapenzi ya Mungu.—Zaburi 81:12; Mhubiri 11:9.

3 Iwe sisi ni wa “kundi dogo” ambao wana tumaini la kwenda mbinguni, au wa “kondoo wengine” ambao wana tumaini la kuishi duniani, kila mmoja wetu anapaswa kutii shauri la kutembea kwa imani bali si kwa kuona. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Hebu tuone jinsi kufuata shauri hilo lililoongozwa kwa roho ya Mungu kunavyoweza kutulinda ‘tusifurahie dhambi kwa muda,’ tusinaswe na mtego wa kupenda mali, na tusisahau kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. Pia, tutazungumzia hatari za kutembea kwa kuona.—Waebrania 11:25.

Kukataa “Kufurahia Dhambi kwa Muda”

4. Musa alichagua nini, na kwa nini?

4 Hebu wazia maisha ambayo Musa, mwana wa Amramu, angekuwa nayo. Kwa kuwa Musa alilelewa pamoja na watoto wa familia ya kifalme katika Misri ya kale, angeweza kupata mamlaka, utajiri, na umashuhuri. Musa angeweza kufikiri hivi: ‘Nina elimu nyingi katika hekima inayosifika ya Misri, nami nina nguvu katika maneno na matendo. Nikiendelea kushirikiana na familia ya mfalme, ninaweza kutumia cheo changu kuwafaidi ndugu zangu Waebrania wanaoonewa!’ (Matendo 7:22) Badala yake, Musa alichagua “kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu.” Kwa nini? Ni nini kilichomfanya Musa akatae mambo yote ambayo angepata Misri? Biblia inajibu hivi: “Kwa imani [Musa] aliondoka Misri, lakini bila kuogopa hasira ya mfalme, kwa maana aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:24-27) Musa aliamini kwamba Yehova hakosi kubariki uadilifu, na hilo lilimsaidia kukataa dhambi na kujihusisha katika raha zake za muda.

5. Mfano wa Musa unatutiaje moyo?

5 Mara nyingi sisi pia huhitaji kufanya maamuzi magumu kuhusiana na mambo kama haya: ‘Je, niache mazoea au tabia fulani ambazo hazipatani na kanuni za Biblia? Je, nikubali kufanya kazi inayoweza kunifaidi kimwili lakini inayoweza kunizuia nisifanye maendeleo ya kiroho?’ Mfano wa Musa unatutia moyo tusifanye maamuzi kama watu wa ulimwengu huu wasioona mbali; bali tunapaswa kuwa na imani katika hekima ya “Yeye asiyeonekana”—Yehova Mungu—ambayo inaona mambo ya wakati ujao. Kama Musa, acheni tuthamini urafiki wetu pamoja na Yehova kuliko kitu kingine chochote katika ulimwengu huu.

6, 7. (a) Esau alionyeshaje kwamba alipendelea kutembea kwa kuona? (b) Mfano wa Esau unatuonyaje?

6 Hebu ona tofauti kati ya Musa na Esau, mwana wa Isaka, mzee wa ukoo. Esau alitaka kutosheleza tamaa yake papo hapo. (Mwanzo 25:30-34) Kwa kuwa Esau ‘hakuthamini mambo matakatifu,’ alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza “kwa kubadilishana na mlo mmoja.” (Waebrania 12:16) Hakufikiria jinsi ambavyo uamuzi wake wa kuuza haki yake ya kuzaliwa ungeathiri uhusiano wake pamoja na Yehova au jinsi ambavyo wazao wake wangeathiriwa. Hakuwa na mtazamo wa kiroho. Esau alipuuza ahadi za Mungu zenye thamani na kuziona kuwa zenye thamani ndogo. Alitembea kwa kuona, si kwa imani.

7 Mfano wa Esau ni onyo kwetu leo. (1 Wakorintho 10:11) Tunapohitaji kufanya maamuzi, yawe makubwa au madogo, hatupaswi kushawishiwa na propaganda za ulimwengu wa Shetani, zinazosema kwamba mtu anapaswa kupata kile anachotaka papo hapo. Inafaa tujiulize hivi: ‘Je, ninaonyesha mtazamo kama wa Esau ninapofanya maamuzi? Je, kujitahidi kupata vitu ninavyotaka sasa kutanizuia nisitangulize mambo ya kiroho? Je, maamuzi ninayoyafanya yanahatarisha urafiki nilio nao pamoja na Mungu na tazamio la kupata thawabu wakati ujao? Ninawawekea wengine mfano gani?’ Maamuzi yetu yakionyesha kwamba tunathamini mambo matakatifu, Yehova atatubariki.—Methali 10:22.

Kuepuka Mtego wa Kupenda Mali

8. Wakristo wa Laodikia walipewa onyo gani, na kwa nini tunahitaji kulizingatia?

8 Katika ufunuo uliotolewa kwa mtume Yohana karibu na mwisho wa karne ya kwanza, Yesu Kristo aliyetukuzwa alituma ujumbe kwa kutaniko lililokuwa Laodikia, huko Asia Ndogo. Ujumbe huo ulionya juu ya kupenda mali. Ingawa Wakristo wa Laodikia walikuwa matajiri kimwili, walikuwa maskini kiroho. Badala ya kuendelea kutembea kwa imani, waliruhusu mali ziwazuie wasiwe na mtazamo wa kiroho. (Ufunuo 3:14-18) Upendo wa mali una matokeo hayohayo leo. Kupenda mali hudhoofisha imani yetu na kufanya tuache ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio’ la uzima. (Waebrania 12:1) Tusipokuwa waangalifu, “raha za maisha haya” zinaweza kufanya tupuuze mambo ya kiroho na kuyafanya ‘yasongwe kabisa.’—Luka 8:14.

9. Tunalindwaje tunaporidhika na kuthamini chakula cha kiroho?

9 Tunaweza kulindwa kiroho tukiwa na uradhi badala ya kutumia ulimwengu huu kwa ukamili na kujitajirisha kimwili. (1 Wakorintho 7:31; 1 Timotheo 6:6-8) Tunapotembea kwa imani bali si kwa kuona, tunapata shangwe katika paradiso ya kiroho ya sasa. Tunapokula chakula cha kiroho kinachotujenga, je, hatuchochewi ‘kupiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo’? (Isaya 65:13, 14) Isitoshe, tunafurahia kushirikiana na wale wanaoonyesha matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Ni muhimu kama nini turidhike na kuburudishwa na maandalizi ya kiroho ya Yehova!

10. Inafaa tujiulize maswali gani?

10 Inafaa tujiulize maswali haya: ‘Mimi huona mali kuwa muhimu kadiri gani? Je, ninatumia mali zangu kuponda raha tu au ninazitumia kuendeleza ibada ya kweli? Ni nini huniridhisha zaidi? Je, ni kujifunza Biblia na kufurahia ushirika kwenye mikutano ya Kikristo, au ni kuepuka madaraka ya Kikristo mwishoni mwa juma ili kufanya mambo mengine? Je, mimi hutenga siku nyingi za mwisho wa juma kwa ajili ya tafrija badala ya kutumia wakati huo katika huduma ya shambani na katika shughuli nyingine zinazohusiana na ibada safi?’ Kutembea kwa imani kunamaanisha tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Ufalme, huku tukitegemea kabisa ahadi za Yehova. —1 Wakorintho 15:58.

Kukumbuka Kwamba Mwisho Uko Karibu

11. Kutembea kwa imani hutusaidiaje kukumbuka kwamba mwisho uko karibu?

11 Kutembea kwa imani hutusaidia kuepuka kuwa na maoni ya kimwili kwamba mwisho uko mbali sana au hautakuja kamwe. Tofauti na watu wenye shaka ambao hudhihaki unabii wa Biblia, sisi hutambua jinsi matukio ya ulimwengu yanavyopatana na mambo ambayo Neno la Mungu lilitabiri kuhusu siku zetu. (2 Petro 3:3, 4) Kwa mfano, je, mtazamo na tabia za watu wengi hazionyeshi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho”? (2 Timotheo 3:1-5) Tukiwa na macho ya imani, tunatambua kwamba mambo yanayotukia sasa ulimwenguni si mambo yaliyotukia zamani tu ambayo yanajirudia. Badala yake, matukio hayo ni “ishara ya kuwapo [kwa Kristo] na ya umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 24:1-14.

12. Maneno ya Yesu kwenye Luka 21:20, 21 yalitimizwaje katika karne ya kwanza?

12 Fikiria jambo fulani lililotukia katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida ambalo lina ulinganifu leo. Yesu Kristo alipokuwa duniani, aliwaonya wafuasi wake hivi: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke.” (Luka 21:20, 21) Katika utimizo wa unabii huo, majeshi ya Roma, yakiongozwa na Sesho Galo, yalizingira Yerusalemu katika mwaka wa 66 W.K. Lakini majeshi hayo yaliondoka kwa ghafula, na hilo likatoa ishara na nafasi ili Wakristo waliokuwa huko ‘wakimbilie milimani.’ Katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalirudi, yakalishambulia jiji la Yerusalemu na kuharibu hekalu. Yosefo anaripoti kwamba zaidi ya Wayahudi milioni moja walikufa, na 97,000 walipelekwa utekwani. Mungu alitekeleza hukumu juu ya mfumo huo wa mambo wa Kiyahudi. Wale waliotembea kwa imani na kutii onyo la Yesu waliepuka msiba huo.

13, 14. (a) Ni mambo gani yatakayotukia hivi karibuni? (b) Kwa nini tunapaswa kuendelea kuwa macho kuona utimizo wa unabii wa Biblia?

13 Jambo kama hilo litatukia hivi karibuni katika siku zetu. Sehemu fulani za Umoja wa Mataifa zitahusika katika utekelezaji wa hukumu ya Mungu. Kama vile majeshi ya Roma katika karne ya kwanza yalivyokusudiwa kudumisha ile Pax Romana (Amani ya Roma), leo kusudi la Umoja wa Mataifa ni kudumisha amani. Ingawa majeshi ya Roma yalijaribu kudumisha usalama wa kadiri fulani kotekote katika ulimwengu wa wakati huo, majeshi hayo ndiyo yaliyoharibu Yerusalemu. Vivyo hivyo leo, unabii wa Biblia unaonyesha kwamba mamlaka fulani za kijeshi katika Umoja wa Mataifa zitaona dini kuwa kitu cha kuchukiza, nazo zitaharibu Yerusalemu la leo, yaani, dini zinazodai kuwa za Kikristo, pamoja na sehemu zile nyingine za Babiloni Mkubwa. (Ufunuo 17:12-17) Naam, dini zote za uwongo ulimwenguni zitaharibiwa hivi karibuni.

14 Uharibifu wa dini za uwongo ndio utakaokuwa mwanzo wa ile dhiki kuu. Mwishoni mwa ile dhiki kuu, sehemu zilizobaki za mfumo huu mbovu wa mambo zitaharibiwa. (Mathayo 24:29, 30; Ufunuo 16:14, 16) Kutembea kwa imani hutuwezesha kuendelea kuwa macho kuona utimizo wa unabii wa Biblia. Hatudanganywi kufikiri kwamba shirika lolote la kibinadamu kama vile Umoja wa Mataifa ndiyo njia ya Mungu ya kuleta amani na usalama wa kweli. Hivyo basi, je, njia yetu ya maisha haipasi kuonyesha kwamba tuna uhakika kuwa “ile siku kuu ya Yehova iko karibu?”—Sefania 1:14.

Kutembea kwa Kuona Ni Hatari Kadiri Gani?

15. Licha ya kuona baraka za Mungu, taifa la Israeli lilinaswa na mtego gani?

15 Mambo yaliyowapata Waisraeli wa kale yanaonyesha hatari za kuruhusu imani yetu idhoofishwe kwa sababu ya kutembea kwa kuona. Licha ya kuona yale mapigo kumi yaliyoaibisha miungu ya uwongo ya Misri na kushuhudia ukombozi wa ajabu kwenye Bahari Nyekundu, Waisraeli hawakutii nao wakatengeneza ndama ya dhahabu na kuanza kuiabudu. Walikosa subira nao wakachoka kumngojea Musa ambaye ‘alichukua muda mrefu kushuka kutoka mlimani.’ (Kutoka 32:1-4) Kukosa subira kuliwafanya waabudu sanamu inayoonekana kwa macho. Yehova alichukia jinsi walivyotembea kwa kuona, na “watu wapatao elfu tatu” wakauawa. (Kutoka 32:25-29) Inasikitisha kama nini wakati mwabudu wa Yehova leo anapofanya maamuzi yanayoonyesha kwamba hamtegemei Yehova na kwamba hana uhakika katika uwezo wa Mungu wa kutimiza ahadi zake!

16. Waisraeli waliathiriwaje na mambo waliyoona kwa macho?

16 Mambo ambayo Waisraeli waliona kwa macho yao yaliwaathiri kwa njia nyingine pia. Kutembea kwa kuona kulifanya watetemeke kwa woga mbele ya adui zao. (Hesabu 13:28, 32; Kumbukumbu la Torati 1:28) Kulifanya wadharau mamlaka ambayo Musa alipewa na Mungu na kulalamika kuhusu maisha yao. Ukosefu huo wa imani uliwafanya wapende nchi ya Misri iliyoongozwa na roho waovu badala ya Nchi ya Ahadi. (Hesabu 14:1-4; Zaburi 106:24) Hapana shaka kwamba Yehova alihuzunika sana alipoona jinsi watu wake walivyomdharau kabisa Mfalme wao asiyeonekana!

17. Ni nini kilichofanya Waisraeli wakatae mwongozo wa Yehova katika siku za Samweli?

17 Katika siku za nabii Samweli, taifa teule la Israeli lilinaswa tena na mtego wa kutembea kwa kuona. Watu walianza kutamani kuwa na mfalme ambaye wangeweza kumwona. Hata ingawa Yehova alikuwa ameonyesha kwamba yeye ndiye Mfalme wao, hilo halikutosha kuwawezesha kutembea kwa imani. (1 Samweli 8:4-9) Kwa hasara yao wenyewe, walikataa kwa upumbavu mwongozo mkamilifu wa Yehova, na badala yake wakatamani kuwa kama mataifa jirani.—1 Samweli 8:19, 20.

18. Tunajifunza nini kuhusu hatari za kutembea kwa kuona?

18 Tukiwa watumishi wa Yehova leo, tunathamini uhusiano wetu mzuri pamoja na Mungu. Tunataka sana kujifunza kutokana na matukio ya zamani na kutumia maishani mwetu maonyo hayo muhimu. (Waroma 15:4) Waisraeli walipotembea kwa kuona, walisahau kwamba Mungu ndiye aliyekuwa akiwaongoza kupitia Musa. Tusipokuwa waangalifu, sisi pia tunaweza kusahau kwamba Yehova Mungu na Musa Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, ndio wanaoliongoza kutaniko la Kikristo leo. (Ufunuo 1:12-16) Tunapaswa kujihadhari tusiwe na maoni ya kibinadamu kuelekea sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Tukiwa na maoni ya kibinadamu tunaweza kuanza kuwa na roho ya kulalamika na kuacha kuthamini wawakilishi wa Yehova na chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45.

Azimia Kutembea kwa Imani

19, 20. Umeazimia kufanya nini, na kwa nini?

19 Biblia inasema hivi: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Adui yetu mkuu ni Shetani Ibilisi. Lengo lake ni kuharibu imani yetu katika Yehova. Atatumia kishawishi chochote ambacho kinaweza kutuzuia tusitekeleze uamuzi wetu wa kumtumikia Mungu. (1 Petro 5:8) Ni nini kitakachotusaidia tusidanganywe na mambo tunayoyaona katika mfumo wa Shetani? Ni kutembea kwa imani, si kwa kuona! Kutegemea na kuamini ahadi za Yehova kutatulinda ili ‘imani yetu isivunjike.’ (1 Timotheo 1:19) Basi, acheni tuazimie kuendelea kutembea kwa imani, huku tukiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatubariki. Acheni tuendelee kusali ili tuponyoke mambo yote yaliyokusudiwa kutukia hivi karibuni.—Luka 21:36.

20 Tunapotembea kwa imani, si kwa kuona, tuna Kielelezo bora. Biblia inasema hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Makala inayofuata itaeleza jinsi tunavyoweza kuendelea kutembea kama vile alivyotembea.

Je, Unakumbuka?

• Mfano wa Musa na wa Esau ulikufunza nini kuhusu kutembea kwa imani bali si kwa kuona?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka kupenda mali?

• Kutembea kwa imani hutusaidiaje tusione kwamba mwisho uko mbali sana?

• Kwa nini kutembea kwa kuona ni hatari?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Musa alitembea kwa imani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, mara nyingi tafrija hukuzuia usitimize mambo ya kiroho?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Unalindwaje kwa kusikiliza Neno la Mungu?