Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utatembea Pamoja na Mungu?

Je, Utatembea Pamoja na Mungu?

Je, Utatembea Pamoja na Mungu?

“[Uwe] na kiasi katika kutembea na Mungu wako.” —Mika 6:8.

1, 2. Hisia za Yehova kutuelekea zinaweza kulinganishwaje na zile za mzazi anayemfundisha mtoto kutembea?

MTOTO anasimama huku miguu yake ikiyumbayumba. Anamwendea mzazi wake ambaye amenyoosha mikono na anapiga hatua zake za kwanza. Huenda tukaona hilo kuwa jambo dogo, lakini kwa mama na baba ya mtoto huyo, hiyo ni hatua kubwa inayowapa matumaini ya wakati ujao. Wazazi wanatazamia kwa hamu sana kutembea na mtoto wao kwa muda mrefu huku wakiwa wamemshika mkono. Wanatumaini kumwongoza na kumtegemeza mtoto huyo kwa njia nyingi sasa na wakati ujao.

2 Yehova Mungu ana hisia kama hizo kuelekea watoto wake duniani. Wakati fulani alisema hivi kuhusu watu wake Israeli, au Efraimu: “Nilimfundisha Efraimu kutembea, nikawachukua mikononi mwangu . . . Nilizidi kuwavuta kwa kamba za mtu wa udongo, kwa kamba za upendo.” (Hosea 11:3, 4) Hapa Yehova anajieleza kuwa mzazi mwenye upendo ambaye kwa subira anamfundisha mtoto wake kutembea, labda hata kumchukua mikononi anapoanguka. Kwa kuwa Yehova ni Mzazi bora, anataka kutufundisha kutembea. Pia yeye hufurahi kuandamana nasi tunapoendelea kufanya maendeleo. Kama andiko letu la msingi linavyoonyesha, tunaweza kutembea pamoja na Mungu! (Mika 6:8) Lakini ni nini maana ya kutembea pamoja na Mungu? Kwa nini tunahitaji kutembea pamoja naye? Inawezekanaje kutembea pamoja naye? Na tunapata baraka gani tunapotembea pamoja na Mungu? Acheni tuzungumzie maswali hayo manne, moja baada ya lingine.

Ni Nini Maana ya Kutembea Pamoja na Mungu?

3, 4. (a) Ni nini kinachovutia kuhusu mfano wa kutembea pamoja na Mungu? (b) Ni nini maana ya kutembea pamoja na Mungu?

3 Bila shaka, mwanadamu mwenye mwili wa nyama na damu hawezi kutembea pamoja na Yehova kihalisi kwa kuwa Yehova ni mtu wa roho. (Kutoka 33:20; Yohana 4:24) Kwa hiyo, Biblia inapotaja wanadamu wanaotembea pamoja na Mungu, inatumia lugha ya mfano. Inatoa mfano mzuri sana ambao unaweza kueleweka katika taifa lolote lile na utamaduni wowote ule na katika kipindi chochote cha wakati. Je, kweli kuna mtu wa kizazi chochote asiyeweza kuelewa wazo la mtu mmoja kutembea pamoja na mwingine? Mfano huo unaonyesha hisia ya upendo na ya ukaribu, sivyo? Hisia hizo hutusaidia kuelewa maana ya kutembea pamoja na Mungu. Hata hivyo, acheni tueleze mambo waziwazi zaidi.

4 Kumbuka wale wanaume waaminifu Enoko na Noa. Kwa nini inasemwa kwamba walitembea pamoja na Mungu? (Mwanzo 5:24; 6:9) Mara nyingi katika Biblia neno “kutembea” humaanisha kufuata mwendo fulani. Enoko na Noa walichagua mwendo wa maisha ambao ulipatana na mapenzi ya Yehova Mungu. Tofauti na watu waliowazunguka, wao walitegemea mwongozo wa Yehova na kutii maagizo yake. Walimtumaini. Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova aliwafanyia maamuzi? Hapana. Yehova amewapa wanadamu uhuru wa kuchagua, na anataka tutumie zawadi hiyo pamoja na ‘nguvu zetu za kufikiri.’ (Waroma 12:1) Hata hivyo, tunapofanya maamuzi, kwa unyenyekevu, sisi hukubali nguvu zetu za kufikiri ziongozwe na hekima ya Yehova ya hali ya juu. (Methali 3:5, 6; Isaya 55:8, 9) Hivyo, tunapotembea maishani, ni kana kwamba tunatembea kwa ukaribu pamoja na Yehova.

5. Kwa nini Yesu alizungumza kuhusu kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wa mtu?

5 Mara nyingi Biblia hufananisha maisha na safari au kutembea. Katika visa fulani, ulinganifu huo huonyeshwa kwa njia ya moja kwa moja, lakini katika visa vingine, huonyeshwa kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Kwa mfano, Yesu alisema: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” (Mathayo 6:27) Huenda ukashangazwa na jambo fulani kuhusu maneno hayo. Kwa nini Yesu alitumia kipimo cha umbali badala ya kipimo cha wakati alipozungumza kuhusu kuongeza “kipimo cha mkono mmoja” kwenye uhai? * Inaonekana Yesu alikuwa akilinganisha uhai na safari. Hivyo, alikuwa akifundisha kwamba kuhangaika hakuwezi kukusaidia kuongeza hata hatua ndogo katika safari yako ya maisha. Lakini, je, hiyo inamaanisha kwamba hakuna kitu tunachoweza kufanya kuhusiana na muda ambao tutatembea? Bila shaka la! Hilo linatuleta kwenye swali letu la pili, Kwa nini tunahitaji kutembea pamoja na Mungu?

Kwa Nini Tunahitaji Kutembea Pamoja na Mungu?

6, 7. Wanadamu wasio wakamilifu wanahitaji nini sana, na kwa nini tunapaswa kumtegemea Yehova atutimizie hilo?

6 Sababu moja ya kutembea pamoja na Yehova Mungu inazungumziwa kwenye Yeremia 10:23: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” Kwa hiyo, sisi wanadamu hatuna uwezo wala haki ya kuelekeza maisha yetu. Tunahitaji sana mwongozo. Wale wanaosisitiza kufuata njia yao wenyewe bila kumtegemea Mungu, wanafanya kosa lilelile ambalo Adamu na Hawa walifanya. Wenzi hao wa ndoa wa kwanza walijitwalia haki ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. (Mwanzo 3:1-6) Kwa hakika, haki hiyo “haimo” ndani yetu.

7 Je, huoni kwamba unahitaji mwongozo katika safari ya maisha? Kila siku tunahitaji kufanya maamuzi makubwa au madogo. Baadhi ya maamuzi hayo ni mazito na yanaweza kuathiri wakati wetu ujao na wa wapendwa wetu pia. Hata hivyo, hebu wazia kwamba mtu fulani mwenye umri mkubwa zaidi na mwenye hekima nyingi zaidi kuliko sisi anafurahia kutuongoza kwa upendo tunapofanya maamuzi hayo! Inasikitisha kwamba watu wengi leo wanapenda kujitegemea na kuongoza hatua zao wenyewe. Wanapuuza ukweli huu kwenye Methali 28:26: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga, lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.” Yehova anataka tuponyoke matatizo yanayotokana na kutegemea moyo wetu wenye hila. (Yeremia 17:9) Anataka tutembee katika hekima, tumtegemee akiwa Kiongozi na Mfundishaji wetu mwenye hekima. Tunapofanya hivyo, tunatembea kwa usalama katika njia inayotupa uradhi maishani.

8. Dhambi na kutokamilika huwapeleka watu wapi, lakini Yehova anataka tufurahie nini?

8 Sababu nyingine inayofanya tuhitaji kutembea pamoja na Mungu inahusiana na muda ambao tunataka kutumia katika kutembea. Biblia inataja ukweli wenye kuhuzunisha. Kwa njia fulani, wanadamu wote wasio wakamilifu wanaelekea mahali palepale. Linapofafanua matatizo ambayo huja uzeeni, andiko la Mhubiri 12:5 linasema hivi: “Mwanadamu anakwenda kwenye nyumba yake ya muda mrefu, nao waombolezaji wamezunguka barabarani.” Hiyo ‘nyumba ya muda mrefu’ ni nini? Ni kaburi, mahali ambapo dhambi na kutokamilika hutupeleka. (Waroma 6:23) Hata hivyo, Yehova anataka tufurahie mengi zaidi kuliko kutembea kwa shida kwa muda mfupi kisha tufe. (Ayubu 14:1) Tukitembea pamoja na Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutatembea milele kama alivyokusudia. Je, sivyo unavyotaka? Basi, unapaswa kutembea pamoja na Baba yako.

Tunaweza Kutembeaje Pamoja na Mungu?

9. Kwa nini nyakati nyingine Yehova alijificha kutoka kwa watu wake, lakini alitoa uhakikisho gani kwenye Isaya 30:20?

9 Tunapaswa kuzingatia kwa makini swali la tatu. Nalo ni, Tunaweza kutembeaje pamoja na Mungu? Tunapata jibu katika andiko la Isaya 30:20, 21: “Mfundishaji wako Mkuu hatajificha tena, na macho yako yatakuwa macho yanayomwona Mfundishaji Mkuu wako. Na masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake,’ iwe mtakwenda upande wa kuume au iwe mtakwenda upande wa kushoto.” Katika masimulizi hayo yenye kutia moyo, huenda maneno ya Yehova katika mstari wa 20 yaliwakumbusha watu wake kwamba walipomwasi ni kana kwamba alijificha kutoka kwao. (Isaya 1:15; 59:2) Hata hivyo, hapa Yehova haonyeshwi akiwa amejificha bali kama ambaye amesimama mbele ya watu wake waaminifu. Huenda tukafikiria jinsi mwalimu husimama mbele ya wanafunzi wake, akiwaonyesha kile anachotaka wafanye.

10. Ni katika njia gani unaweza ‘kusikia neno nyuma yako’ kutoka kwa Mfundishaji wako Mkuu?

10 Mstari wa 21 unaeleza mfano mwingine. Yehova anaelezwa kuwa anatembea nyuma ya watu wake akitoa mwongozo kuhusu njia inayofaa ya kutembea. Wasomi wa Biblia wameeleza kwamba maneno hayo yanahusiana na jinsi mchungaji nyakati nyingine anavyowafuata kondoo wake na kupaaza sauti ili kuwaongoza na kuwazuia wasipitie njia isiyofaa. Mfano huo unatuhusuje? Tunapotafuta mwongozo katika Neno la Mungu, tunasoma maneno yaliyoandikwa maelfu ya miaka iliyopita. Ni kana kwamba maneno hayo yanatoka nyuma yetu kwa sababu yaliandikwa zamani sana. Lakini yangali yanatufaa leo sawa na yalivyokuwa wakati yalipoandikwa. Shauri la Biblia linaweza kutuongoza katika maamuzi yetu ya kila siku na linaweza kutusaidia kupanga maisha yetu ya wakati ujao. (Zaburi 119:105) Tunapojitahidi kutafuta shauri hilo na kulitumia, Yehova anakuwa Kiongozi wetu. Hivyo, tunatembea pamoja na Mungu.

11. Kulingana na Yeremia 6:16, Yehova aliwapa watu wake mfano gani wenye kugusa moyo, lakini wao waliitikiaje?

11 Je, tunaliruhusu Neno la Mungu lituongoze kwa ukaribu hivyo? Ni muhimu kutua kidogo wakati mwingine na kujichunguza kwa unyoofu. Ona mstari utakaotusaidia kufanya hivyo: “Yehova amesema hivi: ‘Simameni tuli katika njia, na kuona, na kuuliza juu ya barabara za zamani za kale, mahali ambapo sasa pana njia nzuri; na mtembee ndani yake, na kustarehesha nafsi zenu.’” (Yeremia 6:16) Maneno hayo yanaweza kutukumbusha kuhusu msafiri anayesimama kwenye makutano ya barabara ili kuulizia njia. Kwa njia ya kiroho, Waisraeli waliomwasi Yehova walipaswa kufanya vivyo hivyo. Walipaswa kurudi katika “barabara za zamani za kale.” Hiyo “njia nzuri” ndiyo njia ambayo babu zao walitembea ndani yake, na ambayo taifa lao lilikuwa limeiacha kwa upumbavu. Inasikitisha kwamba Waisraeli walikaidi kikumbusho hicho chenye upendo kutoka kwa Yehova. Mstari huohuo unaendelea kusema hivi: “Lakini waliendelea kusema: ‘Hatutatembea.’” Hata hivyo, watu wa Mungu leo wameitikia kwa njia tofauti.

12, 13. (a) Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wameitikiaje lile shauri katika Yeremia 6:16? (b) Tunaweza kujichunguzaje kuhusiana na jinsi tunavyotembea leo?

12 Tangu mwishoni mwa karne ya 19, wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wametii shauri la Yeremia 6:16. Wakiwa kikundi, wamewaongoza wengine warudi kwa moyo wote katika “barabara za zamani za kale.” Tofauti na dini zinazodai kuwa za Kikristo, wao wameshikamana kwa uaminifu na “kielelezo cha maneno yenye afya” kilichowekwa na Yesu Kristo na kufuatwa na wafuasi wake waaminifu wa karne ya kwanza W.K. (2 Timotheo 1:13) Mpaka leo, watiwa-mafuta wanasaidiana na kuwasaidia waandamani wao, “kondoo wengine” kufuata njia ya maisha yenye afya na yenye furaha ambayo imeachwa na dini zinazodai kuwa za Kikristo.—Yohana 10:16.

13 Kwa kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa, jamii ya mtumwa mwaminifu imewasaidia mamilioni ya watu kupata “barabara za zamani za kale” na kutembea pamoja na Mungu. (Mathayo 24:45-47) Je, uko miongoni mwao? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili usipeperushwe na kufuata njia yako mwenyewe? Ni jambo la hekima kutua kidogo na kuchunguza jinsi unavyotembea maishani. Ikiwa unasoma kwa ukawaida Biblia na vichapo vinavyoifafanua na kuhudhuria programu za mafundisho zinazopangwa na watiwa-mafuta leo, basi unazoezwa kutembea pamoja na Mungu. Na unapotumia kwa unyenyekevu shauri unalopewa, kwa kweli unatembea pamoja na Mungu na kufuata “barabara za zamani za kale.”

Tembea Kana Kwamba ‘Unamwona Yeye Asiyeonekana’

14. Maamuzi tunayofanya yataonyeshaje kwamba Yehova ni halisi kwetu?

14 Ili tutembee pamoja na Yehova, ni lazima awe halisi kwetu. Kumbuka, Yehova aliwahakikishia Waisraeli waaminifu wa kale kwamba hakuwa amejificha kutoka kwao. Vivyo hivyo leo, anajifunua kwa watu wake kuwa Mfundishaji Mkuu. Je, Yehova yuko halisi hivyo kwako, kana kwamba anasimama mbele yako ili akufundishe? Ikiwa tutatembea pamoja na Mungu, tunahitaji imani kama hiyo. Musa alikuwa na imani kama hiyo, “kwa maana aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Ikiwa Yehova ni halisi kwetu, basi tutafikiria hisia zake tunapofanya maamuzi. Kwa mfano, hatutajiingiza katika mwenendo mpotovu kisha tujaribu kuwaficha wazee Wakristo au watu wa familia yetu dhambi zetu. Badala yake, tunajitahidi kutembea pamoja na Mungu hata wakati wanadamu wenzetu hawatuoni. Tunaazimia hivi kama Mfalme Daudi wa kale: “Nitatembea katika utimilifu wa moyo wangu ndani ya nyumba yangu.”—Zaburi 101:2.

15. Kushirikiana na waamini wenzetu hutusaidiaje kumwona Yehova kuwa halisi?

15 Yehova anaelewa kwamba sisi ni viumbe wasio wakamilifu wenye mwili wa nyama na kwamba wakati mwingine inakuwa vigumu kuamini vitu tusivyoona. (Zaburi 103:14) Yeye hufanya mengi ili kutusaidia kushinda udhaifu huo. Kwa mfano, amewakusanya “watu kwa ajili ya jina lake” kutoka katika mataifa yote ya dunia. (Matendo 15:14) Tunapoendelea kutumikia pamoja, tunatiana nguvu. Mungu wetu huwa halisi kwetu hata zaidi tunaposikia jinsi ambavyo amemsaidia mwamini mwenzetu kushinda udhaifu fulani au kukabiliana na tatizo kubwa.—1 Petro 5:9.

16. Kujifunza juu ya Yesu kutatusaidiaje kutembea pamoja na Mungu?

16 Isitoshe, Yehova ametupa mfano wa Mwana wake. Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Kujifunza juu ya maisha ya Yesu duniani ni mojawapo ya njia bora zaidi za kutusaidia kumwona Yehova kuwa halisi zaidi. Mambo yote ambayo Yesu alisema au kufanya yalionyesha kwa ukamili utu na njia za Baba yake wa mbinguni. (Yohana 14:9) Tunapofanya maamuzi, tunapaswa kufikiria kwa makini jinsi ambavyo Yesu angetenda katika hali hiyo. Tunapofanya maamuzi baada ya kusali na kutafakari kwa njia hiyo, tunafuata hatua za Kristo. (1 Petro 2:21) Hivyo, tunatembea pamoja na Mungu.

Kuna Baraka Gani?

17. Tukitembea katika njia ya Yehova, ‘tutastareheshaje’ nafsi zetu?

17 Tukitembea pamoja na Yehova Mungu tutakuwa na maisha yenye kuridhisha. Kumbuka kile ambacho Yehova aliwaahidi watu wake kuhusu kutafuta “njia nzuri.” Aliwaambia hivi: “Mtembee ndani yake, na kustarehesha nafsi zenu.” (Yeremia 6:16) “Kustarehesha” kunamaanisha nini? Je, kujistarehesha kunamaanisha kuwa na maisha ya raha na anasa? Hapana. Yehova anaandaa kitu bora zaidi, kitu ambacho hata watu ambao ni matajiri zaidi hawapati kwa urahisi. Kustarehesha nafsi yako ni kupata amani ya akili, shangwe, na uradhi wa kiroho. Starehe hiyo inamaanisha kwamba unaweza kuwa na uhakika kwamba umechagua njia bora maishani. Amani hiyo ya akili haipatikani kwa urahisi katika ulimwengu huu wenye shida!

18. Yehova anataka kukupa baraka gani, na umeazimia kufanya nini?

18 Bila shaka, uhai wenyewe ni baraka kubwa. Hata kutembea kwa muda mfupi ni bora kuliko kutotembea kabisa. Hata hivyo, Yehova hakukusudia utembee kwa muda mfupi tu kuanzia unapokuwa na nguvu za ujana hadi unapopata maumivu ya uzee. Yehova anataka upate baraka kubwa zaidi ya baraka zote. Anataka utembee pamoja naye milele! Andiko la Mika 4:5 linaonyesha hivyo linaposema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” Je, unataka kufurahia baraka hiyo? Je, unataka kuishi maisha ambayo Yehova anayataja kuwa “uzima ulio wa kweli”? (1 Timotheo 6:19) Basi, azimia kutembea pamoja na Yehova leo, kesho, na kila siku, mpaka milele!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Tafsiri fulani za Biblia zimebadili “kipimo cha mkono mmoja” katika mstari huo kuwa kipimo cha wakati, kama vile, “muda” (Biblia Habari Njema) au “saa moja” (Neno—Agano Jipya). Hata hivyo, neno la awali lililotumiwa linamaanisha kihalisi kipimo cha mkono mmoja, ambacho kilikuwa na urefu wa sentimeta 45 hivi.

Utajibuje?

• Inamaanisha nini kutembea pamoja na Mungu?

• Kwa nini unahitaji kutembea pamoja na Mungu?

• Ni nini kitakachokusaidia utembee pamoja na Mungu?

• Wale wanaotembea pamoja na Mungu wanapata baraka gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kupitia Biblia, tunasikia sauti ya Yehova nyuma yetu ikisema, “Hii ndiyo njia”

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tunapata chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa mikutanoni