Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endeleeni Kukesha”—Saa ya Hukumu Imefika!

“Endeleeni Kukesha”—Saa ya Hukumu Imefika!

“Endeleeni Kukesha”—Saa ya Hukumu Imefika!

Habari zilizo katika makala hii ya funzo zinategemea broshua Endeleeni Kukesha! iliyotolewa kwenye makusanyiko ya wilaya yaliyofanywa ulimwenguni pote katika mwaka wa 2004/2005.

“Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—MATHAYO 24:42.

1, 2. Kwa kufaa, Yesu alilinganisha kuja kwake na nini?

UNGEFANYA nini ukijua kwamba kuna mwizi anayezunguka huku na huku akitafuta nafasi ya kuiba katika nyumba za eneo lenu? Ili uwalinde wapendwa wako na mali zako, ungehitaji kuwa macho, kukaa chonjo. Mwizi hatumi barua kusema wakati anapokuja. Badala yake, yeye huja kimyakimya bila kutarajiwa.

2 Yesu alitumia mfano wa mwizi mara kadhaa. (Luka 10:30; Yohana 10:10) Akizungumza kuhusu matukio ambayo yatatokea wakati wa mwisho kabla ya yeye kuja kutekeleza hukumu, Yesu alitoa onyo hili: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja. Lakini jueni jambo moja, kwamba ikiwa mwenye nyumba angalijua mwizi anakuja katika kesha gani, angaliendelea kukaa macho na hangaliruhusu nyumba yake ivunjwe.” (Mathayo 24:42, 43) Hivyo, Yesu alilinganisha kuja kwake na kuja kwa mwizi, yaani, pasipo kutarajiwa.

3, 4. (a) Kutii onyo la Yesu kuhusu kuja kwake kunahusisha nini? (b) Ni maswali gani yanayozuka?

3 Mfano huo ulifaa, kwa sababu tarehe hususa ya kuja kwa Yesu haingejulikana. Mapema, katika unabii huohuo, Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Hivyo, Yesu aliwahimiza wasikilizaji wake hivi: “Iweni tayari.” (Mathayo 24:44) Wale wanaotii onyo la Yesu wangekuwa tayari, wakijiendesha kwa njia inayofaa, wakati wowote ule ambapo angekuja kutekeleza hukumu ya Yehova.

4 Maswali fulani muhimu yanatokea: Je, onyo la Yesu linawahusu watu wa ulimwengu tu, au je, Wakristo wa kweli pia wanahitaji ‘kuendelea kukesha’? Kwa nini ni muhimu ‘kuendelea kukesha,’ na hilo linahusisha nini?

Onyo kwa Ajili ya Nani?

5. Tunajuaje kwamba onyo la ‘kuendelea kukesha’ linawahusu Wakristo wa kweli?

5 Ni kweli kabisa kwamba Bwana atakuja kama mwizi kwa watu wa ulimwengu ambao hupuuza onyo la msiba unaokaribia. (2 Petro 3:3-7) Lakini namna gani Wakristo wa kweli? Mtume Paulo aliwaandikia waamini wenzake hivi: “Ninyi wenyewe mnajua vema kabisa kwamba siku ya Yehova inakuja sawasawa kabisa kama mwizi usiku.” (1 Wathesalonike 5:2) Hatuna shaka yoyote kwamba “siku ya Yehova inakuja.” Lakini je, hilo linamaanisha kwamba hatuhitaji kuendelea kukesha? Ona kwamba Yesu alikuwa akiongea na wanafunzi wake aliposema: “Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” (Mathayo 24:44) Mapema, alipokuwa akiwahimiza wanafunzi wake waendelee kutafuta Ufalme, Yesu alisema: “Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyoitazamia.” (Luka 12:31, 40) Je, si wazi kwamba Yesu alikuwa akiwafikiria wafuasi wake alipotoa onyo hili: “Endeleeni kukesha”?

6. Kwa nini tunahitaji ‘kuendelea kukesha’?

6 Kwa nini tunahitaji ‘kuendelea kukesha’ na ‘kuendelea kuwa tayari’? Yesu alieleza hivi: “Watu wawili watakuwa shambani: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe la kusagia: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.” (Mathayo 24:40, 41) Wale watakaokuwa tayari ‘watachukuliwa,’ yaani, wataokolewa wakati ulimwengu huu usiomwogopa Mungu utakapoharibiwa. Wengine ‘wataachwa’ waharibiwe kwa sababu wamekuwa wakihangaikia kwa ubinafsi maisha yao wenyewe. Huenda baadhi yao watakuwa watu ambao wakati fulani waliijua kweli lakini hawakuendelea kukesha.

7. Kutojua siku ambayo mwisho utakuja hutupa nafasi ya kufanya nini?

7 Kutojua siku hususa ya mwisho wa mfumo huu wa kale hutupa nafasi ya kuonyesha kwamba tunamtumikia Mungu kwa nia safi. Jinsi gani? Huenda ikaonekana kwamba mwisho umekawia sana. Inasikitisha kwamba Wakristo fulani wanaohisi hivyo wamepunguza bidii yao katika utumishi wa Yehova. Hata hivyo, tulipojiweka wakfu, tulijitoa kwa Yehova bila masharti ili tumtumikie. Wale wanaomjua Yehova wanatambua kwamba hatapendezwa na bidii inayoonyeshwa katika dakika ya mwisho. Yeye huona kilicho moyoni.—1 Samweli 16:7.

8. Kumpenda Yehova hutuchocheaje kuendelea kukesha?

8 Kwa sababu tunampenda Yehova kikweli, tunapendezwa kabisa kufanya mapenzi yake. (Zaburi 40:8; Mathayo 26:39) Tunataka kumtumikia Yehova milele. Tumaini hilo halipotezi thamani eti kwa sababu tu tunahitaji kungoja kwa muda mrefu zaidi kuliko tulivyotarajia. Zaidi ya yote, tunaendelea kukesha kwa sababu tunatazamia kwa hamu kubwa kuona jinsi ambavyo siku ya Yehova itatimiza kusudi lake. Tamaa yetu ya kutoka moyoni ya kumpendeza Mungu hutuchochea kutumia mashauri ya Neno lake na kutanguliza Ufalme wake maishani mwetu. (Mathayo 6:33; 1 Yohana 5:3) Acheni tuone jinsi ambavyo kuendelea kukesha kunapaswa kutuongoza katika maisha yetu ya kila siku na pia wakati tunapofanya maamuzi.

Maisha Yako Yanaelekea Wapi?

9. Kwa nini watu wa ulimwengu wanahitaji kutambua haraka umuhimu wa nyakati zetu?

9 Watu wengi leo wanatambua kwamba matatizo makubwa na matukio ya kushtua yamekuwa mambo ya kawaida, na hawafurahii mahali ambapo maisha yao yanaelekea. Lakini je, wanatambua umuhimu wa hali za ulimwengu? Je, wanatambua kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo”? (Mathayo 24:3) Je, wanatambua kwamba kuenea kwa ubinafsi, jeuri, na hata mitazamo ya kutomwogopa Mungu, ni mambo yanayoonyesha kwamba hizi ni “siku za mwisho”? (2 Timotheo 3:1-5) Wanahitaji kutambua haraka umuhimu wa yote hayo na kufikiria mahali ambapo maisha yao yanaelekea.

10. Tunapaswa kufanya nini ili tuwe na uhakika kwamba tunaendelea kukesha?

10 Namna gani sisi? Kila siku tunahitaji kufanya maamuzi yanayohusiana na kazi yetu, afya yetu, familia yetu, na ibada yetu. Tunajua yale ambayo Biblia inasema, na tunajitahidi kuyafuata. Hivyo, inafaa tujiulize hivi: ‘Je, nimeruhusu mahangaiko ya maisha yanikengeushe? Je, ninaruhusu falsafa au maoni ya ulimwengu yaathiri maamuzi ninayofanya?’ (Luka 21:34-36; Wakolosai 2:8) Tunahitaji kuendelea kuonyesha kwamba tunamtegemea Yehova kwa moyo wetu wote wala hatutegemei uelewaji wetu wenyewe. (Methali 3:5) Tukifanya hivyo, tutaendelea ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli’—uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Timotheo 6:12, 19.

11-13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kilichotukia (a) katika siku za Noa? (b) katika siku za Loti?

11 Biblia ina mifano mingi yenye kuonya ambayo inaweza kutusaidia kuendelea kukesha. Fikiria kilichotukia katika siku za Noa. Muda mrefu kabla ya kuchukua hatua, Mungu alihakikisha kwamba onyo linatolewa. Lakini watu hawakujali, isipokuwa Noa na familia yake tu. (2 Petro 2:5) Yesu alisema hivi kuhusiana na jambo hilo: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37-39) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo? Ikiwa yeyote kati yetu anaruhusu mambo ya kimwili, hata mambo ya kawaida ya maisha, yachukue mahali pa mambo ya kiroho ambayo Mungu anatuhimiza tuyatangulize, basi anapaswa kufikiria kwa uzito hali yake.—Waroma 14:17.

12 Pia, fikiria siku za Loti. Ingawa jiji la Sodoma ambamo Loti na familia yake waliishi lilikuwa lenye ufanisi, lilikuwa pia na ukosefu mwingi wa adili. Yehova aliwatuma malaika zake wapaharibu mahali hapo. Malaika hao walimhimiza Loti na familia yake wakimbie kutoka Sodoma na wasitazame nyuma. Baada ya kuhimizwa na malaika, waliondoka jijini. Hata hivyo, yaonekana kwamba mke wa Loti aliendelea kufikiria nyumba yake huko Sodoma. Kwa kutotii, alitazama nyuma, naye akafa. (Mwanzo 19:15-26) Yesu alitoa onyo hili la kinabii: “Mkumbukeni mke wa Loti.” Je, tunatii onyo hilo?—Luka 17:32.

13 Wale waliotii maonyo ya Mungu waliokoka. Noa na familia yake na Loti na binti zake waliokoka. (2 Petro 2:9) Tunapoyatafakari maonyo yaliyo katika mifano hiyo, mioyo yetu pia inasisimuliwa na ujumbe wa ukombozi ulio katika masimulizi hayo kwa ajili ya watu wanaopenda uadilifu. Jambo hilo hufanya tutarajie kwa uhakika utimizo wa ahadi ya Mungu ya “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

‘Saa ya Hukumu Imefika’!

14, 15. (a) “Saa” ya hukumu inatia ndani nini? (b) Ni nini kinachohusika katika ‘kumwogopa Mungu na kumpa utukufu’?

14 Tunapaswa kutarajia nini tunapoendelea kukesha? Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha jinsi kusudi la Mungu litakavyotimizwa hatua kwa hatua. Kutii mambo yanayosemwa katika kitabu hicho ni muhimu ili tuwe tayari. Unabii huo unaonyesha waziwazi matukio ambayo yangetukia katika “siku ya Bwana,” ambayo ilianza wakati Kristo alipotawazwa kuwa mfalme mbinguni mwaka wa 1914. (Ufunuo 1:10) Kitabu cha Ufunuo hutueleza kuhusu malaika aliyepewa “habari njema ya milele ili aitangaze.” Anatangaza hivi kwa sauti kubwa: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.” (Ufunuo 14:6, 7) “Saa” hiyo ya hukumu ni kipindi kifupi; ambacho kinatia ndani tangazo hilo na utekelezaji wa hukumu zinazoelezwa katika unabii huo. Tunaishi katika kipindi hicho sasa.

15 Sasa, kabla ya saa ya hukumu kwisha, tunahimizwa hivi: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.” Hiyo inatia ndani nini? Tukimwogopa Mungu kwa njia inayofaa hatutafanya mabaya. (Methali 8:13) Ikiwa tunamheshimu Mungu, tutamsikiliza kwa heshima nyingi. Hatutajishughulisha sana na mambo mengine hivi kwamba tupuuze kusoma Neno lake, Biblia, kwa ukawaida. Hatutapuuza shauri lake la kuhudhuria mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Tutathamini sana pendeleo la kutangaza habari njema za Ufalme wa Kimasihi wa Mungu, na tutafanya hivyo kwa bidii. Tutamtegemea Yehova nyakati zote na kwa moyo wetu wote. (Zaburi 62:8) Kwa kuwa tunatambua kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, tunamheshimu kwa kujitiisha kwake kwa hiari na kukubali aongoze maisha yetu. Je, wewe humwogopa Mungu kikweli na kumpa utukufu katika njia hizo zote?

16. Kwa nini tunaweza kusema kwamba hukumu inayotajwa kwenye Ufunuo 14:8 juu ya Babiloni Mkubwa tayari imetimizwa?

16 Sura ya 14 ya kitabu cha Ufunuo inaendelea kueleza matukio mengine yatakayotukia katika ile saa ya hukumu. Babiloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, ndiye anayetajwa kwanza: “Na mwingine, malaika wa pili, akafuata, akisema: ‘Ameanguka! Babiloni Mkubwa ameanguka!’” (Ufunuo 14:8) Naam, kwa maoni ya Mungu, tayari Babiloni Mkubwa ameanguka. Katika mwaka wa 1919, watumishi wa Yehova watiwa-mafuta waliwekwa huru kutoka katika utekwa wa mafundisho na desturi za Babiloni, ambazo zimeongoza vikundi vya watu na mataifa kwa maelfu ya miaka. (Ufunuo 17:1, 15) Hivyo, watumishi hao wangeweza kujitoa kuendeleza ibada ya kweli. Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kuhusu habari njema ya Ufalme wa Mungu imekuwa ikiendelea tangu wakati huo.—Mathayo 24:14.

17. Kutoka katika Babiloni Mkubwa kunahusisha nini?

17 Hukumu ya Mungu juu ya Babiloni Mkubwa haikomei hapo. Hivi karibuni, Babiloni Mkubwa ataharibiwa kabisa. (Ufunuo 18:21) Basi, Biblia ina sababu nzuri ya kuwahimiza watu kila mahali hivi: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa] . . . ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake.” (Ufunuo 18:4, 5) Tunatokaje katika Babiloni Mkubwa? Hilo linahusisha mengi zaidi ya kukatilia mbali uhusiano wowote na dini ya uwongo. Uvutano wa Babiloni unaonekana katika sherehe na desturi nyingi zinazopendwa na wengi, katika maoni ya ulimwengu yaliyopotoka kuhusu ngono, katika burudani inayohusisha kuwasiliana na pepo, na katika mambo mengine mengi. Ili tuendelee kukesha ni muhimu tuonyeshe kupitia matendo yetu na tamaa za moyo wetu kwamba sisi si sehemu ya Babiloni Mkubwa hata kidogo.

18. Kulingana na mambo yanayoelezwa katika Ufunuo 14:9, 10, Wakristo walio macho hawakubali nini?

18 Katika Ufunuo 14:9, 10, jambo lingine linaelezwa kuhusu “saa ya hukumu.” Malaika mwingine anasema: “Yeyote akimwabudu yule mnyama-mwitu na sanamu yake, na kupokea alama juu ya paji la uso wake au juu ya mkono wake, yeye pia atakunywa kutokana na divai ya hasira ya Mungu.” Kwa nini? “Yule mnyama-mwitu na sanamu yake” huwakilisha utawala wa wanadamu ambao hauikubali enzi kuu ya Yehova. Iwe ni kwa mtazamo au kwa matendo, Wakristo walio macho hawakubali kuathiriwa wala kupokea alama ambayo inaonyesha kwamba wao ni watumwa wa wale wanaoikataa enzi kuu ya Mungu wa kweli, Yehova. Wakristo wanajua kwamba tayari Ufalme wa Mungu umesimamishwa mbinguni, wanajua kwamba utakomesha utawala wote wa wanadamu, na kwamba utasimama milele.—Danieli 2:44.

Usiache Kutambua Umuhimu wa Nyakati Zetu!

19, 20. (a) Siku za mwisho zinapoendelea kusonga, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Shetani atajaribu kufanya nini? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Siku za mwisho zinapoendelea kusonga, matatizo na vishawishi vitaongezeka. Kwa kuwa tunaishi katika mfumo huu wa kale na kwa sababu ya kutokamilika kwetu, tunasumbuliwa na mambo kama vile matatizo ya afya, uzee, kifo cha wapendwa, kuumia kihisia, kuvunjika moyo wakati ambapo watu hawapendezwi na jitihada zetu za kuhubiri Neno la Mungu, na mambo mengine mengi. Usisahau kwamba Shetani angependa sana kutumia matatizo tunayokabili ili atuvunje moyo tusiendelee kuhubiri habari njema au kufuata viwango vya Mungu maishani. (Waefeso 6:11-13) Huu si wakati wa kuacha kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi!

20 Kwa kuwa Yesu alijua kwamba tungekabili mikazo mingi ya kutuvunja moyo, alitushauri hivi: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mathayo 24:42) Basi, acheni tuendelee kuwa macho kutambua umuhimu wa nyakati zetu. Acheni tujihadhari na mbinu za Shetani ambazo zinaweza kutufanya tulegee au kuiacha kweli. Acheni tuazimie kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu kwa bidii na kwa ujasiri zaidi. Naam, acheni tuendelee kutambua umuhimu wa nyakati zetu, huku tukitii shauri hili la Yesu: “Endeleeni kukesha.” Tukifanya hivyo, tutamletea Yehova heshima na kuwa kati ya wale watakaopata baraka zake za milele.

Ungejibuje?

• Tunajuaje kwamba onyo la Yesu la ‘kuendelea kukesha’ linawahusu Wakristo wa kweli?

• Ni mifano gani yenye kuonya iliyo katika Biblia ambayo inaweza kutusaidia ‘kuendelea kukesha’?

• Saa ya hukumu ni nini, nasi tunahimizwa tufanye nini kabla haijakwisha?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alisema angekuja kama vile mwizi anavyokuja

[Picha katika ukurasa wa 24]

Babiloni Mkubwa ataharibiwa hivi karibuni

[Picha katika ukurasa wa 25]

Acheni tuazimie kuhubiri kwa bidii na kwa ujasiri zaidi