Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi, Mnataka Watoto Wenu Wawe na Maisha ya Aina Gani Wakati Ujao?

Wazazi, Mnataka Watoto Wenu Wawe na Maisha ya Aina Gani Wakati Ujao?

Wazazi, Mnataka Watoto Wenu Wawe na Maisha ya Aina Gani Wakati Ujao?

“Enyi vijana, nanyi mabikira pia . . . Na walisifu jina la Yehova.”—Zaburi 148:12, 13.

1. Wazazi huhangaikia mambo gani kuhusu watoto wao?

NI MZAZI gani asiyehangaikia wakati ujao wa watoto wake? Kuanzia wakati ambapo mtoto anazaliwa, au hata kabla ya wakati huo, wazazi huanza kuhangaikia hali yake. Je, atakuwa mwenye afya? Je, atakua bila kasoro? Mtoto anapozidi kukua, mahangaiko huongezeka. Kwa kawaida, wazazi hutaka watoto wao wawe na maisha bora.—1 Samweli 1:11, 27, 28; Zaburi 127:3-5.

2. Kwa nini wazazi wengi leo wanataka sana watoto wao wafurahie maisha mazuri wanapokuwa watu wazima?

2 Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, ni vigumu kwa wazazi kuwasaidia watoto wao wawe na maisha bora. Wazazi wengi wamekabili hali ngumu kama vile vita, misukosuko ya kisiasa, matatizo ya kiuchumi, kimwili, kihisia, na kadhalika. Kwa kawaida, hawataki watoto wao wakabili matatizo hayohayo. Katika nchi zenye ufanisi, huenda wazazi wakaona wana na mabinti wa marafiki wao na watu wa ukoo wakifanikiwa katika kazi ya kimwili na kufurahia maisha yenye mafanikio. Hivyo, wanaona ni lazima wajitahidi juu chini kuhakikisha kwamba watoto wao pia wanafurahia maisha mazuri wanapokuwa watu wazima, yaani, maisha salama na ya kustarehesha.—Mhubiri 3:13.

Kuchagua Maisha Bora

3. Wakristo wamechagua kufanya nini?

3 Kwa kuwa wao ni wafuasi wa Yesu Kristo, Wakristo wamechagua kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Wametii maneno haya ya Yesu: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata sikuzote.” (Luka 9:23; 14:27) Naam, Mkristo anahitaji kuishi maisha ya kujidhabihu. Hata hivyo, hayo si maisha ya umaskini na taabu. Badala yake, ni maisha yanayofurahisha na kuridhisha, yaani, maisha mazuri, kwa sababu yanahusisha kutoa, na kama Yesu alivyosema “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

4. Yesu aliwahimiza wafuasi wake watafute nini?

4 Katika siku za Yesu watu walikabili hali ngumu sana. Zaidi ya kufanya kazi ili kupata riziki, iliwabidi wavumilie utawala mkatili wa Waroma na uonevu mkali wa wanadini wa wakati huo walioshikilia sana mapokeo. (Mathayo 23:2-4) Hata hivyo, watu wengi waliomsikiliza Yesu walikubali kwa hiari kuacha kufuatia mambo yao binafsi, hata kazi zao, nao wakawa wafuasi wake. (Mathayo 4:18-22; 9:9; Wakolosai 4:14) Je, wanafunzi hao walikuwa wakihatarisha maisha yao ya wakati ujao? Ona maneno haya ya Yesu: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mathayo 19:29) Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba Baba yao wa mbinguni anajua mahitaji yao. Kwa hiyo, aliwahimiza hivi: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:31-33.

5. Wazazi fulani huhisije kuhusu uhakikisho wa Yesu kwamba Mungu atawatunza watumishi wake?

5 Hivyo ndivyo mambo yalivyo leo. Yehova anajua mahitaji yetu. Wale wanaotanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao, hasa wale walio katika huduma ya wakati wote, wana uhakikisho huohuo kwamba atawatunza. (Malaki 3:6, 16; 1 Petro 5:7) Hata hivyo, wazazi fulani wana mashaka kuhusu jambo hilo. Kwa upande mmoja, wanataka watoto wao wafanye maendeleo katika utumishi wa Yehova, na hata baadaye waanze huduma ya wakati wote. Kwa upande mwingine, wanapofikiria hali ya kiuchumi na ya kikazi katika ulimwengu wa leo, wanahisi kwamba ni muhimu vijana wapate elimu bora kwanza ili wafaulu kupata kazi nzuri au wawe na kitu fulani cha kuwategemeza hali zitakapobadilika. Wazazi hao huona kwamba elimu ya juu ndiyo elimu bora.

Kupangia Wakati Ujao

6. Katika makala hii, maneno “elimu ya juu” yametumiwa kumaanisha nini?

6 Mfumo wa elimu hutofautiana katika nchi mbalimbali. Kwa mfano, huko Marekani, shule za umma hutoa elimu ya msingi kwa miaka 12. Baadaye, wanafunzi wanaweza kuchagua kwenda chuo kikuu au chuo cha mafunzo kwa miaka minne au zaidi na kupata digrii ya kwanza au digrii nyingine za juu kwa kusomea tiba, sheria, kazi ya injinia, na kadhalika. Tunapozungumzia “elimu ya juu” katika makala hii, tunamaanisha elimu hiyo ya chuo kikuu. Kwa upande mwingine, kuna shule za ufundi, ambazo hutoa masomo kwa muda mfupi halafu mwishowe wanafunzi wanapata cheti au diploma ya ufundi au ya kutoa huduma fulani.

7. Wanafunzi hupata mikazo gani katika shule za sekondari?

7 Siku hizi, shule za sekondari huhangaikia sana kuwatayarisha wanafunzi kwa ajili ya elimu ya juu. Hivyo, shule nyingi za sekondari hukazia masomo yatakayowawezesha wanafunzi kupita mtihani wa kuingia chuo kikuu badala ya kukazia masomo yatakayowasaidia wanafunzi kupata kazi. Leo, wanafunzi wa shule za sekondari hukazwa sana na walimu, washauri, na wanafunzi wenzao wajitahidi sana ili waitwe katika vyuo vikuu vya hali ya juu, ambako huenda wakapata digrii ambazo zitawawezesha kupata kazi zenye mshahara mnono.

8. Wazazi Wakristo hukabili maamuzi gani?

8 Basi, wazazi Wakristo wanapaswa kufanya nini? Bila shaka, wanataka watoto wao wafanye vema shuleni na kupata ustadi utakaowasaidia kupata riziki katika siku za usoni. (Methali 22:29) Lakini je, wanapaswa kuacha watoto wao waathiriwe na roho ya mashindano ya kutaka kufanikiwa kimwili? Kupitia maneno na mfano wao, wazazi wanawatia moyo watoto wao wawe na miradi gani? Wazazi fulani hufanya kazi kwa bidii sana na kuweka pesa akibani ili baadaye wawapeleke watoto wao kwenye taasisi za elimu ya juu. Wengine huwa tayari kukopa pesa ili wafanye hivyo. Hata hivyo, uamuzi huo hauhusu gharama za pesa tu. Ni gharama zipi zinazohusika katika kufuatia elimu ya juu leo?—Luka 14:28-33.

Gharama za Kufuatia Elimu ya Juu

9. Tunaweza kusema nini kuhusu gharama ya kifedha ya kupata elimu ya juu leo?

9 Mara nyingi tunapofikiri kuhusu gharama, sisi hufikiria pesa. Katika nchi fulani, serikali hulipia elimu ya juu, na wanafunzi wanaostahili hawahitaji kulipia masomo yao. Hata hivyo, katika sehemu nyingi, gharama ya kupata elimu ya juu ni kubwa sana na inazidi kuongezeka. Makala fulani katika gazeti moja (New York Times) inasema: “Zamani, elimu ya juu ilionwa kuwa njia ya kupata kazi. Siku hizi, inaonyesha wazi tofauti iliyopo kati ya matajiri na wasio matajiri sana.” Kwa maneno mengine, siku hizi matajiri na watu mashuhuri ndio wanaoweza kugharimia elimu ya juu, nao wanahakikisha kwamba watoto wao wanapata elimu hiyo ili wao pia wawe matajiri na mashuhuri katika mfumo huu. Je, wazazi Wakristo wanapaswa kuwatia moyo watoto wao wafuatie mradi kama huo?—Wafilipi 3:7, 8; Yakobo 4:4.

10. Elimu ya juu inahusianaje sana na kuendeleza mfumo huu wa mambo?

10 Hata katika maeneo ambako elimu ya juu hutolewa bure, huenda kukawa na masharti mengine yasiyoonekana wazi. Kwa mfano, gazeti fulani (The Wall Street Journal) linasema kwamba katika nchi moja huko Kusini-Mashariki mwa Asia, serikali huwa na ‘mfumo wa elimu unaowainua kimakusudi wanafunzi bora.’ ‘Kuwainua’ kunamaanisha kuwaingiza katika taasisi bora zaidi ulimwenguni kama vile Chuo Kikuu cha Oxford na cha Cambridge huko Uingereza, vyuo vya Ivy League nchini Marekani, na vyuo vingine. Kwa nini serikali ya nchi hiyo huandaa mpango huo? Kulingana na ripoti hiyo, serikali hufanya hivyo “ili kuimarisha uchumi wa taifa.” Huenda elimu hiyo ikatolewa bure, lakini wanafunzi hulipia kwa kutumia maisha yao kuendeleza mfumo huu wa mambo. Ingawa hayo ndiyo maisha ambayo watu katika ulimwengu hutafuta kwa bidii nyingi, je, wazazi Wakristo wangependa watoto wao wawe na maisha kama hayo?—Yohana 15:19; 1 Yohana 2:15-17.

11. Habari zinasema nini kuhusu kutumia kileo kupita kiasi na ukosefu wa adili katika ngono miongoni mwa wanafunzi wa chuo kikuu?

11 Jambo lingine linalohitaji kufikiriwa ni hali za chuoni. Vyuo vikuu na vyuo vya mafunzo hujulikana sana kwa mazoea mabaya kama vile matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kileo, ukosefu wa adili, udanganyifu, kuwatesa wanafunzi wapya wanaojiunga na vikundi fulani chuoni, na mazoea mengine mengi. Acha tuzungumze kuhusu kutumia kileo kupita kiasi. Gazeti moja (New Scientist) linasema hivi kuhusu zoea la kunywa kileo ili kulewa: “Asilimia 44 hivi ya [wanafunzi wa chuo kikuu nchini Marekani] hulewa kupindukia angalau mara moja katika kipindi cha majuma mawili.” Vijana huko Australia, Uingereza, Urusi, na kwingineko hujihusisha katika zoea hilo. Kuhusu ukosefu wa adili katika ngono, wanafunzi wengi leo wanatumia usemi fulani ambao kulingana na gazeti moja (Newsweek), “unafafanua zoea la kujihusisha kingono mara moja, iwe ni kwa kupigana busu au kufanya ngono. Zoea hilo hufanywa na watu wanaojuana tu ambao hata hawakusudii kuzungumza baada ya kufanya tendo hilo.” Uchunguzi unaonyesha kwamba kati ya asilimia 60 hadi 80 ya wanafunzi hushiriki zoea hilo. Mtafiti mmoja alisema hivi: “Ikiwa wewe ni mwanafunzi asiye na kasoro, ni lazima ufanye hivyo.”—1 Wakorintho 5:11; 6:9, 10.

12. Wanafunzi hukabili mikazo gani chuoni?

12 Zaidi ya kuwapo kwa hali mbaya chuoni, kuna mkazo unaotokana na mitihani na kazi za chuoni. Ili wanafunzi wapite mitihani, wanahitaji kusoma na kufanya kazi wanazogawiwa. Huenda wengine wakahitaji kufanya kazi ya muda huku wakiendelea na masomo. Yote hayo yanahitaji wakati mwingi na nguvu nyingi. Ikiwa hali ziko hivyo, je, wanaweza kupata wakati na nguvu za kutosha kutimiza mambo ya kiroho? Mikazo ikiongezeka, watatanguliza nini? Je, watatanguliza mambo ya Ufalme au watayapuuza? (Mathayo 6:33) Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Inasikitisha kama nini kwamba wengine wameanguka kutoka kwenye imani kwa sababu wameruhusu shughuli zimalize wakati na nguvu zao au kwa sababu wamejihusisha na mwenendo usiopatana na Maandiko chuoni!

13. Wazazi Wakristo wanapaswa kufikiria maswali gani?

13 Bila shaka, ukosefu wa adili, tabia mbaya, na mikazo, haipo tu katika vyuo vikuu au vyuo vya mafunzo. Hata hivyo, vijana wengi wa ulimwengu huona mambo hayo yote kuwa sehemu ya elimu yao na wanayaona kuwa sawa kabisa. Je, inafaa wazazi Wakristo wawaache watoto wao kimakusudi wakabiliane na mambo hayo kwa miaka minne, au labda hata kwa miaka mingi zaidi? (Methali 22:3; 2 Timotheo 2:22) Je, faida ambazo huenda vijana wakapata kwa kwenda chuoni zinaweza kulipia hatari zinazohusika? Na zaidi ya yote, vijana hufundishwa nini chuoni kuhusu mambo ambayo wanapaswa kutanguliza maishani mwao? * (Wafilipi 1:10; 1 Wathesalonike 5:21) Wazazi wanapaswa kusali na kufikiri kwa uzito kuhusu maswali hayo na kuhusu hatari ya kuwapeleka watoto wao kusomea katika mji mwingine au nchi nyingine.

Je, Kuna Njia Nyingine za Kupata Elimu?

14, 15. (a) Licha ya maoni ya watu wengi, ni shauri gani la Biblia linalofaa hali za leo? (b) Vijana wanaweza kujiuliza maswali gani?

14 Leo, watu wengi hufikiri kwamba ili vijana wafanikiwe wanahitaji tu kupata elimu ya chuo kikuu. Hata hivyo, badala ya kufuata tu maoni ya watu wengi, Wakristo hutii himizo hili la Biblia: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Mapenzi ya Mungu ni nini kwa ajili ya watu wake, vijana kwa wazee, katika kipindi hiki cha kumalizia cha wakati wa mwisho? Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Tunza akili zako katika mambo yote, vumilia uovu, fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” Bila shaka, maneno hayo yanatuhusu sote leo.—2 Timotheo 4:5.

15 Badala ya kuathiriwa na roho ya ulimwengu huu ya kupenda mali, sote tunahitaji ‘kutunza akili zetu,’ yaani, mtazamo wetu wa kiroho. Ikiwa wewe ni kijana, jiulize: ‘Je, ninajitahidi niwezavyo “kutimiza huduma yangu,” kwa kujitahidi kustahili kuwa mhudumu wa Neno la Mungu? Nimefanya mipango gani ili nitimize huduma yangu “kwa ukamili”? Je, nimefikiria kufanya utumishi wa wakati wote kuwa kazi yangu kuu maishani?’ Hayo ni maswali mazito, hasa unapowaona vijana wenzako wakifuatia miradi ya ubinafsi na “kujitafutia makuu,” huku wakifikiri kwamba yatawasaidia kuwa na maisha mazuri wakati ujao. (Yeremia 45:5) Basi, kwa kutumia hekima, wazazi Wakristo huwaandalia watoto wao tangu utotoni hali nzuri ya kiroho na mazoezi yanayofaa.—Methali 22:6; Mhubiri 12:1; 2 Timotheo 3:14, 15.

16. Wazazi Wakristo wanawezaje kuandaa kwa hekima hali nzuri ya kiroho kwa ajili ya watoto wao?

16 Mvulana wa kwanza katika familia yenye wavulana watatu anaeleza hivi kuhusu mama yake ambaye amekuwa mtumishi wa wakati wote kwa miaka mingi: “Mama alihangaikia sana mashirika yetu. Rafiki zetu hawakuwa wanashule wenzetu, bali wale wenye sifa nzuri za kiroho katika kutaniko. Pia, aliwaalika kwa ukawaida watumishi wa wakati wote kama vile wamishonari, waangalizi wanaosafiri, Wanabetheli, na mapainia ili tushirikiane nao. Kusikia masimulizi yao na kuona shangwe yao kulisitawisha tamaa moyoni mwetu ya kutaka kuwa watumishi wa wakati wote.” Inafurahisha kama nini kwamba wavulana wote hao watatu ni watumishi wa wakati wote! Mmoja anatumikia Betheli, mwingine amehudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na mwingine ni painia!

17. Wazazi wanaweza kuwapa vijana wao mwongozo gani wanapochagua masomo ya shule na kazi ambayo watafanya maishani? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 29.)

17 Zaidi ya kuwaandalia watoto wao hali nzuri ya kiroho, ni lazima pia wazazi waanze mapema kuwapa watoto wao mwongozo unaofaa katika kuchagua masomo ya shule na kazi watakayofanya maishani. Kijana mwingine, ambaye sasa anatumikia Betheli, anasema hivi: “Wazazi wangu walifanya upainia kabla na baada ya kuoana, nao walijitahidi wawezavyo kueneza roho ya upainia katika familia yote. Wakati wowote ambapo tulichagua masomo ya shule au kufanya maamuzi yaliyohusu wakati wetu ujao, walituhimiza tufanye uamuzi ambao utatuwezesha kupata kazi ya muda na kufanya upainia.” Badala ya kuchagua masomo ambayo yanawaelekeza watu kupata elimu ya chuo kikuu, wazazi na watoto wanahitaji kufikiria masomo yanayoweza kuwasaidia watoto wafuatie utumishi wa wakati wote. *

18. Vijana wanaweza kufikiria kufanya kazi gani?

18 Uchunguzi unaonyesha kwamba katika nchi nyingi kuna uhitaji mkubwa wa kupata wafanyakazi wanaojua ufundi fulani au wanaoweza kutoa huduma fulani, bali si uhitaji wa wale waliomaliza chuo kikuu. Gazeti moja (USA Today) linaripoti kwamba “asilimia 70 ya wafanyakazi katika miaka inayokuja hawatahitaji digrii ya chuo kikuu inayopatikana baada ya masomo ya miaka minne, bali watahitaji tu kuwa na digrii ya chuo cha kiserikali au cheti cha ufundi.” Vyuo vingi kama hivyo huandaa masomo ya muda mfupi ya kuwawezesha watu wajue kufanya kazi za ofisi, kurekebisha magari, kurekebisha kompyuta, kurekebisha mabomba ya maji, kutengeneza nywele, na kazi nyingine nyingi za ufundi. Je, kazi hizo zinapendeza? Bila shaka! Huenda zisiwapendeze sana wengine, lakini zinawawezesha wale wanaotaka hasa kumtumikia Yehova maishani mwao kupata riziki na wakati.—2 Wathesalonike 3:8.

19. Ni ipi njia hakika ya kupata shangwe na uradhi maishani?

19 “Enyi vijana, nanyi mabikira pia,” Biblia inawahimiza ‘mlisifu jina la Yehova, kwa maana jina lake peke yake liko juu sana lisiweze kufikiwa. Utukufu wake uko juu ya dunia na mbingu.’ (Zaburi 148:12, 13) Kwa kulinganisha na umashuhuri na mafanikio yanayopatikana katika ulimwengu, hapana shaka kwamba kumtumikia Yehova wakati wote ndiyo njia hakika ya kupata shangwe na uradhi maishani. Kumbukeni uhakikisho huu wa Biblia: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ili upate masimulizi kuhusu watu waliothamini elimu ya kiroho zaidi ya elimu ya chuo kikuu, ona gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1982, ukurasa wa 3-6; Aprili 15, 1979, ukurasa wa 5-10; magazeti ya Amkeni! ya Juni 8, 1978, ukurasa wa 15; na Agosti 8, 1974, ukurasa wa 3-7, au gazeti la Kifaransa la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1982, ukurasa wa 3-6; Agosti 1, 1979, ukurasa wa 5-10; gazeti la Amkeni! la Septemba 22, 1978, ukurasa wa 15; na Machi 22, 1980, ukurasa wa 3-6.

^ fu. 17 Ona gazeti la Amkeni! la Oktoba 8, 1998, “Kutafuta Maisha Yenye Usalama,” ukurasa wa 4-6, na Februari 8, 1990, “Napaswa Kuchagua Kazi Gani ya Maisha?” ukurasa wa 12-14.

Je, Unaweza Kueleza?

• Wakristo huweka wapi matumaini yao ya kuwa na wakati ujao ulio salama?

• Wazazi Wakristo hukabili maamuzi gani magumu yanayohusiana na wakati ujao wa watoto wao?

• Ni nini kinachopaswa kufikiriwa wakati wa kukadiria gharama za kufuatia elimu ya juu?

• Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao wafanye kumtumikia Yehova kuwa kazi yao kuu maishani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Je, Elimu ya Juu Ina Faida?

Watu wengi wanaoingia chuo kikuu hutazamia kupata digrii ambayo itawawezesha kupata kazi ya kudumu na yenye mshahara mnono. Hata hivyo, ripoti za serikali zinaonyesha kwamba karibu asilimia 25 tu ya wale wanaoenda chuo kikuu ndio wanaopata digrii katika kipindi cha miaka sita. Idadi hiyo ni ndogo sana. Hata hivyo, je, digrii hiyo inahakikisha kwamba watapata kazi nzuri? Ona matokeo ya uchunguzi wa karibuni kuhusiana na jambo hilo.

“Kusomea [vyuo vikuu vya] Harvard au Duke hakumaanishi kwamba mtu atapata kazi nzuri na mshahara mnono moja kwa moja. . . . Makampuni hayajui mengi kuhusu vijana wanaotafuta kazi. Ni kweli kwamba digrii nzuri (kama ile ya vyuo vikuu vya Ivy League) inaweza kuvutia. Lakini wakubwa wa kazi hutaka kujua hasa kile ambacho mtu anaweza au hawezi kufanya.”—Newsweek, Novemba 1, 1999.

“Ingawa leo mtu anahitaji ustadi mwingi zaidi kuliko zamani ili apate kazi . . . , kile kinachohitajiwa si ustadi unaopatikana katika chuo cha mafunzo . . . , bali ni ustadi ambao watu hupata katika shule za sekondari, yaani, kujua kufanya hesabu, kusoma, na kuandika vizuri kama mwanafunzi aliye katika mwaka wa tisa shuleni. . . . Wanafunzi hawahitaji kwenda vyuo vya mafunzo ili wapate kazi nzuri, lakini wanahitaji kupata ustadi kupitia shule za sekondari.”—American Educator, Spring 2004.

“Vyuo vingi vya mafunzo haviwatayarishi wanafunzi ifaavyo kwa ajili ya kazi. Sasa wanafunzi wanaongezeka . . . katika shule za ufundi. Shule hizo zilipata ongezeko la wanafunzi la asilimia 48 kuanzia mwaka wa 1996 hadi 2000. . . . Wakati huohuo, diploma ambazo watu hupata baada ya kutumia wakati mwingi sana chuoni zinazidi kuwa bure.”—Time, Januari 24, 2005.

“Makadirio ya Wizara ya Kazi ya Marekani kuhusu mwaka wa 2005 yanaonyesha kwamba angalau theluthi moja ya wanafunzi wanaomaliza masomo ya miaka minne chuoni hawatapata kazi zinazolingana na digrii zao.”—The Futurist, Julai/Agosti 2000.

Kutokana na sababu hizo zote, wasimamizi wa elimu wanazidi kutilia shaka faida ya elimu ya juu leo. Ripoti ya gazeti Futurist inasema hivi: “Elimu tunayowapa watu haipatani na miradi yao.” Tofauti na hilo, ona yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:17, 18.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Waliacha kufuatia mambo yao binafsi, wakamfuata Yesu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kwa kutumia hekima, wazazi Wakristo huwaandalia watoto wao tangu utotoni hali nzuri ya kiroho