Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Pamoja na Mungu, Ukavune Mema

Tembea Pamoja na Mungu, Ukavune Mema

Tembea Pamoja na Mungu, Ukavune Mema

“Wao huendelea kupanda upepo, nao watavuna upepo wa dhoruba.”—HOSEA 8:7.

1. Tunaweza kutembeaje pamoja na Yehova?

KUSAFIRI katika eneo hatari kwaweza kuwa salama zaidi ikiwa kiongozi mwenye uzoefu atatuongoza njiani. Lingekuwa jambo la hekima kutembea pamoja na kiongozi kama huyo kuliko kutembea peke yetu. Mfano huo unaonyesha kwa njia fulani hali yetu. Ni kana kwamba Yehova amejitolea kutuongoza katika jangwa kubwa la ulimwengu mwovu wa sasa. Ni jambo la hekima tutembee pamoja naye badala ya kujaribu kuongoza hatua zetu wenyewe. Tunaweza kutembeaje pamoja na Mungu? Ni kwa kufuata mwongozo ambao ametoa katika Neno lake.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Makala iliyotangulia ilichanganua drama ya mfano iliyo katika kitabu cha Hosea sura ya kwanza hadi ya tano. Kama tulivyoona, drama hiyo inatufundisha mambo yanayoweza kutusaidia kutembea pamoja na Mungu. Acheni sasa tuzungumzie baadhi ya mambo makuu katika sura ya sita hadi tisa. Ni vizuri tuanze kwa muhtasari wa sura hizo nne.

Muhtasari

3. Eleza kwa ufupi yaliyomo katika Hosea sura ya sita hadi tisa.

3 Yehova alimtuma Hosea ili atoe unabii hasa kwa ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi. Taifa hilo, linaloitwa pia Efraimu, kufuatia jina la kabila lake kubwa, lilikuwa limemwacha Mungu. Kwenye Hosea sura ya sita hadi tisa, tunajifunza kwamba watu hao hawakuwa washikamanifu, nao walivunja agano la Yehova na kutenda uovu. (Hosea 6:7) Badala ya kumrudia Yehova, waliyatumaini mataifa ya ulimwengu. Kwa kuwa waliendelea kupanda mabaya, wangevuna mabaya. Naam, hukumu kali ilikuwa inakaribia. Hata hivyo, unabii wa Hosea pia una ujumbe unaochangamsha moyo. Watu hao walihakikishiwa kwamba wangeweza kumrudia Yehova na kuonyeshwa rehema ikiwa wangetubu kutoka moyoni.

4. Tutachunguza mambo gani katika unabii wa Hosea?

4 Kutokana na sura hizo nne za unabii wa Hosea, tunaweza kupata mwongozo zaidi utakaotusaidia kutembea pamoja na Mungu. Acheni tuchunguze mambo manne tunayoweza kujifunza: (1) Toba ya kweli huonyeshwa kwa matendo wala si kwa maneno matupu; (2) dhabihu peke yake hazimpendezi Mungu; (3) Yehova huhuzunika waabudu wake wanapomwacha; na (4) ili tuvune mema, ni lazima tupande mema.

Jinsi Toba ya Kweli Inavyoonyeshwa

5. Eleza jambo kuu linalozungumziwa katika Hosea 6:1-3.

5 Unabii wa Hosea unatufundisha mengi kuhusu toba na rehema. Tunasoma hivi kwenye Hosea 6:1-3: “Njooni, turudi kwa Yehova, kwa maana yeye mwenyewe amerarua vipande-vipande, lakini atatuponya. Alizidi kupiga, lakini atatufunga kitambaa. Atatufanya hai baada ya siku mbili. Katika siku ya tatu atatuinua, nasi tutaishi mbele zake. Nasi tutajua, tutafanya bidii kumjua Yehova. Kutokea kwake kumefanywa imara kama mapambazuko. Naye atakuja kwetu kama mvua inayonyesha; kama mvua ya masika ambayo huilowesha dunia.”

6-8. Toba ya Israeli ilikuwa na tatizo gani?

6 Ni nani aliyesema maneno yaliyoandikwa katika mistari hiyo? Watu fulani husema kwamba Waisraeli wasio waaminifu ndio waliosema maneno hayo, na kwamba watu hao wasiotii walikuwa wakijifanya kuwa wametubu na kuchezea rehema za Mungu. Hata hivyo, wengine husema kwamba nabii Hosea ndiye aliyeyasema, akiwasihi watu wamrudie Yehova. Hata iwe ni nani aliyesema maneno hayo, je, watu wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi walimrudia Yehova kwa ujumla, wakionyesha toba ya kweli? La hasha. Yehova anasema hivi kupitia Hosea: “Nitakufanyia nini, Ee Efraimu? Nitakufanyia nini, Ee Yuda, wakati fadhili zenu zenye upendo ni kama mawingu ya asubuhi na kama umande ambao hutoweka mapema?” (Hosea 6:4) Hilo lilionyesha wazi kabisa hali mbaya ya kiroho ya watu wa Mungu! Fadhili zenye upendo, au upendo mshikamanifu, zilikuwa zimekaribia kutoweka kabisa kama ukungu wa asubuhi ambao hutoweka haraka jua linapowaka. Ingawa inaonekana watu hao walijifanya kuwa wametubu, Yehova hakuona sababu yoyote ya kuwarehemu. Kwa nini?

7 Toba ya Israeli haikutoka moyoni. Andiko la Hosea 7:14 linaonyesha kwamba Yehova hakufurahishwa na watu wake linaposema hivi: “Hawakuniita mimi kwa moyo wao niwape msaada, ingawa waliendelea kupiga mayowe vitandani mwao.” Mstari wa 16 unaongeza hivi: “Wakaanza kurudi, lakini hawakurudi kwenye ibada ya kweli.” Watu hao hawakuwa tayari kuirudia ibada ya Yehova iliyokwezwa kwa kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa ili kurekebisha uhusiano wao pamoja naye. Naam, hawakutaka kutembea pamoja na Mungu.

8 Kulikuwa na tatizo lingine kuhusu toba ya Waisraeli. Watu waliendelea kutenda dhambi, naam, dhambi nyingi tofauti-tofauti kama vile udanganyifu, uuaji, wizi, ibada ya sanamu, na kufanya miungano isiyo ya hekima pamoja na mataifa mengine. Katika Hosea 7:4, watu hao wanafananishwa na “tanuru,” au jiko la mwokaji, labda kwa sababu ya tamaa mbaya zilizowaka ndani yao. Kutokana na hali hiyo mbaya ya kiroho, je, watu hao walistahili rehema? Sivyo hata kidogo! Hosea anawaambia waasi hao kwamba Yehova “atakumbuka kosa lao” na ‘kukazia fikira dhambi zao.’ (Hosea 9:9) Hawataonyeshwa rehema hata kidogo!

9. Maneno ya Hosea yanatufunza nini kuhusu toba na rehema?

9 Tunaposoma maneno ya Hosea, tunajifunza nini kuhusu toba na rehema? Mfano wenye kuonya wa Waisraeli wasio na imani unatufundisha kwamba ili tufaidike kutokana na rehema za Yehova, ni lazima tuonyeshe toba inayotoka moyoni. Toba hiyo huonyeshwaje? Hatuwezi kumpumbaza Yehova kwa machozi au kwa maneno matupu. Toba ya kweli huonyeshwa kwa matendo. Ili mkosaji apokee rehema, ni lazima aache kabisa njia yake ya dhambi na aishi kupatana na viwango vya juu vya ibada ya Yehova iliyokwezwa.

Dhabihu Peke Yake Hazimpendezi Yehova

10, 11. Kama inavyoonyeshwa na taifa la Israeli, kwa nini dhabihu peke yake hazimpendezi Yehova?

10 Sasa acheni tuzungumzie jambo la pili linaloweza kutusaidia kutembea pamoja na Yehova. Jambo hilo ni: Dhabihu peke yake hazimpendezi Mungu. Andiko la Hosea 6:6 linasema: “Mimi [Yehova] ninapendezwa na fadhili zenye upendo, na si dhabihu; ninapendezwa na kumjua Mungu kuliko matoleo mazima ya kuteketezwa.” Ona kwamba Yehova anapendezwa na fadhili zenye upendo, au upendo mshikamanifu, ambayo ni sifa inayotoka moyoni, na vilevile kumjua. Lakini labda unajiuliza: ‘Kwa nini mstari huo unasema kwamba Yehova hapendezwi na “dhabihu” na “matoleo mazima ya kuteketezwa”? Je, vitu hivyo havikuwa takwa chini ya Sheria ya Musa?’

11 Ni kweli kwamba dhabihu na matoleo yalikuwa takwa chini ya Sheria. Hata hivyo, watu wa siku za Hosea walikuwa na tatizo kubwa. Inaonekana kwamba Waisraeli fulani walikuwa wakitoa matoleo hayo kidesturi ili kuonyesha tu ujitoaji wao, huku wakiendelea kutenda dhambi. Kwa kutenda dhambi, walionyesha kwamba mioyo yao haikuwa na upendo mshikamanifu. Pia, walionyesha kwamba wamekataa kumjua Mungu kwa sababu hawakuwa wakiishi kupatana na ujuzi wa Mungu. Ikiwa watu hao hawakuwa na moyo unaofaa wala hawakuishi maisha manyoofu, je, kweli dhabihu zao zilikuwa na maana yoyote? Dhabihu zao zilimchukiza Yehova Mungu.

12. Andiko la Hosea 6:6 lina onyo gani kwa watu wanaoishi leo?

12 Maneno ya Hosea ni onyo kwa watu wengi wanaoenda kanisani leo. Wao humtolea Mungu matoleo kupitia shughuli zao za kidini. Lakini ibada yao haina maana yoyote katika maisha yao ya kila siku. Je, kweli watu hao wanampendeza Mungu ikiwa mioyo yao haiwachochei kupata ujuzi sahihi juu yake na kutumia ujuzi huo kwa kuacha kutenda mabaya? Yeyote asifikiri kwamba shughuli za kidini peke yake zinampendeza Mungu. Yehova hapendezwi na wanadamu wanaojaribu kupata kibali chake kwa kujifanya kuwa waabudu wake bila kuishi kikweli kulingana na Neno lake.—2 Timotheo 3:5.

13. Sisi hutoa dhabihu za aina gani, lakini tunapaswa kukumbuka nini kuhusu thamani ya dhabihu hizo?

13 Tukiwa Wakristo wa kweli tunatambua kwamba dhabihu peke yake hazimpendezi Mungu. Ni kweli kwamba hatumtolei Yehova dhabihu za wanyama. Hata hivyo, sisi ‘humtolea Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.’ (Waebrania 13:15) Ni muhimu kwamba tusiwe kama Waisraeli watenda-dhambi wa siku za Hosea, huku tukifikiri kwamba tunaweza kulipia makosa yetu kwa kumtolea Mungu dhabihu hizo za kiroho. Fikiria mfano wa msichana mmoja aliyefanya uasherati kisiri-siri. Baadaye alikubali hivi: “Niliongeza utumishi wangu wa shambani, nikifikiri kwamba kufanya hivyo labda kutafunika kosa langu.” Hivyo ndivyo Waisraeli wapotovu walivyojaribu kufanya. Hata hivyo, Yehova ataikubali dhabihu yetu ya sifa ikiwa tu inaambatana na moyo mnyoofu na mwenendo unaompendeza Mungu.

Yehova Huhuzunika Waabudu Wake Wanapomwacha

14. Unabii wa Hosea hufunua nini kuhusu hisia za Mungu?

14 Jambo la tatu ambalo tunajifunza kutokana na Hosea sura ya sita hadi tisa ni jinsi Yehova anavyohisi wakati waabudu wake wanapomwacha. Mungu ana hisia thabiti na nyororo. Ana hisia nyororo kama vile shangwe na huruma, naye huzionyesha kwa wale wanaotubu dhambi zao. Lakini watu wake wasipotubu, yeye huchukua hatua kali. Kwa sababu Mungu anatujali sana, yeye hushangilia tunapotembea pamoja naye kwa uaminifu. Zaburi 149:4 inasema: “Yehova anawafurahia watu wake.” Hata hivyo, Mungu huhisije watumishi wake wanapokosa kuwa waaminifu?

15. Kulingana na andiko la Hosea 6:7, Waisraeli fulani walikuwa wakitendaje?

15 Yehova anasema hivi kuhusu Waisraeli wasio waaminifu: “Wao wenyewe, kama mtu wa udongo, wamevunja lile agano. Hapo ndipo wamenitendea kwa hila.” (Hosea 6:7) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘tenda kwa hila’ pia linamaanisha “tenda kwa udanganyifu, (tenda) kwa kukosa uaminifu.” Katika Malaki 2:10-16, neno hilohilo la Kiebrania linatumiwa kufafanua mwenendo usio mshikamanifu wa Waisraeli ambao hawakuwa waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa. Kichapo kimoja kinasema hivi kuhusu matumizi ya neno hilo katika Hosea 6:7: ‘Ni neno la mfano linalotumiwa kuhusu ndoa na ambalo linaonyesha hisia za mtu katika uhusiano huo. Ndivyo anavyohisi mtu aliye katika uhusiano ambamo upendo umevunjwa.’

16, 17. (a) Taifa la Israeli lilitendaje kuhusiana na agano ambalo Mungu alifanya pamoja nalo? (b) Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu matendo yetu?

16 Yehova aliona Israeli kuwa mke wake wa mfano kwa sababu ya agano lake pamoja na taifa hilo. Kwa hiyo watu wake walipovunja matakwa ya agano hilo, ni kana kwamba walikuwa wakifanya uzinzi. Mungu alikuwa kama mume mwaminifu, lakini watu wake walimwacha!

17 Namna gani sisi? Tukitembea pamoja na Mungu au tukikosa kufanya hivyo, hilo hugusa hisia zake. Ni vema tukumbuke kwamba “Mungu ni upendo” na matendo yetu hugusa hisia zake. (1 Yohana 4:16) Tukifuata njia mbaya, tunaweza kumhuzunisha na kumchukiza Yehova. Kukumbuka jambo hilo kwaweza kutulinda sana tusianguke katika jaribu.

Jinsi Tunavyoweza Kuvuna Mema

18, 19. Ni kanuni gani iliyo katika Hosea 8:7, na kanuni hiyo ilitimiaje kwa Waisraeli?

18 Acheni tufikirie jambo la nne ambalo tunajifunza kutokana na unabii wa Hosea, yaani, jinsi tunavyoweza kuvuna mema. Hosea anaandika hivi kuhusu upumbavu na ubatili wa mwendo wa Waisraeli wasio na imani: “Wao huendelea kupanda upepo, nao watavuna upepo wa dhoruba.” (Hosea 8:7) Hapa tunapata kanuni ambayo tunapaswa kukumbuka: Kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya yale tunayotenda sasa na yale yatakayotupata baadaye. Kanuni hiyo ilitimiaje kwa Waisraeli wasio waaminifu?

19 Kwa kuendelea kutenda dhambi, Waisraeli hao walikuwa wakipanda mabaya. Je, wangeendelea kufanya hivyo bila kuvuna matokeo mabaya? Bila shaka, hawangeweza kuepuka hukumu kali. Andiko la Hosea 8:13 linasema hivi: “[Yehova] atakumbuka kosa lao na kutoza hesabu kwa sababu ya dhambi zao.” Na tunasoma hivi kwenye Hosea 9:17: “Mungu wangu atawakataa, kwa maana hawakumsikiliza, nao watakuwa wakimbizi katikati ya mataifa.” Yehova angewatoza hesabu Waisraeli kwa sababu ya dhambi zao. Kwa sababu walipanda mabaya, wangevuna mabaya. Hukumu ya Mungu ilikuja juu yao mwaka wa 740 K.W.K., wakati Waashuru walipoupindua ufalme wa Israeli wa makabila kumi na kuwapeleka wakaaji wake utekwani.

20. Yale yaliyowapata Waisraeli yanatufunza nini?

20 Yale yaliyowapata Waisraeli hao yanatufundisha ukweli fulani muhimu: Tunavuna tunachopanda. Neno la Mungu linatuonya hivi: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Tukipanda mabaya, tutavuna mabaya. Kwa mfano, wale wanaofuatia maisha mapotovu watavuna mabaya. Mkosaji asiyetubu atapata hali yenye kuhuzunisha.

21. Tunaweza kuvunaje mema?

21 Basi, tunaweza kuvunaje mema? Swali hilo linaweza kujibiwa kwa mfano huu rahisi. Mkulima akitaka kuvuna mahindi, je atapanda ngano? Hapana! Ni lazima apande kile anachotaka kuvuna. Vivyo hivyo, tukitaka kuvuna mema, lazima tupande mema. Je, unataka kuendelea kuvuna mema, yaani, kuishi maisha yanayoridhisha sasa na kuwa na tarajio la kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu? Ikiwa ndivyo, basi ni lazima uendelee kupanda mema kwa kutembea pamoja na Mungu na kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu.

22. Tumejifunza nini katika Hosea sura ya sita hadi tisa?

22 Kuanzia Hosea sura ya sita hadi tisa, tumejifunza mambo manne yanayoweza kutusaidia kutembea pamoja na Mungu: (1) Toba ya kweli huonyeshwa kwa matendo; (2) dhabihu peke yake hazimpendezi Mungu; (3) Yehova huhuzunika waabudu wake wanapomwacha; na (4) ili tuvune mema, ni lazima tupande mema. Sura tano za mwisho za kitabu hiki cha Biblia zinaweza kutusaidiaje kutembea pamoja na Mungu?

Ungejibuje?

• Toba ya kweli huonyeshwaje?

• Kwa nini dhabihu peke yake hazimpendezi Baba yetu wa mbinguni?

• Mungu huhisije waabudu wake wanapomwacha?

• Ni lazima tupande nini ili tuvune mema?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Upendo mshikamanifu wa Israeli ulitoweka kama mawingu ya asubuhi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tamaa mbaya za Israeli ziliwaka kama tanuru

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kwa nini Yehova alikataa dhabihu za watu wake?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ili tuvune mema, ni lazima tupande mema