Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii wa Hosea Hutusaidia Kutembea Pamoja na Mungu

Unabii wa Hosea Hutusaidia Kutembea Pamoja na Mungu

Unabii wa Hosea Hutusaidia Kutembea Pamoja na Mungu

“Watatembea kwa kumfuata Yehova.”—HOSEA 11:10.

1. Kuna drama gani ya mfano katika kitabu cha Hosea?

JE, UNAPENDA drama zenye waigizaji wanaovutia na zenye hadithi motomoto? Basi, kitabu cha Biblia cha Hosea kina drama ya mfano. * Drama hiyo inazungumzia hali zilizokuwepo katika familia ya nabii wa Mungu Hosea, nayo inaonyesha ndoa ya mfano ambayo Yehova alifunga pamoja na taifa la kale la Israeli kupitia agano la Sheria ya Musa.

2. Tunajua nini kumhusu Hosea?

2 Sura ya kwanza ya kitabu cha Hosea inaonyesha kikao cha drama hii. Inaonekana kwamba Hosea aliishi katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi (ambao pia uliitwa Efraimu, jina la kabila lake kubwa zaidi). Hosea alitoa unabii katika siku za watawala saba wa mwisho wa Israeli na wakati wa utawala wa Mfalme Uzia, Yothamu, Ahazi, na Hezekia wa Yuda. (Hosea 1:1) Hivyo, Hosea alitoa unabii angalau kwa miaka 59. Ingawa kitabu cha Hosea kilikamilishwa muda mfupi baada ya mwaka wa 745 K.W.K., kinafaa siku zetu, wakati ambapo mamilioni ya watu wanatenda kulingana na maneno haya ya unabii: “Watatembea kwa kumfuata Yehova.”—Hosea 11:10.

Muhtasari Unaonyesha Nini?

3, 4. Eleza kwa ufupi habari zilizomo katika Hosea sura ya kwanza hadi ya tano.

3 Kuchunguza muhtasari wa kitabu cha Hosea sura ya kwanza hadi ya tano kutaimarisha azimio letu la kutembea pamoja na Mungu kwa kuonyesha imani na kuishi kupatana na mapenzi yake. Ingawa wakaaji wa ufalme wa Israeli walikuwa na hatia ya kufanya uzinzi wa kiroho, Mungu angewarehemu ikiwa wangetubu. Hilo linaonyeshwa na jinsi ambavyo Hosea alishughulika na mke wake, Gomeri. Baada ya kumzalia Hosea mtoto mmoja, inaonekana Gomeri alipata watoto wengine wawili kwa njia ya uzinzi. Hata hivyo, Hosea alimkubali tena, sawa na vile Yehova alivyokuwa tayari kuwarehemu Waisraeli waliotubu.—Hosea 1:1–3:5.

4 Yehova alifanya kesi ya kisheria dhidi ya Israeli kwa sababu hakukuwa na ukweli, fadhili zenye upendo, wala ujuzi juu ya Mungu katika nchi hiyo. Yehova angelitoza hesabu taifa la Israeli lenye kuabudu sanamu na vilevile ufalme wa Yuda wenye kuasi. Lakini, wakati ambapo watu wa Mungu ‘wangekuwa katika dhiki kali,’ wangemtafuta Yehova.—Hosea 4:1–5:15.

Drama Yaanza

5, 6. (a) Uasherati ulikuwa umeenea kadiri gani katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi? (b) Kwa nini onyo lililotolewa kwa Israeli la kale ni muhimu kwetu?

5 Mungu alimwamuru Hosea hivi: “Nenda, jichukulie mke wa uasherati na watoto wa uasherati, kwa maana kwa sababu ya uasherati hakika nchi imegeuka isimfuate Yehova.” (Hosea 1:2) Uasherati ulikuwa umeenea kadiri gani katika Israeli? Tunaambiwa hivi: “Roho ya uasherati imewafanya [watu wa ufalme wa makabila kumi] watange-tange, nao kwa uasherati hutoka chini ya Mungu wao. . . . Binti zenu hufanya uasherati na binti-wakwe zenu hufanya uzinzi. . . . Kwa habari ya wanaume, hujiendea zao wenyewe pamoja na makahaba, nao hutoa dhabihu pamoja na wanawake makahaba wa hekaluni.”—Hosea 4:12-14.

6 Uasherati, wa kiroho na wa kimwili pia, ulikuwa umeenea sana katika Israeli. Kwa hiyo, Yehova ‘angewatoza hesabu’ Waisraeli. (Hosea 1:4; 4:9) Onyo hilo ni muhimu kwetu kwa sababu Yehova atawatoza hesabu wale wanaojihusisha na ukosefu wa adili na kushiriki ibada isiyo safi leo. Lakini wale wanaotembea pamoja na Mungu wanafuata viwango vyake vya ibada safi na wanatambua kwamba “hakuna mwasherati . . . aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.”—Waefeso 5:5; Yakobo 1:27.

7. Ni nini kilichofananishwa na ndoa kati ya Hosea na Gomeri?

7 Hosea alipomwoa Gomeri, inaonekana kwamba Gomeri alikuwa bikira, naye alikuwa mke mwaminifu wakati ‘alipomzalia mwana.’ (Hosea 1:3) Kama vile drama hiyo ya mfano inavyoonyesha, muda mfupi baada ya kuwaweka huru Waisraeli kutoka utumwani huko Misri mwaka wa 1513 K.W.K., Mungu alifanya agano pamoja nao ambalo lilikuwa kama mapatano ya ndoa safi. Kwa kukubali agano hilo, taifa la Israeli liliahidi kwamba litadumisha uaminifu kwa Yehova, ‘mume wake.’ (Isaya 54:5) Naam, ndoa hiyo ya mfano kati ya Mungu na Israeli ndiyo iliyofananishwa na ndoa safi kati ya Hosea na Gomeri. Lakini mambo yalibadilika sana!

8. Ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulianzaje, na unaweza kueleza nini kuhusu ibada yake?

8 Mke wa Hosea “akapata mimba tena, akazaa binti.” Huenda Gomeri alimzaa kwa njia ya uzinzi msichana huyo na mtoto mwingine aliyezaliwa baadaye. (Hosea 1:6, 8) Kwa kuwa Gomeri alifananisha Israeli, huenda ukauliza, ‘Taifa la Israeli lilifanyaje ukahaba?’ Katika mwaka wa 997 K.W.K., makabila kumi ya Israeli yalitengana na makabila ya kusini ya Yuda na Benyamini. Ibada ya ndama ikaanzishwa katika ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi ili watu wasiende Yuda kumwabudu Yehova kwenye hekalu lake huko Yerusalemu. Ibada ya mungu wa uwongo Baali, iliyotia ndani karamu za ngono, ikatia mizizi katika Israeli.

9. Kama ilivyotabiriwa kwenye Hosea 1:6, taifa la Israeli lilipatwa na nini?

9 Wakati Gomeri alipomzaa mtoto wake wa pili labda kwa njia ya uzinzi, Mungu alimwambia Hosea hivi: “Mwite jina lake Lo-ruhama [linalomaanisha “Hakuonyeshwa Rehema”], maana sitaionyesha rehema tena nyumba ya Israeli, kwa sababu hakika nitawaondolea mbali.” (Hosea 1:6) Yehova ‘aliwaondolea mbali’ wakati Waashuru walipowapeleka Waisraeli utekwani mwaka wa 740 K.W.K. Lakini Mungu alionyesha rehema kwa ufalme wa Yuda wa makabila mawili na akauokoa bila upinde, upanga, vita, farasi, wala wapanda-farasi. (Hosea 1:7) Katika usiku mmoja katika mwaka wa 732 K.W.K., malaika mmoja tu aliwaua askari-jeshi 185,000 wa Ashuru waliokuwa wamezingira Yerusalemu, jiji kuu la Yuda.—2 Wafalme 19:35.

Yehova Afanya Kesi ya Kisheria Dhidi ya Israeli

10. Mwenendo wa uzinzi wa Gomeri ulionyesha nini?

10 Gomeri alimwacha Hosea na kuwa “mke wa uasherati,” naye akaishi maisha ya uzinzi na mwanamume mwingine. Hilo lilionyesha jinsi ufalme wa Israeli ulivyofanya mapatano ya kisiasa pamoja na mataifa yenye kuabudu sanamu na kuanza kuyategemea. Badala ya kumsifu Yehova kwa sababu ya baraka za kimwili alizowapa, taifa la Israeli lilisifu miungu ya mataifa hayo na kuvunja agano la ndoa kati yake na Mungu kwa kujihusisha na ibada ya uwongo. Si ajabu kwamba Yehova alifanya kesi ya kisheria dhidi ya taifa hilo lililofanya uzinzi wa kiroho!—Hosea 1:2; 2:2, 12, 13.

11. Agano la Sheria lilipatwa na nini wakati Yehova alipoacha Israeli na Yuda wapelekwe uhamishoni?

11 Taifa la Israeli lilipata adhabu gani kwa kumwacha Mume Wake? Mungu alifanya Israeli “aende nyikani” huko Babilonia, taifa lililoshinda Ashuru, ambako Waisraeli walipelekwa utekwani mwaka wa 740 K.W.K. (Hosea 2:14) Yehova alipokomesha ufalme wa makabila kumi, hakuvunja agano lake la ndoa pamoja na taifa la awali la Israeli la makabila 12. Hata wakati ambapo Mungu aliruhusu Yerusalemu liharibiwe na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K., na kuacha watu wa Yuda wawe mateka, hakukomesha agano la Sheria ya Musa ambalo lilikuwa limemuunganisha katika ndoa ya mfano pamoja na taifa la Israeli la makabila 12. Uhusiano huo ulikoma wakati viongozi Wayahudi walipomkataa Yesu Kristo na kufanya auawe mwaka wa 33 W.K.—Wakolosai 2:14.

Yehova Ashauri Israeli

12, 13. Ni nini jambo kuu katika Hosea 2:6-8, na maneno hayo yalihusuje Israeli?

12 Mungu alishauri Israeli ‘aondolee mbali uasherati wake,’ lakini Israeli alitaka kuwafuata wale waliompenda kwa tamaa nyingi. (Hosea 2:2, 5) “Kwa sababu hiyo,” Yehova akasema, “ninazungushia njia yako ukuta wa miiba; nami nitasimamisha ukuta wa mawe juu yake, ili asipate kuona barabara zake. Naye kwa kweli atawafuata wale wanaompenda kwa tamaa nyingi, lakini hatawafikia; naye hakika atawatafuta, lakini hatawapata. Naye atasema, ‘Nataka kwenda, nirudi kwa mume wangu, yule wa kwanza, kwa maana hali ilikuwa nzuri zaidi kwangu wakati huo kuliko ilivyo sasa.’ Lakini yeye mwenyewe hakutambua kwamba mimi ndiye niliyempa nafaka na divai tamu na mafuta, na kwamba nilimfanya awe na fedha nyingi, na dhahabu, ambayo waliitumia kwa Baali [au, ambayo waliitumia kutengeneza sanamu ya Baali].”—Hosea 2:6-8.

13 Ingawa Israeli alitafuta msaada wa mataifa ambayo yalikuwa ‘yamempenda kwa tamaa nyingi,’ hakuna taifa lolote ambalo liliweza kumsaidia. Ni kana kwamba alikuwa amezingirwa na ua usioweza kupenywa hivi kwamba hayangeweza kufikisha msaada wowote kwake. Baada ya Ashuru kuzingira Israeli kwa miaka mitatu, jiji lake kuu Samaria lilianguka mwaka wa 740 K.W.K., na ufalme wa makabila kumi haukurudishwa tena. Ni wachache tu kati ya Waisraeli waliotekwa ambao wangeona jinsi maisha yalivyokuwa mazuri wakati mababu zao walipomtumikia Yehova. Mabaki hao wangekataa ibada ya Baali na kujitahidi kuwa na uhusiano wa kiagano tena pamoja na Yehova.

Kutazama Tena Drama Hiyo

14. Kwa nini Hosea alianzisha tena uhusiano wa ndoa pamoja na Gomeri?

14 Ili kuelewa kwa ukamili zaidi ulinganifu uliopo kati ya ndoa ya Hosea na uhusiano wa Israeli pamoja na Yehova, fikiria maneno haya: “Yehova akaendelea kuniambia: ‘Nenda tena, mpende mwanamke anayependwa na rafiki yako na ambaye anafanya uzinzi.’” (Hosea 3:1) Hosea alitii amri hiyo kwa kumnunua Gomeri kutoka kwa mwanamume aliyekuwa anaishi naye. Kisha Hosea akampa mke wake shauri hili kali: “Utakaa ukiwa wangu muda wa siku nyingi. Usifanye uasherati, nawe usiwe wa mwanamume mwingine.” (Hosea 3:2, 3) Gomeri alikubali nidhamu hiyo, naye Hosea akaanzisha tena uhusiano wa ndoa pamoja naye. Hilo linahusianaje na jinsi Mungu alivyoshughulika na watu wa Israeli na Yuda?

15, 16. (a) Taifa la Mungu lililotiwa nidhamu lingepataje rehema zake? (b) Andiko la Hosea 2:18 limetimizwaje?

15 Wakati watu wa Israeli na Yuda walipokuwa mateka huko Babiloni, Mungu alitumia manabii wake ‘kufikia mioyo yao.’ Ili wapate rehema zake, watu wake walipaswa kuonyesha toba na kumrudia Mume Wao, kama vile Gomeri alivyomrudia mume wake. Kisha, Yehova angetoa taifa lake, lililo kama mke aliyetiwa nidhamu, kutoka katika ‘nyika’ ya Babiloni na kulirudisha Yuda na Yerusalemu. (Hosea 2:14, 15) Alitimiza ahadi hiyo mwaka wa 537 K.W.K.

16 Pia, Mungu alitimiza ahadi hii: “Hakika nitafanya agano siku hiyo na mnyama wa mwituni na kiumbe kinachoruka cha mbinguni na kitu kinachotambaa cha nchi, nami nitavunja kutoka katika nchi upinde na upanga na vita, nami nitawafanya walale salama salimini.” (Hosea 2:18) Mabaki ya Wayahudi waliorudi katika nchi yao waliishi salama salimini, bila kuwaogopa wanyama. Unabii huo pia ulitimia mwaka wa 1919 W.K., wakati mabaki ya Israeli wa kiroho walipowekwa huru kutoka “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Sasa, wanaishi kwa usalama na wanafurahia kuwa katika paradiso ya kiroho pamoja na waandamani wao wanaotumaini kuishi milele duniani. Wakristo hao wa kweli hawana tabia za kinyama.—Ufunuo 14:8; Isaya 11:6-9; Wagalatia 6:16.

Tilia Maanani Mambo Tunayojifunza Hapa

17-19. (a) Ni sifa gani za Mungu ambazo tunasihiwa tuziige? (b) Tunapaswa kuchochewaje na rehema na huruma za Yehova?

17 Mungu ni mwenye rehema na mwenye huruma, na hivyo ndivyo tunavyopaswa kuwa. Hilo ni jambo moja ambalo tunajifunza katika sura za kwanza-kwanza za Hosea. (Hosea 1:6, 7; 2:23) Utayari wa Mungu wa kuwarehemu Waisraeli waliotubu unapatana na methali hii iliyoandikwa kwa mwongozo wa roho: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Methali 28:13) Pia, maneno haya ya mtunga-zaburi yanawafariji wakosaji wanaotubu: “Dhabihu kwa Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.”—Zaburi 51:17.

18 Unabii wa Hosea unakazia huruma na rehema za Mungu tunayemwabudu. Hata wengine wakiacha njia zake za uadilifu, wanaweza kutubu na kugeuka. Wakifanya hivyo, Yehova anawakaribisha. Aliwaonyesha rehema watu waliotubu katika taifa la Israeli, taifa ambalo alikuwa amefunga ndoa nalo kwa njia ya mfano. Ingawa walimwasi Yehova na ‘kumtia uchungu Mtakatifu wa Israeli, yeye alikuwa mwenye rehema, naye akaendelea kukumbuka kwamba wao ni wenye mwili wa nyama.’ (Zaburi 78:38-41) Rehema hizo zinapaswa kutuchochea tuendelee kutembea pamoja na Mungu wetu mwenye huruma, Yehova.

19 Ingawa dhambi kama vile uuaji, wizi, na uzinzi zilikuwa zimeenea sana katika Israeli, Yehova ‘alisema kwa kuufikia moyo wake.’ (Hosea 2:14; 4:2) Tunapotafakari kuhusu rehema na huruma za Yehova, mioyo yetu inapaswa kuguswa, na uhusiano wetu pamoja naye unapaswa kuimarika. Hivyo, acheni tujiulize hivi: ‘Ninaweza kuigaje rehema na huruma za Yehova kwa kadiri kubwa zaidi ninaposhughulika na wengine? Mkristo mwenzangu aliyeniudhi akiomba msamaha, je, mimi niko tayari kusamehe kama Mungu?’—Zaburi 86:5.

20. Toa mfano ili kuonyesha kwamba tunapaswa kuwa na uhakika katika tumaini tulilopewa na Mungu.

20 Mungu hutoa tumaini la kweli. Kwa mfano, aliahidi hivi: “Nitampa . . . nchi tambarare ya chini ya Akori kama lango la tumaini.” (Hosea 2:15) Tengenezo la Yehova la kale lililokuwa kama mke lilikuwa na tumaini hakika la kurudishwa katika nchi yake, mahali “nchi tambarare ya chini ya Akori” ilipokuwa. Kwa kuwa ahadi hiyo ilitimia mwaka wa 537 K.W.K., hilo linatupa sababu nzuri ya kushangilia tumaini hakika ambalo Yehova ametupa.

21. Ujuzi unahusikaje katika kutembea pamoja na Mungu?

21 Ili tuendelee kutembea pamoja na Mungu, tunahitaji kuendelea kupata ujuzi juu yake na kuutumia katika maisha yetu. Ujuzi juu ya Yehova ulikuwa haba sana katika Israeli. (Hosea 4:1, 6) Hata hivyo, wengine walithamini sana mafundisho ya Mungu, wakayatumia, nao wakapata baraka nyingi. Hosea alikuwa mmoja wao. Ndivyo ilivyokuwa pia na wale 7,000 katika siku za Eliya ambao hawakupiga magoti mbele ya Baali. (1 Wafalme 19:18; Waroma 11:1-4) Kuthamini mafundisho ya Mungu kutatusaidia tuendelee kutembea pamoja naye.—Zaburi 119:66; Isaya 30:20, 21.

22. Tunapaswa kuonaje uasi-imani?

22 Yehova anatazamia wanaume wanaowaongoza watu wake wakatae uasi-imani. Hata hivyo, andiko la Hosea 5:1 linasema hivi: “Sikieni hili, enyi makuhani, na mkaze uangalifu, enyi nyumba ya Israeli, na ninyi, enyi nyumba ya mfalme, tegeni sikio, kwa maana hukumu hii inawahusu ninyi; kwa maana mmekuwa mtego katika Mispa na kama wavu uliotandazwa juu ya Tabori.” Viongozi waasi-imani walikuwa mtego na wavu kwa Waisraeli kwa sababu waliwashawishi kuabudu sanamu. Inaonekana Mlima Tabori na mahali palipoitwa Mispa vilikuwa vituo vya ibada hiyo ya uwongo.

23. Umefaidikaje kwa kuchunguza kitabu cha Hosea sura ya kwanza hadi ya tano?

23 Kufikia sasa, unabii wa Hosea umetuonyesha kwamba Yehova ni Mungu mwenye rehema anayetoa tumaini na kuwabariki wale wanaoishi kulingana na mafundisho yake na kukataa uasi-imani. Basi, kama Waisraeli wa kale waliotubu, acheni tumtafute Yehova na kujitahidi sikuzote kumpendeza. (Hosea 5:15) Tukifanya hivyo, tutavuna mema na kupata shangwe na amani isiyo na kifani ambayo inapatikana kwa wote wanaotembea pamoja na Mungu kwa uaminifu.—Zaburi 100:2; Wafilipi 4:6, 7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Drama fulani ya mfano inasimuliwa kwenye Wagalatia 4:21-26. Kwa habari zaidi kuhusiana nayo, ona Buku la 2, ukurasa 693-694 katika kitabu Insight on the Scriptures (au Buku la 2 la Étude perspicace des Écritures, ukurasa 677-678), kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Ndoa ya Hosea na Gomeri ilifananisha nini?

• Kwa nini Yehova alifanya kesi ya kisheria dhidi ya Israeli?

• Ni jambo gani ambalo limekupendeza kati ya yale uliyojifunza katika Hosea sura ya kwanza hadi ya tano?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unajua mke wa Hosea anafananisha nani?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wakaaji wa Samaria walishindwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Watu wenye shangwe warudi kwenye nchi yao