Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mchungaji Wetu

Yehova Ni Mchungaji Wetu

Yehova Ni Mchungaji Wetu

“Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.”—Zaburi 23:1.

1-3. Kwa nini haishangazi kwamba Daudi alimfananisha Yehova na mchungaji?

KAMA ungeulizwa ueleze jinsi Yehova anavyowashughulikia watu wake, ungesema nini? Ungetumia mfano gani kuonyesha jinsi anavyowajali sana watumishi wake waaminifu? Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Daudi alimfafanua Yehova vizuri sana katika zaburi, akitumia ulinganifu ambao ulihusiana na kazi ambayo Daudi alifanya mapema maishani.

2 Daudi alikuwa mchungaji alipokuwa kijana. Hivyo, alijua kuwashughulikia kondoo. Alijua vizuri kwamba kondoo wakiachwa peke yao, wanaweza kupotea kwa urahisi na kuibwa au kuliwa na wanyama wa mwitu. (1 Samweli 17:34-36) Bila mchungaji anayejali, hawawezi kupata mahali pa malisho. Bila shaka, katika miaka ya baadaye, Daudi alikumbuka sana jinsi alivyotumia saa nyingi kuwaongoza, kuwalinda, na kuwalisha kondoo.

3 Haishangazi kwamba Daudi alikumbuka daraka la mchungaji alipoongozwa kwa roho kueleza jinsi Yehova anavyowashughulikia watu wake. Zaburi ya 23 iliyoandikwa na Daudi, inaanza kwa maneno haya: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” Acheni tuone kwa nini usemi huo unafaa. Kisha, Zaburi ya 23 itatusaidia kuona ni katika njia gani Yehova anawashughulikia waabudu wake kama vile mchungaji anavyowashughulikia kondoo wake.—1 Petro 2:25.

Ulinganifu Unaofaa

4, 5. Biblia hufafanuaje tabia za kondoo?

4 Maandiko hutumia majina mengi ya cheo yanapomtaja Yehova, lakini jina “Mchungaji” linaonyesha zaidi jinsi alivyo mwenye huruma nyingi. (Zaburi 80:1) Ili tuelewe ni kwa nini Yehova anaitwa Mchungaji, ni muhimu tujue mambo mawili: kwanza, tabia za kondoo, na pili, madaraka na sifa za mchungaji mwema.

5 Mara nyingi Biblia hutaja tabia za kondoo, na kuonyesha kwamba wao humtii kwa hiari mchungaji anayewaonyesha upendo (2 Samweli 12:3), si wachokozi (Isaya 53:7), wala hawawezi kujilinda. (Mika 5:8) Mwandishi mmoja aliyefuga kondoo kwa miaka mingi alisema: “Kondoo ‘hawajitunzi wenyewe’ kama vile huenda wengine wakafikiri. Wanahitaji kuhangaikiwa na kutunzwa daima kuliko wanyama wengine wa kufugwa.” Ili wawe salama, viumbe hao wapole wanahitaji mchungaji anayewajali.—Ezekieli 34:5.

6. Kulingana na kamusi moja ya Biblia, mchungaji wa kale alifanya nini siku nzima?

6 Mchungaji wa kale alifanya nini siku nzima? Kamusi moja ya Biblia inaeleza hivi: “Mapema asubuhi aliwatoa kondoo zizini, kisha akawaongoza hadi malishoni huku akitembea mbele yao. Akiwa huko, aliwachunga siku nzima huku akihakikisha kwamba hakuna kondoo yeyote anayetanga-tanga, na iwapo mmoja wao angeponyoka na kuwaacha wengine bila yeye kujua, angemtafuta kwa bidii mpaka ampate na kumrudisha. . . . Usiku, alirudisha kundi zizini, akiwahesabu huku wakipita mlangoni chini ya fimbo ili kuhakikisha kwamba hakuna aliyekosekana. . . . Mara nyingi alilazimika kulinda zizi usiku ili kondoo wasishambuliwe na wanyama wa mwitu au wezi.” *

7. Kwa nini wakati mwingine mchungaji alihitaji kuwa mwenye subira na mwenye huruma zaidi?

7 Wakati mwingine kondoo wenye mimba na wale wachanga walihitaji subira na huruma zaidi. (Mwanzo 33:13) Kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Mara nyingi kondoo huzaliwa mbali sana milimani. Mchungaji humlinda kwa makini mama aliye dhaifu kisha humbeba mwana-kondoo na kumpeleka zizini. Kwa siku kadhaa baada ya kuzaliwa, mpaka atakapoweza kutembea, huenda akambeba mikononi mwake au katika mapindo ya vazi lake la juu.” (Isaya 40:10, 11) Bila shaka, mchungaji mzuri alihitaji kuwa mwenye nguvu na mwenye huruma.

8. Daudi anataja sababu gani zilizomfanya awe na uhakika katika Yehova?

8 “Yehova ni Mchungaji wangu,” kwa kweli hiyo ni njia bora ya kumfafanua Baba yetu wa mbinguni. Tunapoendelea kuchunguza Zaburi ya 23, tutaona jinsi Mungu anavyotujali akiwa mchungaji mwenye nguvu na mwenye huruma. Katika mstari wa kwanza, Daudi anaonyesha uhakika wa kwamba Mungu atafanya mipango inayohitajiwa kwa ajili ya kondoo Wake ili ‘wasikose chochote.’ Katika mistari inayofuata, Daudi anataja sababu tatu za kuwa na uhakika huo: Yehova huwaongoza, huwalinda, na kuwalisha kondoo Wake. Acheni tuzungumzie sababu hizo moja baada ya nyingine.

“Ananiongoza”

9. Daudi anaeleza hali gani ya amani, na kondoo wangekuwaje katika hali hiyo?

9 Kwanza, Yehova anawaongoza watu wake. Daudi anaandika hivi: “Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha. Anaiburudisha nafsi yangu. Ananiongoza katika mapito ya uadilifu kwa ajili ya jina lake.” (Zaburi 23:2, 3) Kundi la kondoo linalala chini kwa amani katikati ya malisho mengi—hapa Daudi anaeleza hali yenye kuridhisha, yenye kuburudisha, na yenye usalama. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “malisho” linaweza kumaanisha “mahali panapopendeza.” Yaelekea, kondoo wakiwa peke yao hawawezi kupata mahali penye kuburudisha ili kulala chini kwa amani. Lazima mchungaji wao awaongoze hadi “mahali [hapo] panapopendeza.”

10. Mungu anaonyeshaje kwamba anatuamini?

10 Yehova hutuongozaje leo? Njia moja ni kwa kielelezo. Neno lake linatuhimiza ‘tuwe waigaji wa Mungu.’ (Waefeso 5:1) Muktadha wa maneno hayo hutaja huruma, msamaha, na upendo. (Waefeso 4:32; 5:2) Bila shaka, Yehova huweka kielelezo bora zaidi katika kuonyesha sifa hizo zenye kuvutia. Je, anadai mengi mno anapotuambia tumwige? Hapana. Shauri hilo lililoongozwa kwa roho linaonyesha kwamba kwa kweli anatuamini. Kwa njia gani? Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, na hiyo inamaanisha kwamba tumepewa sifa za kiadili na uwezo wa kuhangaikia mambo ya kiroho. (Mwanzo 1:26) Hivyo, Yehova anajua kwamba ingawa sisi si wakamilifu, tuna uwezo wa kukuza sifa zilezile ambazo anaonyesha. Hebu wazia, Mungu wetu mwenye upendo ana uhakika kwamba tunaweza kuwa kama yeye. Tukifuata kielelezo chake, atatuongoza, kwa njia ya mfano mpaka “mahali pa kupumzika” panapopendeza. Katika ulimwengu huu wenye jeuri, ‘tutakaa kwa usalama,’ tukiwa na amani inayotokana na kujua kwamba tunakubaliwa na Mungu.—Zaburi 4:8; 29:11.

11. Yehova hufikiria nini anapowaongoza kondoo wake, na hilo linaonyeshwaje na mambo anayotaka tufanye?

11 Yehova hutuongoza kwa huruma na subira. Mchungaji hukumbuka udhaifu wa kondoo wake, hivyo huwaongoza “kulingana na mwendo wa mifugo.” (Mwanzo 33:14) Vivyo hivyo, Yehova huongoza kondoo wake “kulingana na mwendo” wao. Yeye hufikiria uwezo na hali zetu. Hivyo, yeye hubadili mwendo, bila kudai mengi mno kuliko uwezo wetu. Anataka tu tujitoe kwa nafsi yote. (Wakolosai 3:23) Lakini, namna gani ikiwa umezeeka na huwezi kufanya kama ulivyofanya zamani? Au namna gani ikiwa una ugonjwa mbaya unaokuzuia kufanya zaidi? Tunapokabili hali hizo, sisi hufarijiwa sana na takwa la kujitoa kwa nafsi yote. Hakuna nafsi mbili zinazofanana kabisa. Kutumikia kwa nafsi yote kunamaanisha kutumia uwezo wako wote na nguvu zako zote kadiri uwezavyo katika utumishi wa Mungu. Licha ya udhaifu ambao huenda ukaathiri mwendo wetu, Yehova huthamini ibada yetu ya nafsi yote.—Marko 12:29, 30.

12. Ni mfano gani katika Sheria ya Musa unaoonyesha kwamba Yehova huongoza “kulingana na mwendo wa” kondoo wake?

12 Ili kuonyesha kwamba Yehova anaongoza kondoo wake “kulingana na mwendo” wao, fikiria matoleo fulani ya hatia yanayotajwa katika Sheria ya Musa. Yehova alitaka matoleo mazuri yaliyotolewa kutoka moyoni. Wakati huohuo, matakwa ya kutoa matoleo hayo yalipatana na uwezo wa mtoaji. Sheria ilisema hivi: “Ikiwa hana uwezo wa kutoa kondoo, basi atamletea Yehova njiwa-tetere wawili au hua wawili wachanga.” Namna gani ikiwa hakuwa na uwezo wa kutoa hua wawili? Basi angetoa “unga laini.” (Mambo ya Walawi 5:7, 11) Hiyo inaonyesha kwamba Mungu hakudai kitu ambacho mtoaji hangeweza kupata. Kwa kuwa Mungu habadiliki, tunaweza kufarijika kujua kwamba yeye hatutarajii tufanye mengi kuliko uwezo wetu; badala yake, anakubali kile tunachoweza kumpa. (Malaki 3:6) Inafurahisha kama nini kuongozwa na Mchungaji huyo mwenye uelewaji!

“Siogopi Chochote Kibaya, kwa Maana Wewe Uko Pamoja Nami”

13. Daudi anazungumzaje kwa hisia nyingi zaidi kwenye Zaburi 23:4, na kwa nini hilo halishangazi?

13 Daudi anataja sababu ya pili iliyomfanya awe na uhakika: Yehova huwalinda kondoo wake. Tunasoma hivi: “Hata ingawa nitatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.” (Zaburi 23:4) Sasa Daudi anazungumza kwa hisia nyingi zaidi, akiongea na Yehova kwa kutumia neno “wewe.” Hilo halishangazi kwa kuwa Daudi anazungumzia jinsi Mungu alivyomsaidia kuvumilia matatizo. Daudi alikuwa amepitia mabonde mengi yenye giza, yaani, uhai wake ulipokuwa hatarini. Lakini hakuruhusu woga umtawale, kwa kuwa alihisi kwamba Mungu, akiwa tayari na “fimbo” na “gongo” Lake, alikuwa pamoja naye. Bila shaka, Daudi alifarijika kujua kwamba analindwa na hivyo akamkaribia Yehova zaidi. *

14. Biblia inatupa uhakika gani kuhusu jinsi Yehova anavyotulinda, lakini hilo halimaanishi nini?

14 Yehova anawalindaje kondoo wake leo? Biblia inatuhakikishia kwamba hakuna mpinzani, awe ni roho mwovu au mwanadamu, atakayefanikiwa kuwaondoa kondoo wa Yehova duniani. Yehova hataruhusu hilo kamwe. (Isaya 54:17; 2 Petro 2:9) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba Mchungaji wetu atatulinda kutokana na kila msiba. Tunapatwa na majaribu yanayowapata wanadamu kwa ukawaida, na tunakabili upinzani unaowapata Wakristo wote wa kweli. (2 Timotheo 3:12; Yakobo 1:2) Wakati mwingine, huenda kwa njia ya mfano ‘tukatembea katika bonde lenye kivuli kizito.’ Kwa mfano, kwa sababu ya mateso au afya mbaya sana huenda tukakabili kifo. Au mtu tumpendaye anaweza kukaribia kufa au hata kufa. Katika nyakati zinazoonekana kuwa zenye giza sana, Mchungaji wetu huwa pamoja nasi na kutulinda. Kwa njia gani?

15, 16. (a) Yehova hutusaidia kwa njia gani kushughulikia matatizo ambayo huenda tukakabili? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova anavyotusaidia wakati wa majaribu.

15 Yehova haahidi kuingilia kati kimuujiza. * Lakini tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hili: Yehova atatusaidia tushinde tatizo lolote ambalo huenda tukakabili. Anaweza kutupa hekima ya kukabili “majaribu ya namna mbalimbali.” (Yakobo 1:2-5) Mbali na kutumia fimbo au gongo lake kuwafukuza wawindaji, mchungaji huzitumia pia kuwaelekeza kondoo kwa wororo upande unaofaa. Yehova anaweza “kutuelekeza kwa wororo,” labda kupitia mwabudu mwenzetu, ili tutumie shauri la Biblia ambalo linaweza kutusaidia sana. Isitoshe, Yehova anaweza kutupa nguvu za kuvumilia. (Wafilipi 4:13) Kupitia roho yake takatifu, anaweza kutupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Roho ya Mungu inaweza kutusaidia kuvumilia jaribu lolote ambalo huenda Shetani akatuletea. (1 Wakorintho 10:13) Je, haifariji kujua kwamba sikuzote Yehova yuko tayari kutusaidia?

16 Naam, hata tujipate katika bonde lenye giza namna gani, hatuhitaji kutembea humo peke yetu. Mchungaji wetu yuko pamoja nasi, akitusaidia kwa njia ambazo huenda tusielewe mwanzoni. Fikiria simulizi la mzee Mkristo aliyepatikana na uvimbe hatari wa ubongo. Anasema hivi: “Nakubali kwamba mwanzoni nilifikiri kwamba Yehova alikuwa amenikasirikia au hata hanipendi. Lakini niliazimia kutomwacha Yehova. Badala yake, nilimweleza mahangaiko yangu. Yehova alinisaidia, na mara nyingi alinifariji kupitia ndugu na dada zangu wa kiroho. Wengi wao walinieleza habari muhimu juu ya jinsi walivyoshughulikia magonjwa hatari. Maelezo yao yenye usawaziko, yalinikumbusha kwamba yale yaliyonipata yalikuwa ya kawaida tu. Kwa kuwa walinisaidia na wengine wakajitolea kunitendea kwa fadhili, hilo lilinihakikishia kwamba Yehova hanichukii. Bila shaka, nitaendelea kupambana na ugonjwa huu na sijui matokeo yatakuwa nini. Lakini nina uhakika kwamba Yehova yuko pamoja nami, naye ataendelea kunisaidia kukabiliana na jaribu hili.”

“Mbele Yangu Wewe Unatayarisha Meza”

17. Kwenye Zaburi 23:5, Daudi anamfafanuaje Yehova, na kwa nini hiyo haipingani na ule mfano wa mchungaji?

17 Sasa Daudi anataja sababu ya tatu ya kuwa na uhakika katika Mchungaji wake: Yehova huwalisha kondoo wake, naye hufanya hivyo kwa wingi. Daudi anaandika hivi: “Mbele yangu wewe unatayarisha meza mbele ya wale wanaonionyesha uadui. Umepaka kichwa changu mafuta; kikombe changu kimejazwa vizuri.” (Zaburi 23:5) Katika mstari huo, Daudi anamfafanua Mchungaji wake kuwa mkaribishaji mkarimu ambaye huandaa chakula na kinywaji kwa wingi. Mifano hiyo miwili kuhusu mchungaji anayejali na mkaribishaji mkarimu, haipingani. Mchungaji mwema hujua mahali penye malisho mazuri na maji ya kutosha ili kundi lake ‘lisikose chochote.’—Zaburi 23:1, 2.

18. Ni nini huonyesha kwamba Yehova ni mkaribishaji mkarimu?

18 Je, Mchungaji wetu ni mkaribishaji mkarimu pia? Bila shaka! Hebu fikiria jinsi tunavyopata na kufurahia chakula bora cha kiroho kwa wingi na cha aina mbalimbali. Kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yehova ametuandalia vichapo na programu bora kwenye mikutano na makusanyiko ambayo hutosheleza mahitaji yetu ya kiroho. (Mathayo 24:45-47) Bila shaka, hakuna upungufu wa chakula cha kiroho. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameandaa mamilioni ya Biblia na vichapo vya kujifunza Biblia, navyo sasa vinapatikana katika lugha 413. Yehova ametuandalia chakula hiki cha kiroho cha aina mbalimbali kwa wingi, nacho kinatia ndani “maziwa,” ambayo ni mafundisho ya msingi ya Biblia, na hata “chakula kigumu,” ambacho ni mambo ya kiroho yenye kina. (Waebrania 5:11-14) Hivyo, tunapokabili matatizo au maamuzi, tunaweza kupata msaada tunaohitaji. Bila chakula cha kiroho tungekuwa wapi? Mchungaji wetu hutuandalia kwa ukarimu sana!—Isaya 25:6; 65:13.

“Nitakaa Katika Nyumba ya Yehova”

19, 20. (a) Daudi anaelezaje uhakika wake kwenye Zaburi 23:6, nasi tunawezaje kuwa na uhakika kama huo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

19 Baada ya kufikiria matendo ya Mchungaji wake na yule aliyetosheleza mahitaji yake, Daudi anakata kauli hivi: “Kwa hakika wema na fadhili zenye upendo zitanifuata siku zote za maisha yangu; nami nitakaa katika nyumba ya Yehova siku nyingi.” (Zaburi 23:6) Daudi anasema hivyo akichochewa na moyo uliojaa shukrani na imani. Anashukuru anapokumbuka wakati uliopita na kutazamia wakati ujao kwa imani. Daudi aliyekuwa mchungaji yuko salama, akijua kwamba maadamu anaendelea kuwa karibu na Mchungaji wake wa mbinguni, kana kwamba anakaa katika nyumba Yake, Yehova ataendelea kumtunza sikuzote kwa upendo.

20 Tunashukuru sana kwa maneno hayo mazuri ya Zaburi ya 23! Daudi alipata njia bora zaidi ya kufafanua jinsi Yehova huwaongoza, huwalinda, na kuwalisha kondoo wake. Maneno hayo ya Daudi yenye kuvutia yamehifadhiwa ili kutuhakikishia kwamba sisi pia tunaweza kumtegemea Yehova akiwa Mchungaji wetu. Naam, maadamu tunaendelea kuwa karibu na Yehova, atatutunza kwa “siku nyingi” hata milele, akiwa Mchungaji mwenye upendo. Hata hivyo, tukiwa kondoo wake, tuna wajibu wa kutembea pamoja na Mchungaji wetu mkuu, Yehova. Makala inayofuata itazungumzia yale yanayohusika.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Katika zaburi kadhaa ambazo Daudi aliandika, alimsifu Yehova kwa kumkomboa kutoka hatarini.​—Ona kwa mfano, maandishi yanayotangulia Zaburi ya 18, 34, 56, 57, 59, na 63.

^ fu. 15 Ona makala “Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2003.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini inafaa kwamba Daudi alimfananisha Yehova na mchungaji?

• Yehova anatuongozaje kwa uelewaji?

• Yehova hutusaidia kuvumilia majaribu katika njia gani?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova ni mkaribishaji mkarimu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kama mchungaji katika Israeli, Yehova anawaongoza kondoo Wake