Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukristo Waenea Miongoni mwa Wayahudi wa Karne Ya Kwanza

Ukristo Waenea Miongoni mwa Wayahudi wa Karne Ya Kwanza

Ukristo Waenea Miongoni mwa Wayahudi wa Karne Ya Kwanza

MKUTANO muhimu ulifanywa huko Yerusalemu yapata mwaka wa 49 W.K. “Wale walioonekana kuwa nguzo” za kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, yaani, Yohana, Petro, na Yakobo ndugu-nusu ya Yesu, walikuwapo. Watu wengine wawili wanaotajwa kuwa walihudhuria mkutano huo ni mtume Paulo na mwenzake Barnaba. Katika mkutano huo walizungumzia jinsi ya kugawanya eneo kubwa lililokuwapo kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Paulo alieleza hivi: “Walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa kushirikiana pamoja, ili sisi twende kwa mataifa, bali wao waende kwa wale waliotahiriwa.”—Wagalatia 2:1, 9. *

Tunapaswa kuelewaje makubaliano hayo? Je, eneo ambako habari njema ingehubiriwa lingegawanywa mara mbili, Wayahudi na wageuza-imani upande mmoja na wasio Wayahudi upande mwingine? Au je, makubaliano hayo yalihusu kugawanya eneo halisi? Ili kupata jibu, tunahitaji habari za kihistoria kuhusu Wayahudi walioishi nje ya Palestina.

Ulimwengu wa Wayahudi Katika Karne ya Kwanza

Ni Wayahudi wangapi walioishi nje ya Palestina katika karne ya kwanza? Yaelekea wasomi wengi wanakubaliana na kichapo Atlas of the Jewish World kinachosema hivi: “Ni vigumu kujua hesabu kamili, lakini imekadiriwa kwamba muda mfupi kabla ya mwaka wa 70 kulikuwa na Wayahudi milioni mbili na nusu huko Yudea na zaidi ya milioni nne katika sehemu ile nyingine iliyotawaliwa na Roma. . . . Yaelekea kwamba Wayahudi walifanyiza asilimia 10 hivi ya watu walioishi chini ya milki ya Roma, na katika maeneo yenye Wayahudi wengi, katika majiji ya mikoa ya mashariki, huenda walifanyiza asilimia 25 au zaidi ya idadi ya wakaaji.”

Vituo vikuu vya Wayahudi vilikuwa Siria, Asia Ndogo, Babiloni, na Misri, katika Mashariki, na jamii ndogo za Wayahudi zilikuwa huko Ulaya. Baadhi ya Wakristo Wayahudi wa mapema waliojulikana sana waliishi nje ya Israeli, kama vile Barnaba kutoka Kipro, Priska na Akila kutoka Ponto na Roma, Apolo kutoka Aleksandria, na Paulo kutoka Tarso.—Matendo 4:36; 18:2, 24; 22:3.

Wayahudi walioishi nje ya Palestina waliunganishwa na nchi yao kwa njia nyingi. Njia moja ilikuwa kodi ya kila mwaka iliyotumwa kwenye hekalu huko Yerusalemu ambayo iliwawezesha Wayahudi hao kushiriki katika ibada na shughuli za hekalu. Kuhusiana na hilo, msomi John Barclay anasema hivi: “Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba jamii za Wayahudi zilizoishi nje ya Palestina zilikusanya kwa bidii pesa hizo na vilevile michango ya ziada iliyotolewa na matajiri.”

Pia, makumi ya maelfu ya watu walienda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya sherehe mbalimbali. Masimulizi kwenye Matendo 2:9-11 kuhusu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., yanaonyesha hivyo. Wasafiri wa Kiyahudi waliokuwapo walitoka Parthia, Umedi, Elamu, Mesopotamia, Kapadokia, Ponto, Asia, Frigia, Pamfilia, Misri, Libya, Roma, Krete, na Arabia.

Wasimamizi wa hekalu huko Yerusalemu waliwasiliana na Wayahudi walioishi nje ya Palestina kwa kuandikiana nao. Inajulikana kwamba Gamalieli, mwalimu wa sheria anayetajwa kwenye Matendo 5:34, alituma barua Babiloni na sehemu nyingine za ulimwengu. Mtume Paulo alipofika huko Roma akiwa mfungwa yapata mwaka wa 59 W.K., “wakuu wa Wayahudi” walimwambia hivi: “Wala sisi hatujapokea barua zinazokuhusu wewe kutoka Yudea, wala hakuna yeyote wa akina ndugu ambaye amefika aliyetujulisha au kusema jambo lolote baya juu yako.” Hilo linaonyesha kwamba barua na ripoti zilitumwa kwa ukawaida kutoka Israeli hadi Roma.—Matendo 28:17, 21.

Biblia iliyotumiwa na Wayahudi walioishi nje ya Palestina, ilikuwa tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania iliyoitwa Septuajinti. Kichapo kimoja kinasema hivi: “Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba tafsiri ya LXX [Septuajinti] ilisomwa kotekote katika jumuiya ya Wayahudi walioishi nje ya Palestina na kukubaliwa kuwa Biblia ya Kiyahudi au ‘maandiko matakatifu.’” Tafsiri hiyohiyo ilitumiwa sana na Wakristo wa mapema katika mafundisho yao.

Washiriki wa baraza linaloongoza la Kikristo huko Yerusalemu walijua vizuri hali hizo. Habari njema tayari zilikuwa zimewafikia Wayahudi walioishi huko Siria na mbali zaidi, kutia ndani Damasko na Antiokia. (Matendo 9:19, 20; 11:19; 15:23, 41; Wagalatia 1:21) Kwenye mkutano uliofanywa mwaka wa 49 W.K., yaelekea wale walioshiriki katika mkutano huo walipanga kazi kwa ajili ya wakati ujao. Acheni tuchunguze habari za Biblia kuhusu kupanuka kwa kazi miongoni mwa Wayahudi na wale waliogeuzwa imani.

Safari za Paulo na Wayahudi Walioishi Nje ya Palestina

Mgawo wa kwanza wa mtume Paulo ulikuwa “kupeleka jina [la Yesu Kristo] kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” * (Matendo 9:15) Baada ya mkutano huo wa Yerusalemu, Paulo aliendelea kuwatembelea Wayahudi walioishi nje ya Palestina popote pale aliposafiri. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 14.) Yaelekea makubaliano hayo yalihusu maeneo wala si Wayahudi au watu wasio Wayahudi. Paulo na Barnaba walipanua kazi yao ya umishonari hadi upande wa magharibi, na wengine wakatumikia katika eneo la nyumbani la Wayahudi na katika jamii kubwa za Wayahudi zilizokuwa upande wa Mashariki.

Paulo na wenzake walipoanza safari yao ya pili ya umishonari kutoka Antiokia huko Siria, walielekea upande wa magharibi kupitia Asia Ndogo hadi Troa. Kutoka huko walivuka hadi Makedonia kwa sababu walikata kauli kwamba ‘Mungu alikuwa amewaita watangaze habari njema kwa Wamakedonia.’ Baadaye, makutaniko ya Kikristo yalianzishwa katika majiji mengine ya Ulaya, kutia ndani Athene na Korintho.—Matendo 15:40, 41; 16:6-10; 17:1–18:18.

Mwishoni mwa safari yake ya tatu ya umishonari, yapata mwaka wa 56 W.K., Paulo alipanga kusafiri mbali zaidi upande wa magharibi na kuhubiri zaidi katika eneo alilogawiwa kwenye mkutano wa Yerusalemu. Aliandika hivi: “Nina hamu ya kuitangaza habari njema kwenu pia mlio huko Roma,” na, “nitaondoka nikipitia kwenu kwenda Uhispania.” (Waroma 1:15; 15:24, 28) Hata hivyo, ingekuwaje kwa jumuiya kubwa za Wayahudi walioishi nje ya Palestina upande wa Mashariki?

Jumuiya za Wayahudi Zilizokuwa Mashariki

Katika karne ya kwanza W.K., Misri ilikuwa na Wayahudi wengi zaidi, hasa katika mji wake mkuu, Aleksandria. Kituo hicho cha biashara na utamaduni kilikuwa na mamia ya maelfu ya Wayahudi, pamoja na masinagogi yaliyotawanyika katika jiji lote. Philo, Myahudi wa Aleksandria, alidai kwamba katika nchi yote ya Misri kulikuwa na Wayahudi milioni moja hivi wakati huo. Pia, Wayahudi wengi waliishi karibu na Libya, katika jiji la Kirene na maeneo jirani.

Baadhi ya Wayahudi waliokuwa Wakristo walitoka katika maeneo hayo. Tunasoma kuhusu watu fulani waliolitegemeza kutaniko huko Antiokia ya Siria, kama vile “Apolo, mzaliwa wa Aleksandria,” “wanaume fulani wa Kipro na Kirene,” na “Lukio wa Kirene.” (Matendo 2:10; 11:19, 20; 13:1; 18:24) Hata hivyo, Biblia haisemi kuhusu kazi ya Wakristo wa karne ya kwanza katika nchi ya Misri na ujirani wake, isipokuwa jinsi mhubiri Mkristo Filipo alivyomhubiria towashi Mwethiopia.—Matendo 8:26-39.

Eneo la Babiloni, lililotia ndani Parthia, Umedi, na Elamu, lilikuwa kituo kingine kikuu cha Wayahudi. Mwanahistoria mmoja anasema kwamba “kila eneo katika bonde la Tigri na Efrati, toka Armenia hadi ghuba ya Uajemi, na pia toka upande wa kaskazini-mashariki hadi Bahari ya Kaspiani, na toka upande wa mashariki hadi Umedi, lilikuwa na Wayahudi.” Kichapo Encyclopaedia Judaica kinakadiria hesabu yao kuwa 800,000 au zaidi. Yosefo, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza, anatueleza kwamba Wayahudi wengi wa Babiloni walisafiri kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe za kila mwaka.

Miongoni mwa wale waliobatizwa kwenye Pentekoste mwaka wa 33 W.K., je, kulikuwamo watu fulani waliosafiri kutoka Babiloni hadi Yerusalemu? Hatujui. Hata hivyo, kati ya wale waliomsikiliza mtume Petro siku hiyo walikuwamo watu kutoka Mesopotamia. (Matendo 2:9) Tunajua kwamba mtume Petro alikuwa Babiloni yapata mwaka wa 62-64 W.K. Alipokuwa huko, aliandika barua yake ya kwanza na inawezekana pia barua yake ya pili. (1 Petro 5:13) Ni wazi kwamba Babiloni ambalo lilikuwa na idadi kubwa ya Wayahudi lilionwa kuwa sehemu ya eneo ambalo Petro, Yohana, na Yakobo waligawiwa wakati wa mkutano unaozungumziwa katika barua kwa Wagalatia.

Kutaniko la Yerusalemu na Wayahudi Walioishi Nje ya Palestina

Yakobo, ambaye alihudhuria pia mkutano huo ambapo habari kuhusu maeneo ilizungumziwa, alikuwa mwangalizi katika kutaniko la Yerusalemu. (Matendo 12:12, 17; 15:13; Wagalatia 1:18, 19) Kwenye Pentekoste mwaka wa  33 W.K., alijionea jinsi maelfu ya Wayahudi walioishi nje ya Palestina ambao walikuja Yerusalemu walivyoitikia habari njema na kubatizwa.—Matendo 1:14; 2:1, 41.

Tangu hapo na baadaye, Wayahudi wengi walikuja kwa ajili ya sherehe zilizofanywa kila mwaka. Jiji lilijaa watu kupita kiasi, na wageni walilazimika kukaa katika vijiji vilivyokuwa kwenye ujirani au kupiga kambi katika mahema. Zaidi ya kukutana na marafiki wao, kichapo Encyclopaedia Judaica kinaeleza kwamba wasafiri hao waliingia hekaluni ili kuabudu, kutoa dhabihu, na kujifunza Torati.

Bila shaka, Yakobo na washiriki wengine wa kutaniko la Yerusalemu walichukua nafasi hizo kuwahubiria Wayahudi hao walioishi nje ya Palestina. Huenda mitume walifanya hivyo kwa busara nyingi katika kipindi cha ‘mateso makubwa yaliyotokea juu ya kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu’ kwa sababu ya kuuawa kwa Stefano. (Matendo 8:1) Kabla na baada ya tukio hilo, ripoti inaonyesha kwamba bidii ya Wakristo hao katika kazi ya kuhubiri iliendelea kuongezeka.—Matendo 5:42; 8:4; 9:31.

Tunaweza Kujifunza Nini?

Naam, Wakristo wa mapema walijitahidi kwa unyoofu kuwahubiria Wayahudi popote pale walipoishi. Wakati huohuo, Paulo na wengine waliwafikia watu wasio Wayahudi katika maeneo ya Ulaya. Walitii amri ya kufanya wanafunzi kutoka kwa “watu wa mataifa yote” ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake kabla ya kuondoka.—Mathayo 28:19, 20.

Kutokana na kielelezo chao, tunaweza kujifunza umuhimu wa kuhubiri kwa utaratibu ili tupate kutegemezwa na roho ya Yehova. Pia, tunaweza kuona faida za kukutana na wale wanaoliheshimu Neno la Mungu, hasa katika maeneo yaliyo na idadi ndogo sana ya Mashahidi wa Yehova. Je, kuna sehemu fulani za eneo ambalo kutaniko lenu limegawiwa zilizo na matokeo zaidi kuliko zingine? Huenda ikafaa kutembelea sehemu hizo zote kwa ukawaida. Je, unaweza kufanya mipango ili kuhubiri isivyo rasmi na barabarani wakati wa matukio ya pekee katika eneo lenu?

Zaidi ya kufaidika tu kwa kusoma Biblia kuhusu Wakristo wa mapema, tunafaidika pia kwa kujua mambo ya kihistoria na ya kijiografia. Kifaa kimoja ambacho tunaweza kutumia ili kupanua uelewaji wetu ni broshua ‘Ona Nchi Nzuri,’ yenye ramani na picha nyingi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Huenda mkutano huo ulifanywa wakati wa mazungumzo ya baraza linaloongoza la karne ya kwanza kuhusu suala la tohara au ulifanywa kwa kutegemea mazungumzo hayo.—Matendo 15:6-29.

^ fu. 13 Makala hii inazungumzia hasa mahubiri ya Paulo kwa Wayahudi, wala si utendaji wake mbalimbali akiwa “mtume kwa mataifa.”—Waroma 11:13.

[Chati katika ukurasa wa 14]

HANGAIKO LA MTUME PAULO KUELEKEA WAYAHUDI WALIOISHI NJE YA PALESTINA

KABLA YA MKUTANO HUKO YERUSALEMU MWAKA WA 49 W.K.

Matendo 9:19, 20 Damasko — ‘akaanza kuhubiri katika masinagogi’

Matendo 9:29 Yerusalemu — “akiongea . . . na Wayahudi wenye kusema Kigiriki”

Matendo 13:5 Salami, Kipro — “kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi”

Matendo 13:14 Antiokia huko Pisidia — “wakaingia ndani ya sinagogi”

Matendo 14:1 Ikoniamu — “wakaingia . . . katika sinagogi la Wayahudi”

BAADA YA MKUTANO HUKO YERUSALEMU MWAKA WA 49 W.K.

Matendo 16:14 Filipi — “Lidia, . . . mwabudu wa Mungu”

Matendo 17:1 Thesalonike — “sinagogi la Wayahudi”

Matendo 17:10 Beroya — “sinagogi la Wayahudi”

Matendo 17:17 Athene — “kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi”

Matendo 18:4 Korintho — “akitoa hotuba katika sinagogi”

Matendo 18:19 Efeso — “akaingia ndani ya sinagogi akajadiliana na Wayahudi”

Matendo 19:8 Efeso — “akaingia katika sinagogi, akasema kwa ujasiri kwa miezi mitatu”

Matendo 28:17 Roma — “akawaita pamoja . . . wakuu wa Wayahudi”

[Ramani katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wale waliosikia habari njema mnamo Pentekoste 33 W.K. walitoka katika maeneo mengi

ILIRIKAMU

ITALIA

Roma

MAKEDONIA

UGIRIKI

Athene

KRETE

Kirene

LIBYA

BITHINIA

GALATIA

ASIA

FRIGIA

PAMFILIA

KIPRO

MISRI

ETHIOPIA

PONTO

KAPADOKIA

KILIKIA

MESOPOTAMIA

SIRIA

SAMARIA

Yerusalemu

YUDEA

UMEDI

Babiloni

ELAMU

ARABIA

PARTHIA

[Bodies of water]

Bahari ya Mediterania

Bahari Nyeusi

Bahari Nyekundu

Ghuba ya Uajemi