Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli

Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli

Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli

“Utawaokoa watu wanyenyekevu.”—2 SAMWELI 22:28.

1, 2. Watawala wengi wa ulimwengu wanafanana katika njia gani?

PIRAMIDI za Misri zinaonyesha watu waliotawala nchi hiyo zamani. Watu wengine wa kale wanaojulikana sana ni Senakeribu wa Ashuru, Aleksanda Mkuu wa Ugiriki, na Kaisari Yulio wa Roma. Watawala wote hao walifanana kwa njia moja. Hawakujulikana kuwa na unyenyekevu wa kweli.—Mathayo 20:25, 26.

2 Je, unaweza kuwazia yeyote kati ya watawala hao waliotajwa hapo juu akiwa na zoea la kutafuta watu wa hali ya chini wanaohitaji faraja katika ufalme wake? Haiwezekani hata kidogo! Pia, huwezi kuwazia kwamba wangeenda katika nyumba ndogo za watu wa hali ya chini ili kuwafariji. Mtazamo wao kuelekea wanadamu wa hali ya chini ni tofauti sana na ule wa Mtawala Mkuu Zaidi wa ulimwengu wote, Yehova Mungu!

Mfano Bora Zaidi wa Unyenyekevu

3. Mtawala Mkuu Zaidi huwatendeaje raia zake wanadamu?

3 Ingawa Yehova ni mkuu sana na mwenye fahari nyingi, “macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Yehova hufanya nini anapowaona waabudu wa hali ya chini ambao wamepondwa roho kwa sababu ya majaribu mbalimbali? Kwa njia fulani, yeye ‘hukaa’ pamoja nao kupitia roho yake takatifu “ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Hivyo, waabudu wake wanaotiwa nguvu kwa njia hiyo huendelea kumtumikia kwa shangwe. Lo! Jinsi Mungu anavyoonyesha unyenyekevu!

4, 5. (a) Mtunga-zaburi alihisije kuhusu njia ya Mungu ya kutawala? (b) Inamaanisha nini kwamba Mungu “anajishusha” kumsaidia “mtu wa hali ya chini”?

4 Hakuna mtu mwingine katika ulimwengu ambaye amejinyenyekeza ili kuwasaidia wanadamu wenye dhambi kama Bwana Mwenye Enzi Kuu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Yehova amekuwa juu ya mataifa yote; utukufu wake uko juu ya mbingu. Ni nani aliye kama Yehova Mungu wetu, yeye anayefanya makao yake juu? Yeye anajishusha kutazama mbingu na dunia, akimwinua mtu wa hali ya chini kutoka kwenye mavumbi; humwinua maskini kutoka kwenye shimo la majivu.”—Zaburi 113:4-7.

5 Kwa kuwa Yehova ni safi na mtakatifu yeye hana “majivuno.” (Marko 7:22, 23) Neno ‘kujishusha’ linaweza kumaanisha kujiweka chini ili kufikia kiwango cha mtu aliye chini katika jamii au kujiondoa katika cheo chako au ukuu wako unaposhughulika na mtu aliye chini yako. Andiko la Zaburi 113:6 linafafanua vizuri sana jinsi Mungu wetu mnyenyekevu anavyohangaikia kwa upendo mahitaji ya wanadamu wasio wakamilifu ambao wanamwabudu!—2 Samweli 22:36.

Kwa Nini Yesu Alikuwa Mnyenyekevu?

6. Yehova alionyeshaje unyenyekevu kwa njia kubwa zaidi?

6 Mungu alionyesha unyenyekevu na upendo kwa njia kubwa zaidi alipomtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza azaliwe duniani na kulelewa akiwa mwanadamu ili awaokoe watu. (Yohana 3:16) Yesu alitufundisha kweli kuhusu Baba yake wa mbinguni, kisha akatoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ili kuondolea mbali “dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29; 18:37) Kwa kuwa Yesu alimwiga Baba yake kwa ukamili, kutia ndani sifa yake ya unyenyekevu, alikuwa tayari kufanya yale ambayo Mungu alitaka afanye. Huo ndio mfano bora zaidi wa unyenyekevu na upendo kuwahi kuonyeshwa na kiumbe yeyote wa Mungu. Sio wote waliothamini unyenyekevu wa Yesu. Adui zake walimwona kuwa “mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” (Danieli 4:17) Hata hivyo, mtume Paulo alitambua kwamba waamini wenzake wanapaswa kumwiga Yesu na kuwa wanyenyekevu wanaposhirikiana.—1 Wakorintho 11:1; Wafilipi 2:3, 4.

7, 8. (a) Yesu alijifunzaje kuwa mnyenyekevu? (b) Yesu anawatolea himizo gani wale wanaotaka kuwa wanafunzi wake?

7 Paulo alikazia mfano bora wa Yesu, alipoandika hivi: “Iweni na mtazamo huu wa akili ndani yenu ambao ulikuwa pia ndani ya Kristo Yesu, ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu. Zaidi ya hayo, alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.”—Wafilipi 2:5-8.

8 Huenda wengine wakajiuliza, ‘Yesu alijifunzaje kuwa mnyenyekevu?’ Alijifunza sifa hiyo kwa kushirikiana kwa ukaribu na Baba yake wa kimbingu kwa miaka mingi sana, na katika kipindi hicho alitumikia akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu katika kuumba vitu vyote. (Methali 8:30) Baada ya uasi huko Edeni, mwana Mzaliwa wa Kwanza wa Mungu aliona jinsi Baba yake alivyoshughulika kwa unyenyekevu na wanadamu watenda-dhambi. Basi, alipokuwa duniani, Yesu alionyesha unyenyekevu wa Baba yake, naye akatoa himizo hili: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:29; Yohana 14:9.

9. (a) Ni jambo gani kuwahusu watoto lililomvutia Yesu? (b) Yesu alimtumia mtoto mchanga kufundisha nini?

9 Kwa kuwa Yesu alionyesha unyenyekevu wa kweli, watoto wadogo hawakumwogopa. Badala yake, walivutiwa naye. Yeye pia aliwapenda watoto na kuwajali. (Marko 10:13-16) Ni jambo gani kuwahusu watoto lililomvutia sana Yesu? Bila shaka, walikuwa na sifa nzuri ambazo baadhi ya wanafunzi wake waliokuwa watu wazima walikosa kuonyesha nyakati nyingine. Kwa kawaida, watoto wadogo huwaona watu wazima kuwa wakubwa kuliko wao. Unaweza kuona jambo hilo katika maswali mengi ambayo watoto huuliza. Naam, tofauti na watu wazima wengi, watoto hukubali kufundishwa na hawana kiburi sana kama watu wazima. Wakati mmoja, Yesu alimwita mtoto mchanga na kuwaambia hivi wafuasi Wake: “Msipogeuka na kuwa kama watoto wachanga, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.” Kisha akaongeza hivi: “Yeyote atakayejinyenyekeza mwenyewe kama mtoto huyu mchanga ndiye aliye mkuu zaidi katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:3, 4) Yesu alitaja kanuni hii: “Kila mtu anayejiinua atanyenyekezwa na yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 14:11; 18:14; Mathayo 23:12.

10. Tutazungumzia maswali gani?

10 Kanuni hiyo inatokeza maswali muhimu. Tazamio letu la kupata uzima wa milele linategemea kwa kadiri fulani kusitawisha unyenyekevu wa kweli. Lakini, kwa nini nyakati nyingine Wakristo huona ni vigumu kuwa wanyenyekevu? Kwa nini ni vigumu kwetu kupambana na kiburi na kukabili majaribu kwa unyenyekevu? Ni nini kitakachotusaidia tufaulu kusitawisha unyenyekevu wa kweli?—Yakobo 4:6, 10.

Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa Wanyenyekevu?

11. Kwa nini haishangazi kwamba tunahitaji kupambana ili tuwe wanyenyekevu?

11 Ikiwa unaona ni vigumu kuwa mnyenyekevu, basi hauko peke yako. Huko nyuma katika mwaka wa 1920, gazeti hili la Mnara wa Mlinzi lilizungumzia shauri la Biblia kuhusu umuhimu wa unyenyekevu kwa kusema: “Baada ya kuona jinsi Bwana anavyokazia sana umuhimu wa unyenyekevu, hilo linapaswa kuwachochea wanafunzi wote wa kweli kusitawisha sifa hiyo kila siku.” Kisha, gazeti hilo likakubali hivi waziwazi: “Licha ya mashauri yote hayo ya Maandiko, hali ya kibinadamu ya kutokamilika inafanya wale wanaokuwa watu wa Bwana na ambao huamua kufuata njia hii wakabili matatizo mengi na vipingamizi vingi wanapojitahidi kusitawisha sifa hii kuliko wanapositawisha sifa nyingine.” Hilo linaonyesha sababu moja inayowafanya Wakristo wa kweli wapambane ili wawe wanyenyekevu, yaani, hali yetu ya kibinadamu ya kutenda dhambi hutufanya tutamani kupata utukufu ambao hatustahili. Hiyo ni kwa sababu sisi ni wazao wa wale wenzi wa ndoa wenye dhambi, Adamu na Hawa, ambao walijiacha washindwe na tamaa za ubinafsi.—Waroma 5:12.

12, 13. (a) Ulimwengu unafanyaje iwe vigumu kusitawisha unyenyekevu wa Kikristo? (b) Ni nani anayefanya pambano letu la kusitawisha unyenyekevu liwe gumu hata zaidi?

12 Sababu nyingine inayoweza kufanya iwe vigumu kwetu kuwa wanyenyekevu ni kwamba tunaishi katika ulimwengu ambao unawahimiza watu wajitahidi kuwa bora kuliko wengine. Miradi ya ulimwengu huu inatia ndani kujitahidi kutosheleza “tamaa ya mwili [wenye dhambi] na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yohana 2:16) Badala ya kuongozwa na tamaa hizo za ulimwengu, wanafunzi wa Yesu wanapaswa kudumisha jicho lao likiwa rahisi na kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.—Mathayo 6:22-24, 31-33; 1 Yohana 2:17.

13 Sababu ya tatu inayofanya iwe vigumu kusitawisha na kuonyesha unyenyekevu ni kwamba mwanzilishi wa majivuno, Shetani Ibilisi, anatawala ulimwengu huu. (2 Wakorintho 4:4; 1 Timotheo 3:6) Shetani huwachochea watu waendeleze sifa zake mbaya. Kwa mfano, aliahidi kumpa Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo” ikiwa tu angemwabudu. Kwa kuwa Yesu alikuwa mnyenyekevu nyakati zote, alikataa katakata ombi hilo la Ibilisi. (Mathayo 4:8, 10) Vivyo hivyo, Shetani huwashawishi Wakristo wajitafutie utukufu. Lakini, Wakristo wanyenyekevu hujitahidi kufuata mfano wa Yesu na kuelekeza sifa na utukufu kwa Mungu.—Marko 10:17, 18.

Kusitawisha na Kuonyesha Unyenyekevu wa Kweli

14. Ni nini maana ya “unyenyekevu wa kujifanya”?

14 Katika barua yake kwa Wakolosai, mtume Paulo alionya kuhusu kujifanya kwa nje kuwa mnyenyekevu ili kuwapendeza wanadamu. Paulo alisema kwamba huo ni “unyenyekevu wa kujifanya.” Wale wanaojifanya kwa nje kwamba wao ni wanyenyekevu si watu wa kiroho. Badala yake, wanaonyesha kwamba kwa kweli ‘wanajivuna’ kwa kiburi. (Wakolosai 2:18, 23) Yesu alitaja mifano ya watu wenye unyenyekevu huo bandia. Aliwashutumu Mafarisayo kwa sababu ya sala zao za kujionyesha na jinsi walivyofunga huku wakiwa na nyuso zenye huzuni na zenye kukunjamana ili waonekane na watu. Tofauti na wao, ili sala zetu za faragha ziwe na thamani mbele za Mungu, tunapaswa kuzitoa kwa unyenyekevu.—Mathayo 6:5, 6, 16.

15. (a) Tunaweza kufanya nini ili kudumisha unyenyekevu wa akili? (b) Kuna mifano gani mizuri ya unyenyekevu?

15 Wakristo wanaweza kudumisha unyenyekevu wa kweli wa akili kwa kukazia fikira mifano bora ya unyenyekevu, yaani, Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kufanya hivyo kunahusisha kujifunza kwa ukawaida Biblia na vichapo vinavyoifafanua ambavyo vimeandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Funzo hilo ni muhimu kwa waangalizi Wakristo, ‘ili mioyo yao isijiinue juu ya ndugu zao.’ (Kumbukumbu la Torati 17:19, 20; 1 Petro 5:1-3) Tafakari mifano mingi ya watu waliobarikiwa kwa sababu ya kuwa wanyenyekevu, kama vile Ruthu, Hana, Elisabeti, na wengine wengi. (Ruthu 1:16, 17; 1 Samweli 1:11, 20; Luka 1:41-43) Pia, fikiria kuhusu mifano mingi mizuri ya wanaume mashuhuri ambao waliendelea kuwa wanyenyekevu katika utumishi wao kwa Yehova, kama vile Daudi, Yosia, Yohana Mbatizaji, na mtume Paulo. (2 Mambo ya Nyakati 34:1, 2, 19, 26-28; Zaburi 131:1; Yohana 1:26, 27; 3:26-30; Matendo 21:20-26; 1 Wakorintho 15:9) Namna gani juu ya mifano ya unyenyekevu tunayoona leo katika kutaniko la Kikristo? Kwa kutafakari kuhusu mifano hiyo, Wakristo wa kweli wataweza kuwa na “unyenyekevu wa akili kuelekeana.”—1 Petro 5:5.

16. Huduma ya Kikristo hutusaidiaje kuwa wanyenyekevu?

16 Kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya Kikristo kunaweza kutusaidia pia kuwa wanyenyekevu. Unyenyekevu wa akili unaweza kutusaidia tuwe na matokeo tunapozungumza na watu tusiowajua tunapoenda kuhubiri nyumba kwa nyumba na katika sehemu nyinginezo. Hilo linaonekana hasa wakati ambapo wenye nyumba hawapendezwi mwanzoni na ujumbe wa Ufalme au wanapotutendea kwa jeuri. Mara nyingi mafundisho yetu hutiliwa shaka, na unyenyekevu unaweza kumsaidia Mkristo aendelee kujibu maswali “kwa tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Petro 3:15) Watumishi wa Mungu walio wanyenyekevu wamehamia maeneo mengine na kuwasaidia watu wenye utamaduni na viwango tofauti vya maisha. Huenda ikawabidi wahudumu hao wakabili kwa unyenyekevu kazi ngumu ya kujifunza lugha nyingine ili wawahubirie watu habari njema na kuwapa msaada unaofaa. Wanastahili pongezi!—Mathayo 28:19, 20.

17. Ni madaraka gani ya Kikristo yanayohitaji unyenyekevu?

17 Kwa sababu ya kuwa wanyenyekevu, wengi wametimiza madaraka yao ya Kikristo huku wakitanguliza faida za wengine. Kwa mfano, baba Mkristo anahitaji kuwa mnyenyekevu ili aache shughuli zake na kutumia wakati kujitayarisha kwa ajili ya funzo la Biblia kisha ajifunze na watoto wake. Unyenyekevu pia huwasaidia watoto kuwaheshimu na kuwatii wazazi wao ambao si wakamilifu. (Waefeso 6:1-4) Mara nyingi wake walio na waume wasioamini hukabili hali ambazo wanahitaji kushughulikia kwa unyenyekevu wanapojaribu kuwavuta waume zao kwenye kweli kupitia ‘mwenendo wao ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.’ (1 Petro 3:1, 2) Unyenyekevu na upendo wa kujidhabihu ni muhimu sana pia wakati tunaposhughulikia kwa upendo mahitaji ya wagonjwa na wazazi wenye umri mkubwa.—1 Timotheo 5:4.

Unyenyekevu Husuluhisha Matatizo

18. Unyenyekevu unawezaje kutusaidia kusuluhisha matatizo?

18 Wanadamu wote ambao wanamtumikia Mungu si wakamilifu. (Yakobo 3:2) Nyakati nyingine, kutoelewana huenda kukatokea kati ya Wakristo wawili. Huenda mmoja akawa na sababu halali ya kulalamika kuhusu mwingine. Kwa kawaida, hali hizo zinaweza kusuluhishwa kwa kutumia shauri hili: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Wakolosai 3:13) Ni kweli kwamba si rahisi kufuata shauri hilo, lakini unyenyekevu utatusaidia tulitumie maishani.

19. Tunapaswa kukumbuka nini tunapozungumza na mtu ambaye ametukosea?

19 Nyakati nyingine, Mkristo anaweza kuhisi kwamba ana sababu nzuri ya kulalamika ambayo haiwezi kupuuzwa tu. Wakati huo, unyenyekevu utamsaidia kumwendea yule aliyemkosea akiwa na nia ya kufanya amani. (Mathayo 18:15) Sababu moja inayofanya hali ya kutoelewana kati ya Wakristo wawili iendelee kwa muda mrefu ni kwamba mmoja wao au huenda wote wawili wana kiburi na hawataki kukubali kwamba walikosea. Au yule anayechukua hatua ya kwanza ya kumwendea yule mwingine anaweza kufanya hivyo huku akijiona kuwa hana kosa lolote au akiwa na nia ya kuchambua. Lakini, unyenyekevu wa kweli utatusaidia kusuluhisha matatizo mengi ya kutoelewana.

20, 21. Ni jambo gani kuu linaloweza kutusaidia kuwa wanyenyekevu?

20 Jambo moja kuu ambalo litatusaidia kusitawisha unyenyekevu ni kuomba msaada wa Mungu na roho yake. Lakini kumbuka kwamba “Mungu . . . huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa [kutia ndani roho yake takatifu].” (Yakobo 4:6) Kwa hiyo, ikiwa umekosana na Mkristo mwenzako, sali kwa Yehova akusaidie kukubali kwa unyenyekevu kosa lako lolote ambalo lilisababisha hali hiyo, liwe ni kosa kubwa au dogo. Ikiwa umeumia kihisia, na yule aliyekukosea anakuambia, “Pole,” msamehe kwa unyenyekevu. Ikiwa unaona ni vigumu kufanya hivyo, sali kwa Yehova akusaidie kuondoa majivuno yoyote yaliyobaki moyoni mwako.

21 Kuelewa faida nyingi za unyenyekevu kunapaswa kutuchochea kusitawisha na kudumisha sifa hiyo yenye thamani. Tunaweza kufanya hivyo tukiiga mfano bora wa Yehova Mungu na Yesu Kristo! Usisahau kamwe uhakikisho huu kutoka kwa Mungu: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

Mambo ya Kutafakari

• Ni nani walio mifano bora zaidi ya unyenyekevu?

• Kwa nini ni vigumu kusitawisha unyenyekevu?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa wanyenyekevu?

• Kwa nini ni muhimu sana kuendelea kuwa wanyenyekevu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yesu alionyesha unyenyekevu wa kweli

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ulimwengu huwachochea watu wajitahidi kuwa bora kuliko wengine

[Hisani]

WHO photo by L. Almasi/K. Hemzǒ

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unyenyekevu hutusaidia kuwahubiria watu tusiowajua

[Picha katika ukurasa wa 30]

Hali za kutoelewana zinaweza kusuluhishwa mara nyingi ikiwa tutaonyesha unyenyekevu na kufunika kosa kwa upendo

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wakristo huonyesha unyenyekevu kwa njia nyingi