Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

WAZIA jinsi kijana Myahudi aliyeitwa Andrea alivyofurahi sana kumsikiliza Yesu wa Nazareti kwa mara ya kwanza! Biblia inasema kwamba Andrea alikimbia kwa ndugu yake na kumwambia: “Tumempata Masihi [au, Kristo].” (Yohana 1:41) Katika Kiebrania na Kigiriki, maneno yanayotafsiriwa “Masihi” na “Kristo” yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Yesu alikuwa Mtiwa-Mafuta, au Mchaguliwa wa Mungu—Kiongozi aliyeahidiwa. (Isaya 55:4) Maandiko yalikuwa na unabii mbalimbali kumhusu, na Wayahudi wa wakati huo walikuwa wakimtarajia.—Luka 3:15.

Tunajuaje kwamba kwa kweli Yesu alikuwa Mchaguliwa wa Mungu? Acheni tuchunguze yale yaliyotukia mwaka wa 29 W.K., Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30. Alimwendea Yohana Mbatizaji ili abatizwe naye katika Mto Yordani. Biblia inasema: “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: ‘Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” (Mathayo 3:16, 17) Baada ya kusikia maneno hayo yaliyoonyesha kibali, je, Yohana angekuwa na shaka yoyote kwamba Yesu ni Mchaguliwa wa Mungu? Kwa kummwagia Yesu roho Yake takatifu, Yehova Mungu alimtia mafuta, au kumweka rasmi, awe Mfalme wa Ufalme Wake unaokuja. Hivyo, Yesu akawa Kristo, yaani, Mtiwa-Mafuta. Hata hivyo, kwa nini Yesu anaitwa Mwana wa Mungu? Alitoka wapi?

Asili Yake Ni “Kutoka Nyakati za Kale”

Maisha ya Yesu yanaweza kugawanywa katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza ilianza muda mrefu kabla hajazaliwa kama mwanadamu. Andiko la Mika 5:2 linasema kwamba asili yake ilikuwa “kutoka nyakati za kale, kutoka siku za wakati usio na kipimo.” Yesu mwenyewe alisema: “Mimi ninatoka kwenye makao ya juu,” yaani, mbinguni. (Yohana 8:23) Alikuwa mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu.

Kwa kuwa viumbe vyote vilikuwa na mwanzo ni wazi kwamba kuna wakati ambapo Mungu alikuwa peke yake. Hata hivyo, miaka mingi iliyopita, Mungu alianza kuumba. Alimuumba nani kwanza? Kitabu cha mwisho katika Biblia humtambulisha Yesu kuwa “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14) Yesu ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” Hiyo ni “kwa sababu kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana.” (Wakolosai 1:15, 16) Naam, Yesu pekee ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu mwenyewe. Hivyo, anaitwa ‘Mwana mzaliwa-pekee’ wa Mungu. (Yohana 3:16) Mwana huyo wa kwanza pia anaitwa “Neno.” (Yohana 1:14) Kwa nini? Kwa sababu kabla ya kuzaliwa kama mwanadamu, alizungumza kwa niaba ya Mungu huko mbinguni.

“Neno” alikuwa pamoja na Yehova Mungu “hapo mwanzo,” wakati “mbingu na dunia” zilipoumbwa. Yeye ndiye aliyeambiwa hivi na Mungu: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” (Yohana 1:1; Mwanzo 1:1, 26) Mwana huyo mzaliwa wa kwanza wa Yehova alikuwa kando ya Baba yake akifanya kazi kwa bidii pamoja naye. Kwenye Methali 8:22-31 anawakilishwa akisema: “Ndipo nilipokuwa kando yake [Muumba] nikiwa stadi wa kazi, nami nikawa yule ambaye yeye alimpenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku, nami nikawa nikifurahi mbele zake wakati wote.”

Haikosi Yehova Mungu na Mwana wake mzaliwa-pekee walisitawisha uhusiano wa karibu sana walipofanya kazi pamoja! Ushirika huo wa karibu pamoja na Yehova kwa muda mrefu ulikuwa na uvutano mkubwa sana kwa Mwana wa Mungu. Mwana huyo mtiifu akaja kuwa kama Baba yake, Yehova. Andiko la Wakolosai 1:15 linamtaja Yesu kuwa “mfano wa Mungu asiyeonekana.” Hiyo ni sababu moja inayothibitisha kwamba ni muhimu kumjua Yesu ili kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho na tamaa yetu ya asili ya kumjua Mungu. Akiwa duniani, Yesu alifanya kila kitu ambacho Yehova alimtazamia afanye. Hivyo, kumjua Yesu kunamaanisha pia kumjua Yehova zaidi. (Yohana 8:28; 14:8-10) Lakini, Yesu alikujaje duniani?

Maisha Yake Akiwa Mwanadamu

Sehemu ya pili ya maisha ya Yesu ilianza wakati Mungu alipomtuma Mwana wake duniani. Yehova alifanya hivyo kwa kuhamisha kimuujiza maisha ya Yesu kutoka mbinguni hadi katika tumbo la Maria, bikira Myahudi aliyekuwa mwaminifu. Yesu hakurithi kutokamilika kwa sababu hakuwa na baba wa kibinadamu. Roho takatifu, au nguvu ya utendaji ya Yehova, ilikuja juu ya Maria, na nguvu zake ‘zikamfunika’ naye akapata mimba kimuujiza. (Luka 1:34, 35) Hivyo, Maria akamzaa mtoto mkamilifu. Akiwa mwana aliyelelewa na seremala Yosefu, alikua katika familia ya hali ya chini akiwa wa kwanza katika familia yenye watoto kadhaa.—Isaya 7:14; Mathayo 1:22, 23; Marko 6:3.

Hatujui mambo mengi kuhusu maisha ya Yesu ya utotoni, lakini kuna tukio moja linalojulikana. Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimpeleka Yerusalemu kwa ajili ya sherehe ya Pasaka ya kila mwaka kama ilivyokuwa desturi yao. Huko alitumia wakati mwingi hekaluni akiwa “ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” Isitoshe, “wale wote waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wakishangazwa daima na uelewaji wake na majibu yake.” Naam, kijana Yesu hakuuliza tu maswali ya kiroho yenye kuchochea fikira bali pia alitumia akili kutoa majibu yaliyowashangaza wengine. (Luka 2:41-50) Alipoendelea kukua katika jiji la Nazareti, bila shaka, Yosefu, baba yake mlezi, alimfundisha useremala.—Mathayo 13:55.

Yesu aliishi Nazareti hadi alipokuwa na umri wa miaka 30. Kisha akaenda kubatizwa na Yohana. Baada ya kubatizwa, Yesu alianza huduma yake kwa bidii. Kwa miaka mitatu na nusu, alisafiri kotekote katika nchi ya kwao akihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Alithibitisha kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Kwa njia gani? Kwa kufanya miujiza mingi, yaani, matendo yenye nguvu yanayopita uwezo wa kibinadamu.—Mathayo 4:17; Luka 19:37, 38.

Yesu alikuwa pia na hisia na huruma nyingi. Alionyesha huruma hasa kupitia jinsi alivyowaona na kuwatendea wengine. Watu walivutiwa na Yesu kwa kuwa alikuwa mwenye urafiki na fadhili. Hata watoto walistarehe walipokuwa naye. (Marko 10:13-16) Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima ingawa watu wengine wa siku zake waliwadharau. (Yohana 4:9, 27) Aliwasaidia maskini na watu walioonewa ‘wapate burudisho kwa ajili ya nafsi zao.’ (Mathayo 11:28-30) Alifundisha kwa njia iliyo wazi, rahisi, na kufanya mambo yawe halisi. Mambo aliyofundisha yalionyesha kwamba alitamani kutoka moyoni kuwaeleza wasikilizaji wake kumhusu Mungu wa kweli, Yehova.—Yohana 17:6-8.

Akitumia roho takatifu ya Mungu kufanya miujiza, Yesu aliwahurumia na kuwaponya wagonjwa na watu walioteseka. (Mathayo 15:30, 31) Kwa mfano, mtu mwenye ukoma alimjia na kusema: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu alifanya nini? Aliunyoosha mkono wake akamgusa na kumwambia: “Ninataka. Takasika.” Na mtu huyo akaponywa!—Mathayo 8:2-4.

Fikiria pia pindi fulani umati ulipomjia Yesu na kukaa naye siku tatu bila kula. Aliwahurumia na kuwalisha kimuujiza “wanaume elfu nne, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mathayo 15:32-38) Pindi nyingine, Yesu alinyamazisha dhoruba iliyohatarisha uhai wa rafiki zake. (Marko 4:37-39) Aliwafufua, au kuwarudisha kwenye uhai, wale waliokuwa wamekufa. * (Luka 7:22; Yohana 11:43, 44) Yesu hata alikubali kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ili wanadamu wasio wakamilifu wawe na tumaini la wakati ujao. Naam, Yesu aliwapenda watu sana!

Yesu Yuko Wapi Leo?

Yesu alikufa juu ya mti wa mateso akiwa na miaka 33 1/2. * Lakini huo haukuwa mwisho wa maisha yake. Sehemu ya tatu ya maisha yake ilianza Yehova Mungu alipomfufua Mwana wake akiwa mtu wa roho. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea mamia ya watu walioishi katika karne ya kwanza W.K. (1 Wakorintho 15:3-8) Kisha ‘akaketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu’ na kungojea kupokea mamlaka ya kifalme. (Waebrania 10:12, 13) Wakati huo ulipofika, Yesu alianza kutawala akiwa Mfalme. Hivyo, tumwoneje Yesu leo? Je, tumwone kama mtu anayeteswa na kuuawa? Au je, tumwone kama mtu anayepaswa kuabudiwa? Leo, Yesu si mwanadamu wala Mungu Mweza-Yote. Yeye ni kiumbe wa roho mwenye nguvu, Mfalme anayetawala. Karibuni sana ataelekeza utawala wake juu ya dunia yetu yenye taabu.

Katika Ufunuo 19:11-16 Yesu Kristo anatajwa kwa lugha ya mfano akiwa mfalme aliyeketi juu ya farasi mweupe akija kuhukumu na kufanya vita kwa uadilifu. Ana ‘upanga mrefu mkali wa kuyapiga mataifa nao.’ Ndiyo, Yesu atatumia nguvu zake nyingi kuwaharibu waovu. Itakuwaje kwa wale wanaojitahidi kufuata kielelezo alichoweka alipokuwa duniani? (1 Petro 2:21) Yeye pamoja na Baba yake watawahifadhi waokoke “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” ambayo mara nyingi huitwa, Har–Magedoni, ili waishi milele duniani wakiwa raia wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu.—Ufunuo 7:9, 14; 16:14, 16; 21:3, 4.

Yesu atawafanyia wanadamu miujiza mingi kama nini wakati wa utawala wake wa amani! (Isaya 9:6, 7; 11:1-10) Atawaponya wagonjwa na kukomesha kifo. Mungu atamtumia Yesu kufufua mabilioni ya watu na kuwapa nafasi ya kuishi milele duniani. (Yohana 5:28, 29) Hatuwezi hata kuwazia jinsi maisha yetu yatakavyokuwa mazuri chini ya utawala wa Ufalme! Ni muhimu basi tuendelee kujifunza Biblia na kumjua Yesu Kristo vizuri zaidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Miujiza ambayo Yesu alifanya ilijulikana sana. Hata adui za Yesu walikubali kwamba ‘alifanya ishara nyingi.’—Yohana 11:47, 48.

^ fu. 17 Kwa maelezo yanayoonyesha ikiwa Kristo alikufa kwenye mti wa mateso au msalabani, ona kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko ukurasa 211-213, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

JE, YESU NI MUNGU MWEZA-YOTE?

Wanadini wengi husema kwamba Yesu ni Mungu. Wengine hudai kwamba Mungu ni Utatu. Kulingana na fundisho hilo, “Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Takatifu ni Mungu, na wote si Miungu watatu bali Mungu mmoja.” Inaaminiwa kwamba wote watatu “ni wa umilele na wana cheo sawa.” (The Catholic Encyclopedia) Je, maoni hayo ni sahihi?

Yehova Mungu ndiye Muumba. (Ufunuo 4:11) Hana mwanzo wala mwisho, na ndiye Mweza-Yote. (Zaburi 90:2) Kwa upande mwingine, Yesu alikuwa na mwanzo. (Wakolosai 1:15, 16) Yesu alimwita Mungu Baba yake na kusema hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Yesu alieleza pia kwamba kuna mambo fulani ambayo yeye wala malaika hawakuyajua ila Baba peke yake.—Marko 13:32.

Isitoshe, Yesu alisali kwa Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Yesu alikuwa akisali kwa nani ikiwa si kwa Aliye mkuu zaidi? Isitoshe, Mungu ndiye aliyemfufua Yesu, bali Yesu hakujifufua mwenyewe. (Matendo 2:32) Bila shaka, Baba na Mwana hawakuwa na cheo sawa kabla ya Yesu kuja duniani wala wakati wa maisha yake duniani. Namna gani baada ya Yesu kufufuliwa na kwenda mbinguni? Andiko la 1 Wakorintho 11:3 linasema: “Kichwa cha Kristo ni Mungu.” Sikuzote Mwana atajitiisha kwa Mungu. (1 Wakorintho 15:28) Hivyo, Maandiko yanaonyesha kwamba Yesu si Mungu Mweza-Yote. Badala yake, yeye ni Mwana wa Mungu.

Yule anayedaiwa kuwa mtu wa tatu wa Utatu, yaani, roho takatifu, si mtu. Akizungumza na Mungu katika sala, mtunga-zaburi alisema: “Ukiituma roho yako, wanaumbwa.” (Zaburi 104:30) Roho hiyo si Mungu mwenyewe; ni nguvu ya utendaji ambayo anatuma au anatumia kutimiza chochote anachotaka. Kupitia roho hiyo, Mungu aliumba mbingu zinazoonekana, dunia, na vitu vyote vyenye uhai. (Mwanzo 1:2; Zaburi 33:6) Mungu alitumia roho takatifu yake kuwaongoza wanaume walioandika Biblia. (2 Petro 1:20, 21) Basi, Utatu si fundisho la Kimaandiko. * Biblia inasema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”—Kumbukumbu la Torati 6:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Kwa habari zaidi, ona broshua Je! Uamini Utatu? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Alipobatizwa, Yesu akawa Mtiwa-Mafuta wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alitumia nguvu zake kufanya kazi aliyopewa na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Leo, Yesu ni Mfalme mwenye nguvu