Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Njia za Yehova Zimenyooka”

“Njia za Yehova Zimenyooka”

“Njia za Yehova Zimenyooka”

“Njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo.”—HOSEA 14:9.

1, 2. Yehova aliwapa Waisraeli mwanzo gani, lakini walipatwa na nini?

YEHOVA aliwapa Waisraeli mwanzo mzuri kabisa katika siku za nabii Musa. Hata hivyo, kufikia mwanzoni mwa karne ya nane K.W.K., hali yao ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Mungu akaona wana makosa mazito. Tunaona hilo katika Hosea sura ya 10 hadi 14.

2 Moyo wa Waisraeli ulikuwa na unafiki. Watu wa ufalme huo wa makabila kumi walikuwa ‘wamelima uovu’ na kuvuna ukosefu wa uadilifu. (Hosea 10:1, 13) Yehova alisema hivi: “Israeli alipokuwa mvulana, ndipo nikampenda, na kutoka Misri nilimwita mwanangu.” (Hosea 11:1) Ingawa Mungu aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri, walimlipa kwa uwongo na udanganyifu. (Hosea 11:12) Kwa hiyo, Yehova aliwapa shauri hili: “Inakupasa kurudi kwa Mungu wako, ushike fadhili zenye upendo na haki.”—Hosea 12:6.

3. Watu wa Samaria wenye kuasi wangepatwa na nini, lakini Waisraeli wangepataje rehema?

3 Watu wa Samaria wenye kuasi pamoja na mfalme wao wangeangamizwa. (Hosea 13:11, 16) Lakini sura ya mwisho ya unabii wa Hosea inaanza kwa kusihi hivi: “Ee Israeli, rudi kwa Yehova Mungu wako.” Ikiwa Waisraeli wangetubu na kutafuta msamaha, Mungu angewaonyesha rehema. Bila shaka, wangelazimika kukubali kwamba “njia za Yehova zimenyooka” kisha watembee ndani yake.—Hosea 14:1-6, 9.

4. Tutachunguza kanuni gani katika unabii wa Hosea?

4 Sehemu hii ya unabii wa Hosea ina kanuni nyingi zinazoweza kutusaidia tutembee pamoja na Mungu. Tutachunguza kanuni zifuatazo: (1) Yehova anataka ibada isiyo na unafiki, (2) Mungu huwaonyesha watu wake upendo mshikamanifu, (3) tunahitaji kumtumaini Yehova sikuzote, (4) njia za Yehova huwa zimenyooka sikuzote, na (5) watenda-dhambi wanaweza kumrudia Yehova.

Yehova Anataka Ibada Isiyo na Unafiki

5. Mungu anataka tumtolee utumishi wa aina gani?

5 Yehova anataka tumtolee utumishi mtakatifu kwa njia safi, bila unafiki. Hata hivyo, Israeli aligeuka kuwa “mzabibu unaoharibika.” Wakaaji wa Israeli walikuwa ‘wamezidisha madhabahu’ za kutumia katika ibada ya uwongo. Waasi-imani hao hata walikuwa wamesimamisha nguzo, ambazo huenda zilikuwa minara iliyojengwa ili kutumiwa katika ibada chafu. Yehova angevunja madhahabu hizo na kuharibu nguzo hizo.—Hosea 10:1, 2.

6. Ili tutembee pamoja na Mungu, tunapaswa kuepuka sifa gani?

6 Watumishi wa Yehova hawapaswi kuwa wanafiki hata kidogo. Lakini ni nini kilichokuwa kimewapata Waisraeli? ‘Moyo wao ulikuwa na unafiki’! Ingawa awali walikuwa wameingia katika agano pamoja na Yehova wakiwa watu waliojiweka wakfu kwake, aliwapata na hatia ya kuwa wanafiki. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hayo? Ikiwa tumejiweka wakfu kwa Mungu, hatupaswi kuwa wanafiki. Andiko la Methali 3:32 linaonya hivi: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.” Ili tutembee pamoja na Mungu, ni lazima tuonyeshe upendo “kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 Timotheo 1:5.

Mungu Huwaonyesha Watu Wake Upendo Mshikamanifu

7, 8. (a) Tunaweza kupokeaje upendo mshikamanifu wa Mungu? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tumefanya kosa zito?

7 Tukimwabudu Yehova bila unafiki na kwa unyoofu, atatuonyesha fadhili zake zenye upendo, au upendo mshikamanifu. Waisraeli waasi waliambiwa hivi: “Mjipandie mbegu kwa uadilifu; mvune kulingana na fadhili zenye upendo. Mjilimie udongo unaofaa kwa kilimo, kukiwa kungali na wakati wa kumtafuta Yehova mpaka atakapokuja na kuwatolea ninyi mafundisho kwa uadilifu.”—Hosea 10:12.

8 Laiti Waisraeli wangetubu na kumtafuta Yehova! Kama wangefanya hivyo, angefurahi ‘kuwatolea mafundisho kwa uadilifu.’ Ikiwa tumefanya kosa zito, acheni tumtafute Yehova kwa kusali ili kumwomba msamaha na pia kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa wazee Wakristo. (Yakobo 5:13-16) Acheni pia tutafute mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, kwa kuwa “yeye anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake, lakini yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho.” (Wagalatia 6:8) ‘Tukipanda kwa roho,’ tutaendelea kufurahia upendo mshikamanifu wa Mungu.

9, 10. Andiko la Hosea 11:1-4 liliwahusuje Waisraeli?

9 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yehova huwatendea watu wake kwa upendo. Uthibitisho wa jambo hilo unapatikana katika Hosea 11:1-4, ambapo tunasoma hivi: “Israeli alipokuwa mvulana, ndipo nikampenda, na kutoka Misri nilimwita mwanangu. . . . Wakaanza kutoa dhabihu kwa sanamu za Baali, nao wakaanza kufukiza moshi wa dhabihu kwa sanamu za kuchongwa. Lakini mimi, nilimfundisha Efraimu [Waisraeli] kutembea, nikawachukua mikononi mwangu; wala hawakutambua kwamba nilikuwa nimewaponya. Nilizidi kuwavuta kwa kamba za mtu wa udongo, kwa kamba za upendo, hata nikawa kwao kama wale wanaoondoa nira kwenye mfupa wa mataya yao, nami kwa upole nikamletea kila mmoja wao chakula.”

10 Katika andiko hilo, Waisraeli wanalinganishwa na mtoto mchanga. Yehova aliwafundisha Waisraeli kutembea, akawachukua mikononi mwake. Naye alizidi kuwavuta kwa “kamba za upendo.” Mfano huo unavutia kama nini! Wazia kwamba wewe ni mzazi nawe unamsaidia mtoto wako mchanga atembee kwa mara ya kwanza. Unanyoosha mikono yako. Huenda ukatumia kamba ili mtoto wako aishike, asije akaanguka. Naam, hivyo ndivyo Yehova anavyokupenda sana. Anafurahi kukuongoza kwa “kamba za upendo.”

11. Ni kwa njia gani Mungu ‘alikuwa kama mtu anayeondoa nira’?

11 Yehova aliposhughulika na Waisraeli, ‘alikuwa kwao kama wale wanaoondoa nira kwenye mfupa wa mataya yao, naye kwa upole akamletea kila mmoja wao chakula.’ Mungu alikuwa kama mtu anayeondoa nira au kuirudisha nyuma mbali vya kutosha ili kumwezesha mnyama ale kwa starehe. Waisraeli walipovunja nira ya ujitiisho kwa Yehova ndipo walipotiwa chini ya nira yenye kukandamiza ya adui zao. (Kumbukumbu la Torati 28:45, 48; Yeremia 28:14) Na tusianguke kamwe mikononi mwa adui wetu mkuu, Shetani, ili nira yake yenye kukandamiza isije ikatuumiza. Badala yake, acheni tuendelee kutembea kwa ushikamanifu pamoja na Mungu wetu mwenye upendo.

Mtumaini Yehova Sikuzote

12. Kulingana na Hosea 12:6, ni nini kinachohitajiwa ili tuendelee kutembea pamoja na Mungu?

12 Ili tuendelee kutembea pamoja na Mungu, ni lazima tumtumaini sikuzote. Waisraeli waliambiwa hivi: “Na wewe inakupasa kurudi kwa Mungu wako, ushike fadhili zenye upendo na haki; nawe umtumaini Mungu wako sikuzote.” (Hosea 12:6) Wakaaji wa Israeli wangeweza kuthibitisha kwamba wametubu na wamemrudia Yehova ikiwa wangeonyesha fadhili zenye upendo, kutenda haki, na ‘kumtumaini Mungu sikuzote.’ Hata tuwe tumetembea pamoja na Mungu kwa muda gani, tunapaswa kuazimia kuonyesha fadhili zenye upendo, kutenda haki, na kumtumaini Mungu sikuzote.—Zaburi 27:14.

13, 14. Paulo anatumiaje Hosea 13:14, na hilo linatupa sababu gani ya kumtumaini Yehova?

13 Unabii wa Hosea kuwahusu Waisraeli unatupa sababu ya pekee ya kumtumaini Mungu. Yehova alisema hivi: “Nitawakomboa wao kutoka katika mkono wa Kaburi; nitawaokoa wao kutoka kwenye kifo. Ee Kifo, iko wapi michomo yako? Ee Kaburi, yako wapi maangamizi yako?” (Hosea 13:14) Yehova hakukusudia kuwaokoa Waisraeli kutoka katika kifo wakati huo, lakini mwishowe angemeza kifo milele na kubatilisha ushindi wa kifo.

14 Paulo alipowaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta, alinukuu unabii wa Hosea. Aliandika hivi: “Huu ulio wenye kuharibika utakapovaa kutoweza kuharibika na huu unaoweza kufa utakapovaa kutoweza kufa, ndipo litakapotimia hili neno lililoandikwa: ‘Kifo kimemezwa milele.’ ‘Kifo, uko wapi ushindi wako? Kifo, uko wapi mchomo wako?’ Mchomo unaotokeza kifo ni dhambi, lakini nguvu za dhambi ni Sheria. Lakini shukrani kwake Mungu, kwa maana yeye hutupa sisi ushindi kupitia Bwana wetu Yesu Kristo!” (1 Wakorintho 15:54-57) Yehova alimfufua Yesu kutoka kwa wafu, na hivyo akatoa uhakikisho wenye kufariji kwamba watu walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa. (Yohana 5:28, 29) Hiyo ni sababu bora kama nini ya kumtumaini Yehova! Lakini, mbali na tumaini la ufufuo, kuna jambo lingine linalotuchochea kutembea pamoja na Mungu.

Njia za Yehova Huwa Zimenyooka Sikuzote

15, 16. Ni nini kilichotabiriwa kuhusu Samaria, na unabii huo ulitimiaje?

15 Kuamini kwamba “njia za Yehova zimenyooka” hutusaidia tuendelee kutembea pamoja na Mungu. Wakaaji wa Samaria hawakutembea katika njia za Mungu za uadilifu. Kwa hiyo, lazima wangetozwa hesabu kwa sababu ya dhambi zao na ukosefu wao wa imani katika Yehova. Ilitabiriwa hivi: “Samaria atahesabiwa kuwa na hatia, kwa maana kwa kweli yeye amemwasi Mungu wake. Wataanguka kwa upanga. Watoto wao wenyewe watavunjwa vipande-vipande, na wanawake wao wenye mimba watapasuliwa.” (Hosea 13:16) Maandishi ya kale yanaonyesha kwamba Waashuru, ambao waliteka Samaria, walitenda ukatili huo mkubwa.

16 Samaria lilikuwa jiji kuu la ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Hata hivyo, katika andiko hilo huenda jina Samaria linatumiwa kumaanisha eneo lote la ufalme huo. (1 Wafalme 21:1) Mfalme wa Ashuru Shalmanesa wa Tano alizingira jiji la Samaria katika mwaka wa 742 K.W.K. Samaria lilipoanguka hatimaye katika mwaka wa 740 K.W.K., wakaaji wake wengi walio mashuhuri walipelekwa uhamishoni huko Mesopotamia na Umedi. Haijulikani kama Shalmanesa wa Tano ndiye aliyeteka Samaria au ni Sargoni wa Pili, aliyetawala baada yake. (2 Wafalme 17:1-6, 22, 23; 18:9-12) Hata hivyo, maandishi ya Sargoni yanataja kuhamishwa kwa Waisraeli 27,290, waliopelekwa katika maeneo ya Efrati ya Juu na Umedi.

17. Badala ya kudharau viwango vya Mungu, tunapaswa kufanya nini?

17 Wakaaji wa Samaria walipatwa na hali mbaya sana kwa kukosa kufuata njia za Yehova zilizonyooka. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, sisi pia tutapatwa na hali mbaya sana ikiwa tutazoea kutenda dhambi na kudharau viwango vya uadilifu vya Mungu. Tusifuate kamwe mwendo huo mwovu! Badala yake, acheni kila mmoja wetu atende kupatana na shauri hili la mtume Petro: “Yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mtenda-maovu au mwenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine. Lakini akiteseka kwa sababu yeye ni Mkristo, asione aibu, bali na aendelee kumtukuza Mungu katika jina hili.”—1 Petro 4:15, 16.

18. Tunaweza ‘kuendeleaje kumtukuza Mungu’?

18 Sisi ‘huendelea kumtukuza Mungu’ kwa kutembea katika njia zake zilizonyooka badala ya kufuata njia zetu wenyewe. Kaini aliua kwa sababu alifuata njia yake mwenyewe naye hakutii onyo la Yehova kuhusu dhambi iliyokuwa ikimvizia. (Mwanzo 4:1-8) Balaamu alikubali malipo kutoka kwa mfalme wa Moabu, akajaribu kulaani Israeli, lakini hakufaulu. (Hesabu 24:10) Na Mungu alimuua Kora Mlawi pamoja na wengine kwa sababu waliasi mamlaka ya Musa na Haruni. (Hesabu 16:1-3, 31-33) Bila shaka, sisi hatutaki kwenda katika ‘pito la uuaji la Kaini,’ kukimbia kuingia katika “mwendo wenye kosa wa Balaamu,” wala kuangamia katika “maneno ya uasi ya Kora.” (Yuda 11) Hata hivyo, tukifanya kosa zito, unabii wa Hosea unatufariji.

Watenda-Dhambi Wanaweza Kumrudia Yehova

19, 20. Waisraeli waliotubu wangeweza kutoa dhabihu gani?

19 Hata wale ambao wamejikwaa kwa kutenda dhambi nzito wanaweza kumrudia Yehova. Andiko la Hosea 14:1, 2, linatuhimiza hivi: “Ee Israeli, rudi kwa Yehova Mungu wako, kwa maana umejikwaa katika kosa lako. Chukueni maneno pamoja nanyi mrudi kwa Yehova. Mwambieni hivi, enyi nyote, ‘Samehe kosa letu; na ukubali lililo jema, nasi tutatoa ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu.’”

20 Waisraeli waliotubu wangeweza kumtolea Mungu ‘ng’ombe-dume wachanga wa midomo yao.’ Hizo zilikuwa dhabihu za sifa za unyoofu. Paulo alitaja unabii huo alipowasihi Wakristo ‘wamtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.’ (Waebrania 13:15) Ni pendeleo kubwa kama nini kutembea pamoja na Mungu na kutoa dhabihu za aina hiyo leo!

21, 22. Ni kwa njia gani Waisraeli waliotubu wangerudishwa?

21 Waisraeli walioacha mwendo wao mpotovu na kumrudia Mungu walimtolea ‘ng’ombe-dume wachanga wa midomo yao.’ Hivyo, walirudishwa katika hali nzuri ya kiroho, kama Mungu alivyoahidi. Andiko la Hosea 14:4-7 linasema hivi: “[Mimi Yehova] nitaponya ukosefu wao wa uaminifu. Nitawapenda kwa kupenda kwangu mwenyewe, kwa maana hasira yangu imegeuka kutoka kwake. Nitakuwa kama umande kwa Israeli. Atachanua kama yungiyungi, na kueneza mizizi yake kama mti wa Lebanoni. Matawi yake yatasambaa, na utukufu wake utakuwa kama ule wa mzeituni, na harufu yake nzuri itakuwa kama ile ya mti wa Lebanoni. Watakaa tena katika kivuli chake. Watakuza nafaka, nao watachipuka kama mzabibu. Ukumbusho wake utakuwa kama divai ya Lebanoni.”

22 Waisraeli waliotubu wangeponywa kiroho na kuufurahia tena upendo wa Mungu. Yehova angekuwa kama umande wenye kuburudisha kwao kwa kuwa angewapa baraka nyingi. Watu wake waliorudishwa wangekuwa na utukufu “kama ule wa mzeituni,” nao wangetembea katika njia za Mungu. Kwa kuwa tumeazimia kutembea pamoja na Yehova Mungu, tunapaswa kufanya nini?

Endelea Kutembea Katika Njia za Yehova Zilizonyooka

23, 24. Kitabu cha Hosea kinamalizia na unabii gani wenye kutia moyo, nao unatuchocheaje?

23 Ili tuendelee kutembea pamoja na Mungu ni lazima tuwe na “hekima inayotoka juu” na tutende sikuzote kupatana na njia zake zilizonyooka. (Yakobo 3:17, 18) Mstari wa mwisho wa unabii wa Hosea unasema hivi: “Ni nani aliye na hekima, apate kuelewa mambo haya? Mwenye busara, apate kuyajua? Kwa maana njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo; bali wakosaji ndio watakaojikwaa katika hizo.”—Hosea 14:9.

24 Badala ya kufuata hekima na viwango vya ulimwengu huu, acheni tuazimie kutembea katika njia za Mungu zilizonyooka. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hosea alifanya hivyo kwa miaka 59 au zaidi. Alitangaza kwa uaminifu ujumbe wa Mungu, akijua kwamba watu wenye hekima na busara wataelewa maneno hayo. Namna gani sisi? Maadamu Yehova anaturuhusu kutoa ushahidi, tutaendelea kuwatafuta wale ambao kwa hekima watakubali fadhili zake zisizostahiliwa. Nasi tunafurahi kufanya hivyo tukishirikiana kwa ukamili na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45-47.

25. Uchanganuzi wetu wa unabii wa Hosea unapaswa kutusaidia kufanya nini?

25 Uchanganuzi wetu wa unabii wa Hosea unapaswa utusaidie kuendelea kutembea pamoja na Mungu huku tukitazamia uzima wa milele katika ulimwengu wake mpya ambao ameahidi. (2 Petro 3:13; Yuda 20, 21) Hilo ni tumaini zuri kama nini! Sisi binafsi tutaona tumaini hilo likitimia ikiwa tutaendelea kuthibitisha kwa maneno na kwa matendo kwamba tunasadiki kabisa maneno haya: “Njia za Yehova zimenyooka.”

Ungejibuje?

• Mungu atatutendeaje tukimtolea ibada safi?

• Kwa nini tunapaswa kumtumaini Yehova sikuzote?

• Kwa nini unasadiki kwamba njia za Yehova zimenyooka?

• Tunaweza kuendeleaje kutembea katika njia za Yehova zilizonyooka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kubali msaada wa kiroho kutoka kwa wazee Wakristo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unabii wa Hosea unatupa sababu ya kutumaini ahadi za Yehova za ufufuo

[Picha katika ukurasa wa 31]

Endelea kutembea pamoja na Mungu huku ukitazamia uzima wa milele