Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha

Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha

Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha

NENO “Har–Magedoni” linatokana na neno la Kiebrania Har–Magedon, au “Mlima wa Megido.” Neno hilo linapatikana kwenye andiko la Ufunuo 16:16 linalosema hivi: “Yakawakusanya pamoja mahali panapoitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.” Ni nani wanaokusanywa kwenye Har–Magedoni, na kwa nini? Kwenye Ufunuo 16:14, tunasoma hivi: “Wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wanakusanywa pamoja “kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Maandiko hayo yanatokeza maswali zaidi yenye kupendeza. “Wafalme” hao wanapigania wapi? Wanapigania nini, na wanapigana na nani? Je, watatumia silaha za maangamizi makubwa kama watu wengi wanavyoamini? Je, kutakuwa na waokokaji wa Har–Magedoni? Acha Biblia ijibu.

Je, kutajwa kwa “Mlima wa Megido” kunamaanisha kwamba Har–Magedoni itapiganwa katika mlima fulani huko Mashariki ya Kati? La. Kwanza kabisa, hakuna mlima unaoitwa hivyo—mahali Megido ya kale ilipokuwa, kuna kilima tu chenye urefu wa meta 20 hivi kando ya bonde. Isitoshe, eneo la Megido haliwezi kuwatosha “wafalme [wote] wa dunia na majeshi yao.” (Ufunuo 19:19) Hata hivyo, Megido lilikuwa eneo ambako baadhi ya vita vikali sana na vya kukata maneno katika historia ya Mashariki ya Kati vilipiganwa. Hivyo, jina Har–Magedoni linawakilisha vita vya kukata maneno, vyenye mshindi mmoja tu.—Ona sanduku “Megido Ni Mfano Unaofaa,” katika ukurasa wa 5.

Har–Magedoni haiwezi kuwa tu vita kati ya mataifa ya dunia, kwa kuwa andiko la Ufunuo 16:14 linasema kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wanaungana pamoja katika “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Katika unabii wake ulioongozwa kwa roho, Yeremia alisema kwamba “wale waliouawa na Yehova” watatawanyika “kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia.” (Yeremia 25:33) Hivyo, Har–Magedoni si vita vya wanadamu vinavyopiganwa katika eneo fulani huko Mashariki ya Kati. Ni vita vya Yehova, na vinahusisha dunia nzima.

Ona kwamba kwenye Ufunuo 16:16, Har–Magedoni inatajwa kuwa “mahali.” Katika Biblia, “mahali” panaweza kufananisha hali fulani. Katika kisa hiki, ulimwengu wote utaungana kumpinga Yehova. (Ufunuo 12:6, 14) Kwenye Har–Magedoni, mataifa yote ya dunia yanaungana pamoja dhidi ya ‘majeshi yaliyo mbinguni’ chini ya amri ya kijeshi ya “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” Yesu Kristo.—Ufunuo 19:14, 16.

Namna gani lile dai la kwamba Har–Magedoni ni vita vinavyohusisha silaha za maangamizi makubwa au mgongano wa dunia na vitu vya angani? Je, Mungu mwenye upendo anaweza kuruhusu wanadamu na makao yao ya dunia, wapatwe na mwisho kama huo wenye kuogopesha? La. Anasema waziwazi kwamba hakuumba dunia “bila sababu” lakini “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18; Zaburi 96:10) Kwenye Har–Magedoni, Yehova hataharibu dunia yetu kwa kuiteketeza. Badala yake, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—Ufunuo 11:18.

Har–Magedoni Itatukia Wakati Gani?

Kwa karne nyingi, watu wamekisia-kisia jibu la swali hili, Har–Magedoni itatukia wakati gani? Kuchunguza kitabu cha Ufunuo kwa kukilinganisha na sehemu nyingine za Biblia kunaweza kutusaidia kujua wakati wa pigano hilo muhimu. Andiko la Ufunuo 16:15 linahusianisha Har–Magedoni na kuja kwa Yesu kama mwizi. Yesu alitumia mfano huo pia kueleza jinsi atakavyokuja kutekeleza hukumu juu ya mfumo huu wa mambo.—Mathayo 24:43, 44; 1 Wathesalonike 5:2.

Kama vile unabii wa Biblia uliotimizwa unavyoonyesha, tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo tangu mwaka wa 1914. * Sehemu ya mwisho ya siku za mwisho ni kile kipindi ambacho Yesu alikiita “dhiki kuu.” Biblia haitaji muda wa dhiki hiyo, lakini misiba inayohusiana nayo itakuwa mibaya zaidi kuliko mingine yote iliyowahi kutokea ulimwenguni. Dhiki kuu itafikia upeo wake kwenye Har–Magedoni.—Mathayo 24:21, 29.

Kwa kuwa Har–Magedoni ni “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” hakuna kitu ambacho wanadamu wanaweza kufanya ili kuiahirisha. Yehova amepanga “wakati uliowekwa” wa vita hivyo kuanza. ‘Havitachelewa.’—Habakuki 2:3.

Mungu Mwenye Uadilifu Apigana Vita vya Haki

Hata hivyo, kwa nini Mungu apigane vita vya ulimwenguni pote? Vita vya Har–Magedoni vinahusiana sana na haki, ambayo ni mojawapo ya sifa zake kuu. Biblia inasema: “Yehova ni mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Ameona matendo yote ya ukosefu wa haki yaliyofanywa katika historia ya wanadamu. Bila shaka, hilo humfanya aonyeshe chuki yake inayoongozwa na uadilifu. Hivyo, amemchagua Mwana wake apigane vita vya haki ili kuondolea mbali mfumo huu mwovu wa mambo.

Yehova tu ndiye anayeweza kupigana vita vya haki vya kuwaharibu waovu peke yao, na kuwaokoa watu wenye mioyo minyoofu popote walipo duniani. (Mathayo 24:40, 41; Ufunuo 7:9, 10, 13, 14) Na kwa sababu dunia yote ni uumbaji wake, ni yeye tu aliye na haki ya kuitawala.—Ufunuo 4:11.

Yehova atatumia njia gani dhidi ya adui zake? Kwa kweli, hatujui. Lakini tunajua kwamba ana njia za kuyaangamiza kabisa mataifa maovu. (Ayubu 38:22, 23; Sefania 1:15-18) Hata hivyo, waabudu wa Mungu duniani hawatashiriki katika pigano hilo. Maono kwenye Ufunuo sura ya 19 yanaonyesha kwamba ni majeshi ya mbinguni tu yatakayojiunga na Yesu Kristo katika vita hivyo. Hakuna mtumishi yeyote Mkristo wa Yehova hapa duniani atakayeshiriki.—2 Mambo ya Nyakati 20:15, 17.

Mungu Mwenye Hekima Hutoa Maonyo Mengi

Namna gani waokokaji? Kwa kweli, hakuna mtu anayepaswa kuangamizwa kwenye Har–Magedoni. Mtume Petro aliandika hivi: “Yehova . . . hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Naye mtume Paulo alisema kwamba ‘mapenzi ya Mungu ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.’—1 Timotheo 2:4.

Kwa hekima, Yehova amehakikisha kwamba “habari njema ya Ufalme” inahubiriwa ulimwenguni pote katika lugha mbalimbali ili kutimiza kusudi hilo. Kila mahali watu wanapewa nafasi ya kuokoka na kuendelea kuishi. (Mathayo 24:14; Zaburi 37:34; Wafilipi 2:12) Wale wanaokubali habari njema, wanaweza kuokoka Har–Magedoni na kuishi milele kwa ukamilifu katika paradiso duniani. (Ezekieli 18:23, 32; Sefania 2:3; Waroma 10:13) Tunaweza kutazamia mambo hayo kutoka kwa Mungu ambaye ni upendo.—1 Yohana 4:8.

Je, Mungu Mwenye Upendo Anaweza Kupigana?

Hata hivyo, watu wengi hujiuliza hivi, Kwa nini Mungu aliye mfano bora zaidi wa upendo anaweza kuwaharibu wanadamu wengi? Hali hiyo inaweza kulinganishwa na nyumba yenye panya wengi. Je, hukubali kwamba mwenye nyumba anayejali anapaswa kulinda afya na hali njema ya familia yake kwa kuwaondoa panya hao?

Vivyo hivyo, kwa sababu Yehova anawapenda wanadamu sana, ni lazima vita vya Har–Magedoni vipiganwe. Kusudi la Mungu ni kufanya dunia kuwa paradiso na kuwafanya wanadamu wawe wakamilifu na wenye amani, bila “mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:3, 4; Ufunuo 21:4) Basi, ni hatua gani inayopaswa kuchukuliwa dhidi ya watu wanaohatarisha amani na usalama wa wanadamu wenzao? Ni lazima Mungu awaondoe “panya” hao—waovu wasioweza kubadilika—kwa faida ya waadilifu.—2 Wathesalonike 1:8, 9; Ufunuo 21:8.

Migogoro na umwagaji mwingi wa damu unaotukia leo husababishwa na watawala wanadamu wasio wakamilifu na wenye tamaa ya ubinafsi ya kufaidi mataifa yao. (Mhubiri 8:9) Kwa sababu ya kujitahidi kujiongezea mamlaka, serikali za kibinadamu hupuuza kabisa Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Hakuna dalili yoyote inayoonyesha kwamba watamwachia Mungu na Kristo mamlaka hayo. (Zaburi 2:1-9) Kwa hiyo, serikali hizo lazima ziondolewe ili kuupa nafasi utawala wa uadilifu wa Ufalme wa Yehova chini ya Kristo. (Danieli 2:44) Ni lazima Har–Magedoni ipiganwe ili kusuluhisha kabisa suala la haki ya kutawala dunia na wanadamu.

Yehova ataingilia kati wakati wa Har–Magedoni kwa faida ya wanadamu. Hali za ulimwengu zinapoendelea kuzorota, ni utawala mkamilifu wa Mungu tu ndio utakaoweza kutosheleza kwa ukamilifu mahitaji ya wanadamu. Kutakuwa na amani ya kweli na mafanikio kupitia Ufalme wake tu. Hali za ulimwengu zinaweza kuwaje Mungu asipoingilia kati? Je, chuki, jeuri, na vita havitaendelea kuwasumbua wanadamu kama vile imekuwa katika karne zote za utawala wa mwanadamu? Kwa hakika, vita vya Har–Magedoni ni muhimu sana kwetu!—Luka 18:7, 8; 2 Petro 3:13.

Vita Vitakavyokomesha Vita Vyote

Har–Magedoni itatimiza jambo ambalo hakuna vita vingine vimewahi kutimiza, yaani, kukomesha vita vyote. Bila shaka, sisi sote tunatamani wakati ambapo vita havitakuwapo tena. Hata hivyo, jitihada za wanadamu zimeshindwa kukomesha vita. Jitihada hizo za muda mrefu za kukomesha vita zinaonyesha ukweli wa maneno haya ya Yeremia: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Biblia inaahidi hivi kuhusiana na yale ambayo Yehova atatimiza: “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—Zaburi 46:8, 9.

Mataifa yatakaposhambuliana kwa kutumia silaha zao hatari na kutisha kuharibu mazingira, Mtengenezaji wa dunia atachukua hatua wakati wa vita vya Har–Magedoni vinavyotajwa katika Biblia! (Ufunuo 11:18) Vita hivyo vitatimiza yale ambayo watu wanaomwogopa Mungu wametumaini kwa miaka mingi. Vitatetea haki ya utawala wa Mwenye dunia, Yehova Mungu, juu ya uumbaji wake wote.

Kwa hiyo, watu wanaopenda uadilifu hawapaswi kuogopa Har–Magedoni. Badala yake vita hivyo vinawapa tumaini. Vita vya Har–Magedoni vitaondolea mbali ufisadi na uovu wote kutoka duniani na kuleta mfumo mpya wa mambo wenye uadilifu chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi. (Isaya 11:4, 5) Badala ya kuwa mwisho wa kuogopesha wenye msiba, Har–Magedoni italeta mwanzo mpya wenye furaha kwa wanadamu waadilifu ambao wataishi milele katika dunia paradiso.—Zaburi 37:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ona kitabu, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, sura ya 11, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

MEGIDO NI MFANO UNAOFAA

Megido ya kale ilikuwa mahali muhimu sana, karibu na sehemu ya magharibi ya Bonde la Yezreeli lenye rutuba, kaskazini mwa Israeli. Barabara zilizotumiwa na wafanyabiashara na wanajeshi kutoka mataifa mbalimbali zilifika huko. Hivyo, Megido ikawa mahali pa vita vya kukata maneno. Profesa Graham Davies aliandika hivi katika kitabu chake (Cities of the Biblical WorldMegiddo): ‘Wafanyabiashara na wahamiaji kutoka sehemu mbalimbali wangeweza kufika katika jiji la Megido kwa urahisi; lakini wakati ambapo jiji hilo lilikuwa na uwezo, lingeweza kudhibiti njia za kuingia humo na hivyo kusimamia maendeleo ya kibiashara na ya kivita. Kwa hiyo, haishangazi kwamba mara nyingi jiji hilo lilipiganiwa, na walioshinda, walililinda sana.’

Historia ya jiji la Megido ilianza zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, wakati mtawala wa Misri, Thutmose wa Tatu, alipowashinda watawala wa Kanaani huko. Iliendelea kwa karne nyingi hadi mwaka wa 1918 wakati ambapo Jenerali Mwingereza, Edmund Allenby, alipoyashinda majeshi ya Uturuki. Mungu alimwezesha Mwamuzi Baraka kumshinda Mfalme Yabini wa Kanaani huko Megido. (Waamuzi 4:12-24; 5:19, 20) Mwamuzi Gideoni aliwashinda Wamidiani katika eneo hilohilo. (Waamuzi 7:1-22) Pia, Wafalme Ahazia na Yosia waliuawa huko.—2 Wafalme 9:27; 23:29, 30.

Hivyo, kuhusianisha Har–Magedoni na sehemu hiyo ni jambo linalofaa kwa kuwa Megido ni eneo lililotumiwa kwa ajili ya mapambano mengi ya kukata maneno. Ni mfano unaofaa kuonyesha ushindi kamili wa Mungu juu ya wote wanaompinga.

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Duniani pote, watu wanaonywa na kupewa nafasi ya kuokoka Har–Magedoni

[Picha katika ukurasa wa 7]

Har–Magedoni italeta mwanzo mpya wenye furaha