Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Neno la Yehova Laenea Katika “Nchi ya Tai”

Neno la Yehova Laenea Katika “Nchi ya Tai”

Neno la Yehova Laenea Katika “Nchi ya Tai”

“NCHI ya Tai.” Hivyo ndivyo Waalbania wanavyoiita nchi yao katika lugha yao. Nchi hiyo inayoelekeana na Bahari ya Adriatiki iko kwenye Peninsula ya Balkan, katikati ya Ugiriki na Yugoslavia ya zamani. Ingawa kuna dhana nyingi kuhusu asili ya Waalbania, wanahistoria wengi wanakubali kwamba Waalbania na lugha yao walitokana na Wailiria wa kale ambao, kulingana na kitabu The Encyclopædia Britannica, utamaduni wao ulianza mwaka wa 2000 K.W.K.

Vitu vya asili vyenye kuvutia huko Albania vinatia ndani milima iliyochongoka iliyo kaskazini ya mbali, na fuo ndefu zenye mchanga mweupe zilizo kusini kwenye Bahari ya Adriatiki. Hata hivyo, watu ndio wanaovutia zaidi. Ni wenye shauku na wakarimu, wachangamfu na wenye hisia, wenye akili chapuchapu, na wanaoeleza maoni yao kwa ishara nyingi.

Ziara ya Mmishonari Mashuhuri

Karne nyingi zilizopita, msafiri wa pekee alivutiwa na watu hao wenye utu wa kupendeza pamoja na umaridadi wa nchi hiyo. Yapata mwaka wa 56 W.K., mtume Paulo ambaye alisafiri sana aliandika hivi: “Mpaka Ilirikamu nimehubiri kikamili habari njema juu ya Kristo.” (Waroma 15:19) Sehemu iliyokuwa kusini mwa Ilirikamu ndiyo Albania ya kaskazini na ya kati. Paulo aliandika akiwa Korintho, Ugiriki, kusini mwa Ilirikamu. Anaposema kwamba alihubiri kikamili “mpaka Ilirikamu” anaonyesha kwamba alifika hata kwenye mpaka wa Ilirikamu au ndani ya eneo. Kwa vyovyote vile, inawezekana alihubiri eneo linalojulikana sasa kuwa Albania ya kusini. Hivyo, inaweza kusemwa kwamba Paulo ndiye aliyehubiri kwanza ujumbe wa Ufalme huko Albania.

Karne nyingi zilipita. Milki zikatokea na kuanguka. Nchi nyingi zenye mamlaka zilitawala sehemu hiyo ndogo iliyo pembeni mwa Ulaya mpaka wakati Albania ilipopata uhuru mwaka wa 1912. Mapema katika miaka ya 1920, ujumbe kuhusu Ufalme wa Yehova ulihubiriwa tena huko Albania.

Mwanzo Mpya Unaochochea

Katika miaka ya 1920, wahamiaji wachache wa Kialbania walioenda Marekani na ambao walishirikiana na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama walivyoitwa Mashahidi wa Yehova, walirudi Albania kuwaeleza wengine yale waliyojifunza. Nasho Idrizi alikuwa miongoni mwao. Baadhi ya watu waliitikia vizuri. Ili kushughulikia watu wengi waliopendezwa, mwaka wa 1924 tawi la Rumania lilisimamia kazi ya kuhubiri huko Albania.

Thanas Duli (Athan Doulis) alikuwa miongoni mwa wale waliojifunza kumhusu Yehova huko Albania katika miaka hiyo. Alisema hivi: “Mnamo 1925 kulikuwa na makutaniko matatu yaliyosimamiwa vizuri huko Albania. Kulikuwa pia na Wanafunzi wa Biblia walioishi katika maeneo ya mbali na watu waliopendezwa waliokuwa katika sehemu mbalimbali nchini. Kwa kuonyeshana upendo miongoni mwao . . . walikuwa tofauti na majirani wao!” *

Ilikuwa vigumu kusafiri kwa sababu ya ukosefu wa barabara nzuri. Hata hivyo, wahubiri wenye bidii walikubali daraka hilo gumu. Kwa mfano, katika kusini mwa pwani huko Vlorë, Areti Pina alibatizwa mnamo 1928 alipokuwa na umri wa miaka 18. Alipanda na kushuka milima mirefu huku akihubiri akiwa na Biblia mkononi. Alishirikiana na kutaniko lenye bidii huko Vlorë katika miaka ya mapema ya 1930.

Kufikia mwaka wa 1930 kazi ya kuhubiri huko Albania ilisimamiwa na ofisi ya tawi ya Athene, Ugiriki. Mnamo 1932 mwangalizi aliyesafiri kutoka Ugiriki alitembelea Albania ili kuwatia moyo na kuwaimarisha akina ndugu. Wengi kati ya wale waliojifunza kweli ya Biblia wakati huo walikuwa na tumaini la mbinguni. Sifa yao nzuri ya kuwa safi na wanyoofu iliwafanya waheshimiwe sana kila mahali. Kazi ya ndugu hao waaminifu ilikuwa yenye matokeo sana. Wakaaji wa Albania walipokea jumla ya vitabu 6,500 vya Biblia katika mwaka wa 1935 na vilevile katika mwaka wa 1936.

Siku moja, katikati ya mji wa Vlorë, Nasho Idrizi alichezesha santuri ya hotuba za J. F. Rutherford. Watu waliacha biashara zao wakaja kusikiliza, huku Ndugu Idrizi akitafsiri katika Kialbania. Bidii ya walimu hao wa Biblia wa mapema, wasiokata tamaa ilibarikiwa. Kufikia mwaka wa 1940, kulikuwa na Mashahidi 50 nchini Albania.

Nchi Isiyomwamini Mungu

Mnamo 1939, Wafashisti wa Kiitaliano waliteka nchi hiyo. Mashahidi wa Yehova hawakutambuliwa tena kisheria, na kazi yao ya kuhubiri ikapigwa marufuku. Muda mfupi baadaye, majeshi ya Ujerumani yakavamia nchi hiyo. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokaribia kwisha, kulitokea kiongozi wa kijeshi mwenye uvutano aliyeitwa Enver Hoxha. Chama chake cha Kikomunisti kilishinda uchaguzi wa mwaka wa 1946, naye akawa waziri mkuu. Miaka iliyofuata iliitwa wakati wa ukombozi, lakini kwa watu wa Yehova miaka hiyo ilikuwa wakati wa mateso.

Hatua kwa hatua, serikali ikawa isiyovumilia dini. Kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo, Mashahidi wa Yehova huko Albania walikataa kuchukua silaha na kujihusisha katika siasa. (Isaya 2:2-4; Yohana 15:17-19) Wengi walifungwa, bila chakula au mahitaji ya msingi ya maisha. Katika visa vingi, dada zao wa kiroho ambao hawakufungwa waliwafulia nguo na kuwapikia chakula.

Kukabili Mateso Bila Woga

Katika miaka ya mapema ya 1940, Frosina Xheka, aliyekuwa tineja wakati huo katika kijiji kilichokuwa karibu na Përmet, alisikia kwamba ndugu zake wakubwa wa kimwili walikuwa wakijifunza na Shahidi mshona-viatu aliyeitwa Nasho Dori. * Wenye mamlaka walikuwa wakiwakamata Mashahidi wa Yehova, lakini imani ya Frosina iliendelea kuwa yenye nguvu zaidi hata ingawa wazazi wake walichukizwa. “Walikuwa wakificha viatu vyangu na kunipiga ikiwa nilienda kwenye mikutano ya Kikristo. Walijaribu kufanya mipango ili niolewe na mtu asiyeamini. Nilipokataa, walinifukuza nyumbani. Siku hiyo kulikuwa na theluji. Nasho Dori alimwomba Ndugu Gole Flloko huko Gjirokastër anisaidie. Walifanya mipango ili niishi na familia yake. Ndugu zangu walikuwa gerezani kwa miaka miwili kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo. Baada ya wao kufunguliwa, nilihamia Vlorë kuishi pamoja nao.

“Polisi walijaribu kunilazimisha kushiriki katika mambo ya siasa. Nilikataa. Walinifunga, na kunipeleka ndani ya chumba kimoja, nao wakanizunguka. Mmoja wao alinitisha kwa kusema: ‘Je, unajua tunaweza kukufanya nini?’ Nikajibu: ‘Mnaweza tu kufanya kile ambacho Yehova anawaruhusu mfanye.’ Kisha akajibu: ‘Haikosi una wazimu! Ondoka hapa!’”

Kwa miaka mingi, ndugu wa Albania walionyesha roho hiyohiyo ya ushikamanifu. Kufikia mwaka wa 1957, kilele cha wahubiri wa Ufalme kilifikia 75. Katika miaka ya mapema ya 1960, makao makuu ya Mashahidi wa Yehova yalifanya mipango ili John Marks, mhamiaji Mwalbania aliyeishi Marekani, atembelee Tiranë ili kusaidia kupanga kazi ya Kikristo. * Hata hivyo, punde tu, Luçi Xheka, Mihal Sveci, Leonidha Pope, na ndugu wengine wenye madaraka walipelekwa kwenye kambi za kazi za kulazimishwa.

Mwishowe Kukawa na Tumaini

Kabla ya mwaka wa 1967, dini zote hazikukubaliwa nchini Albania. Baadaye, hazikuvumiliwa tena. Hakuna makasisi Wakatoliki, Waothodoksi, au Waislamu walioendesha sherehe za ibada. Makanisa na misikiti ilifungwa au kugeuzwa kuwa majumba ya mazoezi ya mwili, majumba ya ukumbusho, au masoko. Hakuna mtu aliyeruhusiwa kuwa na Biblia wala kusema kwamba anamwamini Mungu.

Ilikuwa vigumu sana kuhubiri au kufanya mikutano. Kila Shahidi alifanya yote awezayo ili kumtumikia Yehova, licha ya kutenganishwa na wengine. Kuanzia miaka ya 1960 hadi miaka ya 1980, idadi ya Mashahidi ilipungua sana. Hata hivyo, walikuwa wenye nguvu kiroho.

Mwishoni mwa miaka ya 1980, hatua kwa hatua kukawa na mabadiliko ya kisiasa nchini Albania. Chakula na nguo vilikosekana. Watu hawakufurahi. Mabadiliko yaliyokuwa yakifanyika Ulaya Mashariki yalifika pia Albania katika miaka ya mapema ya 1990. Baada ya miaka 45 ya utawala wa kimabavu, serikali mpya iliruhusu uhuru wa ibada kwa mara nyingine tena.

Kwa mwongozo wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ofisi za tawi huko Austria na Ugiriki zilianza kuwasiliana haraka na akina ndugu huko Albania. Ndugu wa Ugiriki waliojua Kialbania walipeleka baadhi ya tafsiri za karibuni za vichapo vinavyofafanua Biblia huko Tiranë na Berat. Ndugu wenyeji waliotawanyika hapo awali walishangilia walipokutana kwa mara ya kwanza na Mashahidi kutoka nchi nyingine baada ya miaka mingi.

Mapainia Wenye Bidii Kutoka Nchi Nyingine Waongoza Kazi

Mapema mnamo 1992, Baraza Linaloongoza lilifanya mipango ili Michael na Linda DiGregorio, wenzi wa ndoa wamishonari wenye asili ya Kialbania, wasafiri kwenda Albania. Waliwasiliana na Mashahidi waaminifu wenye umri mkubwa, nao wakawasaidia kuungana tena katika undugu wa ulimwenguni pote. Kikundi chenye bidii cha mapainia wa pekee 16, au waeneza-injili wa wakati wote, kutoka Italia, kilifika mnamo Novemba, pamoja na mapainia wanne kutoka Ugiriki. Mipango ilifanywa ili kuwasaidia wajifunze Kialbania.

Mapainia hao wageni walikabili hali ngumu. Umeme haukupatikana kwa ukawaida. Katika majira ya baridi kali kulikuwa na baridi na unyevu. Watu walipiga foleni kwa saa nyingi ili kupata chakula na mahitaji mengine ya maisha. Hata hivyo, tatizo kubwa zaidi ambalo ndugu hao walikabili lilikuwa jinsi ya kupata nyumba kubwa vya kutosha ili kukaribisha umati mkubwa wa watu waliopendezwa na kweli!

Mapainia waliokuwa wakijitahidi kujifunza Kialbania waligundua kwamba kujua lugha ni njia ya kuwasilisha tu ujumbe. Mwalimu mmoja wa Biblia mwenye uzoefu aliwaambia hivi: “Hatuhitaji kuzungumza kupatana na sarufi ili kutabasamu kwa shauku au kuwakumbatia ndugu zetu. Waalbania wataitikia upendo ambao mnaonyesha kutoka moyoni mwenu wala si kuzungumza kwa usahihi kupatana na sarufi. Msijali, wataelewa.”

Baada ya kipindi cha kwanza cha kujifunza lugha, mapainia walianza kuhubiri huko Berat, Durres, Gjirokastër, Shkodër, Tiranë, na Vlorë. Punde si punde, makutaniko yalianzishwa katika majiji hayo. Areti Pina, aliyekuwa na umri wa zaidi ya miaka 80 na ambaye alikuwa na matatizo ya afya, alikuwa bado huko Vlorë. Mapainia wa pekee wawili walitumwa kuhubiri na Areti. Watu walishangaa kuona wageni wakizungumza Kialbania: “Wamishonari wa dini nyingine wanatuambia kwamba ili tujifunze jambo lolote tunapaswa kujifunza kwanza Kiingereza au Kiitaliano. Kwa kuwa ninyi mmejifunza Kialbania, ni wazi kwamba mnatupenda sana na kwamba mna ujumbe muhimu!” Areti aliyekuwa na tumaini la mbinguni alikufa mnamo Januari 1994, akiwa mwenye bidii katika kazi ya kuhubiri hadi mwezi wa mwisho wa maisha yake. Bidii ambayo yeye na mapainia hao walionyesha ilibarikiwa. Kutaniko lilianzishwa tena huko Vlorë mnamo 1995. Leo, makutaniko matatu yenye kusitawi yanahubiri kwa bidii katika mji huo wenye bandari.

Nchini kote, watu walikuwa na njaa ya kiroho na hawakuwa wenye ubaguzi sana wa kidini. Walikubali na kusoma kwa hamu nyingi vichapo vyovyote vinavyofafanua Biblia walivyopokea kutoka kwa Mashahidi. Vijana wengi walianza kujifunza, nao wakafanya maendeleo ya haraka.

Zaidi ya vikundi na makutaniko 90 yanaendelea “kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku” nchini kote. (Matendo 16:5) Mashahidi 3,513 wa huko Albania bado wana kazi nyingi. Watu 10,144 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo ulioadhimishwa mnamo Machi 2005. Kuzungumza pamoja na watu wakarimu katika kazi ya kuhubiri kumewezesha mafunzo ya Biblia zaidi ya 6,000 yaanzishwe. Bila shaka, maelfu ya watu watafaidika kutokana na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyotolewa hivi majuzi katika Kialbania. Kwa kweli, neno la Yehova linaenea katika “Nchi ya Tai” kwa utukufu wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kuhusu simulizi la maisha la Thanas Duli, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1968 (Kiingereza).

^ fu. 17 Kuhusu simulizi la maisha la Nasho Dori, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1996.

^ fu. 19 Kuhusu simulizi la maisha la Helen, mke wa John Marks, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2002.

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

VITA VYA KIKABILA VYAKOMA HUKO KOSOVO!

Kosovo ilitajwa mara kwa mara mwishoni mwa miaka ya 1990 wakati kulipokuwa na mizozo kuhusu maeneo na chuki ya kikabila iliyosababisha vita ambavyo vilifanya mataifa yaingilie kati.

Wakati wa vita katika nchi za Balkani, Mashahidi wengi walikimbilia nchi mbalimbali jirani. Baada ya vita kupungua, kikundi kidogo cha Mashahidi hao kilirudi Kosovo, kikiwa tayari kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Mapainia wa pekee wa Albania na Italia walijitolea kwenda Kosovo ili kuwasaidia wakaaji 2,350,000 wa eneo hilo. Kuna makutaniko manne na vikundi sita, yakiwa na jumla ya wahubiri 130 hivi ambao wanamtumikia Yehova katika eneo hilo.

Kusanyiko la pekee lilifanywa huko Priština mwaka wa 2003, na watu 252 walihudhuria. Kati ya wahudhuriaji kulikuwa na Waalbania, Wagypsy, Waitaliano, Wajerumani, na watu wenye asili ya Kiserbia. Mwishoni mwa hotuba ya ubatizo, msemaji aliuliza maswali mawili. Watu watatu walisimama ili kujibu: Mwalbania, Mgypsy, na Mserbia.

Watu waliitikia kwa kupiga makofi baada ya kusikia wakati uleule: “Va!,” “Da!,” na “Po!” kutoka kwa wale watu watatu waliokuwa tayari kubatizwa. Walikumbatiana. Walipata suluhisho kwa matatizo mazito ya kikabila yaliyoathiri nchi yao.

[Ramani katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Bahari ya Mediterania

ITALIA

ALBANIA

UGIRIKI

[Picha katika ukurasa wa 18]

Vijana Mashahidi wanaiga bidii ya walio wazee

[Picha katika ukurasa wa 18]

Areti Pina alitumikia kwa uaminifu tangu 1928 hadi kifo chake mnamo 1994

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kikundi cha kwanza cha mapainia wageni wakihudhuria masomo ya kujifunza lugha

[Picha katika ukurasa wa 16]

Eagle: © Brian K. Wheeler/VIREO