Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni “Tajiri kwa Mungu”?

Je, Wewe Ni “Tajiri kwa Mungu”?

Je, Wewe Ni “Tajiri kwa Mungu”?

KATI ya mifano mingi yenye kuchochea fikira aliyoitoa Yesu Kristo, kuna ule unaohusu mmiliki wa shamba aliye tajiri. Katika jitihada zake za kujitayarishia wakati ujao ulio salama, mmiliki huyo alifanya mipango ya kujenga maghala makubwa zaidi. Hata hivyo, katika mfano wa Yesu, mtu huyo anaitwa ‘asiye na akili.’ (Luka 12:16-21) Hata tafsiri nyingi za Biblia zinatumia neno “mpumbavu.” Kwa nini alihukumiwa vikali hivyo?

Yaonekana, mtu huyo tajiri hakumfikiria Mungu alipofanya mipango yake; wala hakumpa Mungu sifa kwa kuwa yeye ndiye hufanya ardhi iweze kutokeza mazao. (Mathayo 5:45) Badala yake alijisifu hivi: “Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.” Naam, alifikiri kwamba matokeo ya jitihada zake yangekuwa kama “ukuta wa ulinzi.”—Methali 18:11.

Mwanafunzi Yakobo alitoa onyo kuhusu roho kama hiyo ya kujivuna alipoandika hivi: “Haya, basi, ninyi ambao husema: ‘Leo au kesho tutasafiri kwenda jiji fulani nasi tutakaa mwaka mmoja huko, tutafanya biashara na kupata faida,’ ingawa hamjui uzima wenu utakuwa namna gani kesho. Kwa maana ninyi ni ukungu unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka.”—Yakobo 4:13, 14.

Maneno hayo yalithibitika kuwa ya kweli, kwa kuwa mtu tajiri katika mfano wa Yesu aliambiwa hivi: “Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?” Kama vile ukungu unaotoweka, mtu huyo tajiri angekufa kabla ya kuona utimizo wa ndoto zake. Je, tunatambua somo? Yesu alisema: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” Je, wewe ni “tajiri kwa Mungu”?