Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dhamiri Yako Imezoezwa Vizuri?

Je, Dhamiri Yako Imezoezwa Vizuri?

Je, Dhamiri Yako Imezoezwa Vizuri?

JE, UMEWAHI kusema hivi, “Ninajua moyoni mwangu kwamba jambo hilo si sawa,” au “Siwezi kufanya unachotaka nifanye. Kuna kitu fulani ndani yangu kinachoniambia kwamba jambo hilo si sawa”? Hiyo ni “sauti” ya dhamiri yako, uwezo ulio ndani yako wa kutambua mema na mabaya, ambao unaweza kukutetea au kukushtaki. Naam, tunazaliwa tukiwa na dhamiri.

Ingawa mwanadamu amejitenga na Mungu, kwa ujumla bado ana uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya. Hiyo ni kwa sababu ameumbwa kwa mfano wa Mungu, hivi kwamba ana uwezo wa kudhihirisha kwa kiwango fulani sifa za kimungu kama vile hekima na uadilifu. (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo, Mungu alimwongoza mtume Paulo aandike hivi: “Maana wakati watu wa mataifa wasio na sheria wanapofanya kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ijapokuwa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. Wao ndio wanaoonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao, huku dhamiri yao ikiwatolea ushahidi na, katikati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata kutetewa.” *Waroma 2:14, 15.

Uwezo huo wa asili wa kufanya maamuzi ya kiadili uliorithiwa kutoka kwa mtu wa kwanza, Adamu, hufanya kazi ndani ya watu wa jamii na mataifa yote kama “sheria,” au kanuni ya mwenendo. Ni uwezo wa kujichunguza na kujihukumu. (Waroma 9:1) Adamu na Hawa walionyesha uwezo huo kwa kujificha baada tu ya kuvunja sheria ya Mungu. (Mwanzo 3:7, 8) Mfano mwingine wa jinsi dhamiri inavyofanya kazi ni namna Mfalme Daudi alivyohisi alipotambua kwamba alitenda dhambi kwa kuhesabu watu. Biblia inasema kwamba “moyo wa Daudi ukaanza kumpiga.”—2 Samweli 24:1-10.

Uwezo wa kuchunguza mambo ambayo mtu alifanya zamani na kuchanganua mwenendo wake unaweza kumfanya achukue hatua muhimu ya kutubu kwa njia inayokubalika na Mungu. Daudi aliandika hivi: “Nilipokaa kimya mifupa yangu ilichakaa kwa sababu ya kuugua kwangu mchana kutwa. Mwishowe niliungama dhambi yangu kwako, wala sikufunika kosa langu. Nilisema: ‘Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.’ Nawe mwenyewe ukanisamehe kosa la dhambi zangu.” (Zaburi 32:3, 5) Hivyo, dhamiri inayofanya kazi inaweza kumsaidia mkosaji amrudie Mungu, na hivyo kumwezesha kutambua uhitaji wa kupata msamaha wa Mungu na kufuata njia Zake.—Zaburi 51:1-4, 9, 13-15.

Pia, dhamiri huonya au kutoa mwongozo tunapofanya maamuzi ya kiadili. Huenda jambo hilo kuhusu dhamiri ndilo lililomsaidia Yosefu kutambua kimbele kwamba kufanya uzinzi ni kosa na ni dhambi mbele za Mungu. Baadaye sheria hususa kuhusiana na uzinzi iliingizwa ndani ya Amri Kumi ambazo Waisraeli walipewa. (Mwanzo 39:1-9; Kutoka 20:14) Ni wazi kwamba tutafaidika zaidi ikiwa dhamiri yetu imezoezwa kutuongoza badala ya kutuhukumu tu. Je, dhamiri yako hufanya kazi jinsi hiyo?

Kuzoeza Dhamiri Ifanye Maamuzi Mazuri

Ingawa tunazaliwa tukiwa na dhamiri, inasikitisha kwamba zawadi hiyo huwa na kasoro. Ijapokuwa wanadamu waliumbwa wakiwa wakamilifu, “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa sababu ya dhambi na kutokamilika, huenda dhamiri yetu ikapotoka na kutofanya kazi kikamilifu kama ilivyokusudiwa. (Waroma 7:18-23) Zaidi ya hayo, mambo yanayotuzunguka yanaweza kuathiri dhamiri yetu. Inaweza kuathiriwa na malezi yetu au mila, imani, na mazingira. Kwa hakika, dhamiri njema haipaswi kuongozwa na maadili yaliyopotoka na viwango vya ulimwengu vinavyozidi kuzorota.

Hivyo, Mkristo anapaswa pia kuwa na msaada wa kanuni zilizo thabiti na za uadilifu za Neno la Mungu, Biblia. Kanuni kama hizo zinaweza kuongoza dhamiri yetu ili kuchanganua mambo kwa njia inayofaa na kuyanyoosha. (2 Timotheo 3:16) Dhamiri yetu inapoelimishwa kulingana na viwango vya Mungu, inaweza kutusaidia kuepuka matendo yatakayotudhuru kiadili, na kutuwezesha “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Bila viwango vya Mungu, huenda dhamiri yetu isituonye tunapojiingiza katika mwenendo mbaya. Biblia inasema hivi: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”—Methali 16:25; 17:20.

Katika hali fulani za maisha, Neno la Mungu hutoa maagizo na miongozo iliyo wazi, nasi hufaidika tunapoifuata. Kwa upande mwingine, kuna mambo mengi ambayo Biblia haitoi maagizo hususa juu yake. Hayo yanatia ndani kuchagua kazi, mambo yanayohusu afya, vitumbuizo, mavazi na mapambo, na kadhalika. Si rahisi kujua jambo la kufanya katika kila hali na kufanya uamuzi unaofaa. Kwa sababu hiyo, tunahitaji kuwa na mwelekeo kama wa Daudi, aliyesali hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe. Nitembeze katika kweli yako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu wangu wa wokovu.” (Zaburi 25:4, 5) Kadiri tunavyoelewa vizuri zaidi maoni na njia za Mungu, ndivyo tutakavyoweza kukadiria hali zetu kwa usahihi zaidi na kufanya maamuzi tukiwa na dhamiri safi.

Hivyo, tunapokabili suala au uamuzi fulani, tunapaswa kwanza kufikiria kanuni za Biblia ambazo huenda zikahusika. Baadhi ya kanuni hizo huenda ni: kuheshimu ukichwa (Wakolosai 3:18, 20); unyoofu katika mambo yote (Waebrania 13:18); kuchukia lililo baya (Zaburi 97:10); kufuatia amani (Waroma 14:19); kutii wenye mamlaka (Mathayo 22:21; Waroma 13:1-7); kujitoa kabisa kwa Mungu (Mathayo 4:10); kutokuwa sehemu ya ulimwengu (Yohana 17:14); kuepuka mashirika mabaya (1 Wakorintho 15:33); kuwa na kiasi katika mavazi na mapambo (1 Timotheo 2:9, 10); na kutowakwaza wengine (Wafilipi 1:10). Hivyo, kutambua kanuni muhimu za Biblia kunaweza kuimarisha dhamiri yetu na kutusaidia kufanya maamuzi yafaayo.

Sikiliza Dhamiri Yako

Ili dhamiri yetu itusaidie, tunapaswa kuitii. Tunaweza tu kufaidika na dhamiri iliyozoezwa na Biblia ikiwa tunatii maonyo inayotoa bila kukawia. Tunaweza kulinganisha dhamiri iliyozoezwa na taa za kuonya zilizo karibu na usukani wa gari. Tuseme taa moja inawaka na kutuonya kwamba shinikizo la mafuta limepungua. Itakuwaje tusipochukua hatua haraka na badala yake tuendelee kuendesha gari? Huenda tukaliharibu gari. Vivyo hivyo, dhamiri yetu, au sauti ya ndani, inaweza kutuonya kwamba mwenendo fulani ni mbaya. Tunapolinganisha matendo yetu au mambo tunayofikiria kuyafanya na viwango na kanuni za Maandiko, dhamiri yetu hutuonya kama ile taa. Kutii onyo hilo kutatusaidia kuepuka matokeo mabaya ya kutenda isivyo sawa na pia kutawezesha dhamiri yetu iendelee kufanya kazi vizuri.

Ni nini kitatukia tukiamua kupuuza onyo hilo? Hatua kwa hatua, dhamiri inaweza kuacha kutenda. Madhara tunayoweza kupata kwa kuzoea kupuuza au kukandamiza dhamiri yetu yanaweza kuwa kama yale ya kuunguza ngozi kwa chuma cha kutilia alama. Kovu lililo kwenye ngozi hufa ganzi kabisa. (1 Timotheo 4:2) Dhamiri kama hiyo haiitikii tena mtu anapotenda dhambi, wala haitoi maonyo ili kumzuia asirudie tena dhambi hiyo. Dhamiri iliyokufa ganzi hupuuza viwango vya Biblia vya mema na mabaya na hiyo ni dhamiri mbaya. Ni dhamiri iliyochafuka, na aliye nayo ‘ameishiwa na ufahamu wote wa maadili’ na kutenganishwa na Mungu. (Waefeso 4:17-19; Tito 1:15) Kwa kweli, kupuuza dhamiri yetu huwa na matokeo yenye kusikitisha.

“Iweni na Dhamiri Njema”

Kudumisha dhamiri njema kunahitaji jitihada ya kuendelea. Mtume Paulo alisema hivi: “Ninajizoeza mwenyewe sikuzote kudhamiria kutomkosea Mungu na wanadamu.” (Matendo 24:16) Akiwa Mkristo, Paulo aliendelea kuchunguza na kurekebisha mwenendo wake ili kuhakikisha kwamba hakumkosea Mungu. Paulo alijua kwamba hatimaye, ni Mungu atakayeamua ikiwa yale tunayofanya ni mema au mabaya. (Waroma 14:10-12; 1 Wakorintho 4:4) Paulo alisema hivi: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.”—Waebrania 4:13.

Paulo alisema pia kuhusu kutowakosea wanadamu. Mfano mmoja unaofaa ni shauri ambalo alitoa kwa Wakristo wa Korintho kuhusu “kula vyakula vinavyotolewa kwa sanamu.” Alikuwa akionyesha kwamba hata ikiwa matendo ya mtu hayakiuki Neno la Mungu, ni muhimu kufikiria dhamiri za wengine. Tukikosa kufanya hivyo tunaweza ‘kuwaharibu kiroho ndugu zetu ambao Kristo alikufa kwa ajili yao.’ Pia tunaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu.—1 Wakorintho 8:4, 11-13; 10:23, 24.

Kwa hiyo, endelea kuizoeza dhamiri yako ili udumishe dhamiri njema. Unapofanya maamuzi, tafuta mwongozo wa Mungu. (Yakobo 1:5) Jifunze Neno la Mungu, na uache kanuni zake zifinyange akili na moyo wako. (Methali 2:3-5) Mambo mazito yanapotokea, zungumza na Wakristo wakomavu ili uwe na hakika kwamba unaelewa vizuri kanuni za Biblia zinazohusika. (Methali 12:15; Waroma 14:1; Wagalatia 6:5) Fikiria jinsi uamuzi wako utakavyoathiri dhamiri yako, jinsi utakavyowaathiri wengine, na la muhimu zaidi, jinsi utakavyoathiri uhusiano wako pamoja na Yehova.—1 Timotheo 1:5, 18, 19.

Dhamiri yetu ni zawadi ya ajabu kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova Mungu. Kwa kuitumia kulingana na mapenzi ya Yule aliyeitoa, tutamkaribia zaidi Muumba wetu. Tunapojitahidi ‘kuwa na dhamiri njema’ katika kila jambo tunalofanya, tunaonyesha waziwazi zaidi kwamba tumeumbwa kwa mfano wa Mungu.—1 Petro 3:16; Wakolosai 3:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa dhamiri katika andiko hilo linamaanisha “uwezo wa ndani wa kufanya maamuzi ya kiadili,” (The Analytical Greek Lexicon Revised, kilichoandikwa na Harold K. Moulton); “kutofautisha kati ya yaliyo mema na mabaya kiadili.”—Greek-English Lexicon, kilichoandikwa na J. H. Thayer.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, dhamiri yako imezoezwa kukuongoza badala ya kukuhukumu tu?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Dhamiri yetu inazoezwa vizuri tunapojifunza na kutumia kanuni za Biblia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Usipuuze maonyo ya dhamiri yako