Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Mkristo anaweza kudumisha dhamiri njema akikubali kazi inayohusisha kuwa na silaha?

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote huchukua kwa uzito daraka lao walilopewa na Mungu la kutosheleza mahitaji ya kimwili ya familia zao. (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, kazi fulani zinavunja waziwazi kanuni za Biblia, nazo zinapaswa kuepukwa. Hizo zinatia ndani kazi zinazohusiana na kucheza kamari, kutumia damu, na kuunga mkono matumizi ya bidhaa zinazotokana na tumbaku. (Isaya 65:11; Matendo 15:29; 2 Wakorintho 7:1; Wakolosai 3:5) Ijapokuwa kazi fulani hazishutumiwi moja kwa moja katika Biblia, zinaweza kuchafua dhamiri ya mtu au dhamiri za wengine.

Kufanya kazi inayohusisha kubeba bunduki au silaha nyingine ni uamuzi wa mtu binafsi. Hata hivyo, mtu anapofanya kazi inayohusisha kubeba silaha anaweza kuwa na hatia ya damu anapolazimika kutumia silaha hiyo. Hivyo, Mkristo anahitaji kusali na kufikiria ikiwa yuko tayari kukubali wajibu mzito wa kufanya uamuzi wa papo hapo wakati wa dharura ambapo uhai wa mtu unahusika. Pia, kubeba silaha humfanya mtu akabili hatari ya kujeruhiwa au kuuawa anaposhambuliwa au mtu anapolipiza kisasi.

Huenda wengine pia wakaathiriwa na uamuzi wa mtu mwingine. Kwa mfano, daraka la msingi la Mkristo ni kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Je, kweli mtu anaweza kuwafundisha wengine kuwa “wenye kufanya amani na watu wote” ikiwa anapata riziki kwa kubeba silaha? (Waroma 12:18) Namna gani watoto wake au watu wengine wa familia? Je, huenda akahatarisha uhai wao kwa kuwa na bunduki ndani ya nyumba? Isitoshe, je, wengine watakwazika kwa sababu ya msimamo wake kuhusiana na jambo hilo?—Wafilipi 1:10.

Katika ‘siku hizi za mwisho’ watu wanazidi kuwa “wakali” na “wasiopenda wema.” (2 Timotheo 3:1, 3) Hivyo, je, mtu anaweza kubaki ‘bila shtaka’ akichagua kufanya kazi inayohusisha kubeba silaha, ambayo huenda ikamfanya apambane na watu kama hao? (1 Timotheo 3:10) La hasha. Kwa sababu hiyo, kutaniko haliwezi kumwona mtu kama huyo kuwa “asiyelaumika” ikiwa ataendelea kubeba silaha baada ya kupewa shauri la Biblia kwa fadhili. (1 Timotheo 3:2; Tito 1:5, 6) Hivyo, mwanamume au mwanamke anayefanya hivyo hawezi kustahili kupata mapendeleo yoyote ya pekee katika kutaniko.

Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba wakitanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao, hawahitaji kuhangaika kupita kiasi kuhusu kupata mambo ya lazima maishani. (Mathayo 6:25, 33) Naam, tukimtegemea Yehova kabisa, ‘yeye mwenyewe atatutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.’—Zaburi 55:22.