Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unatambua Ile Ishara ya Kuwapo kwa Yesu?

Je, Unatambua Ile Ishara ya Kuwapo kwa Yesu?

Je, Unatambua Ile Ishara ya Kuwapo kwa Yesu?

HAKUNA mtu ambaye angependa kuwa mgonjwa au kupatwa na msiba. Ili kuepuka matatizo kama hayo, mtu mwenye hekima huwa macho kuona ishara zinazoonyesha hatari na kutenda ifaavyo. Yesu Kristo alielezea ishara fulani ambayo tunapaswa kutambua hasa. Mambo aliyosema yangetokea ulimwenguni pote na kuwaathiri wanadamu wote. Hiyo inatia ndani wewe na familia yenu.

Yesu alizungumzia Ufalme wa Mungu ambao utaondoa uovu na kufanya dunia kuwa paradiso. Wanafunzi wake walitaka kujua jambo hilo na pia wakati wa kuja kwa Ufalme huo. Waliuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3.

Yesu alijua kwamba baada ya kufa na kufufuliwa, miaka mingi ingepita ndipo atawazwe kuwa Mfalme wa Kimasihi mbinguni ili awatawale wanadamu. Kwa kuwa wanadamu hawangeweza kuona akitawazwa, Yesu alitoa ishara ambayo ingewawezesha wafuasi wake kutambua “kuwapo” kwake na pia “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ishara hiyo ina sehemu nyingi ambazo huonyesha kuwapo kwa Yesu.

Waandikaji wa Injili, Mathayo, Marko, na Luka waliandika kwa uangalifu jibu la Yesu. (Mathayo, sura ya 24 na 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21) Waandikaji wengine wa Biblia pia waliandika habari zaidi kuhusu ishara hiyo. (2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4; Ufunuo 6:1-8; 11:18) Hatuwezi kuzungumzia habari zote katika makala hii, lakini tutachunguza mambo matano yanayofanyiza ile ishara iliyotajwa na Yesu. Utaona kwamba ni muhimu kwako kuchunguza mambo hayo.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 6.

“Miaka Iliyoanzisha Enzi Mpya”

“Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Kulingana na gazeti Der Spiegel la Ujerumani, kabla ya mwaka wa 1914, watu “walitazamia wakati ujao ulio bora wenye uhuru zaidi, maendeleo, na ufanisi.” Kisha mambo yakabadilika. Gazeti GEO linasema hivi: “Vita vilivyoanza Agosti 1914 na kumalizika Novemba 1918 viliwashangaza watu wengi. Vita hivyo vilileta mabadiliko makubwa kwa kutenganisha mambo ya kale na ya sasa.” Zaidi ya wanajeshi milioni 60 kutoka katika mabara matano walihusika katika pambano kali. Kwa wastani, wanajeshi 6,000 hivi waliuawa kila siku. Tangu wakati huo, wanahistoria wa kila kizazi na wenye maoni tofauti-tofauti ya kisiasa wameiona “miaka ya 1914 hadi 1918 kuwa miaka iliyoanzisha enzi mpya.”

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilileta mabadiliko makubwa katika jamii ya wanadamu na kuwaingiza katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Katika miaka mingine ya karne ya 20 kulikuwa na ongezeko la vita, mapambano yanayohusisha matumizi ya silaha, na ugaidi. Mambo hayajawa mazuri katika miaka ya mapema ya karne hii. Mbali na vita, mambo mengine ya ile ishara yanaonekana.

Njaa, Tauni, na Matetemeko ya Nchi

“Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7) Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, bara la Ulaya lilikumbwa na njaa, na tangu wakati huo wanadamu wamekumbwa na njaa. Mwanahistoria Alan Bullock aliandika kwamba mwaka wa 1933 huko Urusi na Ukrainia, “watu wengi wenye njaa walikuwa wakitangatanga nchini . . . Maiti za watu zilikuwa zimerundikwa kando ya barabara.” Katika mwaka wa 1943, T. H. White, ambaye ni mwandishi wa habari, alishuhudia baa la njaa katika wilaya ya Henan huko China. Aliandika: “Wakati wa njaa, karibu kila kitu kinaweza kuliwa, kumeng’enywa, na kubadilishwa kuwa nishati mwilini. Mtu anapokabili kifo anaweza kula kitu chochote ambacho hapo awali hakufikiri kinaliwa.” Inasikitisha kwamba katika miaka ya karibuni, njaa imekuwa jambo la kawaida barani Afrika. Ingawa dunia inazaa chakula cha kumtosha kila mtu, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa linakadiria kwamba watu milioni 840 duniani hawana chakula cha kutosha.

“Katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni.” (Luka 21:11) Kulingana na gazeti Süddeutsche Zeitung, ‘inakadiriwa kwamba homa ya Kihispania ilisababisha vifo vya kati ya watu milioni 20 na milioni 50 katika mwaka wa 1918, zaidi ya wale waliokufa kutokana na ile tauni ya karne ya 14 au vita vya kwanza vya ulimwengu.’ Tangu wakati huo, watu wengi wameugua magonjwa kama malaria, ndui, kifua kikuu, polio na kipindupindu. Na wanadamu wanasikitika kuona UKIMWI ukienea upesi. Inashangaza kwamba ijapokuwa kuna maendeleo ya kitiba, magonjwa yanazidi kuongezeka. Hali hiyo inayowatatanisha wanadamu inathibitisha kwamba tunaishi wakati wa pekee sana.

“Matetemeko ya nchi.” (Mathayo 24:7) Katika kipindi cha miaka 100 iliyopita, mamia ya maelfu ya watu wamekufa kutokana na matetemeko ya nchi. Kulingana na uchunguzi fulani, matetemeko ya nchi yenye nguvu zinazoweza kuharibu majengo na kupasua ardhi yamefikia wastani wa 18 kila mwaka tangu mwaka wa 1914. Matetemeko ya nchi yenye nguvu sana kiasi cha kuangusha majengo yametokea mara moja hivi kwa mwaka. Ijapokuwa maendeleo ya kitekinolojia, watu wengi wanakufa kwa sababu majiji mengi yaliyo na idadi kubwa ya watu yana uwezekano wa kukumbwa na matetemeko ya nchi.

Habari za Kupendeza!

Sehemu nyingi za ile ishara ya siku za mwisho ni zenye kuhuzunisha. Hata hivyo, Yesu alizungumzia pia habari za kupendeza.

“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Kazi ambayo Yesu mwenyewe alianzisha, yaani, kuhubiri habari njema ya Ufalme, ingefikia kilele katika siku za mwisho. Kazi hiyo, imekuwa ikifanywa kama ilivyotabiriwa. Mashahidi wa Yehova wanahubiri ujumbe wa Biblia na kuwafundisha watu wanaopendezwa kutumia maishani mambo wanayojifunza. Sasa, kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita wanaohubiri katika nchi 235 na katika lugha zaidi ya 400.

Ona kwamba Yesu hakusema shughuli zote maishani zitakoma kwa sababu ya hali za ulimwengu zenye kuhuzunisha. Pia hakusema kwamba ulimwengu wote utakuwa na sehemu moja tu ya ile ishara. Lakini alitabiri matukio mengi ambayo yangefanyiza ile ishara ambayo ingetambuliwa kotekote duniani.

Badala ya kukazia fikira tukio moja, je, unaona mambo fulani yanayojirudia, au ishara yenye sehemu nyingi inayotukia ulimwenguni pote? Mambo yanayotukia yanakuathiri wewe na familia yenu. Huenda ukauliza, Kwa nini ni watu wachache tu wanaoyatilia maanani?

Watu Wanatanguliza Mapendezi Yao

“Usiogelee Hapa,” “Umeme! Hatari!,” “Punguza Mwendo.” Hizo ni baadhi ya ishara na maonyo yanayoonekana lakini ambayo hupuuzwa mara nyingi. Kwa nini? Kwa sababu tunapumbazwa kwa urahisi na mambo tunayofikiri ni muhimu kwetu. Kwa mfano, huenda ukataka kuendesha gari kwa mwendo wa kasi sana kuliko vile inavyoruhusiwa na sheria, au ukatamani sana kuogelea mahali usipopaswa. Hata hivyo, si jambo la hekima kupuuza ishara.

Kwa mfano, maporomoko ya theluji kwenye milima ya Alps ya Austria, Italia, Ufaransa, na Uswisi wakati mwingine husababisha vifo vya watalii ambao hupuuza maonyo yanayowatahadharisha wasiteleze kwenye theluji katika maeneo hatari. Kulingana na gazeti Süddeutsche Zeitung, watalii wengi hupuuza maonyo kama hayo wakisema kwamba, Huwezi kujifurahisha bila kujihatarisha. Inasikitisha kwamba kupuuza maonyo kunaweza kuleta maafa.

Kwa nini watu hupuuza ishara iliyotolewa na Yesu? Huenda wakapumbazika kwa sababu ya tamaa ya mali, kutojali, kushindwa kufanya maamuzi, kulemewa na shughuli za maisha, au kuogopa kupoteza umashuhuri. Je, inawezekana kwamba unapuuza ishara ya kuwapo kwa Yesu kwa sababu moja kati ya hizo? Je, halingekuwa jambo la hekima kutambua ile ishara na kutenda ifaavyo?

Maisha Katika Paradiso Duniani

Idadi ya watu wanaotii ile ishara ya kuwapo kwa Yesu inaongezeka. Kristian, mume kijana huko Ujerumani, aliandika: “Hizi ni nyakati zenye kuvunja moyo. Bila shaka, tunaishi katika ‘siku za mwisho.’” Yeye na mke wake hutumia wakati mwingi kuzungumza na watu kuhusu Ufalme wa Kimasihi. Frank anaishi katika nchi hiyo pia. Yeye na mke wake huwatia wengine moyo na habari njema za Biblia. Frank anasema: “Kwa sababu ya hali za ulimwengu, watu wengi leo wana wasiwasi kuhusu wakati ujao. Sisi hujaribu kuwatia moyo kwa kuwaonyesha unabii wa Biblia unaohusu dunia paradiso.” Hivyo, Kristian na Frank wanashiriki kutimiza sehemu moja ya ile ishara ya Yesu, yaani, kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme.—Mathayo 24:14.

Siku za mwisho zitakapofikia kilele, Yesu atauharibu mfumo huu wa kale pamoja na wanaouunga mkono. Kisha, Ufalme wa Kimasihi utasimamia mambo duniani, na kuifanya dunia kuwa Paradiso kama ilivyotabiriwa. Wanadamu watakuwa huru kutokana na magonjwa na kifo, na wafu watafufuliwa duniani. Hayo ni matumaini mazuri kwa wale wanaotambua ishara za nyakati. Je, halingekuwa jambo muhimu kujifunza mengi kuhusu ile ishara na yale ambayo mtu anaweza kufanya ili aokoke mwisho wa mfumo huu? Kwa hakika hilo linapaswa kuwa jambo la kuhangaikiwa na kila mtu.—Yohana 17:3.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Yesu alitabiri matukio mengi ambayo yangefanyiza ile ishara ambayo ingetambuliwa kotekote duniani

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Je, unaona mambo fulani yanayojirudia, au ishara yenye sehemu nyingi inayotukia ulimwenguni pote?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

MAMBO YANAYOTAMBULISHA SIKU ZA MWISHO

Vita visivyo na kifani.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:4

Njaa.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:5, 6, 8

Tauni.—Luka 21:11; Ufunuo 6:8

Kuongezeka kwa uasi-sheria.—Mathayo 24:12

Matetemeko ya nchi.—Mathayo 24:7

Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.—2 Timotheo 3:1

Kupenda pesa isivyofaa.—2 Timotheo 3:2

Kutotii wazazi.—2 Timotheo 3:2

Kutokuwa na upendo wa asili.—2 Timotheo 3:3

Kupenda raha badala ya kumpenda Mungu.—2 Timotheo 3:4

Kutojizuia.—2 Timotheo 3:3

Kutopenda mema.—2 Timotheo 3:3

Kutojali hatari inayokuja.—Mathayo 24:39

Wadhihaki wanaokataa uthibitisho wa siku za mwisho.—2 Petro 3:3, 4

Kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu duniani pote.—Mathayo 24:14

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

WWI soldiers: From the book The World War—A Pictorial History, 1919; poor family: AP Photo/Aijaz Rahi; polio victim: © WHO/P. Virot