Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfano wa Wazazi Wangu Uliniimarisha

Mfano wa Wazazi Wangu Uliniimarisha

Simulizi la Maisha

Mfano wa Wazazi Wangu Uliniimarisha

LIMESIMULIWA NA JANEZ REKELJ

Ulikuwa mwaka wa 1958. Mimi na mke wangu Stanka, tulikuwa juu ya milima ya Alps ya Karawanken kwenye mpaka wa Yugoslavia na Austria tukijaribu kukimbilia Austria. Ilikuwa hatari kufanya hivyo kwa kuwa jeshi la Yugoslavia lilikuwa likishika doria mpakani ili kuwazuia watu wasivuke. Tuliposonga mbele tulifika kwenye ncha ya mwamba mrefu. Mimi na Stanka hatukuwa tumewahi kuona sehemu ya milima hiyo huko Austria. Tulielekea upande wa mashariki hadi tukafikia mwinuko wenye mawe ya changarawe. Tulijifunga turubai tuliyokuwa tumebeba, na kuteleza mlimani bila kujua kitakachotupata.

ACHENI niwaeleze jinsi tulivyojikuta katika hali hiyo na jinsi mfano mwaminifu wa wazazi wangu ulivyonichochea kubaki mshikamanifu kwa Yehova katika nyakati ngumu.

Nilikulia huko Slovenia, ambayo sasa ni nchi ndogo katika Ulaya ya Kati. Slovenia inapatikana katika milima ya Ulaya ya Alps, Austria ikiwa kaskazini, Italia magharibi, Kroatia kusini, na Hungaria mashariki. Hata hivyo, wazazi wangu, Franc na Rozalija Rekelj, walipozaliwa, Slovenia ilikuwa sehemu ya Milki ya Austria na Hungaria. Mwishoni mwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Slovenia ikawa sehemu ya taifa jipya lililoitwa Ufalme wa Waserbia, Wakroatia, na Waslovenia. Katika mwaka wa 1929, jina la nchi hiyo lilibadilishwa na kuwa Yugoslavia, ambalo linamaanisha “Slavia ya Kusini.” Nilizaliwa Januari 9 mwaka huohuo, nje ya kijiji cha Podhom, karibu na Ziwa Bled lenye kuvutia.

Mama alipewa malezi thabiti ya Kikatoliki. Baba yake mdogo alikuwa kasisi, na shangazi zake watatu walikuwa watawa wa kike. Mama alitamani sana kuwa na Biblia yake mwenyewe, aisome, na kuielewa. Hata hivyo, Baba hakuwa na maoni mazuri kuhusu dini. Alichukizwa na matendo ya dini wakati wa vile Vita Vikuu vya 1914-1918.

Najifunza Kweli

Punde baada ya vita hivyo, binamu ya mama yangu, Janez Brajec, pamoja na mke wake, Ančka, wakawa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Wakati huo, waliishi huko Austria. Tangu 1936 hivi na kuendelea, Ančka alimtembelea Mama mara kadhaa. Alimpa Biblia, na Mama akaisoma haraka sana, pamoja na nakala za Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Kislovenia vinavyofafanua Biblia. Mwishowe, kwa sababu ya Hitler kuiteka Austria mnamo 1938, Janez na Ančka walirudi tena Slovenia. Ninakumbuka kwamba walikuwa wenye elimu na ufahamu, nao walimpenda sana Yehova. Mara nyingi, walizungumza na Mama kweli za Biblia ambazo zilimchochea kujiweka wakfu kwa Yehova. Alibatizwa mwaka wa 1938.

Kulitokea fujo katika eneo hilo wakati Mama alipoacha kufuata desturi zisizopatana na Maandiko, kama vile kusherehekea Krismasi; na alipoacha kula soseji zenye damu; na hasa alipokusanya sanamu zote tulizokuwa nazo na kuzichoma. Upinzani ulitokea haraka. Shangazi za Mama, wale watawa wa kike, walimwandikia barua ili kujaribu kumshawishi arudi kwa Maria na kanisani. Hata hivyo, Mama alipowaandikia na kuwauliza maswali hususa ya Biblia, hakupata jibu lolote. Babu yangu pia alimpinga Mama kabisa. Ingawa babu yangu hakuwa mtu mbaya, watu wa ukoo na watu katika jumuiya yetu walimweka chini ya mkazo mkali. Kwa sababu hiyo, mara kadhaa aliharibu vichapo vya Mama vinavyofafanua Biblia, lakini hakuwahi kuigusa Biblia. Hata alipiga magoti ili kumsihi mama arudi kanisani. Pia, alimtisha mama kwa kisu. Hata hivyo, Baba alimwambia baba-mkwe wake kwa uthabiti kwamba hatavumilia tabia kama hiyo.

Baba aliendelea kutetea haki ya Mama ya kuisoma Biblia na kuamua mwenyewe kuhusu imani yake. Mnamo 1946 Baba alibatizwa pia. Nilichochewa kusitawisha uhusiano wangu pamoja na Mungu nilipoona jinsi Yehova alivyomwimarisha mama yangu kusimama imara kwa ajili ya kweli licha ya upinzani na jinsi Yehova alivyompa thawabu kwa sababu ya imani yake. Pia nilifaidika sana kutokana na zoea la Mama la kunisomea kwa sauti Biblia na vichapo vinavyoifafanua.

Pia, Mama alikuwa akizungumza sana kuhusu Biblia pamoja na dada yake mdogo, Marija Repe, na hatimaye mimi na Shangazi Marija tukabatizwa siku ileile katikati ya Julai 1942. Ndugu mmoja alikuja kutoa hotuba fupi, nasi tukabatizwa ndani ya kidimbwi kikubwa cha mbao.

Kazi ya Kulazimishwa Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu

Mnamo 1942, katikati ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, Ujerumani na Italia zilivamia Slovenia na kuigawanya kati yao na Hungaria. Wazazi wangu walikataa kujiunga na chama cha raia cha Nazi kilichoitwa Volksbund. Nilikataa kusema “Heil Hitler” shuleni. Yaelekea, mwalimu wangu aliwajulisha wakuu jambo hilo.

Tuliwekwa ndani ya gari-moshi kuelekea kwenye ngome iliyokuwa karibu na kijiji cha Hüttenbach, Bavaria, ambayo ilitumiwa kama kambi ya kazi ya kulazimishwa. Baba alifanya mipango ili nifanye kazi na kuishi pamoja na mwokaji mikate wa mahali hapo na familia yake. Wakati huo, nilijifunza kuoka mikate, kazi ambayo ilinisaidia sana baadaye. Baada ya muda, watu wengine wa familia yetu (kutia ndani Shangazi Marija na familia yake) walihamishwa kwenye kambi ya Gunzenhausen.

Mwishoni mwa vita, nilitaka kujiunga na kikundi fulani cha watu na kusafiri pamoja nao hadi mahali walikoishi wazazi wangu. Hata hivyo, jioni ile kabla niondoke, Baba aliwasili. Sijui ni jambo gani lingenipata ikiwa ningesafiri na watu hao kwa kuwa hawakuaminika. Kwa mara nyingine tena, nilihisi upendo wa Yehova kwa kuwa aliwatumia wazazi wangu kunilinda na kunizoeza. Mimi na Baba tulitembea muda wa siku tatu ili kuungana na familia yetu. Mnamo Juni 1945, sote tulifika nyumbani.

Baada ya vita, Wakomunisti, chini ya uongozi wa Rais Josip Broz Tito, walichukua mamlaka nchini Yugoslavia. Hivyo, hali ziliendelea kuwa ngumu kwa Mashahidi wa Yehova.

Mnamo mwaka wa 1948, ndugu mmoja alikuja kutoka Austria, naye akakubali kula mlo pamoja nasi. Kila mahali alipokwenda, polisi walimfuata na kuwafunga ndugu ambao aliwatembelea. Baba pia alifungwa kwa kuwa alimkaribisha na hakumshtaki kwa polisi, na kwa sababu hiyo Baba akafungwa gerezani kwa miaka miwili. Huo ulikuwa wakati mgumu sana kwa Mama, si kwa sababu tu Baba hakuwa nyumbani, bali pia kwa sababu alijua kwamba karibuni mimi na ndugu yangu mdogo tungekabili jaribu kuhusiana na msimamo wetu wa kutokuwamo.

Kufungwa Gerezani Huko Makedonia

Mnamo Novemba 1949, niliitwa kutumikia jeshini. Nilienda kuwaona wakuu wa jeshi ili kuwaeleza kwamba siwezi kutumikia jeshini kwa sababu ya dhamiri yangu. Hawakunisikiliza, nao wakanitia kwenye gari-moshi pamoja na askari wapya kuelekea Makedonia, upande ule mwingine wa Yugoslavia.

Kwa muda wa miaka mitatu, sikuwahi kuwasiliana na familia yangu wala ndugu Wakristo, na sikuwa na kichapo chochote wala Biblia. Hali ilikuwa ngumu sana. Kutafakari juu ya Yehova na mfano wa Mwana wake, Yesu Kristo, kulinitegemeza. Pia mfano wa wazazi wangu uliniimarisha. Isitoshe, kusali daima ili kujiimarisha kuliniwezesha nisikate tamaa.

Baada ya muda, nilitumwa kwenye gereza moja huko Idrizovo, karibu na Skopje. Katika gereza hilo, wafungwa walifanya kazi mbalimbali za ufundi. Kwanza, nilikuwa msafishaji, baadaye nikawa tarishi. Ingawa mara kwa mara nilinyanyaswa na mfungwa fulani ambaye hapo awali alikuwa mmoja wa polisi wa siri, nilikuwa na uhusiano mzuri na kila mtu, yaani, walinzi, wafungwa, na hata msimamizi wa kiwanda cha gereza.

Baadaye, nilipata habari kwamba mwokaji mikate alihitajiwa mahali pa kuokea mikate ya gereza. Siku chache baadaye, msimamizi alikuja kuita majina ya wafungwa. Alitembea akikagua wafungwa, kisha akasimama mbele yangu naye akaniuliza, “Je, wewe ni mwokaji wa mikate?” “Ndiyo, Bwana,” nikajibu. Naye akaniambia: “Kesho asubuhi njoo mahali wanapookea mikate.” Mfungwa aliyekuwa akininyanyasa alipita mara nyingi mahali hapo, lakini hakuwa na lolote la kufanya. Nilifanya kazi mahali hapo toka Februari hadi Julai 1950.

Kisha nilihamishwa kwenda kwenye kambi ya jeshi iliyoitwa Volkoderi, kusini mwa Makedonia, karibu na Ziwa Prespa. Kwa kuwa nilikuwa karibu na Otešovo, niliweza kutuma barua nyumbani. Nilifanya kazi pamoja na wafungwa wengine kwenye ujenzi wa barabara, lakini mara nyingi, nilioka mikate, jambo ambalo lilifanya mambo yawe rahisi zaidi kwangu. Nilifunguliwa mnamo Novemba 1952.

Sikuwapo kutaniko lilipoanzishwa Podhom. Kwanza, mikutano ya kutaniko hilo ilifanyika katika hoteli ndogo huko Spodnje Gorje. Baadaye, Baba aliruhusu chumba kimoja katika nyumba yetu kitumiwe kwa ajili ya mikutano. Niliporudi kutoka Makedonia, nilifurahi sana kujiunga nao. Pia, nilianzisha tena urafiki wangu pamoja na Stanka, niliyekutana naye kabla sijafungwa. Mnamo Aprili 24, 1954 tukafunga ndoa. Hata hivyo, nilikuwa huru kwa muda mfupi tu.

Kufungwa Gerezani Huko Maribor

Mnamo Septemba 1954, niliitwa tena jeshini. Wakati huo, nilihukumiwa kifungo cha zaidi ya miaka mitatu na nusu katika gereza moja huko Maribor, mashariki ya Slovenia. Nilipopata nafasi, nilinunua karatasi na kalamu za risasi. Nilianza kuandika kila kitu nilichoweza kukumbuka, maandiko, manukuu kutoka Mnara wa Mlinzi, na habari nyingine kutoka vichapo vya Kikristo. Nilisoma maandishi yangu mwenyewe na kuongeza mengine katika kitabu hicho kadiri nilivyoendelea kukumbuka mambo zaidi. Hatimaye, kitabu hicho kilijaa, na mambo niliyoandika humo yalinisaidia kukaza akili juu ya kweli na kuendelea kuwa mwenye nguvu kiroho. Pia, kusali na kutafakari kulinisaidia sana kuimarisha hali yangu ya kiroho, na kukaniwezesha kuwa mwenye ujasiri zaidi kuhubiria wengine kweli za Biblia.

Wakati huo, niliruhusiwa kupokea barua moja kwa mwezi na ziara moja ya dakika 15 kwa mwezi. Stanka alisafiri kwa gari-moshi usiku wote ili afike mapema kuniona gerezani, kisha arudi nyumbani siku hiyohiyo. Ziara hizo zilinitia moyo sana. Kisha nilifanya mpango wa kupata Biblia. Mimi na Stanka tulikaa mezani tukielekeana tukiwa pamoja na mlinzi aliyeteuliwa ili kutuchunguza. Mlinzi huyo alipoangalia upande mwingine, niliingiza barua ndani ya mkoba wa Stanka ili kumwomba atie Biblia ndani ya mkoba wake wakati mwingine atakaponitembelea.

Stanka na wazazi wangu walifikiri kwamba ingekuwa hatari sana kufanya hivyo. Hivyo, wakararua kurasa za nakala ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na kuziweka ndani ya mfuko uliokuwa na mikate. Kwa njia hiyo, nilipata Biblia niliyohitaji. Kwa njia hiyohiyo pia, nilipokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi, ambayo Stanka alinakili mwenyewe kwa mkono. Mara tu nilipoyapokea niliyanakili mwenyewe kwa mkono na kuharibu yale ya awali kutoka kwa Stanka ili mtu yeyote asitambue jinsi nilivyoyapata.

Kwa sababu ya kuendelea kuhubiri, wafungwa wenzangu walinieleza kwamba nitakuwa matatani. Pindi moja, nilikuwa na mazungumzo ya Biblia yenye kusisimua pamoja na mfungwa mwenzangu. Tulisikia ufunguo umeingizwa ndani ya kufuli, na mlinzi akaingia. Mara moja nikafikiri kwamba nitawekwa katika kifungo cha upweke. Lakini mlinzi huyo hakuwa na kusudi hilo. Alikuwa amesikia mazungumzo naye alitaka kujiunga nasi katika mazungumzo hayo. Baada ya kuridhika na majibu ambayo alipata kwa maswali yake, aliondoka na kufunga kwa kufuli mlango wa gereza.

Katika mwezi wa mwisho wa kifungo changu, ofisa aliyeshughulikia marekebisho ya wafungwa alinisifu kwa sababu ya msimamo wangu thabiti kwa ajili ya kweli. Niliona pongezi hizo kuwa thawabu kwa ajili ya jitihada zangu za kulitangaza jina la Yehova. Mnamo Mei 1958, niliachiliwa tena kutoka gerezani.

Ninakimbilia Austria, Kisha Australia

Mama alikufa mnamo Agosti 1958. Alikuwa ameugua kwa muda fulani. Kisha mnamo Septemba 1958, niliitwa jeshini kwa mara ya tatu. Jioni hiyo, mimi na Stanka tulifikia uamuzi muhimu ambao ulitufanya tuvuke mpaka tuliozungumzia mwanzoni. Bila kumwambia yeyote, tulipakia mifuko yetu ya mgongoni na kuchukua turubai na kuondoka kupitia dirishani ili kuelekea mpaka wa Austria, magharibi mwa Mlima Stol. Inaonekana kwamba Yehova alifungua mlango wa kutokea kwa ajili yetu kwa kuwa alijua kwamba tunahitaji kitulizo.

Wenye mamlaka huko Austria waliagiza tupelekwe kwenye kambi ya wakimbizi karibu na Salzburg. Kwa muda wa miezi sita tuliyokaa huko, sikuzote tulikuwa pamoja na Mashahidi wenyeji, hivyo hatukukaa sana kambini. Wengine kambini walishangaa jinsi tulivyopata marafiki haraka. Huo ndio wakati tulipohudhuria kusanyiko letu la kwanza. Pia, kwa mara ya kwanza tuliweza kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa uhuru. Ilikuwa vigumu sana kwetu kuachana na marafiki hao wapendwa tulipokuwa tukiondoka huko.

Wakuu wa Austria walituruhusu tuhamie Australia. Hatukuwahi kufikiria kwamba tungesafiri mbali hivyo. Tulisafiri kwa gari-moshi kwenda Genoa, Italia, na kisha tukaingia ndani ya meli iliyoelekea Australia. Hatimaye, tuliishi katika jiji la Wollongong, New South Wales. Mwana wetu Philip alizaliwa huko Machi 30, 1965.

Kuishi Australia kumetupa nafasi nyingi za utumishi, kutia ndani ile ya kuwahubiria wahamiaji waliotoka maeneo ya Yugoslavia ya zamani. Tunamshukuru sana Yehova kwa baraka zake, kutia ndani kutuwezesha kumtumikia tukiwa familia yenye umoja. Philip na mke wake, Susie, wana pendeleo la kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia, na walipata pendeleo la kutumikia kwa miaka miwili katika ofisi ya tawi ya Slovenia.

Licha ya matatizo yanayotokana na uzee na afya mbaya, mimi na mke wangu tunaendelea kufurahia utumishi wetu kwa Yehova. Ninawashukuru sana wazazi wangu kwa mfano wao mzuri! Mfano wao unaendelea kuniimarisha na kunisaidia kufanya yale ambayo mtume Paulo alisema: “Shangilieni katika tumaini. Vumilieni chini ya dhiki. Dumuni katika sala.”—Waroma 12:12.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Wazazi wangu katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1920

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mama yangu, aliye mwisho kulia, pamoja na Ančka, aliyemfundisha kweli

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na mke wangu, Stanka, muda mfupi baada ya kufunga ndoa

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kutaniko lililokusanyika katika nyumba yetu mwaka wa 1955

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na mke wangu, mwana wetu Philip, na mke wake, Susie