Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari Usisitawishe Moyo wa Majivuno

Jihadhari Usisitawishe Moyo wa Majivuno

Jihadhari Usisitawishe Moyo wa Majivuno

“Mungu huwapinga wenye majivuno.”—YAKOBO 4:6.

1. Toa mfano unaoonyesha kwamba si vibaya kujivunia mambo fulani.

JE, UMEWAHI kujivunia jambo lolote? Wengi wetu wamefurahia kuhisi hivyo. Si vibaya kujivunia mambo fulani kwa kiasi. Kwa mfano, wazazi Wakristo huchangamka wanaposoma ripoti ya shule inayoonyesha kwamba binti yao ana mwenendo mzuri na anasoma kwa bidii. Mtume Paulo na wenzake walijivunia kutaniko jipya ambalo walisaidia kulianzisha kwa sababu ndugu wa kutaniko hilo walivumilia mateso kwa uaminifu.—1 Wathesalonike 1:1, 6; 2:19, 20; 2 Wathesalonike 1:1, 4.

2. Kwa nini haifai kuwa na kiburi?

2 Mifano hiyo inatuonyesha kwamba neno kujivunia linaweza kumaanisha kufurahi kwa sababu ya kufanya au kupata jambo fulani. Hata hivyo, neno kiburi linamaanisha kujidai, kujiona kuwa bora kuliko wengine kwa sababu ya vipawa, sura, mali, au cheo. Mara nyingi kiburi huonyeshwa kwa mtazamo wa kujitutumua au kujivuna. Ni lazima sisi Wakristo tujihadhari na kiburi. Kwa nini? Kwa sababu tumezaliwa na mwelekeo wa kuwa na ubinafsi ambao tulirithi kutoka kwa babu yetu Adamu. (Mwanzo 8:21) Hivyo, mioyo yetu inaweza kutupotosha kwa urahisi na kutufanya tujivunie mambo ambayo hatupaswi kujivunia. Kwa mfano, Wakristo wanapaswa kuepuka kujivunia jamii yao, mali zao, elimu yao, vipawa vyao, au mafanikio yao katika kazi huku wakijilinganisha na wengine. Kujivunia mambo hayo hakufai, na Yehova hapendi kuona watu wakifanya hivyo.—Yeremia 9:23; Matendo 10:34, 35; 1 Wakorintho 4:7; Wagalatia 5:26; 6:3, 4.

3. Majivuno ni nini, na Yesu alisema nini kuyahusu?

3 Kuna sababu nyingine inayotufanya tuepuke kiburi. Tukiruhusu kiburi kisitawi moyoni mwetu, kinaweza kuzaa kiburi kingine ambacho kinachukiza hata zaidi, yaani, majivuno. Majivuno ni nini? Zaidi ya kujiona kuwa bora kuliko wengine, mtu mwenye majivuno huwadharau wengine, yaani, watu ambao anawaona kuwa ni wa hali ya chini. (Luka 18:9; Yohana 7:47-49) Yesu aliorodhesha “majivuno” pamoja na mazoea mengine maovu yanayotoka “katika moyo” na ambayo “humtia mtu unajisi.” (Marko 7:20-23) Hivyo, Wakristo wanaweza kuona jinsi ilivyo muhimu kuepuka kusitawisha moyo wa majivuno.

4. Tunaweza kufaidikaje kwa kuchunguza mifano ya watu waliokuwa na majivuno inayotajwa katika Biblia?

4 Unaweza kujua jinsi ya kuepuka majivuno kwa kuchunguza masimulizi fulani ya Biblia kuhusu watu waliokuwa na majivuno. Hilo litakuwezesha kutambua dalili za kiburi ambazo huenda zikawa moyoni mwako au ambazo huenda zikasitawi baadaye. Kufanya hivyo kutakusaidia kukataa mawazo au hisia zinazoweza kutokeza moyo wa majivuno. Hivyo, hutaumia wakati Mungu atakapotenda kulingana na onyo hili lake: “Nitaondoa katikati yako watu wako wanaofurahi kwa majivuno; nawe hutajivuna tena kamwe katika mlima wangu mtakatifu.”—Sefania 3:11.

Mungu Huchukua Hatua Dhidi ya Wenye Majivuno

5, 6. Farao alionyeshaje majivuno, na matokeo yalikuwa nini?

5 Pia, unaweza kuona maoni ya Yehova kuhusu majivuno unapochunguza jinsi alivyoshughulika na watawala wenye nguvu kama Farao. Ni wazi kabisa kwamba Farao alikuwa na moyo wa majivuno. Alijiona kuwa mungu anayepaswa kuabudiwa, naye akawadharau watumwa wake Waisraeli. Kumbuka jinsi alivyoitikia wakati Waisraeli walipoomba ruhusa ya kwenda nyikani ili ‘wamfanyie Yehova sherehe.’ Farao alisema hivi kwa majivuno: “Yehova ni nani, hivi kwamba mimi niitii sauti yake na kuwaruhusu Israeli waende zao?”—Kutoka 5:1, 2.

6 Baada ya Farao kupatwa na mapigo sita, Yehova alimwambia Musa amuulize mtawala huyo wa Misri hivi: “Je, bado unajiendesha kwa majivuno juu ya watu wangu kwa kutowaruhusu waende zao?” (Kutoka 9:17) Kisha, Musa akatangaza pigo la saba, yaani, mvua ya mawe ambayo iliharibu nchi. Waisraeli walipowekwa huru baada ya pigo la kumi, Farao alibadili nia yake na kuwafuata. Hatimaye, Farao na majeshi yake walinaswa katika Bahari Nyekundu. Hebu wazia mambo waliyofikiria maji yalipowazingira pande zote! Matokeo ya majivuno ya Farao yalikuwa nini? Wanajeshi wake bora walisema: “Na tukimbie tusikaribie Israeli hata kidogo, kwa sababu hakika Yehova anawapigania dhidi ya Wamisri.”—Kutoka 14:25.

7. Watawala wa Babiloni walionyeshaje majivuno?

7 Yehova aliwanyenyekeza pia watawala wengine wenye majivuno. Mmoja wao alikuwa Senakeribu, mfalme wa Ashuru. (Isaya 36:1-4, 20; 37:36-38) Hatimaye, Ashuru ilishindwa na Wababiloni, lakini wafalme wawili wa Babiloni wenye majivuno walinyenyekezwa pia. Kumbuka ile karamu ya Mfalme Belshaza ambapo yeye na wageni wake mashuhuri walikunywa divai kwa kutumia vyombo vilivyochukuliwa katika hekalu la Yehova huku wakiisifu miungu ya Babiloni. Kwa ghafula, vidole vya mkono wa mtu vilitokea na kuandika ujumbe fulani ukutani. Alipoombwa aeleze maana ya maandishi hayo yenye fumbo, nabii Danieli alimkumbusha Belshaza hivi: “Mungu Aliye Juu Zaidi alimpa baba yako Nebukadneza ufalme . . . Lakini moyo wake ulipojivuna . . . , alishushwa kutoka katika kiti cha ufalme wake, akaondolewa heshima yake. . . . Na wewe, Belshaza mwana wake, hukunyenyekeza moyo wako, ijapokuwa ulijua hayo yote.” (Danieli 5:3, 18, 20, 22) Usiku huohuo, jeshi la Umedi na Uajemi lilishinda Babiloni, naye Belshaza akauawa.—Danieli 5:30, 31.

8. Yehova alishughulikaje na watu wenye majivuno?

8 Pia, fikiria kuhusu watu wengine wenye majivuno ambao waliwadharau watu wa Yehova: Goliathi lile jitu la Wafilisti, Hamani yule Waziri Mkuu wa Uajemi, na Mfalme Herode Agripa ambaye alitawala mkoa wa Yudea. Kwa sababu ya majivuno yao, watu hao watatu walikufa kifo chenye kuaibisha mkononi mwa Mungu. (1 Samweli 17:42-51; Esta 3:5, 6; 7:10; Matendo 12:1-3, 21-23) Jinsi Yehova alivyoshughulika na watu hao wenye majivuno hukazia jambo hili la kweli: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” (Methali 16:18) Naam, hakuna shaka yoyote kwamba “Mungu huwapinga wenye majivuno.”—Yakobo 4:6.

9. Wafalme wa Tiro walipataje kuwa wasaliti?

9 Tofauti na watawala wa Misri, Ashuru, na Babiloni waliokuwa na majivuno, wakati fulani mfalme wa Tiro aliwasaidia watu wa Mungu. Wakati wa utawala wa Mfalme Daudi na Sulemani, mfalme huyo alitoa mafundi stadi na vifaa kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya kifalme na hekalu la Mungu. (2 Samweli 5:11; 2 Mambo ya Nyakati 2:11-16) Kwa kusikitisha, baadaye Watiro waliwageuka watu wa Yehova. Kwa nini?—Zaburi 83:3-7; Yoeli 3:4-6; Amosi 1:9, 10.

“Moyo Wako Ulikuwa na Majivuno”

10, 11. (a) Ni nani anayeweza kulinganishwa na wafalme wa Tiro? (b) Ni nini kilichowafanya Watiro wabadili mtazamo wao kuwaelekea Waisraeli?

10 Yehova alimwongoza nabii wake Ezekieli kufichua na kushutumu ukoo wa wafalme wa Tiro. Ujumbe huo ulioelekezwa kwa “mfalme wa Tiro” una maneno yanayofafanua vizuri ukoo wa wafalme wa Tiro na vilevile yule msaliti wa kwanza Shetani ambaye “hakusimama imara katika kweli.” (Ezekieli 28:12; Yohana 8:44) Wakati mmoja, Shetani alikuwa kiumbe mshikamanifu wa roho katika tengenezo la Yehova la wana wa kimbingu. Yehova Mungu alimtumia Ezekieli kuonyesha kile kilichosababisha uasi wa wafalme wa Tiro na vilevile uasi wa Shetani:

11 “Ulikuwa katika Edeni, bustani ya Mungu. Kila jiwe la thamani lilikuwa kifuniko chako . . . Wewe ndiye kerubi aliyetiwa mafuta anayefunika . . . Hukuwa na kosa katika njia zako tangu siku ya kuumbwa kwako mpaka ukosefu wa uadilifu ulipoonekana ndani yako. Kwa sababu ya wingi wa mali zako za mauzo walikujaza jeuri katikati yako, nawe ukaanza kutenda dhambi. Nami . . . nitakuharibu wewe, Ee kerubi unayefunika . . . Moyo wako ulikuwa na majivuno kwa sababu ya urembo wako. Uliiharibu hekima yako kwa sababu ya fahari yako inayong’aa.” (Ezekieli 28:13-17) Naam, majivuno yaliwafanya wafalme wa Tiro wawatendee watu wa Yehova kwa jeuri. Jiji la Tiro lilikuwa kituo cha biashara, nalo likapata utajiri mwingi na kujulikana sana kwa bidhaa zake maridadi. (Isaya 23:8, 9) Wafalme wa Tiro walianza kujitutumua sana na kuwaonea watu wa Mungu.

12. Ni nini kilichomfanya Shetani aasi, naye anaendelea kufanya nini?

12 Vivyo hivyo, mwanzoni, yule kiumbe wa roho aliyegeuka kuwa Shetani alikuwa na hekima iliyomwezesha kutimiza kazi yoyote ambayo Mungu alimpa. Badala ya kushukuru, ‘alijivuna kwa kiburi’ na kuanza kudharau njia ya Mungu ya kutawala. (1 Timotheo 3:6) Alijitutumua sana hivi kwamba akaanza kutamani Adamu na Hawa wamwabudu. Tamaa hiyo mbaya ilitunga mimba na kuzaa dhambi. (Yakobo 1:14, 15) Shetani alimshawishi Hawa ale tunda la ule mti mmoja tu ambao Mungu alikuwa amekataza. Kisha, Shetani akamtumia Hawa ili kumshawishi Adamu kula tunda hilo lililokatazwa. (Mwanzo 3:1-6) Basi, wenzi wa kwanza wa kibinadamu walikataa haki ya Mungu ya kuwatawala, wakawa waabudu wa Shetani. Majivuno ya Shetani hayana mipaka. Amejaribu kuwashawishi viumbe wote wenye akili mbinguni na duniani, kutia ndani Yesu Kristo, ili wamwabudu na kukataa enzi kuu ya Yehova.—Mathayo 4:8-10; Ufunuo 12:3, 4, 9.

13. Majivuno yamesababisha nini?

13 Basi, unaweza kuona kwamba majivuno hutokana na Shetani; majivuno ndicho kisababishi kikuu cha dhambi, mateso, na ufisadi uliomo duniani leo. Akiwa “mungu wa mfumo huu wa mambo,” Shetani huendeleza kiburi na majivuno. (2 Wakorintho 4:4) Kwa kuwa anajua kwamba ana wakati mfupi, anapiga vita dhidi ya Wakristo wa kweli. Lengo lake ni kuwaondoa kutoka kwa Mungu, kuwachochea wajipende, wajidai, na kuwa na majivuno. Biblia ilitabiri kwamba tabia hizo zenye ubinafsi zingeonekana sana katika ‘siku hizi za mwisho.’—2 Timotheo 3:1, 2; Ufunuo 12:12, 17.

14. Yehova hutumia kanuni gani anaposhughulika na viumbe wake wenye akili?

14 Yesu Kristo alifichua kwa ujasiri matokeo mabaya yaliyosababishwa na majivuno ya Shetani. Katika angalau pindi tatu akiwa miongoni mwa adui zake waliojiona kuwa waadilifu, Yesu alitaja kanuni hii ambayo Yehova hutumia anaposhughulika na wanadamu: “Kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 14:11; 18:14; Mathayo 23:12.

Linda Moyo Wako Kutokana na Majivuno

15, 16. Ni nini kilichomfanya Hagari awe na majivuno?

15 Huenda umeona kwamba mifano iliyotajwa juu ya watu waliokuwa na majivuno inahusu watu mashuhuri. Je, hiyo inamaanisha kwamba watu wa kawaida hawawezi kuwa wenye majivuno? Sivyo hata kidogo. Fikiria kisa kilichotukia katika nyumba ya Abrahamu. Mzee huyo wa ukoo hakuwa na mwana wa kumrithi, na mke wake Sara alikuwa amepita umri wa kupata watoto. Ilikuwa kawaida kwa mtu aliyekuwa katika hali kama ya Abrahamu kuoa mke wa pili ili apate watoto. Mungu aliruhusu ndoa za aina hiyo kwa sababu wakati haukuwa umefika ili kuanzisha tena kiwango chake cha awali kuhusu ndoa miongoni mwa waabudu wa kweli.—Mathayo 19:3-9.

16 Aliposihiwa na mke wake, Abrahamu alikubali kutokeza uzao wa kumrithi kupitia mjakazi Mmisri wa Sara aliyeitwa Hagari. Hagari akawa mke wa pili wa Abrahamu, naye akapata mimba. Alipaswa kushukuru sana kwa sababu ya cheo chake cha kuheshimika. Badala yake, aliruhusu moyo wake uwe na majivuno. Biblia inasimulia hivi: “Wakati alipojua kwamba ana mimba, ndipo bimkubwa wake akawa mtu wa kudharaulika machoni pake.” Mtazamo huo ulisababisha mgogoro katika familia ya Abrahamu hivi kwamba Sara akamfukuza Hagari. Lakini kulikuwa na suluhisho. Malaika wa Mungu alimshauri Hagari hivi: “Rudi kwa bimkubwa wako ujinyenyekeze chini ya mkono wake.” (Mwanzo 16:4, 9) Inaonekana kwamba Hagari alifuata shauri hilo, akabadili mtazamo wake kumwelekea Sara, naye akawa nyanya ya kundi kubwa la watu.

17, 18. Kwa nini sote tunapaswa kujilinda kutokana na majivuno?

17 Kisa cha Hagari kinaonyesha kwamba hali ya mtu maishani inapoboreka, majivuno yanaweza kutokea. Tunajifunza kwamba hata Mkristo ambaye amemtumikia Mungu akiwa na moyo mzuri anaweza kubadilika akawa mwenye majivuno anapopata mali au mamlaka. Mtazamo huo unaweza kusitawi pia ikiwa wengine wanamsifu kwa mafanikio yake, hekima yake, au kipawa chake. Naam, Mkristo anapaswa kuwa macho asisitawishe moyo wa majivuno. Hilo ni muhimu hasa akipata mafanikio au madaraka zaidi.

18 Maoni ya Mungu kuhusu majivuno ndiyo sababu kubwa zaidi ya kuepuka sifa hiyo mbaya. Neno lake linasema: “Macho yenye majivuno na moyo wa kiburi, taa ya waovu, ni dhambi.” (Methali 21:4) Biblia inawaonya hasa Wakristo “walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu” au wasiwe na majivuno. (1 Timotheo 6:17; Kumbukumbu la Torati 8:11-17) Wakristo ambao si matajiri wanapaswa kuepuka kuwa na “jicho lenye wivu,” nao wanapaswa kukumbuka kwamba mtu yeyote, awe tajiri au maskini, anaweza kusitawisha moyo wa majivuno.—Marko 7:21-23; Yakobo 4:5.

19. Uzia alijiharibiaje sifa?

19 Majivuno na sifa nyingine mbaya zinaweza kuharibu uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Kwa mfano, fikiria kipindi cha kwanza cha utawala wa Mfalme Uzia: ‘Aliendelea kufanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova. Naye akaendelea kuwa na mwelekeo wa kumtafuta Mungu; na katika zile siku alizokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.’ (2 Mambo ya Nyakati 26:4, 5) Lakini kwa kusikitisha, Mfalme Uzia alijiharibia sifa kwa sababu ‘moyo wake ulikuwa na majivuno hata kufikia hatua ya kusababisha uharibifu.’ Alianza kujiona kuwa mtu wa maana sana hivi kwamba aliingia hekaluni na kufukiza uvumba. Makuhani walipomwonya asifanye tendo hilo la kimbelembele, “Uzia akawa na ghadhabu.” Hivyo, Yehova akampiga kwa ukoma, naye Uzia akafa huku akiwa amepoteza kibali cha Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 26:16-21.

20. (a) Ni kwa njia gani Mfalme Hezekia alikuwa karibu kujiharibia sifa? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Unaweza kuona tofauti kwa kulinganisha kisa hicho na mfano wa Mfalme Hezekia. Wakati fulani, mfalme huyo alikuwa karibu kujiharibia sifa kwa sababu “moyo wake ulikuwa wenye majivuno.” Jambo zuri ni kwamba ‘Hezekia alijinyenyekeza kwa sababu ya majivuno ya moyo wake,’ naye akapata tena kibali cha Mungu. (2 Mambo ya Nyakati 32:25, 26) Ona kwamba Hezekia alishinda majivuno kwa kuwa mnyenyekevu. Naam, unyenyekevu ni kinyume cha majivuno. Hivyo, katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi tunavyoweza kusitawisha na kudumisha unyenyekevu wa Kikristo.

21. Wakristo wanyenyekevu wanaweza kutazamia nini?

21 Hata hivyo, tusisahau matokeo yote mabaya ambayo yamesababishwa na majivuno. Kwa kuwa “Mungu huwapinga wenye majivuno,” acheni tuazimie kukataa katakata kiburi. Tunapoendelea kujitahidi kuwa Wakristo wanyenyekevu, tunaweza kutazamia kuokoka siku kuu ya Mungu, wakati ambapo watu wenye majivuno wataondolewa duniani pamoja na matendo yao. Kisha, “majivuno ya mtu wa udongo yatainama, na kiburi cha wanadamu kitashushwa; na Yehova peke yake atainuliwa juu katika siku hiyo.”—Isaya 2:17.

Mambo ya Kutafakari

• Unaweza kumfafanuaje mtu mwenye majivuno?

• Majivuno yalitoka wapi?

• Ni nini kinachoweza kumfanya mtu awe na majivuno?

• Kwa nini ni lazima tujihadhari na majivuno?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Majivuno ya Farao yalifanya anyenyekezwe

[Picha katika ukurasa wa 24]

Hagari alianza kuwa na majivuno wakati hali yake maishani ilipoboreka

[Picha katika ukurasa wa 25]

Hezekia alijinyenyekeza, naye akapata tena kibali cha Mungu