Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Upendo wa Kila Mmoja Wenu Unaongezeka’

‘Upendo wa Kila Mmoja Wenu Unaongezeka’

‘Upendo wa Kila Mmoja Wenu Unaongezeka’

NCHI ya Japani ilikumbwa na misiba mingi mwaka wa 2004. Misiba hiyo ilitia ndani tufani, mafuriko, na matetemeko ya nchi. Iliathiri maisha ya watu wengi, kutia ndani Mashahidi wa Yehova. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, misiba hiyo iliwafanya Mashahidi waonyeshane upendo wa kindugu.—1 Petro 1:22.

Kwa mfano, kwa sababu ya mvua nyingi mwezi wa Julai, mto mmoja ulio katikati ya Japani ulifurika. Mafuriko hayo yaliharibu zaidi ya nyumba 20 za Mashahidi wa Yehova. Katika Jumba moja la Ufalme, maji yalifikia meta moja kutoka sakafuni. Bila kukawia, Mashahidi kutoka makutaniko jirani walikuja kusaidia. Mamia ya wajitoleaji walisafisha nyumba zilizokuwa zimejaa matope. Kwa muda wa majuma mawili tu, Jumba la Ufalme lilikuwa limesafishwa na kurekebishwa.

Mnamo Oktoba 23, eneo hilohilo lilikumbwa na tetemeko la nchi lenye kipimo cha 6.8 kwenye kipimo cha Richter. Watu 40 hivi walikufa na zaidi ya 100,000 wakahamishwa. Hakukuwa na maji, gesi, wala umeme katika eneo hilo. Ingawa tetemeko la nchi lilianzia umbali wa kilometa 50 tu kutoka kwenye lile Jumba la Ufalme lililokuwa limerekebishwa, jumba hilo halikuharibiwa. Lilitumiwa kwa muda kama kituo cha misaada. Waangalizi Wakristo walijitahidi kujua hali ya waamini wenzao nao walifurahi kujua kwamba hakuna aliyeumia wala kufa. Mapema siku iliyofuata, Mashahidi sita ambao walikuwa wameathiriwa na yale mafuriko yaliyotukia Julai, walijitolea kupeleka chakula na maji katika eneo lililokumbwa na tetemeko la nchi. Saa chache tu baada ya tetemeko hilo la nchi, misaada ilikuwa ikitolewa.

Mwangalizi mmoja Mkristo anasema hivi: “Wale walioathiriwa na mafuriko waliona kwamba kuwasaidia wale walioathiriwa na tetemeko la nchi ni njia bora ya kutoa shukrani kwa msaada ambao wao wenyewe walipokea. Walifanya kazi kwa bidii kuanzia mapema asubuhi hadi usiku sana, nao walikuwa na nyuso zenye shangwe nyingi!”

Wala mafuriko wala matetemeko ya nchi hayawezi kuharibu kifungo cha upendo kinachounganisha undugu wa Kikristo wa Mashahidi wa Yehova. Badala yake, misiba kama hiyo inapotokea, Wakristo huhisi kama vile mtume Paulo alivyowaambia waamini wenzake huko Thesalonike: “Upendo wa kila mmoja wenu na wa ninyi nyote unaongezeka kwa mtu na mwenzake.”—2 Wathesalonike 1:3.