Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umati wa Watu Unaanza Kumwabudu Yehova

Umati wa Watu Unaanza Kumwabudu Yehova

“Msaada Wangu Unatoka Kwa Yehova”

Umati wa Watu Unaanza Kumwabudu Yehova

UNABII wa Biblia ulitabiri kwamba katika siku zetu watu kutoka katika mataifa yote watamiminika kwenye ibada ya Yehova iliyoinuliwa. Kwa mfano, kupitia nabii Hagai, Yehova Mungu alitangaza hivi: “Nitayatikisa mataifa yote, navyo vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote vitaingia; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” (Hagai 2:7) Isaya na Mika walitabiri kwamba katika siku zetu, yaani, “siku za mwisho,” mataifa na vikundi vya watu watamwabudu Yehova katika njia inayokubalika.—Isaya 2:2-4; Mika 4:1-4.

Je, kweli unabii huo unatimizwa leo? Acheni tuone mambo ya hakika. Katika miaka kumi tu iliyopita, zaidi ya watu wapya 3,110,000 wamejiweka wakfu kwa Yehova katika nchi zaidi ya 230. Kwa kila Mashahidi wa Yehova 10 wanaotumikia ulimwenguni sasa, 6 kati yao walibatizwa katika miaka 10 iliyopita. Kwa wastani, katika mwaka wa 2004, baada ya kila dakika mbili, mtumishi mpya aliyejiweka wakfu kwa Mungu aliongezwa katika kutaniko la Kikristo! *

Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo ‘hesabu kubwa wamepata kuamini na kugeuka kumwelekea Bwana.’ Ingawa sio ongezeko linalothibitisha baraka za Mungu, linaonyesha kwamba “mkono wa Yehova” uko pamoja na watu wake. (Matendo 11:21) Ni nini kinachowafanya mamilioni wamwabudu Yehova? Wewe unahusikaje katika ukuzi huo?

Watu Wenye Moyo Mnyoofu Wanavutwa

Yesu alisema hivi kwa njia ya moja kwa moja: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yohana 6:44) Hivyo basi, Yehova ndiye anayewavuta watu walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.” (Matendo 13:48) Roho ya Mungu inaweza kuwachochea watu watambue uhitaji wao wa kiroho. (Mathayo 5:3) Kusumbuliwa na dhamiri, tamaa kubwa ya kuwa na tumaini, au tatizo zito linaweza kuwafanya wengine waanze kumtafuta Mungu na hivyo kujifunza kuhusu kusudi lake kwa wanadamu.—Marko 7:26-30; Luka 19:2-10.

Watu wengi wanavutiwa na ibada ya Yehova kwa sababu elimu ya Biblia ambayo imepangwa na kutaniko la Kikristo huwasaidia kupata majibu kwa maswali yanayowasumbua.

“Kama kuna Mungu, kwa nini watu wanaendelea kutendewa isivyo haki?” Hilo ndilo swali lililomsumbua Davide, aliyekuwa mlanguzi wa dawa za kulevya nchini Italia. Hakuwa anapendezwa na mambo ya dini, hivyo alizusha swali hilo gumu ili kutokeza ubishi. Anasema: “Sikufikiri ningepata jibu la maana na lenye kusadikisha. Lakini Shahidi aliyezungumza nami alikuwa mwenye subira sana na alitumia Biblia kuthibitisha mambo aliyosema. Mazungumzo hayo yalinigusa moyo sana.” Leo, Davide amerekebisha maisha yake na anamtumikia Yehova.

Wengine wanakuwa sehemu ya tengenezo la Yehova la duniani kwa sababu wanatafuta kusudi maishani. Ili kupata msaada wa matatizo ya kihisia, mtaalamu wa magonjwa ya akili huko Zagreb, Kroatia, alimwendea daktari mwenzake mashuhuri. Alishangaa sana daktari huyo alipompa namba ya simu ya ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Zagreb, na jina la Shahidi mmoja. Akamwambia: “Nafikiri watu hao wanaweza kukusaidia. Nikikuelekeza kanisani, utakuta sanamu tu, hakuna anayezungumza, na kuna giza la kiroho. Sidhani kanisa linaweza kukusaidia. Nimewaelekeza wagonjwa wengine kwa Mashahidi wa Yehova, na ninafikiri litakuwa jambo bora kwako pia.” Mashahidi walimtembelea na bila kukawia wakaanza kujifunza Biblia naye. Baada ya majuma machache, mtaalamu huyo wa magonjwa ya akili alisema kwa furaha kwamba ujuzi kuhusu kusudi la Mungu ulimpa kusudi maishani.—Mhubiri 12:13.

Watu wengi wamegundua kwamba kweli ya Biblia ndiyo inayoweza kuwafariji wanapopata matatizo. Nchini Ugiriki, mvulana wa miaka saba alianguka kutoka kwenye paa shuleni akafa. Miezi michache baadaye, Mashahidi wawili walikutana na mama yake na kujaribu kumfariji kwa kuzungumza naye kuhusu tumaini la ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Mama huyo alianza kulia. Dada hao wakamuuliza: “Ikiwa unapenda kujua mengi zaidi kuhusu Biblia, ungependa tukutembelee lini?” Mama huyo akajibu: “Sasa hivi.” Mwanamke huyo akawapeleka kwake, na funzo la Biblia likaanzishwa. Leo, yeye pamoja na familia yake yote wanamtumikia Yehova.

Je, Unashiriki?

Mambo kama hayo yanafanyika ulimwenguni pote. Yehova anaukusanya na kuufundisha umati mkubwa wa waabudu wa kweli kutoka katika mataifa yote. Kikundi hicho cha kimataifa kina tumaini zuri la kuokoka mwisho unaokaribia wa mfumo huu wa mambo na kuendelea kuishi katika ulimwengu mpya wenye uadilifu.—2 Petro 3:13.

Kwa sababu ya baraka za Yehova, kazi hiyo ya kukusanya isiyo na kifani inaendelea kusonga bila kusimamishwa hadi ifikie mwisho wake wenye mafanikio. (Isaya 55:10, 11; Mathayo 24:3, 14) Je, unashiriki kwa bidii katika kazi hiyo ya kuhubiri kuhusu Ufalme? Ikiwa ndivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba unategemezwa na Mungu na unaweza kusema hivi kama mtunga-zaburi: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona Kalenda ya Mwaka wa 2005 ya Mashahidi wa Yehova, Septemba/Oktoba.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.”—YOHANA 6:44

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

NI NANI ANAYELETA ONGEZEKO HILO?

“Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.” —Zaburi 127:1.

“Mungu akaendelea kuikuza; hivi kwamba yeye anayepanda si kitu wala yeye anayetia maji, bali Mungu anayeikuza.”—1 Wakorintho 3:6, 7.